Karibu Kwenye “Washika Ukamilifu” Kusanyiko la 1985
MASHAHIDI WA YEHOVA wanajulikana sana si kwa ajili ya huduma yao ya bidii ya nyumba kwa nyumba peke yake bali pia kwa ajili ya makusanyiko yao makubwa ya Kikristo. Yametangazwa kwa miaka zaidi ya mia moja sasa, kurudi nyuma mpaka mwaka wa 1879. Kuna kielelezo kizuri cha Kimaandiko kwa makusanyiko haya.
Mara tatu kila mwaka Waisraeli walitakwa wakusanyike kwa ajili ya sikukuu zao. Yehova aliziona hizo kuwa za maana sana hata kwa kurudia-rudia akamwambia Musa azikazie katika Pentateuki. Ona Kutoka 23:14-17; 34:22-24; Mambo ya Walawi 23:4-22; Hesabu 28:16—29:12; Kumbukumbu la Torati 16:1-16. Pia tunasoma kwamba wazazi wa Yesu walienda kwa ukawaida Yerusalemu kwa ajili ya sikukuu ya Kupitwa (Pasaka).—Luka 2:41,42.
Kwa miaka 38 sasa, makusanyiko ya Mashahidi wa Yehova yamekuwa yakifuata kielelezo kinachofanana na kile katika Israeli wa kale. Mara mbili kila mwaka tunafurahia kuja pamoja kwenye makusanyiko ya mizunguko yetu, yanayoleta pamoja makundi 8 kufikia 20. Halafu tunatazamia kwa shauku kukusanyika mara moja kila mwaka kwa makusanyiko ya wilaya, ya taifa, au ya mataifa yote. Je! tunafurahia mikusanyiko hiyo kwa kadiri kubwa kama tupaswavyo? Si ndugu zetu wote duniani pote walio na baraka hiyo. Kwa sababu hiyo ripoti ya karibuni kutoka nchi moja ya Balka ambako kazi imekuwa chini ya vizuizi kwa muda mrefu inatuambia kwamba “kwa mara ya kwanza tuliweza kuwa na kusanyiko la wilaya katika jumba la watu wote . . . Akina ndugu walifurahi sana kwa ajili ya hilo.”
Walikuwa na sababu ya kufurahi, kwa maana inaelekea kwamba kadiri hesabu kubwa zaidi ya Mashahidi inavyokusanyika ndivyo furaha inavyokuwa nyingi zaidi. Nchi moja iliripoti mwaka wa 1983 kwamba kusanyiko la ‘Umoja wa Ufalme’ katika Desemba kweli kweli lilikuwa jambo la kutokeza sana mwakani,” na nyingine ililieleza kuwa “jambo la kusisimua zaidi mwakani.” Haishangazi kwamba wengi wa Mashahidi wa Yehova wanafanya mipango, mara nyingi kwa kujinyima sana, ili wahudhurie makusanyiko ya wilaya siku zote tatu na nusu.
Mwaka uliopita tulipendelewa kuhudhuria makusanyiko ya “Ongezeko la Ufalme.” Programu ilieleza jinsi kichwa hicho kilivyofaa kwa sababu ya maongezeko makubwa ya wahubiri wa Ufalme ulimwenguni pote. Na zaidi, ilikazia madaraka ya kila Shahidi mmoja mmoja kuhusiana na ongezeko hilo. Na tulipokea vyombo vizuri kama nini kwa ajili ya huduma yetu—Chapa Yenye Marejezo ya New World Translation of the Holy Scriptures, kifaa cha Biblia Survival Into a New Earth (Kuokolewa Kuingia Katika Dunia Mpya), na broshua Jina la Mungu Litakaloendelea Milele’. Mwaka huu tumetayarishiwa uandalizi mwingine! Tunafurahi kukusanyika kwenye “Washika Ukamilifu” kusanyiko. Kichwa hicho kinaelekeza fikira kwenye umaana wa kushiriki kwetu katika kuondolea lawama jina la Yehova kwa kushika ukamilifu mpaka mwisho wa mfumo wa Shetani.
Kichwa hicho ni chenye maana kama nini! Kimefungamanishwa na suala lenye maana zaidi linalokabili viumbe wote wenye akili, yaani, haki ya enzi kuu ya Yehova, yenye kutegemezwa na viumbe wanaoshika ukamilifu wao yajapokuwa yote ambayo Shetani Ibilisi anaweza kufanya. Si rahisi kuwa mshika ukamilifu katika hizi “nyakati za hatari.” (2 Timotheo 3:1-5) Hicho ni kinyume kabisa cha kufuata njia isiyo na magumu sana. Maana yake ni ‘kupitia mlango mwembamba na kutembea kwenye njia iliyosonga inayoongoza kwenye uzima.’—Mathayo7:13, 14.
Kushika ukamilifu kama wahudumu wa Yehova Mungu kunatia ndani matakwa mawili ya msingi. Kwenye upande mmoja kuna uhitaji wa kuzaa matunda ya roho ili ‘tupambe mafundisho ya Mwokozi wetu, Mungu, katika mambo yote.’ (Tito 2:10, NW) Kwenye upande mwingine tuna mgawo wa kuhubiri na kufanya wanafunzi, tunaposhiriki kutimiza unabii wa Biblia.—Mathayo 24:14; 28:19, 20.
Ili kutimiza matakwa hayo mawili, tunahitaji kuendelea kuutafuta Ufalme kwanza na haki ya Mungu. Ni lazima tupigane dhidi ya hila zote za Shetani Ibilisi, vishawishi vyote ambavyo ulimwengu huu wa kale unaweka mbele yetu kwa namna ya kupenda mali na anasa, na ni lazima tufanye kama alivyofanya Paulo, ‘kupiga-piga miili yetu na kuiongoza kama watumwa.’ (1 Wakorintho 9:27, NW; 1 Petro5:8; 1 Yohana 2:15-17) Kufanikiwa kushinda vitisho vinavyouelekea ukamilifu wetu si jambo rahisi.
Tukithamini kikamili pambano la kushika ukamilifu wetu, tutakuja kwenye kusanyiko ‘tukiwa tunatambua uhitaji wetu wa kiroho.’ (Mathayo 5:3, NW) Tutakaza fikira sana kwa yale yanayosemwa kwenye jukwaa, tuandike mambo makuu, tushiriki kwa moyo katika kuimba, na kujipatanisha na sala zinazotolewa. Pia, tutasikiliza kwa uangalifu mashauri yatakayotolewa juu ya kushika ukamilifu wetu kwa Yehova Mungu, kwa wenzi wetu wa ndoa, na kwa Wakristo wenzetu. Kwa hotuba, mahoji, mawonyesho, na michezo ya kuigiza tutatiwa moyo na kutayarishwa tuazimie zaidi ya wakati mwingine wo wote kushika ukamilifu mpaka mwisho wa huu mfumo wa mambo wa kale ulio mbovu.
Pia hatungependa kusahau uhakika wa kwamba mikusanyiko yetu mikubwa inatoa ushuhuda kwa ulimwengu. Januari uliopita “Ongezeko la Ufalme” kusanyiko lilifanywa kwenye Uwanja wa River Plate, Buenos Aires, Argentina, kwa siku nne. Lilitokeza taarifa kubwa-kubwa za habari! Kichapo cha habari cha mahali hapo Ahora kilitoa ripoti yenye picha za rangi nzuri kuhusu kusanyiko hilo, yenye kichwa kikubwa, “Imani Yajaa Viwanja.”
Chini ya kichwa kikubwa, “Ufalme Unaokua—Ule wa Mashahidi wa Yehova,” makala yenye kurasa mbili kwa sehemu ilisema: “Ni ajabu kweli. Kuona ndiko kuamini. Imani inasogeza milima. Lazima iwe ilikuwa ni imani iliyosukuma wastani wa watu 42,000 wakiwa kimya na wenye utaratibu wa kuvutia wajaze viti vya mpira vya Uwanja River Plate wakati wa siku nne za kiangazi kikali kilichopita. Lazima iwe ni imani, pia, iliyowezesha kukusanya waamini wasiopungua 46,000 bila ubaguzi wa jinsia, umri, utamaduni, rangi, au taifa wakati wa siku ya mwisho ya kusanyiko la wilaya la Mashahidi wa Yehova. . . . Tuwe tunashiriki mawazo na mafundisho yao au la, umati wote huo unastahili heshima yetu kubwa. Wanajionyesha kuwa wanyenyekevu, wasiosumbuliwa na mambo madogo ya maisha ya kila siku na ulimwengu wa kisasa ambao sisi ni sehemu; wana fundisho la amani na upendo kati ya ndugu.”
Makala hiyo iliendelea kusema: “Namna gani tengenezo lao? Mambo yote yalikuwa makamilifu. Mapolisi waliopelekwa hapo walikosa la kufanya . . . hakukuwako hata kisa kidogo, uchokozi, wala mvurugo uliotokea katika siku hizo nne. . . . Tunaachwa na amani nyingi ambayo Mashahidi wanaonekana kuwa nayo . . . Liwe ni kosa au la, tumewaheshimu. Ni nini kinawatendesha? Imani ile Imani ile inayosogeza milima.”
Hakuna shaka kwamba, kwa sisi kujiongoza kama wahudumu Wakristo wa Yehova Mungu, tunaweza kutoa ushahidi mzuri kwa watu wa nje. Ni kweli, kuwa Mkristo hakujapata kamwe kuwa rahisi. Yesu alisema ilimaanisha kubeba mti wa mateso. Kutendea ifaavyo kusanyiko letu la “Washika Ukamilifu” kutatusaidia tuwe wafuasi hodari wa Yesu Kristo.—Mathayo 16:24.