Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w85 8/1 kur. 22-27
  • Kufanya Kazi Pamoja na Mtengenezaji wa Ulimwengu Wote

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kufanya Kazi Pamoja na Mtengenezaji wa Ulimwengu Wote
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Maoni ya Hapo Mwanzo juu ya Tengenezo
  • Yerusalemu Aliye Katika Utumwa
  • Yerusalemu Aliye Huru
  • Fanya Kazi Pamoja na Mtengenezaji Mkuu
  • Agano la Mungu Pamoja na “Rafiki” Yake Tayari Lafaidi Mamilioni
    Usalama Ulimwenguni Pote Chini ya “Mwana-Mfalme wa Amani”
  • Yule Mwanamke Tasa Ashangilia
    Unabii wa Isaya II—Nuru kwa Wanadamu Wote
  • “Tukio la Mfano” Ambalo Ni Muhimu Kwetu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
w85 8/1 kur. 22-27

Kufanya Kazi Pamoja na Mtengenezaji wa Ulimwengu Wote

“Kwa maana sisi ni wafanya kazi wenzi wa Mungu. Ninyi watu ni shamba la Mungu linalolimwa, jengo la Mungu.”​—1 WAKORINTHO 3:9 Biblia ya New World Translation.

1. Ni usemi gani uliotumiwa miaka 60 iliyopita ulisisimua waliousikia, na ulikuwa na matokeo gani kwa Wanafunzi wa Biblia wa makini wa wakati huo?

“TENGENEZO LA MUNGU.” Zaidi ya miaka 60 iliyopita usemi huo ulitumiwa na mshiriki wa jamii ya kuhariri vitabu ya Sosaiti yetu wakati wa mazungumzo ya kila siku ya Biblia katika meza za chakula Betheli. Usemi huo ulisisimua jamaa ya makao makuu kama nini katika Brooklyn, New York! Usemi huo wa namna ya pekee, “tengenezo la Mungu,” ulitumika kuwa mwongozo wa fikira, usemi, na uandikaji wa siku za mbele wa Wanafunzi wa Biblia hao. Ulipanua maono yao ya kiroho juu ya uumbaji wote hata ukavuta sana mwelekeo wao juu ya Mtengenezaji wa ulimwengu wote, Yehova Mungu.

2. Kama linavyoonyeshwa na asili yalo ya Kigiriki, neno “tengenezo” laweza kufasiliwaje?

2 Kwa kuwa neno hilo “tengenezo” linatumiwa kwa ukawaida kati ya Mashahidi wa Yehova, wanaothamini pendeleo lao la kufanya kazi pamoja na Mtengenezaji wa ulimwengu wote, huenda hilo likaonekana kuwa jambo geni leo. (1 Wakorintho 3:5-9) Neno “tengenezo” (“organization” kwa Kiingereza) limetokana na neno la Kigiriki orʹga·non. Kati ya mambo mengine, linamaanisha chombo au kifaa cha kutimizia kazi. Linaonekana mara kadha katika Septuagint Version na linatumiwa kuhusu chombo cha muziki, kama vile kinubi cha Daudi. Shina la neno hilo ni er’gon, jina ambalo maana yake ni “kazi.” Basi tengenezo ni mpango wa mambo yaliyoanzishwa ili jambo fulani lifanywe au litimizwe kwa njia iliyo bora zaidi iwezekanayo na bila kupoteza wakati na nishati nyingi.

Maoni ya Hapo Mwanzo juu ya Tengenezo

3. Toleo la Machi 1883 la jarida hili (kwa Kiingereza) lilisema nini juu ya “tengenezo letu”?

3 Lakini, miaka iliyopita Wanafunzi wa Biblia walikuwa na ugumu fulani wa kutumia neno hili “tengenezo.” Kwa mfano, katika toleo la Machi 1883 la Mnara wa Mlinzi (la Kiingereza), ilisemwa hivi:

“Lakini, ijapo haiwezekani kwa mwanadamu wa asili kuona tengenezo letu, kwa sababu yeye hawezi kuyafahamu mambo ya Roho ya Mungu, sisi tunatumaini kwamba ninyi mnaweza kuona kwamba Kanisa la kweli limetengenezwa vya kufaa zaidi, na linafanya kazi kwa utaratibu ulio bora zaidi uwezekanao. . . . Sisi tunayo imani isiyo na mpaka katika Kapteni wetu; na tengenezo kamilifu hili, lisiloonekana kwa ulimwengu, linasonga mbele kuelekea ushindi hakika na wenye utukufu.”

4. Ni maoni gani juu ya kufanya tengenezo yaliyotolewa katika toleo la gazeti hili la Desemba 1,1894 (Kiingereza)?

4 Lakini, toleo la Desemba 1,1894 la Mnara wa Mlinzi lilisema hivi:

“Lakini kama vile kazi hiyo ya kutengeneza kanisa la usimamizi mpya wa Gospeli haikuwa sehemu ya kazi ya mavuno ya usimamizi wa kale wa Kiyahudi, ndivyo kazi ya sasa ya kuvuna ya usimamizi wa Gospeli pia ilivyo tofauti na ni mbali na ile kazi ya usimamizi mpya wa Mileani unaozidi kukaribia sasa. . . . Ni wazi kwamba kufanyizwa kwa tengenezo lionekanalo la wakusanywao hao kungekuwa kusikopatana na roho ya mpango wa kimungu; na kama lingefanyizwa ingeelekea kuonyesha kama kanisa linatamani kufuata wazo la sasa lenye kupendwa na watu wengi la tengenezo au muungano. (Ona Isa. 8:12) Sasa kazi hiyo si tengenezo, bali mgawanyiko, kama ilivyokuwa hasa katika mavuno ya Kiyahudi. (Mt. 10:34-36) . . .

“Kwa hiyo, ingawa sisi hatuoni tengenezo lionekanalo la wakusanywa kuwa sehemu ya mpango wa Bwana katika kazi ya mavuno, kana kwamba tulitarajia tengenezo liendelee kuwa hapa kwa kizazi kingine, sisi tunaona kuwa mapenzi yake kwamba imewapasa wale wanaompenda Bwana wasemezane mara nyingi juu ya matumaini na furaha, au majaribu na fadhaa walizo nazo shirika, huku wakizungumza pamoja mambo bora ya Neno lake.”

5. Kwa habari ya tengenezo, ni jambo gani lililosemwa katika kitabu The New Creation!

5 Hivyo wakati huo kundi la Kikristo halikuonwa kuwa tengenezo. Lakini ilifikiriwa vizuri kufanywe utaratibu wa kundi, au eklezia. Kwa mfano, Somo la 5 la kitabu The New Creation, kilichochapishwa mwaka wa 1904, lilikuwa na kichwa “Tengenezo la Uumbaji Mpya” na linaanza kwa kusema: “Kama vile Uumbaji Mpya hautafikia ukamilifu au utimilifu wake mpaka ufike Ufufuo wa Kwanza, ndivyo tengenezo lake halitatimilika mpaka wakati huo ufike. Mfano wa hekaluni unaonyesha hivi: kama mawe yaliyo hai sisi tunaitwa sasa, au tunaalikwa kwenye mahali palipo katika hekalu lenye utukufu.”

6. Kitabu Thy Kingdom Come kilitambulishaje “mama” ya washiriki wa “uumbaji mpya”?

6 Inapendeza kwamba kitabu Thy Kingdom Come, kilichochapishwa mwaka wa 1891, kilisema hivi juu ya wapakwa-mafuta hao wa “uumbaji mpya”: “Kwa habari ya andiko la Isaya 54:1-8, Mtume Paulo ametoa mwangaza juu ya hekima isiyo ya kibinadamu juu yake, na amelitumia kuhusu Sayuni wa kiroho, mama au agano letu, linalofananishwa na Sara. Ile mbegu ya kimwili ya Abrahamu ilikuwa imetupwa isiwe urithi wa ahadi, na mbegu ya kweli, Kristo (akifananishwa na Isaka na Rebeka), ilikuwa imepokewa kuwa ndiyo mbegu ya pekee ya ahadi.​—Gal. 4:22, 24, 26-31.”

7, 8. Ni nani aliye mume wa “mama” ya kundi la Kikristo, na Isaya 54:1-8 linasema nini juu ya habari hii?

7 Usemi huo haukuwa unahusu chama kinachoitwa Zionist World Organization, kilichoanzishwa na Theodor Herzl mwaka wa 1897. Tengenezo hilo lilishughulika na Yerusalemu wa chini, hapa duniani, halikushughulika na “Yerusalemu wa juu,” aliye “mama” ya kundi la Kikristo. (Wagalatia 4:26) Kitabu Thy Kingdom Come hakikuendelea kukuza uhakika wa kwamba mwenyewe aliye mume wa “mama” ya kundi la Kikristo ni Mungu, aliyefananishwa na Abrahamu. Yehova hakuoa agano la Kiabrahamu wala agano jipya, bali ameoa “Yerusalemu wa juu,” uliofananishwa na Sara, mama ya Isaka. Kama yeye, akiwa “mama,” “Yerusalemu wa juu” lazima uwe kitu fulani kilicho hai na kilicho na utu.

8 Basi, ni nani aliye “Yerusalemu wa juu”? Ili tuelewe, ebu tuangalie kwanza andiko la Isaya 54:1-8, NW, linalosomwa hivi kwa sehemu:

‘“Lia kwa furaha, ewe mwanamke tasa ambaye hakujifungua mtoto! Uwe mwenye kuchangamka kwa kilio chenye furaha na ulie kwa sauti nyembamba, ewe usiye na maumivu ya kuzaa mtoto, kwa maana wana wa mkiwa ni wengi zaidi ya wana wa mwanamke aliye na mwenyewe aliye mume,’ Yehova amesema. . . . ‘Kwa maana Mfanyi Mkuu wako ni mwenyewe aliye mume wako, Yehova wa majeshi likiwa jina lake; na Aliye Mtakatifu wa Israeli ni Mnunua-upya wako. Mungu wa dunia nzima ndivyo atakavyoitwa. Kwa maana Yehova alikuita wewe kana kwamba ulikuwa mke aliyeachwa kabisa na aliyeumizwa rohoni, na kama mke wa wakati wa ujana ambaye ndipo akakataliwa,’ Mungu wako amesema. ‘Kwa maana kwa kitambo kidogo nilikuacha kabisa, lakini kwa rehema zilizo kubwa nitakukusanya pamoja. Kwa mfuriko wa ghadhabu nilificha uso wangu kutoka kwako kwa kitambo tu, lakini kwa fadhili za upendo nitakuonyesha rehema kwa wakati usiojulikana,’ Mnunua-upya wako, Yehova, amesema.”

9. (a) Yehova alikuwa akimwambia nani kwa kufariji katika Isaya 54:1-8? (b) Kulingana na Wagalatia 4:25, 26, ni nani aliye “mwanamke” anayetajwa katika hali ya kufananishwa?

9 Kwa mara ya kwanza katika andiko hilo, Yehova hakuwa akisema na agano. Alikuwa akisema na taifa, watu wake waliochaguliwa katika agano la Torati ya Musa alilofanya pamoja nao. Kwa maoni ya Mungu, taifa hilo lilijumuika likawa “mwanamke” aliyekuwa kama mke kwake. Kulingana na barua ya mtume Paulo kwa Wagalatia, “mwanamke” huyo alikuwa mfano, lakini hasemi kwamba yeye ni agano, au mapatano. Agano halingeweza kufarijiwa, kutulizwa. Badala yake, Paulo anaonyesha kwamba “mwanamke” huyo aliyefananishwa ni kitu fulani kilicho hai, kama “mama,” kama vile Yehova, “mwenyewe aliye mume” alivyo hai akiwa Mtu aliye na akili na uwezo wa kutoa faraja. Akisema juu ya wanawake wa historia ya kale, mtume aliandika hivi: “Sasa Hagari huyo [yaya aliyekuwa badala ya Sara, mamsahibu wake katika kumzalia Abrahamu Ishmaeli] anamaanisha Sinai, mlima ulio katika Arebia, naye [Hagari] analingana na Yerusalemu wa leo [wakati Paulo alipokuwa duniani], kwa maana yeye yuko katika utumwa [wa agano la Torati ya Musa] pamoja na watoto wake. Lakini Yerusalemu wa juu yuko huru, naye ni mama yetu.”​—Wagalatia 4:25, 26, NW.

Yerusalemu Aliye Katika Utumwa

10, 11. (a) Ni jambo gani lenye maana kubwa linalohusu Waisraeli lililotukia kwenye Mlima Sinai? (b) Kwa habari ya agano la Torati, ni jambo gani lililotukia mwaka wa 33 W.K.?

10 Hagari hafananishi, wala kuwakilisha agano la Torati ya Musa. Wala agano hilo pamoja na Amri Kumi zalo halifananishi Mlima Sinai, ambao Hagari analingana nao. Bila shaka, Mungu hakufanya agano lo lote pamoja na Mlima Sinai. Lakini ni huko alikopeleka Waisraeli, aliokuwa ameweka kuwa huru kutoka utumwa wa Kimisri, akawaingiza katika uhusiano wa agano pamoja na yeye mwenyewe, akashughulika nao wakiwa taifa huru. Jambo hilo lilitukia karne nyingi Mungu alipokuwa amekwisha kufanya agano la upande mmoja pamoja na Abrahamu, akimwahidi mbegu (uzao) ya kiume.

11 Musa, aliyekuwa mpatanishi wa agano la Torati aliposhuka kutoka Mlima Sinai, uso wake ulikuwa na mwangaza usio wa kibinadamu, uliokuwa mwingi sana hivi kwamba ilimpasa aufunike ndipo Waisraeli waweze kumtazama. (2 Wakorintho 3:12-16) Lakini akiwa juu katika Mlima Sinai, Musa hakumwona Yehova moja kwa moja, kwa maana Mungu aliingia katika agano pamoja na Waisraeli kupitia malaika. (Matendo 7:37, 38; Waebrania 2:2) Kwa njia hiyo taifa la Israeli likawa chini ya agano la Torati. Lakini, karne zilizofuata, agano hilo liliondolewa, kwa kupigiliwa misumari kwenye mti wa mateso wa Yesu mwaka wa 33 W.K.​—Wakolosai 2:13, 14.

12. (a) Yerusalemu wa kidunia ulikuwa “mama” ya akina nani? (b) Yerusalemu wa hapa duniani ulikuwa chini ya utumwa gani karne 19 zilizopita, na kwa nini haukupata kamwe kuwa huru?

12 Paulo aliandika kwamba Mlima Sinai ulilingana na Yerusalemu wa chini wa wakati wake. Bila shaka, Yerusalemu haukuwa agano; ulikuwa mji wenye maana uliokaliwa na wakazi wa Kiyahudi. Ukiwa mji mkuu, ulisimamia taifa hilo na ulikuwa “mama” ya mfano ya “watoto,” yaani, ya washiriki wote wa taifa la Kiyahudi, au la Kiisraeli. (Mathayo 23:37) Hekalu la Yehova, Mungu yule ambaye Waisraeli walikuwa katika uhusiano wa agano pamoja naye, lilisimama katika Yerusalemu. Lakini wakati huo Wayahudi hawakuwa na ufalme wao wenyewe ulio pekee, wenye kutawalwa na mzao wa Mfalme Daudi. Kwa sababu hiyo, hawakuwa huru bali walikuwa katika utumwa chini ya mamlaka za kisiasa za Mataifa. Zaidi sana, walikuwa katika utumwa wa kidini. Ni Masihi aliyeahidiwa, Yesu Kristo tu, ndiye angeweza kuwaweka huru watoke katika utumwa huo, na pia katika utumwa wa dhambi. Lakini Yerusalemu huo haukumkubali Yesu kuwa Masihi na Mfalme na haukupata kuwa huru kamwe kamwe. Badala ya kuwa huru, uliangamizwa na Waroma mwaka wa 70 W.K., na “watoto” wake wakapatwa na msiba.

Yerusalemu Aliye Huru

13. Paulo alisema nini juu ya Yerusalemu ulio huru, na “watoto” wake wamepaswa wasimame imara wakiwa na uhuru gani?

13 Paulo alitofautisha Yerusalemu wa kidunia aliye katika utumwa na “Yerusalemu wa juu,” aliye “huru.” Akinakili maneno ya Isaya 54:1-8, aliandika hivi:

“Lakini Yerusalemu wa juu yuko huru, naye ni mama yetu. Kwa maana imeandikwa: ‘Furahi, ewe mwanamke aliye tasa ambaye hajifungui mtoto; paaza sauti na kulia kwa sauti kuu, ewe mwanamke usiye na maumivu ya kuzaa mtoto; kwa maana watoto wa mwanamke mkiwa ni wengi zaidi ya wale wa yeye asiye na mume.’ Sasa sisi, akina ndugu, tu watoto walio wa ahadi sawasawa na alivyokuwa Isaka. Lakini kama vile wakati ule yeye aliyezaliwa kwa jinsi ya mwili alivyoanza kumtesa yeye aliyezaliwa kwa jinsi ya roho, ndivyo ilivyo na sasa. Hata hivyo, Andiko lasema nini? ‘Fukuza msichana-mtumishi na mwanaye, kwa maana kamwe kamwe mwana wa msichana-mtumishi hatakuwa mrithi pamoja na mwana wa mwanamke aliye huru.’ Kwa sababu hiyo, akina ndugu, sisi ni watoto, si wa msichana-mtumishi, bali wa mwanamke aliye huru. Kwa uhuru huo Kristo alituweka huru. Kwa hiyo simameni imara, na msijiache wenyewe mfungwe tena katika kongwa la utumwa.”​—Wagalatia 4:26—5:1, NW.

14. Kwa nini uzawa wa Isaka ulikuwa “kwa jinsi ya roho”?

14 Kwa njia hiyo Wakristo wa kule Galatia waliotajwa walikuwa “watoto wa Mungu kwa matokeo ya ahadi yake.” (Wagalatia 4:28, Today’s English Version) Ili kufananisha jambo hilo, Isaka alizaliwa kwa Abrahamu mwenye miaka 100 na Sara mke wake mwenye miaka 90 ili kutimiza ahadi ya Yehova aliyopewa mzee huyo wa ukoo aliye mwaminifu. Ndiyo, uzawa wa Isaka kwa Abrahamu ulikuwa wa kimuujiza, hakuzaliwa kabisa “kwa jinsi ya mwili.” (Mwanzo 18:11-15) Hivyo ulipasa uwe uzawa “kwa jinsi ya roho.” Ndiyo, roho ya Abrahamu Mkubwa Zaidi, Yehova Mungu, ilihitajiwa bila shaka ifufue nguvu za uzazi za Sara, mwanamke aliye huru, na vilevile zile za Abrahamu. (Warumi 4:19) Inafaa kuangaliwa kwamba “ahadi” yenyewe haikuwa ya kale wakati Isaka alipozaliwa mwaka wa 1918 K.W.K., kwani hiyo ilikuwa miaka 25 tu baada ya kuingia kwa Abrahamu katika nchi ya ahadi ya Kanaani mwaka wa 1943 K.W.K., wakati “ahadi” ilipoanza kutenda kazi.

15. “Yerusalemu wa juu” ulikaa bila watoto kwa muda gani, na watoto wake walianza kuwa wengi wakati gani?

15 “Yerusalemu wa juu” ulikuwa “mkiwa,” kana kwamba bila watoto. Na hali hiyo ya bila watoto ilikuwa ya muda mrefu sana kuliko ile ya Sara. Kwa kweli, “Yerusalemu wa juu” ulikuwa katika hali hiyo tangu mwaka wa 1943 K.W.K., wakati ahadi aliyopewa Abrahamu ilipoanza kutenda kazi, mpaka Yesu alipobatizwa mwaka wa 29 W.K. Ni wakati huo Yesu alipozaliwa kwa roho ya yule Abrahamu Mkubwa Zaidi, Yehova, na kupakwa mafuta kwa roho Yake awe ndiye Kristo au Mpakwa-mafuta, yule Masihi. Lakini “Yerusalemu wa juu” ulitakwa uwe na zaidi ya mtoto mmoja wa kiroho. Basi siku ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K., baada ya kufufuliwa kwa Yesu na kupanda kwenda mbinguni, watu kama 120 hivi wa wanafunzi wake waaminifu walizaliwa kwa roho ya Abrahamu Mkubwa Zaidi. Ndipo wakapakwa mafuta kwa roho hiyo wawe ndugu za kiroho za Isaka Mkubwa Zaidi, Yesu Kristo. Baadaye siku hiyo Wayahudi zaidi kama 3,000 wakabatizwa wawe wanafunzi wa Yesu na kupakwa mafuta kwa roho takatifu. (Matendo 2:1-42) Hivyo siku hiyo “Yerusalemu wa juu” ukawa “mama” ya watoto wengi.

16. “Yerusalemu wa juu” ni nini?

16 Mtume Paulo anafunua kwamba yule mwanamke anayetajwa katika Isaya 54:1-8 ndiye “Yerusalemu wa juu.” Yehova Mungu ndiye “mwenyewe aliye mume” wake, pia Mfanyi Mkuu wake. Kwa jinsi ya mfano, yeye ni “mwanamke” wake, “mke” wake, au tengenezo lililo mfano wa mke katika mbingu juu. Kama mume, yeye Ndiye anayemfanya kuwa mwenye kuzaa ili atokeze ule “uzao” ulioahidiwa wakati wa Abrahamu.​—Wagalatia 3:16, 26-29.

17. “Yerusalemu wa juu” ulipataje kuwa “mama” ya “uzao” wa kwanza wa Abrahamu Mkubwa Zaidi?

17 Mwana-mzaliwa-pekee wa Mungu alikuwa ametoka katika tengenezo la mbinguni la Yehova lililo mfano wa mke ili awe “uzao” wa kwanza wa Abrahamu Mkubwa Zaidi. Kwa njia hiyo tengenezo hilo likawa kama ‘‘mama” ya Mwana wa Mungu. Yesu Kristo hakuwa mwana wa mfano wa Yerusalemu wa kidunia wa siku zake akiwa hapa duniani, kwa maana wakati huo mji huo ulikuwa katika utumwa pamoja na “watoto” wake, na Yesu hakupata kamwe kufanywa mtumwa. (Wagalatia 4:25) Yerusalemu wa kidunia ulikuwa ndiye “mama” ya Wayahudi hao wa asili hawakumkataa tu Yesu Kristo kuwa “uzao” ulioahidiwa wa mzee wa ukoo Abrahamu, bali pia kuwa wa Abrahamu Mkubwa Zaidi, Yehova Mungu.​—Mathayo 23:37-39.

Fanya Kazi Pamoja na Mtengenezaji Mkuu

18. Kwa nini Yerusalemu wa kidunia ukawa wenye kuvuta fikira za watu katika siku za Mfalme Sulemani?

18 Yesu Kristo ambaye “mama” yake akawa ni tengenezo la kimbingu la Mungu, alikuwa mkubwa zaidi na mwenye hekima zaidi ya Mfalme Sulemani, yule mwana mwenye sifa sana wa Daudi na aliyekuwa mtawala katika Yerusalemu wa kale wa kidunia. Utukufu na hekima ya Sulemani bila shaka ilivuta fikira za mataifa yasiyo ya Kiisraeli, kama Yesu alivyoonyesha kwa kusema: “Malkia wa kusini atasimama siku ya hukumu pamoja na watu wa kizazi hiki, naye atawahukumu kuwa wamekosa; kwa sababu yeye alikuja kutoka pande za mwisho wa dunia ili asikie hekima ya Sulemani, na hapa yupo aliye mkuu kuliko Sulemani.” (Mathayo 12:42; Luka 11:31) Kwa sehemu, Sulemani alionyesha hekima yenye kutokeza kwa jinsi alivyopanga mambo ya usimamizi wake. Jinsi alivyokuwa ametengenezesha kila jambo kwa hekima ilistaajabisha.

19. Kulikuwako jambo gani juu ya utawala wa Mfalme Sulemani lililostaajabisha malkia wa Sheba?

19 Kwa hiyo, katika 1 Wafalme 10:4, 5 tunasoma hivi: “Malkia wa Sheba alipopata kuona hekima yote ya Sulemani na nyumba aliyokuwa amejenga, na chakula cha meza yake na kikao cha watumishi wake na utumishi wa mezani wa watumishi wake wa mezani na mavazi yao na vinywaji vyao na dhabihu za kuteketezwa zake alizotoa kwa ukawaida katika nyumba ya Yehova, ndipo akawa hana roho tena ndani yake.” (NW; Rotherham; Young; Revised Standard; Septuagint. Ona pia 2 Mambo ya Nyakati 9:4.) Malkia wa Sheba alikuwa na sababu ya kuvutiwa na mpango wa jamii ya watumishi wa Sulemani. Na kwa kupangisha mambo vizuri na kwa utaratibu mzuri, alipatana na Mungu wa Utaratibu.​—1 Wakorintho 14:33.

20. (a) Yehova alimpa Sulemani nini kwa kujibu sala yake? (b) Akiwa “aliye mkuu kuliko Sulemani,” Yesu Kristo anafanya nini, na ni mwendo gani wa kuchukuliwa na wafuasi wake?

20 Kulingana na sala ya unyenyekevu ya Sulemani, Yehova alimpa “moyo wa hekima na wa ufahamu.” (1 Wafalme 3:5-14, NW) Mtengenezaji Mkuu wa ulimwengu wote alimpa Sulemani uwezo wa kutengeneza mambo kwa ajili ya utaratibu mzuri na uhodari wa kazi. Kwa sababu hiyo, ukawa ni wajibu wa mfalme wa watu wa Yehova wa agano kufanya kazi pamoja na Mtengenezaji wa kimungu wa vitu vyote vilivyoumbwa mbinguni na duniani. Kwa kulinganishwa, Yesu Kristo aliyetukuzwa, “aliye mkuu kuliko Sulemani,” anafanya hivyo kwa hekima. Kwa hiyo, wafuasi wake waaminifu duniani pia wanahitaji kufanya hivyo, nao wafanya.

Wewe Wasemaje?

◻ Ungefasilije neno “tengenezo”?

◻ Yerusalemu wa kidunia ulikuwa “mama” ya nani, na haukuwa kamwe umewekwa huru kutoka utumwa gani?

◻ “Yerusalemu wa juu” ni nini, na “watoto” wake ni nani?

◻ Sulemani alitumiaje hekima yake aliyopewa na Mungu, na ni jambo gani linalofanywa na Sulemani Mkubwa Zaidi na wafuasi Wake?

[Picha katika ukurasa wa 24]

Yerusalemu wa kidunia ulikuwaje katika utumwa?

[Picha katika ukurasa wa 26]

Malkia wa Sheba alistaajabu alipomtembelea Sulemani. Sulemani alifanya kazi pamoja na Mtengenezaji wa ulimwengu wote. Je! wewe pia unafanya kazi pamoja na Yehova Mungu?

(Makala ya Funzo la Kitabu)

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki