Kujitegemeza na Utimizo wa Maneno ya Yehova
(Makala ya Funzo la Kitabu)
“Mtu hataishi kwa mkate tu, ila kwa kila neno litokalo katika kinywa cha Mungu.”—MATHAYO 4:4.
1. Ni kwa jinsi gani Yehova ndiye Mwandalizi Mkuu wa Chakula, lakini Yesu alisema nini juu ya mahitaji ya mwanadamu?
YEHOVA ndiye Mwandalizi Mkuu wa Chakula. Alijionyesha kuwa hivyo kwa mwanadamu katika sura ya kwanza kabisa ya Biblia. (Mwanzo 1:29, 30) Muda mrefu baadaye, mtunga zaburi Daudi alimwambia Yehova kwa shukrani hivi: “Macho ya watu wote yakuelekea Wewe. nawe huwapa chakula chao wakati wake. Waufumbua mkono wako, wakishibisha kila kilicho hai matakwa yake.” (Zaburi 145:15, 16) Ndiyo, Yehova ametoa chakula tele kwa wanadamu na wanyama pia. Hata hivyo kuna tofauti. Ingawa wanyama wanahitaji chakula halisi peke yake, Yesu alionyesha kwamba mwanadamu anahitaji zaidi ya chakula cha kimwili. Ni lazima pia ‘aishi kwa kila neno litokalo katika kinywa cha Yehova. ‘—Mathayo 4:4, NW.
2. Tunapaswa kujua nini juu ya maana ya maneno ya Yesu katika Mathayo 4:4?
2 Yesu alisema jambo hilo katika kumjibu Shetani. aliyekuwa amejaribu kumshawishi Yeye ageuze kimuujiza mawe yawe mkate. Ibilisi hakusisitiza jambo hilo lakini upesi akaenda kwenye kishawishi kingine. Tukiamua kulingana na jinsi Shetani alivyotumia Zaburi 91:11, 12 kwa njia yenye kosa, labda hata hakuelewa Yesu alimaanisha nini katika kujibu kishawishi cha kwanza. (Mathayo 4:3-7) Lakini sisi watumishi wa Yehova tunapendezwa sana na aliyosema Yesu. Sisi tunaofurahia kuchimba kwa kina kirefu ndani ya Biblia ili tupate faida kamili ya kiroho tunaweza kuuliza hivi: Je! Yesu alimaanisha kwamba ili kuwa na maisha kamili, ni lazima mtu ajifunze na labda akariri ‘kila neno litokalo katika kinywa cha Yehova’? Au alimaanisha nini?
Maneno ya Yehova
3, 4. Maneno ya Kigiriki na Kiebrania yanayotafsiriwa kuwa “neno” yana maana gani mbili? Toa mfano.
3 Akimkanusha Shetani, Yesu alitaja andiko la Kumbukumbu la Torati 8:3 kulingana na tafsiri ya Septuagint ya Kigiriki ya andiko hilo la Kiebrania. Neno la Kigiriki linalotafsiriwa kuwa “neno” (rheʹma) lina maana mbili. Mara nyingine linatafsiriwa kuwa “neno,” “usemi,” au “tamko.” Lakini, kama lile la Kiebrania linalolingana nalo (da·varʹ). linaweza pia kumaanisha “jambo.”
4 Katika Luka 1:37 (Biblia ya New World) tunasoma hivi: “Kwa Mungu hakuna mtajo [rhe’ma] utakaokuwa usiowezekana.” Andiko la Luka 2:15 linasema: “Wachungaji wakaanza kusemezana: ‘Acheni kwa vyo vyote twende moja kwa moja mpaka Bethlehemu tukaone jambo [rhe’ma] hili ambalo limetukia, ambalo Yehova ametujulisha.’” (NW) Kwa hiyo, hasa linapotumiwa kukamatana na Yehova, neno hilo la Kigiriki linaweza kumaanisha “neno.” “mtajo,” au “tamko” la Mungu. Au linaweza kumaanisha “jambo.” iwe linamaanisha “tukio” au “tendo” linalosimuliwa, matokeo ya yaliyosemwa, kutimizwa kwa neno hilo.
5. Ni nini maana ya Luka 1:37?
5 Tukiwa tumeelewa hivyo, andiko la Luka 1:37 halimaanishi kwamba Mungu anaweza kusema lo lote tu. Binadamu anaweza kusema hivyo, hata ikiwa aliyosema hayaelekei kutimia au hayana maana. Lakini kwa habari ya maneno ya Mungu, maana ya andiko la Luka 1:37 ni kwamba hakuna neno wala mtajo wo wote wa Yehova unaoweza kukosa kutimizwa. Basi ilikuwa lazima mtajo ambao malaika alikuwa amemtolea Mariamu utimie. Wazo linalotolewa na maneno ya Kiebrania na Kigiriki yanayotumiwa kusema “neno,” “tamko,” au “mtajo” wa Yehova linaelezwa kwa njia nzuri katika kitabu cha Isaya. Yehova anasema: “Maana kama vile mvua ishukavyo, na theluji, kutoka mbinguni, wala hairudi huko; bali huinywesha ardhi, na kuizalisha na kuichipuza, ikampa mtu apandaye mbegu, na mtu alaye chakula; ndivyo litakavyokuwa neno [Kiebrania, da·varʹ; Kigiriki rhe’ma] langu, litokalo katika kinywa changu; halitanirudia bure, bali litatimiza mapenzi yangu, nalo litafanikiwa katika mambo yale niliyolituma.”—Isaya 55:10, 11.
“Mtu Hataishi kwa Mkate Tu”
6, 7. Habari ya kihistoria na kijiografia yenye kuhusu Kumbukumbu la Torati 8:2, 3 ilikuwa nini?
6 Sasa, tukirudia jambo lenyewe, Yesu alimaanisha nini wakati, akitumia maneno ya Kumbukumbu la Torati 8:3, alisema kwamba “mtu hataishi kwa mkate tu, ila kwa kila neno litokalo katika kinywa cha [Yehova]”? (Mathayo 4:4) Je! alikuwa akisema kwamba mtu mwenye utawa analishwa na matamko, maneno, au mitajo tu? Je! maarifa ya kichwani juu ya semi hizo za kimungu yangetosha? Ebu tuchunguze habari za kihistoria zenye kuzunguka maneno hayo ya Yesu yaliyotajwa kutoka la Torati.
7 Kifaa cha funzo la Biblia “All Scripture Is Inspired of God and Beneficial”a kinatuarifu hivi, kwenye ukurasa 36: “Kitabu cha Kumbukumbu la Torati kina ujumbe wenye nguvu kwa watu wa Yehova. Baada ya kutanga-tanga jangwani kwa miaka arobaini, wana wa Israeli sasa walisimama kwenye mlango wa Nchi ya Ahadi.” Ulikuwa mwaka wa 1473 K.W.K. Mahali penyewe palikuwa wapi? Nyanda za Moabu. Katika hotuba yake ya pili kwa Waisraeli waliokusanyika, Musa alitangaza hivi: “Nawe utaikumbuka njia ile yote [Yehova], Mungu wako, aliyokuongoza miaka hii arobaini katika jangwa, ili akutweze, kukujaribu, kuyajua yaliyo moyoni mwako, kwamba utashika amri zake, au sivyo. Akakutweza. [akakunyenyekeza, NW] akakuacha uone njaa, akakulisha kwa mana, usiyoijua wewe wala baba zako hawakuijua; apate kukujulisha ya kuwa mwanadamu haishi kwa mkate tu, bali huishi kwa kila [neno] litokalo katika kinywa cha [Yehova].”—Kumbukumbu la Torati 8:2, 3.
8. Hali ya Waisraeli ilikuwa imekuwa nini, na ni kwa sababu gani Yehova alikuwa ameruhusu hilo?
8 Ebu wazia! Waisraeli milioni kadha .—wazee kwa vijana, wanaume, wanawake, na watoto—walikuwa wametembea kwa miaka mirefu arobaini “katika jangwa lile kubwa lenye kitisho, lenye nyoka za [sumu] na nge, nchi ya kiu [iliyokuwa bila] maji.” (Kumbukumbu la Torati 8:15) Walikuwa wamehitaji maji ya kunywa na chakula. Nyakati nyingine, Yehova alikuwa amewaruhusu wawe na kiu na njaa. Kwa sababu gani? Ili akaze katika akili zao kwamba ‘mwanadamu haishi kwa mkate tu, bali huishi kwa kila neno litokalo katika kinywa cha Yehova.’
9. Mahitaji ya Waisraeli yalikuwa yametimizwaje na maneno ya Yehova?
9 Kulikuwa uhusiano gani kati ya mahitaji ya Waisraeli na mitajo, au maneno, yaliyokuwa yakitoka katika kinywa cha Yehova? Ni mambo gani halisi yaliyokuwa yametimia kati ya Waisraeli yakiwa ni matokeo ya maneno ya Yehova? Musa aliandika hivi: “Mavazi yako hayakuchakaa, wala mguu wako haukuvimba, miaka hiyo arobaini. . . . [Yehova alikutolea] maji katika mwamba mgumu, [naye alikulisha] jangwani kwa mana.” (Kumbukumbu la Torati 8:4, 15, 16) Uhusiano ndio huu: Waisraeli hawangepokea lo lote la mambo hayo kama Yehova hangeyaamuru yatokee. Kwa hiyo, kwa halisi walikuwa wameishi ‘kwa kila neno [amri] litokalo katika kinywa cha Yehova.’
Kutegemezwa na Maneno ya Yehova
10, 11. Ni kwa njia gani nyinginezo Waisraeli waliweza kutegemezwa na maneno ya Yehova?
10 Licha ya kutegemea Yehova awape faida za kimwili kama chakula, maji, na mavazi, ni kwa njia gani nyingine Waisraeli walitegemezwa na maneno ya Yehova? Kulikuwa na faida za kiroho pia. Musa aliwaambia Waisraeli kwamba Yehova alikuwa amewapitisha katika mambo hayo jangwani ‘ili awanyenyekeze, awajaribu, ayajue yaliyo moyoni mwao, kwamba watashika amri zake, au sivyo.’ Aliongeza hivi: “Nawe fikiri moyoni mwako, ya kuwa kama vile baba amrudivyo mwanawe, ndivyo [Yehova], Mungu wako, akurudivyo . . . ili kukutendea mema mwisho wako.”—Kumbukumbu la Torati 8:2, 5, 16.
11 Ndiyo, kama Waisraeli wangalitumia kwa faida kamili mambo waliyojionea jangwani, wangalijifunza kuishi ‘kwa kila neno litokalo katika kinywa cha Yehova,’ si kwa kujifunza tu kutii amri zake zilizoandikwa bali kwa kujionea kwa njia halisi matokeo ya maneno ya Yehova katika maisha yao wakiwa taifa zima na katika maisha zao mmoja mmoja. Walikuwa wamepewa nafasi ya kutosha ‘kuonja waone Yehova ni mwema.’ (Zaburi 34:8) Mambo hayo yenye kutajirisha kuhusiana na maneno ya Yehova—yaliyosemwa na hata yakatimizwa—wangalipaswa kuwa wamelishwa nayo kiroho.
12, 13. Yoshua alijifahamishaje na maneno ya Yehova, naye alishuhudia nini?
12 Yoshua, aliyemfuatia Musa kuwa kiongozi wa Israeli, alijiarifu juu ya maneno ya Yehova kwa kujaza akili yake nayo. Imani yake ilitiwa nguvu kwa kuona yakitimizwa. Baada ya kifo cha Musa, Yehova alimpa Yoshua maneno haya: “Kitabu hiki cha torati kisiondoke kinywani mwako, bali yatafakari maneno yake mchana na usiku, upate kuangalia kutenda sawasawa na maneno yote yaliyoandikwa humo: maana ndipo utakapoifanikisha njia yako, kisha ndipo utakapositawi sana.”—Yoshua 1:8.
13 Kuelekea mwisho wa maisha yake, baada ya kutii kwa uaminifu neno la Yehova na kuona likitimizwa juu ya watu wa Yehova, Yoshua aliweza kushuhudia hivi: “Basi [Yehova] aliwapa Israeli nchi hiyo yote. ambayo aliapa kwamba atawapa baba zao; nao wakaimiliki, na kukaa mumo. Kisha [Yehova] akawapa raha pande zote. sawasawa na hayo yote aliyokuwa amewaapia baba zao; wala katika adui zao wote hakusimama hata mtu mmoja miongoni mwao mbele zao; yeye [Yehova] akawatia adui zao wote mikononi mwao. Halikuanguka neno [Kiebrania. da·varʹ; Kigiriki, rhe’ma] lo lote katika jambo lo lote, lililokuwa ni jema ambalo [Yehova] alikuwa amelinena katika habari ya nyumba ya Israeli; yalitimia mambo yote.” (Yoshua 21:43-45) Kweli kweli Yoshua aliishi na kutegemezwa, si na mkate tu, ‘ila kwa kila neno litokalo katika kinywa cha Yehova.’—Mathayo 4:4.
Kuishi Leo kwa Kutegemea Maneno ya Yehova
14. (a) Kwa kuchimba kina kirefu zaidi ndani ya Mathayo 4:4, tunaweza kuelewaje vizuri zaidi aliyomaanisha Yesu? (b) Ni nini kilichotia nguvu wenye kuthamini?
14 Tukiwa tumechimba kina kirefu zaidi ndani ya maneno yaliyo juu yaliyotajwa na Yesu katika kujibu kishawishi cha Ibilisi, tunaweza kuelewa vizuri zaidi aliyomaanisha Yesu. Habari ya kihistoria na kijiografia inayohusiana na masimulizi ya Musa, ambayo Yesu aliyataja, inaonyesha kwamba. maneno ya Yehova ambayo wanaume na wanawake watawa wanapaswa kuishi kwayo si maneno ya kukariri tu, Kwa Waisraeli hao, ‘kila neno la kinywa cha Yehova’ lilikamatanishwa na mana, maji. na mavazi ambayo hayakuchakaa. Ndiyo, maneno hayo yalitia ndani kutimizwa kwayo, na pia yalitia ndani mambo mazuri ajabu ambayo Yehova aliwafanyia watu wake. Walipojionea wenyewe mambo hayo kwa utimizo wa maneno ya Yehova, jambo hilo liliwatia moyo Waisraeli wenye kuthamini.
15. Maneno ya Yehova yanaweza kututegemezaje?
15 Hali moja na hiyo leo, kinachowategemeza watu wa Yehova si kusoma na kujifunza tu maneno ya Yehova, ingawa hilo ni jambo la maana sana. Tunategemezwa na kujionea wenyewe. kama kikundi na mtu mmoja mmoja, njia nzuri ajabu ambayo Yehova anashughulika nasi na kutenda kwa ajili yetu. Kadiri tunavyotambua shughuli za Yehova kwetu, ndivyo maneno hayo yaliyotimizwa yatakavyotutegemeza, kutia nguvu imani yetu, hali yetu ya kiroho.
16. (a) Mtunga zaburi mmoja alijishughulisha na nini? (b) Hali moja na hiyo sisi tufanyeje, na kufanya hivyo kutatusaidiaje?
16 Mtunga zaburi mmoja aliandika hivi: “Nitayakumbuka matendo ya [Yehova]; naam, nitayakumbuka maajabu—yako ya kale. Pia nitaitafakari kazi yako yote: nitaziwaza habari za matendo yako.” (Zaburi 77:11, 12) Tukijishughulisha na matendo, shughuli na kazi za Yehova zilizo kwa ajili ya watu wake, tukitambua kwamba hizo ni wonyesho halisi wa matamko yake, maandalizi hayo ya kimungu yatakuwa kama mkate wa kiroho kwetu. Vitatuvuta kwenye uhusiano wa kibinafsi pamoja na Yehova. Tutakuwa kama Yesu. Alikataa kugeuza mawe yawe mikate alipoombwa na Ibilisi. Hali moja na hiyo sisi tutajihadhari tusiruhusu mahitaji ya kimwili yatuangushe katika mtego wa Ibilisi na kuacha ibada ya Yehova.
17. Ni katika njia gani Yesu alikuwa mfano mzuri sana?
17 Yesu alisema: “Chakula changu ndicho hiki, niyatende mapenzi yake aliyenipeleka, nikaimalize kazi yake.” (Yohana 4:34) Yeye alikuwa mfano mzuri sana, akatuonyesha kwa njia halisi kwamba “mtu hataishi kwa mkate tu, ila kwa kila neno litokalo katika kinywa cha [Yehova].”—Mathayo 4:4.
Kungojea Maagizo Zaidi
18. Ni neno gani la kimungu linalotimizwa sasa?
18 Yehova, kupitia Mwanaye, amesema kwamba “habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu” kabla ya mwisho kuja. (Mathayo 24:14, NW) Neno hilo la kimungu linaendelea kutimizwa kwa sababu ya kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote ya Mashahidi wa Yehova. Je! wewe ‘unaishi’ kwa neno hilo lililotoka kwenye kinywa cha Yehova kwa kushiriki kikamilifu katika kazi ya kuhubiri na hivyo utegemezwe kiroho kwa sababu unafanya mapenzi yake?
19, 20. Ni maneno gani mengine ya kimungu yatakayosababisha karibuni matukio yenye kusisimua?
19 Maneno mengine ya Yehova karibuni yatatokeza matukio yenye kusisimua wakati ujao ulio karibu. “Zile pembe kumi” na “mnyama” watageuka kinyume cha “kahaba,” Babuloni Mkuu. Ndiyo, uangamivu wa dini ya uwongo utakaoletwa na washiriki wa Umoja wa Mataifa ambao wanapinga dini utakuwa tendo la kutazamisha sana likiwa ni utimizo wa moja la maneno ya Yehova.—Ufunuo 17:16, 17.
20 Neno jingine lenye kutokeza litatimia wakati Yehova kwa usemi wa mfano atakapoweka “kulabu” kwenye mataya ya Gogu, au Shetani, amwambie athubutu pamoja na “jeshi” lake kushambulia watu Wake duniani. (Ezekieli 38:2-4, 8-12) Bado tamko jingine la kimungu litaleta uharibifu wa majeshi ya Gogu. (Ezekieli 39:1-6)b Hilo litamaanisha “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” katika Har–Magedoni, (Ufunuo 16:14, 16; 19:11-21) Litakuwa jambo lenye kusisimua kama nini kwa waaminifu wa Yehova kuona utimizo wa maneno hayo ya kimungu, katikati ya ugomvi huo, kusikia kwa njia ya mfano neno hili lingine: “Simameni, mkauone wokovu wa [Yehova] ulio pamoja nanyi.”—2 Mambo ya Nyakati 20:17, NW.
21. Kutekeleza maneno ya Yehova kutaleta matukio gani?
21 Halafu, akitimiza neno jingine la kimungu, Kristo atamfunga Shetani na mashetani wake na kuwatupa katika shimo refu kwa “miaka elfu.” (Ufunuo 20:1-3) Miaka hiyo elfu moja itaruhusu yatimizwe maneno mengine ya Yehova, kutia na kufufuliwa kwa wafu na “kuwaponya mataifa,” yaani, wanadamu watiifu. (Ufunuo 20:11-15; 22:1, 2) Wakati wa kipindi hicho cha hukumu cha miaka elfu moja, kwa wazi Yehova atatoa maagizo ya ziada, tusiyoyajua sasa, kwa kuwa “vitabu” vipya vitafunguliwa. (Ufunuo 20:12) Itakuwa vizuri kama nini kwa waokokaji wa “dhiki kubwa” na wafu waliofufuliwa kupata maagizo na uongozi kutoka kwa maagizo hayo ya ziada yaliyoandikwa katika “vitabu” hivyo vya Yehova ambavyo havijafunguliwa bado na kuyatekeleza kwa furaha!
22. Tunatiwa moyo tufanye nini sasa?
22 Tukiwa na taraja hilo zuri sana mbele yetu, na tutumie kwa faida kamili nafasi tuliyo nayo sasa tujifahamishe juu ya ya Yehova na kufanya funzo la kibinafsi katika kazi ya kuhubiri pamoja na kuendelea daima kutambua matendo ya Yehova kwa ajili yetu.
[Maelezo ya Chini]
a Kwa Kifaransa ni “Toute Ecriture est inspiree de Dieu et utile.”
b Ona sura za 19, 20 za kitabu “The Nations Shall Know That I Am Jehovah”—How? (Kifaransa ni “Les nations sauront que je suis Jehovah”—comment?) kilichochapishwa na Sosaiti yetu.
Je! Unaweza Kukumbuka?
◻ Ni jinsi gani Waisraeli walijifunza kuishi ‘kwa kila neno litokalo katika kinywa cha Yehova’?
◻ Ni jinsi gani Waisraeli wangeweza kula kwa njia ya kiroho maneno ya Yehova?
◻ Ni jinsi gani leo tunaweza kuishi kwa kutegemea maneno ya Yehova?
◻ Ni maneno gani ya Yehova yatakayotimizwa?
[Picha katika ukurasa wa 27]
Jibu la Yesu kwa kishawishi cha Shetani linamaanisha nini kwako?
[Picha katika ukurasa wa 29]
Waisraeli walioishi ‘kwa kila neno litokalo katika kinywa cha Yehova’ walikuwa na faida za kimwili za moja kwa moja