Unaweza Kutembea Pamoja na Mungu
“JE! WATU wawili waweza kutembea pamoja, wasipokuwa wamepatana?” ndivyo alivyouliza nabii Amosi. (Amosi 3:3) Lakini, je, wewe unaweza ‘kupatana’ (‘kuwekeana miadi,’ NW) utembee pamoja na Mungu?
Ndiyo! Kwa maana, kwa kweli ni Mungu anayechukua hatua ya kwanza kwa kututolea mwaliko wa kuwa rafiki zake. Yeye hatukazi tuingie katika urafiki huo. Bali anatuvuta kwa sifa zake zilizo nzuri ajabu. Kwani, uumbaji wenyewe tu unatutolea ushuhuda tele juu ya wema wa Mungu! “Mambo yake yasiyoonekana tangu kuumbwa ulimwengu yanaonekana, na kufahamika kwa kazi zake; yaani, uweza wake wa milele na Uungu wake.” (Warumi 1:20) Au kama vile mtume Paulo alivyosema kwenye Matendo 14:17: “[Mungu] hakujiacha pasipo ushuhuda, kwa kuwa alitenda mema, akiwapeni mvua kutoka mbinguni, na nyakati za mavuno, akiwashibisha mioyo yenu chakula na furaha.”
Basi wanaume kama Enoki na Noa walikuwa na hamu nyingi ya kukubali toleo la Mungu kwamba wafanye urafiki naye. Walihisi kwamba Mungu ‘alistahili kupokea utukufu na heshima.’ (Ufunuo 4:11) Kwa hiyo waliitikia mwaliko wa Mungu na wakamfikia wakiwa na imani. “Pasipo imani haiwezekani kumpendeza yeye vema,” akasema Paulo, “kwa maana yeye anayemkaribia Mungu yampasa aamini kwamba yuko na kwamba anakuwa mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii nyingi.” (Waebrania 11:6, NW) Kwa hiyo kwa kutafuta uhusiano pamoja na Mungu, wewe, pia, unaweza ‘kupatana’ na Yeye. Naye, mtunga zaburi, alisema: “Heri mtu yule umchaguaye [wewe Mungu], na kumkaribisha.”—Zaburi 65:4.
Kwa kuwa urafiki pamoja na Mungu unafanywa kwa kufuata masharti yake, ni lazima mtu ajifunze Neno lake, Biblia, ili ajue “mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.” (Warumi 12:2, NW) “Nitawezaje [kuelewa unabii wa Isaya], mtu asiponiongoza?” akauliza mtu mnyofu aliyekuwa akitafuta Mungu huko nyuma katika nyakati za Biblia. Na labda hata wewe una maoni hayo. Lakini, Mungu alihakikisha kwamba mwanafunzi jina lake Filipo alimfikia mtu huyo akamweleza unabii. (Matendo 8:30-35) Je! leo Mungu amepunguza kupendezwa kwake na wenye kumtafuta yeye kwa unyofu? Uhakika wenyewe tu kwamba wewe unasoma jarida hili linaloitegemea Biblia unaonyesha kwamba Mungu anapendezwa na wewe! Je! halingekuwa jambo la hekima kuwaruhusu wale waliokupatia jarida hili wakusaidie ujifunze habari zaidi juu ya Mungu?
Kumwona Yule Asiyeonekana
Unapokua katika maarifa ya kumjua Mungu, yeye atakuwa zaidi na zaidi wa halisi kwako. Baada ya muda mfupi utathamini kwamba yeye si dude fulani tu la nishati bali ni Mtu mwenye jina! Biblia inasema hivi kwenye Zaburi 83:18: “Wajue ya kuwa Wewe, uitwaye jina lako Yehova, ndiwe peke yako Uliye juu, juu ya nchi yote.” Akiwa Mtu, Yehova ana sifa, ana mapendezi na mambo yasiyompendeza—hata maoni ya moyoni!—Linganisha Kutoka 34:6, 7; Zaburi 78:40.
Pia Mungu ana viwango vya uadilifu. Kwa mfano, Mithali 3:32 inasema: “Mtu mkaidi ni chukizo kwa [Yehova], bali siri yake ni pamoja na wanyofu.” Yusufu alikuwa mmoja wa “wanyofu.” Biblia inaeleza namna mke wa bwana-mkubwa wake Mmisri, Potifa, alimsihi-sihi Yusufu afanye ngono naye. Hata hivyo alikataa, akisema, “Nifanyeje ubaya huu mkubwa nikamkose Mungu?”—Mwanzo 39:9.
Yehova alikuwa halisi kwa Yusufu. Yeye alikuwa na woga wenye afya kuelekea Yehova na alitenda kama kwamba alikuwa mbele Yake kikweli. Yusufu alikuwa kama mtunga zaburi aliyesema: “Nimemweka [Yehova] mbele yangu daima, kwa kuwa yuko kuumeni kwangu, sitaondoshwa.” (Zaburi 16:8; linganisha Mithali 3:5, 6) Musa alikuwa na imani kama hiyo. “Alistahimili kama amwonaye yeye asiyeonekana.”—Waebrania 11:27.
Basi, kutembea pamoja na Mungu kunamaanisha zaidi ya kutwaa maarifa tu. Maana yake ni kuchagua njia ya maisha inayopatana na mapenzi ya Mungu na kusudi lake lililofunuliwa! Ni kama vile mtume Paulo alivyosema: “Basi, mlapo, au mnywapo, au mtendapo neno lo lote, fanyeni yote kwa utukufu wa Mungu.”—1 Wakorintho 10:31.
Kutembea Pamoja na Mungu —Faida Zake
“Kwa kuwa kunahifadhi minofu na kutumia nishati kwa kiasi tu,” wakaandika Sussman na Goode katika kitabu chao The Magic of Walking, “kutembea kumependekezwa na wakuu wa tiba na afya kuwa kunaleta faida za namna mbalimbali.” Kati ya faida zinazosemwa ni kuzuia unene wa mwili usipite kiasi, kumpa mtu usingizi mzuri zaidi, kuondoa mahangaiko ya moyoni, na kuzuia kasoro za moyo. Ikiwa ndivyo ilivyo kuhusu matembezi ya kimwili, tunaweza kutazamia kwamba kutembea pamoja na Mungu kuna faida kubwa zaidi.
Lakini, usitazamie kupata msisimuko mkubwa sana wa moyoni. Bali unapoendelea ‘kumkaribia Mungu’ kwa kusali na kutenda kwa imani, utafurahia ‘amani ya Mungu ipitayo akili zote.’ (Yakobo 4:8; Wafilipi 4:6, 7) Kwa mfano, mwanamke mmoja alikuwa akinywa kupindukia na kutumia dawa za kulevya kwa sababu ya kushuka moyo daima. Pia alijaribu kufuata madhehebu kadha za Jumuiya ya Wakristo. Lakini ndipo akaanza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Alisema: “Ingawa hakuna kitu kinginecho chote nilichojaribu kutumia kiliweza kuondoa hali yangu ya kushuka moyo, kufahamu makusudi ya Yehova kulinipa kusudi halisi maishani.” Ndiyo, mtu anapoanza kutembea pamoja na Mungu, anaongozwa katika njia ambayo pasipo shaka itamletea faida za kiroho na za kimoyo.—Linganisha Isaya 30:21.
Faida nyingine ilionyeshwa na mwanamke mwenye ufahamu jina lake Abigaili. Alimwambia Mfalme Daudi: “Ijapokuwa binadamu angeinuka akuwinde, na kuitafuta nafsi yako, hiyo nafsi ya bwana wangu itafungwa katika furushi ya uhai pamoja na [Yehova], Mungu wako.” Ebu wazia hilo! Akielekewa na hatari ya adui zake, uhai wa Daudi ungekuwa chini ya ulinzi wa Yehova kama kwamba ulikuwa ni kitu kilichofungwa kwa uangalifu kiwekwe salama. Ingawa si lazima jambo hilo liwe na maana ya kwamba watumishi wa Mungu watapewa ulinzi wa kimwili sikuzote, Yeye pasipo shaka atalinda faida za milele za wale wanaotembea pamoja naye leo!—1 Samweli 25:29; linganisha Zaburi 116:15.
Ingawa hivyo, hilo halimaanishi kwamba wewe utaepushwa usipatwe na matatizo yale yaliyo kawaida ya wanadamu, kama kwamba Wakristo wanaishi namna fulani ya maisha ya kulindwa na hirizi. Solomoni aliona kwamba “wakati na tukio lisilotazamiwa huwapata” wanadamu wote. (Mhubiri 9:11, NW) Kwa mfano, mtume Paulo alitaabishwa na “mwiba katika mwili,” labda namna fulani ya udhaifu wa mwili. (2 Wakorintho 12:7; Wagalatia 4:13-15) Vivyo hivyo Timotheo mshiriki mwenzake alikuwa na ‘magonjwa ya mara kwa mara.’ (1 Timotheo 5:23) Vivyo hivyo, Wakristo leo wanapatwa na magonjwa na hata kujisikia mara kwa mara wakiwa na hali ya kuvunjika au kushuka moyo.
Tena, nyakati nyingine Yehova Mungu anaacha majaribu ya muda fulani yatokee ili kutusafisha, kama alivyofanya wakati aliporuhusu Yusufu afungwe gerezani. (Zaburi 105:17-19) Huenda wengine wakapatwa na kifo cha mapema mikononi mwa watesi wenye jeuri, kama kilivyompata Stefano. (Matendo 7:57-60) Lakini rafiki za Mungu wasijisikie kamwe kuwa wameachwa. (Linganisha 2 Wakorintho 4:8, 9.) “Maana Mungu si dhalimu hata aisahau kazi yenu, na pendo lile mlilolidhihirisha kwa jina lake.” (Waebrania 6:10) Alisema hivi mwanamke mmoja Mkristo aliyetegemezwa akaipita miaka ya kufungwa gerezani isivyo haki: “Mimi nasadiki sana sana kwamba hakuna ye yote wa wale wanaovumilia katika utumishi wa Yehova atakayekatishwa tamaa. Kwa moyo wangu mzima nimemtumaini Yehova na maneno yake yenye kufariji, ‘Sitakupungukia kabisa, wala sitakuacha kabisa.’”—Waebrania 13:5.
Msaada wa Kutufanya Tuendeleze Pigano Letu
Kuendelea kufuata mwendo huo wa uaminifu si jambo jepesi. Shetani na majeshi yake ya roho waovu wanakusudia kututega. (Waefeso 6:12) Halafu kuna mfumo mbovu wa mambo pamoja na vyambo vyao vyenye kuvutia. Mkristo mmoja katika karne ya kwanza jina lake Dema alivutwa fikira kando kwa sababu “aliupenda mfumo uliopo wa mambo.” (2 Timotheo 4:10, NW) Mwishowe, kuna mwili wetu wenyewe wenye dhambi pamoja na maelekeo yake ya kutenda uovu. (Warumi 7:21-23) Pigano la daima dhidi ya mavutano hayo linahitajiwa ndipo tuendelee kutembea pamoja na Mungu.
Ingawa hivyo, Mungu amefanya tuweze kupata vyombo vitatu vyenye nguvu vitusaidie: (1) Neno lake, Biblia, linalotoa uongozi unaohitajiwa. (Zaburi 119:105) (2) Tengenezo Lake linaloonekana, kundi la Kikristo, ambalo linaendesha shughuli ya Mungu ya ulishaji wa kiroho. (Mathayo 24:45-47; Waefeso 4:11-16) Sosaiti yetu, inayochapisha gazeti hili, inashirikiana kwa ukaribu na tengenezo hilo. (3) Roho takatifu Yake, ambayo tunapokea kupitia sala, kujifunza Maandiko, na kushirikiana na watu wake. Lingekuwa kosa zito kupuuza lo lote la maandalizi hayo. Nabii Mika anatuhimiza ‘tuwe wenye kiasi katika kutembea pamoja na Mungu wetu.’ (Mika 6:8, NW) Hiyo maana yake ni kutambua hali zetu za kupungukiwa na kumtegemea Mungu kabisa.
Kwa kweli, kutembea kwetu pamoja na Mungu kunaweza kulinganishwa na mtoto mdogo anayetembea pamoja na baba yake wakati wa dhoruba kali. Kama mtoto huyo angeacha kushika mkono wa babaye au aamue kujiendea zake, baada ya muda mfupi angepotea. Lakini akishika sana mkono wake, anaweza kutembea kwa usalama na uhakika pamoja na baba yake. Sisi, pia, lazima tujihadhari ili tunyenyekee mwelekezo wa Mungu kama unavyotolewa kupitia Neno na tengenezo lake. Kujitegemea kunaweza kutupoteza tu tusiwe na tumaini. Lakini, kwa kutembea pamoja na Mungu kwa kiasi tunaweza kuongozwa kwa usalama tuipite dhoruba inayokuja ya Har–Magedoni na kuokoka tuingie katika utaratibu mpya ulioahidiwa. Humo, kifo na maumivu yatakuwa mambo ya zamani. (Ufunuo 16:16; 21:3, 4; 2 Petro 3:13) Basi, je! wewe utakubali mwaliko wenye neema wa Mungu utembee pamoja naye?
[Picha katika ukurasa wa 6]
Neno la Mungu, roho yake, na tengenezo lake linaweza kutusaidia tuendelee ‘kutembea pamoja na Mungu’ kwa uaminifu