Taifa Linaloshika Uaminifu wa Maadili
“Fungueni malango . . . ili taifa lenye uadilifu linalodumisha mwenendo mwaminifu liweze kuingia.”—ISAYA 26:2, NW.
1. Kwa nini taarifa ya Isaya kuhusu “taifa lenye uadilifu” yaweza kushangaza?
LEO, kuna aina zote za mataifa. Mataifa fulani ni ya kidemokrasi, mengine ni ya kidikteta. Mengine ni tajiri, mengine ni maskini. Lakini yote hayo yana jambo fulani kati yayo: Yote ni sehemu ya ulimwengu ambao Shetani ndiye mungu. (2 Wakorintho 4:4) Kwa sababu hiyo, maneno ya Isaya yaweza kushangaza wengine asemapo hivi: “Fungueni malango, enyi wanaume, ili taifa lenye uadilifu linalodumisha mwenendo mwaminifu liweze kuingia.” (Isaya 26:2, NW) Eti taifa lenye uadilifu? Ndiyo, kuna taifa lenye uadilifu, kwa kuwa unabii waonyesha kuwapo kwalo katika siku yetu. Taifa hili lisilo la kawaida laweza kutambuliwaje?
2. “Taifa lenye uadilifu” ni nini? Twajuaje?
2 Katika tafsiri ya New World Translation ya Isaya 26:2, taifa hilo lasemwa kuwa lenye ‘kudumisha mwenendo mwadilifu.’ King James Version (pambizoni) latafsiri neno hilo, “taifa lenye uadilifu lishikalo zile kweli.” Yote mawili ni mafafanuzi yafaayo. Hakika, ni rahisi kutambua taifa lenye uadilifu kwa sababu hilo ndilo taifa la pekee duniani linalojitiisha kwa Kristo aliye Mfalme, na kwa hiyo si sehemu ya ulimwengu wa Shetani. (Yohana 17:16) Kwa hiyo, washiriki walo wamejulikana kuwa watu wa ‘kudumisha mwenendo mzuri kati ya mataifa.’ Wao hufuata mtindo wa maisha utukuzao Mungu. (1 Petro 2:12) Isitoshe, kokote waliko ulimwenguni, wao ni sehemu ya “kanisa [“kutaniko,” NW] la Mungu aliye hai, nguzo na msingi wa kweli.” (1 Timotheo 3:15) Wakitegemeza kweli, wao hukataa falsafa za kipagani zifundishwazo na Jumuiya ya Wakristo, nao hutetea “maziwa yasiyoghushiwa yaliyo ya lile neno”—Neno la Mungu, Biblia. (1 Petro 2:2, NW) Zaidi ya hayo, wao huhubiri kwa bidii habari njema za Ufalme “katika viumbe vyote vilivyo chini ya mbingu.” (Wakolosai 1:23) Je, kwaweza kuwa na shaka lolote kwamba taifa hili limefanyizwa kwa wale wasaliao wa “Israeli wa Mungu,” lile kutaniko la Wakristo watiwa-mafuta? La, hasha!—Wagalatia 6:16.
Taifa Lazaliwa
3. Eleza jinsi “taifa lenye uadilifu” lilivyokuja kuzaliwa.
3 “Taifa lenye uadilifu” lilizaliwa lini? Mwanzo walo ulitolewa unabii katika kitabu cha Isaya. Katika Isaya 66:7, 8, twasoma hivi: “Kabla [Sayuni] hajaona utungu alizaa; kabla maumivu yake hayajampata, alizaa mtoto mwanamume. . . . Sayuni, mara alipoona utungu, alizaa watoto [“wana,” NW] wake.” Jambo lisilo la kawaida kabisa, Sayuni, tengenezo la Mungu la kimbingu, lilikuwa lizae “mtoto mwanamume” kabla ya kuona utungu. Katika 1914 Ufalme wa Kimesiya ulizaliwa mbinguni. (Ufunuo 12:5) Baada ya tukio hilo, vita ya ulimwengu ya kwanza ilikumba mataifa mengi zaidi, nao Wakristo watiwa-mafuta wakapatwa na msononeko na mnyanyaso. Hatimaye, katika 1919, taifa la kiroho, yule “mtoto mwanamume,” lilizaliwa duniani. Kwa hiyo Sayuni ‘akazaa wana wake,’—washiriki watiwa-mafuta wa “taifa [jipya] lenye uadilifu”—nao walipangwa kitengenezo kwa ajili ya kazi ya ushahidi yenye kupanuka zaidi na zaidi.—Mathayo 24:3, 7, 8, 14; 1 Petro 2:9.
4. Kwa nini taifa la Mungu lenye uadilifu lililazimika kujitahidi ili kudumisha uaminifu wa maadili?
4 Tangu lianzishwe, taifa hili limekabili majaribu makali ya uaminifu wa maadili walo. Kwa nini? Ufalme wa kimbingu ulipozaliwa, Shetani na roho waovu wake walitupwa kutoka mbinguni hadi hapa duniani. Sauti kubwa ikatangaza: “Sasa kumekuwa wokovu, na nguvu, na ufalme wa Mungu wetu, na mamlaka ya Kristo wake; kwa maana ametupwa chini mshitaki wa ndugu zetu, yeye awashitakiye mbele za Mungu wetu, mchana na usiku. Nao wakamshinda kwa damu ya Mwana-Kondoo, na kwa neno la ushuhuda wao; ambao hawakupenda maisha yao hata kufa.” Shetani aliitikia badiliko hilo la matukio kwa hasira kali, “akaenda zake afanye vita juu ya wazao wake [wa mwanamke] waliosalia, wazishikao amri za Mungu, na kuwa na ushuhuda wa Yesu.” Wakikabiliwa na mashambulio ya Shetani, Wakristo watiwa-mafuta walisimama imara. Kufikia leo hii, washiriki wenye bidii wa taifa la Mungu lenye uadilifu huwa na imani katika damu ya Yesu yenye kufidi na huendelea kumpa Yehova jibu kwa mdhihaki wake mkuu kwa kushika uaminifu wa maadili “hata kufa.”—Ufunuo 12:1, 5, 9-12, 17; Mithali 27:11.
5. Ni mtazamo gani mzuri wa Mashahidi wa kisasa umewasaidia kushika uaminifu wa maadili?
5 Katika 1919, wakati ushahidi wa kisasa kwa Ufalme wa Mungu ulipoanzishwa, Wanafunzi wa Biblia, kama Mashahidi wa Yehova walivyoitwa wakati huo, walikuwa wachache lakini wenye nguvu katika imani. Wao wakawa washiriki wa msingi wa ‘mji ulio na nguvu, wenye wokovu kuwa kuta na maboma.’ Tumaini lao lilikuwa katika “BWANA YEHOVA [aliye] mwamba wa milele.” (Isaya 26:1, 3, 4) Kama Musa wa kale, wao walitangaza hivi: “Nitalitangaza Jina la BWANA; mpeni ukuu Mungu wetu. Yeye Mwamba, kazi yake ni kamilifu; maana njia zake zote ni haki. Mungu wa uaminifu, asiye na uovu, yeye ndiye mwenye haki na adili.”—Kumbukumbu la Torati 32:3, 4.
6. Ni katika njia gani Yehova amebariki watu wake katika siku za mwisho?
6 Tangu wakati huo, malango ya mpango wa Ufalme wa Mungu yamebaki yakiwa wazi wakati wale wasaliao wa Wakristo watiwa-mafuta 144,000 walipokusanywa kwanza na sasa umati mkubwa wa “kondoo wengine” wanajiunga katika kutangaza makusudi ya Yehova ya Ufalme. (Yohana 10:16) Kwa hiyo, yaweza kutangazwa kwa shangwe kwamba: “Umeliongeza hilo taifa, BWANA, umeliongeza taifa; wewe umetukuzwa, umeipanua mipaka yote ya nchi hii.” (Isaya 26:15) Tuchunguzapo shamba la ulimwengu leo, twaona jinsi maneno hayo yalivyo kweli kama nini! Kwa uwezo wa roho takatifu, ushahidi wa Ufalme wa Kristo unaokuja umetolewa “hata mwisho wa nchi.” (Matendo 1:8) Kadiri ya upanuzi huo yaweza kupimwa kutokana na Ripoti ya Mwaka wa Utumishi wa 1994 ya Mashahidi wa Yehova Ulimwenguni Pote, iliyo katika kurasa 12 hadi 15.
Kilele Kipya cha Wahubiri
7, 8. (a) Kuna uthibitisho gani kwamba watu wa Mungu ‘wameongeza urefu wa kamba zao za hema’? (b) Kwa kutazama Ripoti ya Mwaka wa Utumishi wa 1994, ni maeneo yapi unayoona ‘yanapanua mipaka yao’ kwa njia ya kutokeza sana?
7 Fikiria baadhi ya mambo makuu ya ripoti hii. Kilele cha wahubiri wa Ufalme walio shambani kilifika 4,914,094! Ni jambo la kusisimua kama nini kuona mkusanyo wa daima wa “mkutano mkubwa . . . wa kila taifa, na kabila, na jamaa, na lugha, wamesimama mbele ya kile kiti cha enzi, na mbele za Mwana-Kondoo, wamevikwa mavazi meupe”! Ndiyo, wao pia wamejithibitisha kuwa washika uaminifu wa maadili. “Wamefua mavazi yao, na kuyafanya meupe katika damu ya Mwana-Kondoo,” wakionwa kuwa waadilifu kwa sababu ya kudhihirisha imani katika dhabihu ya fidia ya Yesu.—Ufunuo 7:9, 14.
8 Hasa tangu 1919, tengenezo la Yehova limeamriwa hivi: “Panua mahali pa hema yako, na wayatandaze mapazia ya maskani yako; usiwakataze; ongeza urefu wa kamba zako; vikaze vigingi vya hema yako.” (Isaya 54:2) Kwa itikio, kazi ya kuhubiri huendelea bila kukoma, hata katika Yukon yenye barafu, inayopakana na Alaska, ambako kikundi cha mapainia wawezao kustahimili magumu huvumilia halijoto ziwezazo kupungua kufikia digrii za sentigredi 45 hadi 50 chini ya sufuri kwa majuma kadhaa kwa kipindi kimoja. Katika miaka ya karibuni umati mwingi umekuwa ukimiminikia haraka zaidi taifa la Yehova linaloshika uaminifu wa maadili. Malango yamefunguka zaidi ili kupokea hawa kutoka nchi za Asia ambazo si za Jumuiya ya Wakristo, kutoka zile zilizokuwa zamani ngome za Ukomunisti, kutoka nchi nyingi za Afrika, na kutoka katika milki za Katoliki, kama vile Italia, Hispania, Ureno, na Amerika Kusini. Watu waliopoteza makao wamefungua shamba jingine. Kwa kielelezo, katika Uingereza, Mashahidi wanashughulikia mahitaji ya vikundi 13 vya kikabila vya lugha za kigeni.
“Fulizeni Kufanya Hili”
9. (a) Hudhurio la Ukumbusho wa 1994 laonyesha nini? (b) Ni zipi baadhi ya nchi zenye mahudhurio makubwa isivyo kawaida kwa Ukumbusho?
9 Jambo jingine kuu la ripoti ya mwaka ni hudhurio la Ukumbusho. Muda mfupi kabla afe, Yesu alianzisha Ukumbusho unaoadhimisha kifo chake naye akawaambia wafuasi wake: “Fulizeni kufanya hili katika ukumbuko wangu.” (1 Wakorintho 11:24, NW) Ilisisimua katika 1994 kuona 12,288,917—wengi zaidi ya mara mbili kuliko idadi ya wahubiri watendaji—wakikusanyika pamoja kutii amri hiyo, ama wakiwa washiriki ama wakiwa watazamaji. Katika nchi fulani uwiano wa wahudhuriaji wa Ukumbusho kwa wahubiri ulikuwa juu hata zaidi. Wale wahubiri 4,049 katika Estonia, Latvia, na Lithuania walichachawa kuwa na 12,876 wakihudhuria Ukumbusho, ikipita idadi ya wahubiri kwa zaidi ya mara tatu. Na katika Benin, wale wahudhuriaji 16,786 wa Ukumbusho walipita idadi ya wahubiri kwa karibu mara tano. Kutaniko moja la wahubiri 45 lilikuwa na watu 831 waliohudhuria!
10. (a) Hudhurio kubwa la Ukumbusho laweka daraka gani kwetu? (b) Eleza jambo liwezalo kutendeka wakati mtu ahudhuriaye Ukumbusho apokeapo msaada zaidi.
10 Mashahidi wa Yehova wana furaha kwamba watu wengi wenye kupendezwa walijiunga nao katika pindi hiyo nzuri sana. Sasa wanataka kuwasaidia hawa wafanye maendeleo zaidi katika uelewevu wao na upendo wao kuelekea kweli. Wengine wanaweza kuitikia kama alivyoitikia Alla katika Urusi. Alla alikuwa akijifunza pamoja na dada aliye painia wa pekee lakini hakufanya maendeleo sana kwa hiyo funzo hilo lilikomeshwa. Hata hivyo, Alla alikubali mwaliko wa kuhudhuria Ukumbusho. Mkutano huo, ulio wa maana sana, ulimvutia sana. Aliporudi nyumbani, alitupa picha zake zote za sanamu na kusali kwa Yehova amsaidie. Siku mbili baadaye yule dada painia akamtembelea Alla kuona jinsi alivyofurahia Ukumbusho. Mazungumzo yenye matokeo yakafuata. Funzo la Alla lilianzishwa upya. Upesi alikuwa akishiriki katika kazi ya kutoa ushahidi. Jambo hilo lililoonwa laonyesha ubora wa ziara za kufuatia wale waliohudhuria Ukumbusho. Yaelekea wengi wataitikia kama Alla.
“Tusiache Kukusanyika Pamoja”
11-13. (a) Ni nini sehemu ya mwenendo mwaminifu wa taifa lenye uadilifu? (b) Kwa nini Wakristo wa kweli huhitaji kuhudhuria mikutano?
11 Ukumbusho ndio mkutano muhimu zaidi katika mambo ya Mashahidi wa Yehova, lakini sio mkutano wa pekee. Kila juma Mashahidi wa Yehova hukusanyika pamoja katika kutii maneno ya mtume Paulo: “Tukaangaliane sisi kwa sisi na kuhimizana katika upendo na kazi nzuri; wala tusiache kukusanyika pamoja, kama ilivyo desturi ya wengine; bali tuonyane; na kuzidi kufanya hivyo, kwa kadiri mwonavyo siku ile kuwa inakaribia.” (Waebrania 10:24, 25) Wao wanashirikiana na taifa la Yehova lenye uadilifu linalotambuliwa kwa mwenendo walo mwaminifu. Mwenendo mwaminifu wahusisha kuhudhuria mikutano.
12 Hilo ni jambo ambalo limefahamiwa vizuri katika Filipino, ambako wastani wa hudhurio nchini kote katika mikutano ya Jumapili ni asilimia 125 ya idadi ya wahubiri. Pia limefahamiwa vizuri na kikundi cha Mashahidi na watu wanaopendezwa katika Argentina. Wao waishi kilometa zipatazo 20 kutoka Jumba la Ufalme. Hata hivyo, mwangalizi wa mzunguko aripoti kwamba kama si hali za ugonjwa, hakuna mmoja wao akosaye mikutano wakati wowote. Wao husafiri kwa muda wa saa nne kwa kigari cha kukokotwa na farasi au kwa kupanda farasi, na katika majira ya kipupwe wao husafiri kurudi nyumbani katika giza la usiku.
13 Mwisho wa mfumo huu ukaribiapo, maisha yazidi kuwa magumu, matatizo yaongezeka, na kuhudhuria mikutano kwa ukawaida kwaweza kuwa jambo gumu. Lakini katika hali kama hizo, twahitaji chakula cha kiroho hata zaidi kuliko wakati mwingine wowote na ushirika mchangamfu uwezao kupatikana katika vikusanyiko hivyo pekee.
“Lifanye kwa Hima”
14. Kwa nini Mashahidi wa Yehova wana hisia ya hima kuhusu huduma yao, na ni matokeo gani yanayoonyesha hilo?
14 Mwaka uliopita, Kanisa Katoliki katika Italia lilirejezea kazi ya Mashahidi wa Yehova kuwa “kubadili watu kwa njia ya ukali.” Lakini, kwa kweli, hakuna ukali katika yale Mashahidi hufanya. Badala ya hivyo, huduma yao ni wonyesho wa upendo wa kina kirefu kwa majirani wao. Huo pia ni wonyesho wa kutii kwao maneno ya Paulo: “Lihubiri neno, lifanye kwa hima katika majira yenye kufaa, katika majira yenye taabu.” (2 Timotheo 4:2, NW) Hisi ya kufanya kwa hima husukuma Mashahidi wa Yehova wawe wenye bidii katika huduma yao, kama ionwavyo katika kutumia kwao jumla ya saa 1,096,065,354 katika 1994 wakihubiri majirani, wakifanya ziara za kurudia, na kuongoza mafunzo ya Biblia 4,701,357. Wengi waliweza kushiriki katika utumishi wa upainia, jambo lionyeshalo kwamba roho ya upainia ipo, nayo inasitawi. Wastani wa mapainia 636,202 ulimwenguni pote wathibitisha jambo hilo.
15, 16. (a) Wote vijana kwa wazee wameonyeshaje roho ya upainia? (b) Kwa kutazama nchi moja-moja katika Ripoti ya Mwaka wa Utumishi wa 1994, ni wapi unapoona idadi yenye kutokeza ya mapainia?
15 Miongoni mwa mapainia hao mna vijana wengi. Wengine katika Marekani sasa hutumika wakiwa mapainia wa kawaida wakiwa katika shule za sekondari, wanadarasa wenzao wakiwa eneo lao kuu. Vijana hao wamepata kwamba kupainia ni njia bora zaidi ya kujikinga dhidi ya dawa za kulevya, ukosefu wa adili, na jeuri ambayo imeenea katika shule nyingi nchini humo. Vijana wengine wengi wana mradi wa kuwa mapainia wamalizapo shule. Irina, katika Ukrainia, alifanya upainia-msaidizi katika miaka yake yote ya shule ya sekondari ili ajitayarishe kwa ajili ya upainia baada ya kuhitimu. Alipomaliza shule, familia yake ilijitoa kumsaidia kifedha ili aweze kuiwakilisha katika kazi ya upainia wa kawaida. Mambo si rahisi kiuchumi katika Ukrainia. Lakini Irina asema: “Najua kwamba ninafanya kazi imaanishayo uhai si kwangu tu bali pia kwa wale niwahubirio.” Kwa kweli inafurahisha sana kuona vijana wengi leo wakifikiri kama Irina. Ni njia nzuri kama nini kwao ‘kumkumbuka Muumba wao Mtukufu katika siku za ujana wao’?—Mhubiri 12:1.
16 Idadi kubwa ya mapainia wana umri mkubwa sana. Mmoja aripoti kwamba katika vita ya ulimwengu ya pili, baba yake na ndugu yake waliuawa walipopigana katika vita hiyo, na mama yake na dada yake waliuawa katika mtaa mmoja wa hali ya chini. Baadaye alipoteza mwana wake. Sasa, akizidi kuwa mzee-mzee mno na kuwa na afya mbaya, Yehova amempa, katika kutaniko la Kikristo, familia kubwa zaidi kuliko ile aliyopoteza. Naye hupata shangwe katika kusaidia wengine kuwa mapainia wa kawaida.
17, 18. Kila mmoja wetu, tuwe painia au la, aweza kuonyeshaje roho ya upainia?
17 Bila shaka, si kila mtu awezaye kupainia. Yehova hufurahi kupokea zaka yetu yote, kile tuwezacho kutoa, hata kiwe nini katika hali yetu sisi binafsi. (Malaki 3:10) Kwa kweli sisi sote twaweza kusitawisha roho ya mapainia hawa wenye bidii na kufanya yote tuwezayo kufanya katika hali zetu ili kuendeleza kuhubiriwa kwa habari njema.
18 Kwa mfano, katika Australia, Aprili 16 iliwekwa kando kuwa siku ya pekee kwa ajili ya kuhubiri barabarani. Iliungwa mkono vizuri na wahubiri pamoja na mapainia, kama ilivyothibitishwa na kilele kipya cha wahubiri 58,780 kwa mwezi huo. Kwa kuongezea, magazeti zaidi ya 90,000 yaligawanywa kushinda mwezi uo huo mwaka uliopita. Katika siku hiyo ya pekee, dada mmoja aliangushia mtu fulani magazeti, na alipokuwa akiandika jina lake na anwani yake ili afuatie kupendezwa huko, aligundua kwamba walikuwa watu wa ukoo mmoja! Ikatokea kwamba walikuwa binamu ambao hawakuwa wameonana kwa miaka 30. Hakika hilo lilitokeza ziara za kurudia zenye kufurahisha!
Shika Uaminifu wa Maadili Hadi Mwisho
19. Kwa nini ni jambo la hima kwamba taifa lenye uadilifu la Yehova lishike uaminifu wa maadili kufikia mwisho kabisa?
19 Ni muhimu kwamba wote walio katika taifa la Mungu lenye uadilifu washike uaminifu wa maadili wakati ulimwengu wa Shetani unapofikia hatua za mwisho. Upesi taifa takatifu la Yehova litasikia mwito huu: “Njoni, watu wangu, ingia wewe ndani ya vyumba vyako, ukafunge mlango nyuma yako ujifiche kitambo kidogo, mpaka ghadhabu hii itakapopita.” Ulimwengu huu ulio na hatia ya damu hakika utapata hukumu ya kimungu. “Kwa maana, tazama, BWANA anakuja kutoka mahali pake, ili kuwaadhibu wakaao duniani, kwa sababu ya uovu wao; ardhi nayo itafunua damu yake, wala haitawafunika tena watu wake waliouawa.” (Isaya 26:20, 21) Kila mmoja wetu na asimame imara akiwa Mkristo ashikaye uaminifu wa maadili akishirikiana na taifa la Yehova lenye uadilifu. Kisha tutashangilia kupata uhai wa milele katika makao ya kidunia au ya kimbingu ya Ufalme wa Kristo.
Je, Wakumbuka?
◻ “Taifa lenye uadilifu” lilizaliwa lini?
◻ Kwa nini watu wa Mungu wamehitaji uvumilivu katika hizi siku za mwisho?
◻ Ni nini kionyeshwacho na idadi kubwa ya wahubiri na vilevile muda wa saa zilizotumiwa katika huduma kama inavyoonekana katika Ripoti ya Mwaka wa Utumishi wa 1994?
◻ Kwa nini hudhurio kwenye mikutano ni muhimu sana ulimwengu huu ukaribiapo mwisho wao?
◻ Kwa nini wote walio na ushirikiano na taifa la Mungu lenye uadilifu washike uaminifu wa maadili?
[Chati katika ukurasa wa 12-15]
RIPOTI YA MWAKA WA UTUMISHI WA 1994 YA MASHAHIDI WA YEHOVA ULIMWENGUNI POTE
(Ona buku lililojalidiwa)
[Picha katika ukurasa wa 18]
Washika uaminifu wa maadili katika taifa lenye uadilifu la Yehova watapata uhai wa milele katika ukamilifu