Jizoeze Utawa Kuwa Lengo Lako
“Ujizoeze kupata utawa.”—TIMOTHEO 4:7.
1. Ni kwa sababu gani mwanariadha mmoja hodari hakushinda shindano?
MSICHANA huyo alikuwa ndiye mkimbiaji bora zaidi katika timu ya mashindano yake ya mbio. Ushindi mwingi aliokuwa amepata hapo mbele ulikuwa umemfanya awe miongoni mwa mabingwa wa taifa. Hivyo, ilitazamiwa kwamba angeshinda kwenye riadha hizi kubwa. Lakini, kwa kusikitisha kocha (mwalimu) wake, wanatimu wenzake, na yeye mwenyewe, alikimbia vibaya asivyopata kufanya wakati wo wote. Kwa sababu gani? “Nililegea katika mazoezi nikaacha kujizoeza kwa bidii,” akakubali mwanamke huyo kijana, akiwa ameaibika sana. “Kocha wangu alijaribu kunisukuma nijizoeze kwa bidii zaidi na kunionya, lakini sikusikiliza.” Kukosa kwake kujizoeza inavyopasa kukamkosesha ushindi aliokuwa akitaka kupata.
2. Ni kwa njia gani Wakristo wanapaswa kujizoeza, na ni kwa sababu gani wote watake kujua ni kwa jinsi gani?
2 Ukiwa Mkristo, hasa ikiwa wewe ni kijana, pia una mazoezi ya maana sana. “Ujizoeze kupata [utawa].” (1 Timotheo 4:7) Neno la Kigiriki la “ujizoeze” (gy·mnaʹzo) lilieleza juu ya mazoezi ya kujikaza na mara nyingi yenye maumivu ambayo wanariadha walifanya katika jengo la mazoezi ya viungo. Kwa hiyo, kuhusu utawa na thawabu zake, mtume Paulo aliongeza hivi: “Kwa maana twajitaabisha na kujitahidi kwa kusudi hili.” (1 Timotheo 4:10) Sifa hiyo ya lazima si jambo linalojileta lenyewe au kurithiwa kutoka kwa wazazi wenye kumwogopa Mungu. Lakini ni hatua gani unazopaswa kuchukua? Wakristo wa umri wote wanapaswa kutaka kujua.
Upashanaji Mzuri wa Habari Pamoja na Mungu
3. (a) Ni kwa sababu gani funzo la kibinafsi ni la maana sana? (b) Ni sifa gani za Mungu zinazokuvuta kwake?
3 Kwa kuwa utawa unatia ndani kuthamini kwa moyoni sifa za Yehova, unahitaji kujua jinsi alivyo hasa. Yehova anajulisha hayo katika Biblia. Lakini ni lazima ujifunze kwa uangalifu Neno lake na vichapo vyenye msingi wa Biblia, kwa njia hiyo ulishwe kwa “maneno ya imani, na mafundisho mazuri.” (1 Timotheo 4:6) Funzo la namna hiyo litakusaidia uone ‘uzuri wa Yehova.’—Zaburi 27:4.
4. Ni mambo gani yaliyoonwa yanayoonyesha ubora wa funzo la kibinafsi, na ni maswali gani unayopaswa kuyafikiria kwa uzito?
4 “Kujifunza zaidi juu ya Yehova kunakufanya uhisi kuwa karibu zaidi naye,” asema mwevanjeli wa wakati wote (painia) mwenye umri wa miaka 22. “Ninaposoma unabii mbalimbali na kuona jinsi unavyotimizwa, unafanya nisimame nikiwa na woga wenye heshima kwake. Funzo la kibinafsi ndilo linalonisaidia.” Kijana mmoja wa miaka 16, aliyekuwa amehuzunika sana, aliandika juu ya makala moja katika mfululizo wa “Vijana Wanauliza” zinazotokea kwa ukawaida katika gazeti Amkeni! akisema: “Nilipokuwa tu nimekosa tumaini kabisa, makala hiyo ikaja. Nilisisimuka sana nisiweze kuiweka chini! Ilinifanya nihisi nikiwa karibu zaidi sana na Yehova, nikatambua kwamba anaelewa na kujali sana. Sasa nahisi naweza kufaulu.”a Je! unahakikisha kusoma kila toleo la magazeti yetu? Ingawa inataka kujikaza, je, unatafuta wakati wa kulisha akili na moyo wako kwa funzo la kibinafsi la Biblia? Kwa kujifanyia uchunguzi wako mwenyewe, unaweza kujithibitishia kweli kweli kwamba una ukweli. Maarifa hayo yanapoufikia moyo, bila shaka yatakusukuma kwa maana ndiyo “mafundisho yapatanayo na [utawa].”—1 Timotheo 6:3; Warumi 12:2.
5, 6. Ni sala za aina gani zinazokuvuta karibu na Mungu? Toa mfano.
5 Upashanaji mzuri wa habari pamoja na Mungu pia unatia ndani sala za kutoka moyoni na za kutaja mambo waziwazi. Sala hizo zinasaidia kusitawisha urafiki wa kibinafsi pamoja na Yehova. Unapofanya makosa, uwe na nia ya kusihi kama Daudi: “Usiyakumbuke makosa ya ujana wangu, wala maasi yangu.” (Zaburi 25:7, 11) Na ujue kwamba atakusamehe ikiwa u mwenye toba. Jifunze kudumu katika sala, ukiumwaga moyo wako. Kijana mmoja msichana, ingawa alilelewa katika nyumba ya kimungu, alikuwa ameruhusu tatizo la kusema limzuie asijitie katika dini ya kweli. “Halafu usiku mmoja,” akafunua msichana huyo mwenye miaka 22, “nikamsihi Yehova, ‘Nisaidie nitake kukutumikia, wala si kwa sababu tu wazee au wazazi wangu wanataka nifanye hivyo,’” Jinsi maisha yake yalivyoanza kubadilika! Ajapokuwa mwenye kigugumizi, akajishughulisha kabisa katika huduma. Kwa furaha anatangaza hivi, “Namtumiani Yehova zaidi sana sasa kwa sababu najua sikuzote anajibu.”—Zaburi 62:8.
6 Kijana mmoja Mkristo alisali waziwazi kuhusu mipango yake ya kupainia. Sala zake zilipojibiwa, msichana huyo alisema hivi kwa msisimuko: “Nikajua Yehova ni halisi na kwamba anatujali! Kabla ya hapo nilifikiri nina uhusiano pamoja naye, lakini sasa yeye ni kama rafiki—rafiki yangu bora zaidi.” Yehova hatajibu sikuzote kwa njia fulani yenye kutazamisha, lakini ukiwa mwenye bidii na kutenda kupatana na sala zako, utakuja kuthamini mwelekezo wake wa upendo—Zaburi 145:18.
Uwe na Dhamiri Njema
7. Dhamiri ni nini, na ni kwa sababu gani uwe na dhamiri njema?
7 Paulo alipomsihi Timotheo aendelee kuwa ‘mwenye dhamiri njema,’ mtume huyo alijua kwamba jambo hilo lingetaka jitihada ya kuazimia. (1 Timotheo 1:19) Kwa sababu gani hivyo? Dhamiri yetu ndiyo uwezo tuliokuhukumu mambo tuliyokwisha kufanya au tunayofikiria kufanya. Ama inaweza ‘kutushtaki,’ ikilaumu kwa uchungu mwendo wetu, au ‘kututetea,’ ikikubali tunayofanya kuwa haki. (Warumi 2:15) Lakini ikipotoka, inaweza kutoa ujumbe wenye kasoro. Wengine wenye dhamiri zenye kasoro wanaweza kutenda kama wanyama wakatili, na bado ‘wasishtakiwe’ na ‘sauti ya ndani.’ Hata wanaweza ‘kukiri ya kwamba wanamjua Mungu’ lakini ‘kwa matendo yao wamkane.’ Unaweza kujilindaje usisitawishe dhamiri yenye kasoro?—Tito 1:10-16.
8. Wengine katika karne ya kwanza ‘walisukumiaje mbali’ dhamiri njema?
8 Paulo alikuwa amemwambia Timotheo kwamba Wakristo fulani walikuwa “wameisukumia mbali” dhamiri njema yao kwa ‘kusikiliza hadithi za uwongo’ na “semi zisizo na kitu zinazochafua yaliyo matakatifu.” (1 Timotheo 1:4, 19, 20, NW; UV; 6:20, NW; 2 Timotheo 2:16-18) Kwa sababu walisikiliza mambo hayo, imani yao ilikuwa imepinduliwa, na jambo hilo likatokeza kuvunjikiwa kwa hali ya kiroho. Hata hivyo, Paulo, alionyesha kwamba mambo mengine licha ya mafundisho ya uasi wa imani yalikuwa ‘yasiyopatana na mafundisho yenye uzima.’ Katika 1 Timotheo 1:9, 10 anaorodhesha mambo kama vile kuua, uasherati, na watu wa jinsia moja kulalana.
9, 10. (a) Tunaweza kujifunza nini kwa mfano wa wenzi wawili Wakristo walioshindwa kuwa na dhamiri njema? (b) Tunaweza kuzuiaje dhamiri yetu isichomwe moto na kufa ganzi?
9 Leo jeuri na ngono zisizo za adili ziko kwa wingi kwenye mawonyesho ya sinema na televisheni na pia kwenye kurasa zilizochapwa. Tukilisha akili zetu mambo hayo, dhamiri yetu inaweza kuchomwa moto na kufa ganzi pole kwa pole. Jambo hilo lilipata wenzi wawili Wakristo vijana waliofanya uasherati muda mfupi tu kabla ya siku yao ya arusi. “Nafikiri ni kwa sababu ya yale tuliyokuwa tumekuwa tukitazama kwenye televisheni,” akakubali msichana huyo kijana. “Unaona watu wakati wote wakipigiana busu na kukumbatiana, kwa hiyo halionekani kuwa jambo kubwa. Unazoea. Kwa hiyo tukaanza kufanya hivyo. Kama tu ningalikuwa nimefikiria zaidi juu ya jinsi jambo hilo lilivyokuwa zito!” Kabla hajatambua hilo, akapoteza dhamiri njema yake. Mwanamume huyo kijana aliongeza hivi: “Mimi pia nilikuwa na tatizo la kupiga punyeto, na jambo hilo linafanya dhamiri yako ichomwe moto na kufa ganzi kwa hiyo si vigumu sana kupigiana busu na kukumbatiana na mwishowe kufanya uasherati.” Ingawa walionekana wanaweka mfano mwema mbele ya wengine, waliyotazama kuwa tafrija, pamoja na zoea chafu la sirini, yalikuwa yametokeza kufa kwa dhamiri yao kama vile mwili unavyochomwa moto ukafa ganzi kwa kuguswa-guswa na chuma chenye moto kabisa.—1 Timotheo 4:2.
10 Je! dhamiri yako ingeweza kufishwa jinsi iyo hiyo na yale unayotazama au kusoma kuwa tafrija? Je! kweli kweli unafanya kazi kwa bidii ushinde zoea lo lote baya ambalo lingeweza kuchafua dhamiri yako? Ili iwe ulinzi kwako, ungeweza kuchukua hatua inayofaa kwa kusoma—na kusoma tena—vitabu vyenye msingi wa Biblia vinavyoshughulika hasa na tatizo lako au kwa kuzungumza tatizo hilo pamoja na mzee. Dhamiri njema, iliyo safi ni zawadi yenye thamani kutoka kwa Mungu itakayokusaidia usitawishe utawa. Usiruhusu cho chote kikufanye uipoteze!
Chagua Washiriki Wanaofaa
11, 12. (a) Ni onyo gani linalotolewa katika 2 Timotheo 2:20, 21? (b) Unaweza kulitiije onyo hilo?
11 Mtume Paulo anaandika hivi: “Katika nyumba kubwa [kundini] havimo vyombo vya dhahabu na fedha tu, bali na vya mti, na vya udongo; vingine vina heshima, vingine havina. Basi ikiwa mtu amejitakasa kwa kujitenga na hao, atakuwa chombo cha kupata heshima, kilichosafishwa, kimfaacho [mwenye chombo], kimetengenezwa kwa kila kazi iliyo njema.” (2 Timotheo 2:20, 21) Maono yetu ya moyoni na mwenendo unageuzwa sana na wale tunaochagua wawe marafiki. Bila shaka, wasioamini si washiriki wanaofaa. Lakini Paulo hapa anaonyesha bila kuficha kwamba hata ndani ya kundi mnaweza kuwa watu ambao si washiriki wanaofaa. Ni kweli, huenda ukaona inafurahisha kuwa karibu yao, lakini uvutano wao hautakusaidia kamwe ‘uzikimbie tamaa za ujanani’ au kusitawisha utawa. Tafuta washiriki wenye kujenga ndani ya kundi. Paulo anaendelea kusema hivi katika mstari wa 22: “Ukafuate haki, na imani, na upendo, na amani, pamoja na wale wamwitao Bwana kwa moyo safi.”—Linganisha Wafilipi 4:8, 9.
12 Chukua kisa cha kijana Mkristo ambaye, ajapopewa mazoezi ya kimungu,sikuzote alikuwa anaingia matatani. “Kwa sehemu kubwa ilikuwa kwa sababu ya watu niliokuwa nikishirikiana nao,” akasema msichana huyo. Alipoona maisha yake yakiharibika, alibadili marafiki wake. Anamaliza kwa kusema: “Ikiwa una marafiki karibu nawe wanaompenda Yehova, inakusaidia kuendelea kuwa na dhamiri iliyo chonjo na kuepuka matata. Wanapoonyesha kuchukia kufanya kosa, jambo hilo linakufanya uhisi vivyo hivyo.” Kwa kuepuka washiriki wenye kutilika mashaka, msichana huyo amekuwa chombo ‘kimfaacho mwenyewe, kilichotengenezwa kwa kila kazi iliyo njema.’ Akiwa ametumikia kwa miaka kumi akiwa painia, anaongeza kusema: “Naona kwamba sasa Yehova amenitumia nisaidie wengine.”—2 Timotheo 2:21; Mithali 15:31.
13. Unaweza kuamuaje ni nani walio washiriki wazuri, nao huenda wakawa na uvutano gani juu yako?
13 Kwa hiyo, fikiria vilivyo washiriki wako ni nani. Je! wanafuatia uadilifu, imani, upendo wenye kuongozwa na kanuni, na amani? Je! wao wamejawa na bidii ya Kikristo? Kwa kuwafanya hao wawe wenzi wako wa karibu, wewe mwenyewe huenda ukawa mfano katika kusema, katika mwenendo, katika upendo, katika imani, katika usafi, kama alivyokuwa Timotheo, mshiriki wa karibu wa Paulo. Hiyo haimaanishi kwamba unapaswa kuwa mwenye ubaridi au asiye na urafiki kuelekea wasio mfano mwema sana. Mfano wako wa furaha huenda ukawasukuma wao, pia, wajifanyie njia zilizonyooka kwa ajili ya miguu yao.—1 Timotheo 4:12; Waebrania 12:12-15.
Jinyime Mambo Fulani kwa Ajili ya Mungu
14, 15. (a) Ni nini yaliyokuwa matakwa ya wanariadha wa kale walipokuwa wakifanya mazoezi? (b) Ni kazi gani inayotaka kujinyima, na tuna mifano gani myema?
14 Katika siku za Timotheo, wanariadha walipokuwa wakijizoeza ‘walijizuia katika yote,’ wakajinyima anasa nyingi zinazofaa. (1 Wakorintho 9:25) Walikula aina fulani tu ya chakula, na kulingana na Horesi, mshairi wa karne ya kwanza K.W.K., ‘walijiepusha na wanawake na divai’ ili ‘wafikie mradi waliotamani kwa muda mrefu.’ Hali moja na hiyo, kujizoeza kwa utawa ukiwa lengo lako kunataka kujinyima mambo fulani. Paulo alisema hivi juu ya Timotheo: “Sina mtu mwingine mwenye nia moja [na yake] . . . Maana [wengine] wote wanatafuta vyao wenyewe, sivyo vya Kristo Yesu. Ila . . . [yeye] ametumikia pamoja nami kwa ajili ya Injili. “—Wafilipi 2:19-22.
15 Timotheo aliamriwa hivi: “Ifanye kazi ya mwevanjeli, timiza kwa ukamili huduma yako.” (2 Timotheo 4:5, NW) Hata faida zake za kibinafsi ziwe zilikuwa zenye kuvutia jinsi gani, alijinyima hizo ili akamilishe kazi ya Mungu. Je! wewe una nia ya kufanya vivyo hivyo? Leo vijana fulani Wakristo ambao hawana madaraka yo yote mazito ya Kimaandiko wamefuatia elimu ya juu au kazi za wakati wote zenye mshahara mnono badala ya kufanya huduma ya Kikristo iwe kazi yao ya maisha. Mmoja wa hao alikuwa akingojea kazi ya namna hiyo kwa shauku. Lakini, kabla hajaanza kazi, alikubali mwaliko wa kufanya kazi pamoja na wenzi wawili mapainia katika utumishi wa shambani kiangazi chote. Aliupenda. Kwa hiyo, alijinyima kazi hiyo ya kuajiriwa ya wakati wote yenye kutamanika sana akachukua kazi ya kibarua isiyopendeza sana ili apainie. Akiwa na roho iyo hiyo kama ya Timotheo, sasa anatumikia katika makao makuu ya ulimwengu ya Mashahidi wa Yehova. Nia ya kujinyima ni ushuhuda wa upendo wa kweli, na kujinyima huko kunaongeza kina cha upendo huo, kama alivyoona.
16. Ni mengine gani kati ya mambo ambayo huenda vijana wakapaswa kujinyima?
16 Akiwa “mhubiri na mtume,” Paulo alikazia kufaa kwa kiasi katika mavazi. Je! wewe ungekuwa na nia ya kujinyima mtindo fulani wa mavazi au kujipamba ambako kungeweza kuudhi wengine au kuzuia kuhubiri kwako kuwa mhubiri? (1 Timotheo 2:7-10) Akiendelea, Paulo aliandika hivi: “Wote wapendao kuishi maisha ya [utawa] . . . wataudhiwa.” (2 Timotheo 3:12) Je! wewe una nia ya kuutetea ukweli wakati ambapo kufanya hivyo huenda kukamaanisha kudhihakiwa, kujinyima kuwa na cheo cha kupendelewa kuwa pamoja na wanadarasa wenzako? Kujinyima hayo yote kukiwa kumefanywa kwa kusudi linalofaa kutakusaidia usitawishe utawa na wakati huo huo kukufundishe umtegemee Yehova na kufikiria maoni yake zaidi ya mambo mengine yote.
Endelea Kusonga Mbele
17. Katika kufanya maendeleo, Timotheo alikuwaje mfano kwa wahudumu vijana leo?
17 Kusitawisha utawa ni jambo la kuendelea. Paulo alimwambia Timotheo hivi: “Uyatafakari hayo; ukae katika hayo; ili kuendelea kwako kuwe dhahiri kwa watu wote.” (1 Timotheo 4:15) Wengine, kwa sababu ya kuwa wachanga sana wasiweze kuwa watumishi wa huduma au wazee, huenda wakawa wanahisi hawawezi kusonga mbele, wakiwa wanafikiri kwamba kufanya maendeleo kunapimwa tu kwa kulingana na madaraka na mapendeleo ya kundi aliyo nayo mtu. Ni kweli kwamba Timotheo alikuwa amestahili si katika ukuzi wa kiroho tu bali pia katika umri kuweza kutumikia akiwa mzee. Lakini Timotheo alipaswa kujitahidi, na katika kufanya hivyo aliweka mfano wenye kutokeza kwa wahudumu wote vijana wafuate katika utumishi wo wote unaoweza kuwa tayari kwao.—1 Timotheo 4:12, 13.
18. Ni kwa njia zipi vijana Wakristo wanaweza kufanya maendeleo?
18 Kwa hiyo, kama Timotheo, wewe uliye mtumishi wa Yehova unayeendelea kukomaa, unaweza kuwa “kielelezo kwao waaminio” kwa kuruhusu ukweli uongoze sana jinsi unavyoishi na kwa kufanya huduma yako iwe bora zaidi. Kwa sasa unaweza kujitahidi kusonga mbele kwa kujifunza kusitawisha sifa kama vile kuwa mwenye kiasi katika mazoea, mwenye utaratibu, mkaribishaji, na kuchukua mambo kwa uzito. Kwa kuwa tayari kutumiwa na wazee na kwa kuchukua kwa uzito kazi yo yote wanayokuomba ufanye, unaweza kujitahidi kuthibitisha ‘kufaa kwako chini ya jaribu.’ (1 Timotheo 3:1, 2 8-10, NW) Hata ikiwa maendeleo yako hayaonwi upesi na wengine, uwe na hakika kwamba Yehova anaona. Baadaye, wengine wataona pia.—1 Timotheo 5:25.
19. Ijapokuwa jitihada inayotakwa, ni kwa sababu gani unapaswa kujizoeza utawa kuwa lengo lako?
19 Usisahau kamwe kwamba ni kwa kusitawisha utawa kwamba unaweza kuwa na uhusiano wa kibinafsi unaokubalika kwa Yehova. Kukosa mazoezi ya kiroho kunatokeza hasara kubwa zaidi ya ile ya mwanariadha aliyeaibika ambaye alitajwa mwanzoni mwa makala hii. Kusitawisha utawa ni kazi ngumu. Lakini ulimwenguni pote, umati wa sauti zenye furaha za vijana zinavuma hivi: UNASTAHILI JITIHADA YOTE! Kuwa na sifa hiyo kunaongoza kwenye njia ya maisha yenye kuridhisha sasa, bila masikitiko yo yote, na kunalifungua tumaini la furaha ya milele. Kwa hiyo endelea kujizoeza. Endelea kufanya yote uwezayo, hata inapokuwa vigumu. Uwe na faraja ya kwamba “Mungu wa fadhili zote zisizostahilika . . . mwenyewe atamaliza mazoezi yenu, atawafanya mwe imara, atawafanya mwe na nguvu. Kwake yeye kuwe nguvu milele. Amina.”—1 Petro 5:10, 11, NW.
[Maelezo ya Chini]
a “Sababu Gani Nahuzunika Sana?” katika toleo la Agosti 22, 1982 la Amkeni! (Kiingereza), gazeti-jenzi la Mnara wa Mlinzi.
Je! Unaweza Kujibu?
◻ Ni jitihada gani inayohitajiwa ili kudumisha upashanaji mzuri wa habari pamoja na Mungu?
◻ Ni nini yanayohusika katika kuwa na dhamiri njema?
◻ Andiko la 2 Timotheo 2:20-22 linaweza kutumiwaje katika kusitawisha utawa?
◻ Vijana Wakristo wanaweza kufanyaje maendeleo?
[Sanduku katika ukurasa wa 16]
Baadhi ya Sifa za Mungu Wetu Mwenye Moyo Mchangamfu
◼ Ana hisia. Kwa hiyo, matendo yetu ama yanaweza “kumhuzunisha” ama kumfurahisha.—Zaburi 78:40; Mithali 27:11
◼ Ingawa wanadamu mara nyingi wanaangalia sura ya nje ya mtu, yeye “huutazama moyo.—1 Samweli 16:7.
◼ Anatujali na anatukaribisha tumtupie mahangaiko yetu, naye “ni ngome siku ya taabu.—Nahumu 1:7; 1 Petro 5:7.
◼ Yeye anaitwa “Mungu mwenye furaha,” na “apendezwaye” na watumishi wake.—1 Timotheo 1:11, NW; Zaburi 35:27.
◼ Yeye hatatenda kwa uonevu kamwe wala kupendelea.—Ayubu 34:10; Matendo 10:34, 35.
◼ Ingawa haachilii makosa, tunapotubu kosa au udhaifu, yeye ni “tayari kusamehe,” hatutendi “sawasawa na hatia zetu” wala kutulipa “kwa kadiri ya maovu yetu”—Zaburi 86:5; 103:8-14.
◼ Yeye anafikika, na anatia moyo viumbe wake washikamanifu watumie uwezo wao. Ajapokuwa na hekima isiyo na mwisho, anasikiliza mapendekezo. Mfalme Daudi aliandika: “Unyenyekevu wako umenikuza.”—Zaburi 18:35; 1 Wafalme 22:19-22.
[Picha katika ukurasa wa 19]
Wakristo wengi wanaona furaha ya ndani sana katika huduma kuliko ilivyo katika kazi za mshahara mnono