Kumwamini Mungu—Je! Kunatosha?
“JE! WEWE unaamini kuna Mungu au roho wa ulimwengu wote?” akauliza George Gallup, Mwana, aliye mchunguzi mashuhuri wa maoni ya watu juu ya mambo. Labda wengine watashangaa kujua kwamba asilimia 95 ya watu wazima (wenye umri wa miaka zaidi ya 30) na vijana walioombwa maoni walisema, ndiyo! Lakini ni kwa kadiri gani kuamini kunavyoonyeshwa kwa matendo? Kwa wazi si sana. Hiyo ni kwa sababu Bw. Gallup aliripoti kwamba vijana fulani wakubwa walipoulizwa, “Ni kwa kadiri gani imani zako za kidini zinavyoongoza mawazo au matendo yako ya kila siku,” asilimia 26 tu ndio waliosema, “sana.”a—The Search for America’s Faith, cha George Gallup, Mwana, na David Poling.
Basi, ni wazi kwamba kuamini tu kuna Mungu hakutoshi. Mwanafunzi Yakobo aliandika hivi: “Wewe waamini ya kuwa Mungu ni mmoja; watenda vema. Mashetani nao waamini na kutetemeka. . . . Imani pasipo matendo haizai.” (Yakobo 2:19, 20) Kwa upande mwingine, Biblia inaeleza juu ya watu mmoja mmoja waliochukua hatua inayozidi kuamini tu. Kwa mfano, Enoki ‘aliendelea kutembea pamoja na Mungu wa kweli.’ (Mwanzo 5:24, NW) Hivyo uhusiano wa Enoki na Mungu wake ulikuwa wa karibu sana ikawa kama kwamba walitembea pamoja! Lakini ni kwa sababu gani Enoki alipendelewa kuwa na uhusiano huo usio wa kawaida? Kwanza, ingawa aliishi katikati ya hali ya kidini iliyopotoka sana ambamo ‘kazi za kutomcha Mungu’ zilizoewa kwa njia mbaya sana, Enoki alifuata njia ya uadilifu ya maisha. Alizifunua kwa ushujaa na uwazi njia mbovu za watu wa rika lake, akitabiri hivi: “Angalia, [Yehova] alikuja na watakatifu wake, maelfu maelfu, ili afanye hukumu juu ya watu wote, na kuwaadibisha wote wasiomcha Mungu, kwa ajili ya kazi zao zote za upotevu walizozitenda bila kumcha Mungu, na kwa ajili ya maneno magumu yote ambayo hao wenye dhambi wasiomcha Mungu wameyanena juu yake.”—Yuda 14, 15.
Kutembea pamoja na Mungu kulimtia Enoki katika hatari kubwa. Inaelekea kuwa adui zake walipanga hila ya kumuua na kukomesha utabiri wake wenye kuudhi. Lakini, Mungu ambaye yeye alitembea pamoja naye alichukua hatua. Inasema Biblia: “Kwa imani Enoki alihamishwa, asije akaona mauti, wala hakuonekana, kwa sababu Mungu alimhamisha.” Ndiyo, “Mungu alimtwaa” katika kifo, inaonekana ili amwepushe na kifo chenye jeuri mikononi mwa adui zake.—Waebrania 11:5, 13; Mwanzo 5:24; linganisha Yohana 3:13.
Noa ni mtu mwingine ‘aliyetembea pamoja na Mungu wa kweli.’ Kama Enoki, “Noa alikuwa mtu mwadilifu. Yeye alijitihibitisha kuwa asiye na hatia kati ya watu wa rika lake.” (Mwanzo 6:9, NW) Alifanya hivyo ijapokuwa katika siku zake mwenendo mpotovu ulienea sana na jeuri ikawa haizuiliki. Ingawa hivyo, Noa alionyesha alimcha Mungu akawa tofauti na wengine akiwa “mhubiri wa uadilifu.” Basi Mungu alihifadhi yeye na jamaa yake wakati alipoleta gharaka juu ya ulimwengu huo wa kale!—2 Petro 2:5; Waebrania 11:7; Mwanzo 6:5, 11.
Je! Mungu angali anatolea watu mwaliko wa kutembea pamoja naye? Ndiyo kabisa! Mtume Paulo alisema kwamba Mungu “hawi mbali na kila mmoja wetu,” kama tu ‘tutapapasa-papasa tukamwone.’ (Matendo 17:27) Lakini tunaweza kufanyaje hivyo? Na kwa kweli ni mambo gani yanayohusika katika kutembea pamoja na Mungu?
[Maelezo ya Chini]
a Asilimia 39 walisema “kidogo,” asilimia 14 wakasema “ni mara chache sana,” na asilimia 12 wakasema “hata kidogo.”