Shangwe ya Yubile Kati ya Watu wa Mungu
MANENO ya mfalme Daudi, yaliyotiwa katika kumbukumbu kwenye Zaburi 68, mistari 2-4 (NW), yanatia ndani mwaliko mchangamfu kwa wote wapendao uhuru wa kweli: “Ninyi mwimbieni Mungu, fanyieni jina lake mdundo mtamu wa kimuziki; inueni wimbo kwa Yule anayepita juu ya nyika akiwa Yah, ambalo ndilo jina lake; na mfanye shangwe ya Yubile mbele zake.” Kungeweza kuwa na pendeleo gani lililo kubwa kuliko kufanya shangwe ya Yubile mbele za Mungu wetu? (Isaya 12:2, 3) Katika muda wote wa mwaka 1986, Yehova ametegemeza mashahidi wake kwa njia nzuri ajabu, wakati ambao wameendelea kuzitangazia uhuru jamii za watu wa dunia.
Kurasa zinazofuata zinatoa muhtasari wa utendaji wa ulimwenguni pote wa Mashahidi wa Yehova wakati wa 1986. Ni sababu nzuri kama nini ya kufanya shangwe ya Yubile! Kama vile tarakimu zinavyoonyesha, hesabu ya kilele cha Mashahidi watendaji katika nchi zile 208 zenye kuripoti imepanda kufikia, 3,229,022, hilo likiwa ni ongezeko la asilimia 6.8 wakati wa mwaka. Hesabu ya waliobatizwa ilikuwa 225,868.
Kukumbuka Kifo cha Yesu
Hudhurio kwenye mkutano ule mkuu wa mwaka, Ukumbusho wa kifo cha Yesu, lilipanda likafikia angalau 8,160,597, ingawa ripoti nyingine hazikupokewa kwa sababu ya hali za ulimwengu kuwa mbaya zaidi. Hesabu ya wenye kushiriki mifano ya Ukumbusho ikawa 8,927 maadamu wapakwa-mafuta wenye umri mkubwa walimaliza utumishi wao wa kidunia. —Ufunuo 2:10.
Wengi wa wale waliokusanyika kwa kutii amri ya Yesu walionyesha ushujaa ulio mfano kwa wengine. (1 Wakorintho 11:23-26; Yohana 16:33) Katika nchi moja ya Afrika ambamo kazi ya Yehova imepigwa marufuku, kundi lilikuwa limekusanyika kwenye nyumba ya dada mmoja kuadhimisha Ukumbusho. Baada ya hotuba kuendelea kwa dakika nane tu, wenye mamlaka wa huko walitokea wakija kuwakamata akina ndugu. Wakawaagiza wakomeshe mkutano ule. Akina ndugu walisisitiza kwa fadhili lakini kwa imara kwamba ni lazima watukuze Ukumbusho huo wa kifo cha dhabihu ya Yesu. Baada ya kutoa sababu na kuwaomba sana mapolisi, waliruhusiwa waendelee huku wakisikiwa na maafisa hao. Mkutano ulimalizwa kwa amani, ndipo wote wakakamatwa. Baada ya kipindi cha kuulizwa-ulizwa maulizo, watano walitiwa kizuizini. Wakabaki gerezani kwa muda fulani lakini ndipo wakaachiliwa, wakiwa wenye furaha kwamba waliweza hivyo kusherehekea chakula cha jioni cha Bwana!—1 Yohana 5:3, 4.
Naijeria, ambako hesabu ya Mashahidi imeongezeka kufikia 128,461 ilikuwa na hudhurio la Ukumbusho la 394,370—hesabu iliyo juu zaidi kufikia sasa. Mkutano mmoja wa Ukumbusho ulifanywa kwenye uwanja wa majengo mapya ya Betheli kule Igieduma, na watu zaidi ya 700—karibu kijiji kizima cha mahali hapo—wakawapo!
Kutoka Meksiko inakuja ripoti hii: “Kila mahali tunakokwenda nchini, wahubiri wanabubujika shauku ya ajabu, na nchi nzima inaonekana ni kama imewaka moto wa ukweli. Ukweli umewafunika akina ndugu, na maisha zao zinautegemea ukweli kila upande. Jamaa nzima-nzima zinaingia katika ukweli. Kiasi kikubwa cha asilimia ya watu wanaojifunza kinaanza kuhudhuria mikutano wakati ule ule. Jambo hilo linawasaidia wafanye maendeleo ya haraka sana.” Meksiko iliripoti hudhurio la Ukumbusho la watu 838,467. Katika Agosti, wale wahubiri wa Ufalme 198,003 katika nchi hiyo walikuwa wakiongoza mafunzo ya Biblia 327,664 katika nyumba za watu. Wana uwezekano mkubwa kama nini wa kuendelea kuongezeka!
Mpanuko Zaidi wa Duniani Pote
Kutoka katikati ya Jumuiya ya Wakristo zinakuja ripoti kama hizo za mpanuko. Italia ilifikia kilele kipya cha wahubiri 139,570 katika Agosti, na watu 301,009 walikuwako kwa ajili ya mwadhimisho wa Chakula cha Jioni cha Bwana. Mashahidi wa Yehova ‘wanaacha nuru yao iangaze mbele ya watu’ kweli kweli. (Mathayo 5:16) Kwa mfano: “Dada mmoja alikuwa akitumbukiza pesa ndani ya mashine ya tikiti katika basi wakati mtu anayemfahamu kidogo alipomwambia hakukuwa na uhitaji wa kulipia tikiti maadamu safari yake ilikuwa fupi sana. Dada yule akaeleza kwamba ilikuwa sawa kulipa tikiti ile, hata kwa kituo kimoja tu. Baada ya hapo rafiki yake huyo akatoka ndani ya basi hiyo. Kisha ikawa kwamba, dereva wa basi akamgeukia dada yule na kusema: ‘Je! wewe ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova?’ ‘Ndivyo,’ dada akajibu, ‘ni jambo gani lililokufanya uniulize?’ ‘Nimesikia maongezi yenu juu ya kulipa tikiti ya basi, nami najua kwamba Mashahidi wa Yehova wamo kati ya watu walio wachache sana wanaofanya hivyo na walio wanyofu katika mambo yote.’ Miezi michache baadaye, mwanamume mmoja alimfikia dada yule kwenye mkutano mmoja akasema, ‘Wewe unanijua? Mimi ndimi yule dereva wa basi aliyesema nawe juu ya kulipa tikiti. Kwa kuona mwenendo wako, mimi niliamua kuanza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova.’”
Uingereza ilikuwa na kilele cha wahubiri wa Ufalme 107,767, kutia ndani ndugu huyu aliyebatizwa karibuni: “George sasa ana umri wa miaka 84. Baada ya miaka 50 akiwa mhubiri wa kawaida tu katika kanisa la kwao, yeye alipata maarifa ya kuujua ukweli. Hapo kwanza, alipokuwa amemaliza funzo lake la nyumbani la Biblia, alikuwa akifanya haraka kuingia ndani ya chumba kingine ili avute sigareti moja. Alikuwa amekuwa mvutaji wa kawaida kwa miaka 70. Lakini tangu alipojifunza sura ya 26 ya kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani, hajapata kamwe kuvuta sigareti tena. Sasa George amekuwa mtu aliyebatizwa kwa zaidi ya mwaka mmoja na ni mwenye bidii sana katika utumishi wa shambani, akieleza wengine juu ya baraka ambazo Yehova ataleta katika mfumo wake mpya wa mambo.”
Jamhuri ya Muungano wa Ujeremani inaripoti kilele cha wahubiri 118,645. Pia kuna makumi ya maelfu ya Mashahidi waaminifu ‘wanaoacha nuru yao iangaze’ katika Jamhuri ya Kidemokrasi iliyo jirani. Katika Ujeremani, pia, wazee wa kazi walio waaminifu wanakataa kuweka chini “upanga wa roho.” (Waefeso 6:16, 17, NW) Kundi moja linaripoti hivi: “Sisi tuna dada mmoja aliye karibu na umri wa miaka 103 na bado anaishi pekee yake. Wazee walipanga ili kikundi cha dada saba au nane hivi wawe wakipokezana zamu katika kumtunza kila juma. Wamekuwa wakifanya hivyo sasa kwa miaka mitatu au minne hivi iliyopita. Wafanya kazi wa mitaani, wanaolipwa na watu wenyewe, wanakuja kumwogesha na kumvalisha nguo. Lakini wanapokuwa wagonjwa au katika likizo, dada zetu wanaichukua kazi hiyo. Ushuhuda huo wa upendo na dhabihu ya Kikristo umetumikia kuwa ushahidi mzuri kwa watu wa nje. Dada yetu mwenye umri wa miaka 103 yuko chonjo kiakili na anawaona wafanya kazi wa mitaa kuwa ‘eneo’ lake. Yeye anawahubiria kwa bidii wanapomwogesha na anawapa vitabu.” Kwa kweli, “kuwa na kichwa chenye mvi ni taji ya uzuri wa sura wakati kinapopatikana katika njia ya uadilifu.”—Mithali 16:31, NW.
Ijapokuwa hivyo, mwaliko wa kumsifu Yehova unatolewa kwa watu wa umri wote—“ninyi wanaume vijana na pia ninyi wanawali, ninyi wanaume wazee pamoja na wavulana.” Vijana wengi ‘wanakumbuka Muumba Mtukufu wao katika siku za uanaume wao wa ujana.’ (Zaburi 148:12; Mhubiri 12:1, NW) Katika Brazili, ambako kulikuwa na kilele kipya cha kupendeza sana cha wahubiri 196,948, Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi ilipokea barua moja kutoka mji wa kando kando ambako ndugu wawili vijana walitoa ushahidi kwa miezi kadha. Barua hiyo ilisema hivi kwa sehemu: “Mimi ningependa kuwasifu ninyi kwa sababu ya vijana wazuri sana mlio nao katika dini yenu. Mimi ni mwalimu wa shule na ninashughulika na vijana, nami najua vijana wa siku hizi si kama wale wa zamani. Vijana wenu ni mfano kweli kweli. Wao wanaheshimu wazee wao, ni waungwana na wanavaa kwa kiasi. Nao wanazijua Biblia zao wee! Hiyo ni dini kweli kweli! Ni sikitiko kwamba wamelazimika kuondoka hapa.” Jamaa za ndugu zetu sasa zinahamia daima katika maeneo hayo yaliyo pekee yao ili kutunza wanaopendezwa.
Ukweli unafanya maendeleo gani katika maeneo yasiyo ya Kikristo? Jarida The Wall Street Journal la Julai 9, 1986, lilichapisha makala ndefu chini ya kichwa, “Udongo Tasa—Wamisionari Wakristo Wapanda Mbegu Katika Japani Waione Zikikua Sana.” Misionari mmoja wa United Church of Christ aliripotiwa kuwa akisema, “Hakuna njia ambayo Ukristo utakuja kamwe kutia mizizi katika Japani,” na padri wa kanisa la Francisca akaripotiwa kuwa akisema, “Siku za wamisionari wa kigeni katika Japani zimekwisha.” Wote wawili walikuwa wamefanya kazi ngumu bila matokeo kwa miaka zaidi ya 30. Makala hiyo ilisema: “Kiasi kinachopungua asilimia 1 ya idadi ya watu ni Wakristo, na ijapokuwa kazi yote ya wamisionari, asilimia hiyo inaendelea kupungua.” Dini za Jumuiya ya Wakristo zimetatizika kweli kweli! Lakini namna gani juu ya Mashahidi wa Yehova, wanaofundisha Ukristo ulio safi katika nchi hiyo? Kwa muda wa mfululizo wa miezi 92 iliyopita, wao wameongeza hesabu yao ya wahudumu watendaji, ikafikia kilele cha 113,062 (kutia ndani wastani wa “mapainia” wa wakati wote 46,390 kila mwezi) Yanaongozwa katika Japani mafunzo ya nyumbani ya Biblia 146,316 pamoja na watu walioanza kupendezwa majuzi. Hakika hiyo ni dalili ya kwamba kutakuwa na ongezeko kubwa zaidi. Hapa tunaona utimizo ulio hai wa Isaya 65:13, 14.
Shamba la Upainia
Namna gani kitovu cha utendaji wote huo wenye nguvu za msukumo mwingi—United States ya Amerika? Kule wahubiri wa Ufalme 744,919 walikuwa shambani hicho kikiwa kilele. Lakini je! hao ‘wamisionari wa nyumbani’ wanahitajiwa kweli kweli? Kwa kweli wanahitajiwa, maadamu uhalifu, dawa za kulevya, ukosefu wa adili, magonjwa, na ufisadi unaongezeka kwa kadiri iliyo mbaya sana kuliko katika nyingi za zinazoitwa nchi za kipagani. Watu wanaotamani mambo mazuri zaidi wanahitaji faraja na tumaini, na Mashahidi wa Yehova wana ujumbe kama huo. (Isaya 61:1, 2; Mathayo 24:14) Katika United States, wakati wa 1986, wahudumu hao walitumia saa 146,673,490 kutangaza habari njema za Ufalme. Hiyo ni jumla ya ongezeko la asilimia 12.6, au saa 16,449,229 zaidi ya mwaka uliopita. Wakati huo ulitumiwa kwa faida, maadamu vitabu 6,138,938 viligawanywa kwa watu, hayo yakiwa ni maendeleo ya asilimia 23.2 juu ya mwaka uliopita. Katika Aprili tu, jumla ilikuwa vitabu zaidi ya 1,000,000 vyenye kueleza tumaini la kweli la kupatia amani na usalama.
Moja la mambo yenye kusisimua zaidi juu ya ripoti ya United States ni mpanuko wa utumishi wa painia. Katika Aprili kulikuwa na kilele cha mapainia wa kawaida 45,786, hilo likiwa ni ongezeko la asilimia 23 juu ya mwaka uliopita. Unapounganisha tarakimu hiyo pamoja na wastani wa painia-wasaidizi 43,369 na wastani wa mapainia wa pekee 279, inamaanisha kwamba kila mwezi zaidi ya watu 90,000 walikuwa wakitangaza kote kote Ufalme wa Mungu katika kazi ya upainia. Hao ni vijana na watu wenye umri mkubwa, pia, wanaotumia kwa hekima wakati wao katika kumsifu Yehova.
Kutoa Ushuhuda Ulio Kamili Kabisa
Katika kufundisha peupe na nyumba kwa nyumba, mtume Paulo ‘alitoa ushuhuda kikamili’ kuhusu zile habari njema. (Matendo 20:20, 21 AW) Ushuhuda unaofanana na huo unaendelea kutolea katika maeneo mengi leo. Kwa mfano, ripoti hii inakuja kutoka Guadeloupe: “Kufikia mwisho wa mwaka wa utumishi sisi tulikuwa na mhubiri mmoja kwa watu 72. Hata bila kutaja, ni wazi kwamba tumejulikana sana katika sehemu zote za nchi! Kwa kweli, katika mahali pengi tunaingia eneo lile lile kila juma. Wengine wangeweza kusema kwamba kwa uhakika watu wamechoka kutuona, au kwamba inavunja moyo kuwa katika eneo lile lile moja juma baada ya juma. Lakini kinyume cha hivyo, kadiri ambavyo tunazidi kufanya kazi katika eneo, ndivyo kupendezwa kwingi zaidi kunavyoamshwa. Na kuna uthibitisho gani wa jambo hilo? Ni kile kilele kilichokuwako Aprili uliopita cha mafunzo ya nyumbani ya Biblia 7,136 yaliyoongozwa na wahubiri wetu 4,558! Hivi majuzi gazeti moja lilikuwa na kichwa: ‘Mashahidi wa Yehova—Wafalme Wenye Kwenda Mlango kwa Mlango’! Sisi tunahesabu hiyo kuwa ni heshima kwetu. Wakati wa mwaka wa utumishi ndugu na dada wapya 458 walibatizwa.” Uthabiti na furaha iliyoonyeshwa katika kufanya kazi katika eneo letu tena na tena, kupata kuwajua watu na kufanya urafiki nao, kuvunja-vunja kwa upendo maoni yasiyofaa waliyotangulia kujiwekea —jambo hilo linaweza kufanya tupate watu wengi wa mfano wa kondoo.
Yehova anabariki sana watumishi wake katika nchi moja ya Kiafrika ambamo kazi imepigwa marufuku na vita ya wenyewe kwa wenyewe inawaka moto. Katika nchi hiyo wengi wa ndugu zetu wanataabika magerezani, na mashahidi wengine vijana wameuawa. Hata hivyo, mwezi Aprili ulikuwa na ripoti ya kutokeza, ukiwa na vilele kumi visivyopata kuonekana tena. Tarakimu mpya ya wahubiri ni ongezeko la asilimia 29 juu ya mwaka uliopita. Ni bidii nyingi kama nini wanayodhihirisha ndugu hao wapendwa! Saa za wastani katika Aprili zilikuwa zaidi ya 18 kwa kila mhubiri na mafunzo ya nyumbani ya Biblia 2.6 kwa kila mhubiri.
Ujumbe wa siri uliopokewa na afisi ya tawi inayotunza eneo hilo unatosha kutokeza wazo fulani juu ya hali zilizoko. Unasema hivi: “Joto kali linaendelea kutupiga sana. Jitihada kubwa inayotakwa ndipo tu mtu aweze kwenda hapa na pale akaone mtu fulani ni uthibitisho wa kwamba tunapatwa na wimbi la joto kali. Lakini sisi tunajua tumefanywa kwa njia ya kuweza kujirekebisha tupatane na joto lo lote na mazingira yo yote. Tujapopatwa na mambo yote hayo tunavumilia na kuamini sana tutaokoka.” Ni ukamilifu mwingi kama nini!
Watu mmoja mmoja walio washika-ukamilifu ndio wanaokuwa tengenezo lenye kushika ukamilifu. Tengenezo la duniani pote la Mashahidi 3,229,022 ndivyo lilivyo hasa! Wao wanatazamia kuokoka ‘dhiki kubwa’ inayokuja na kushiriki chini ya Ufalme wa Kristo, katika ile kazi kubwa ya kugeuza dunia iwe paradiso. (Ufunuo 7:14; 21:3, 4; Isaya 65:21-23, 25) Wao wana shangwe juu ya jinsi Yehova anabariki hata sasa utendaji wao wa bidii, wawe wanalihubiri neno “katika majira yanayofaa” au “katika majira yenye taabu.” (2 Timotheo 4:2, NW) Kurasa zinazofuata zinaonyesha kwa picha jinsi wao wametii kichwa cha andiko lao la mwaka 1986: “Nendeni . . . mkautangaze kote kote Ufalme wa Mungu.”—Luka 9:60, NW.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 7]
Mambo Fulani ya Ripoti ya Duniani Pote ya Mashahidi wa Yehova
Ongezeko:
Kilele cha wahubiri: 3,229,022 6.83%
Wastani wa kila mwezi wa painia: 391,294 21.2%
Jumla ya saa zakuhubiri: 680,837,042 15.3%
Wastani wa mafunzo ya nyumbani
ya Biblia kila mwezi: 2,726,252 14.6%
Jumla ya hesabu yawaliobatizwa 1986: 225,868 19%
[Chati katika ukurasa wa 10-13]
RIPOTI YA MWAKA 1986 WA UTUMISHI YA MASHAHIDI WA YEHOVA ULIMWENGUNI POTE
(Ona buku lililojadiliwa)
[Picha katika ukurasa wa 8, 9]
KUTOA USHUHUDA “PEUPENA NYUMBA KWA NYUMBA” “KWENYE SEHEMU YA MBALIZAIDISANA YA DUNIA”
Mji wa Davao Ufilipino
Venice Italia
Castle Combe Uingereza
Gålå Norowei
Kowloon Hong Kong
Taipei Taiwan
Queenstown New Zealand
Bolgatanga Ghana
Paris Ufaransa
Quetzaltenango Guatemala
Kerala India
Banff Kanada