Sababu Gani Wewe Unataka Kutoa Hotuba ya Biblia?
MARA nyingi Yesu Kristo alisema na makutano makubwa ya watu. Na kwa uhakika yeye alikuwa msemaji mwenye matokeo. Kwa kweli, baada ya Yesu kumaliza Mahubiri ya Mlimani yanayojulikana sana, “makutano walishangaa mno kwa mafundisho yake.” (Mathayo 7:28) Hakuwezi kuwa na shaka kwamba Mwana wa Mungu alikuwa na makusudi mazuri kabisa ya kufanya hivyo na kwamba hotuba za watu wote alizotoa zililetea Baba yake wa kimbingu utukufu.—Linganisha Yohana 12:46-50.
Kutoa hotuba za watu wote kulikuwa pia njia ambayo habari njema zilienezwa na wafuasi wa Yesu katika karne ya kwanza ya Wakati wa Kawaida wetu. Kwa mfano, katika Korintho mtume Paulo “alikuwa akitoa hotuba katika sinagogi kila sabato na alikuwa akiwavuta kwa maneno Wayahudi na Wagiriki.” (Matendo 18:1, 4, NW) Zaidi ya hilo, Paulo alimtia moyo Timotheo mfanya kazi mwenzake kwa maneno haya: “Ninapokuwa nikija, endelea kujibidiisha sana kwenye usomaji wa mbele ya watu wote, kwenye kuhimiza, kwenye kufundisha.” (1 Timotheo 4:13, NW) Kwa hiyo ni hakika kwamba watumishi washikamanifu wa Yehova wa karne ya kwanza walikuwa wakifanya usomaji na usemaji mbele ya watu wote, wakiwa na makusudi mazuri sana.
Hata hivyo, tahadhari inahitajiwa. Wakati Herode alipoanza kutoa hotuba ya watu wote akiwa amevaa vazi la kifalme, wakusanyikaji walianza kupaaza sauti wakisema: “Ni sauti ya Mungu, si sauti ya mwanadamu”! Papo hapo malaika wa Yehova akampiga Herode. Kwa sababu gani? “Kwa sababu hakumpa Mungu utukufu.”—Matendo 12:21-23.
Uhitaji wa Kuwa na Nia ya Akilini Inayofaa
Leo, hakika kutoa hotuba ya watu wote ya Kibiblia ni pendeleo la kutamanika sana wanalopewa wanaume Wakristo waliokomaa. Lakini, ingefaa kila mhudumu achunguze moyo wake aone kusudi lake ni nini. (Mwanzo 8:21; Yeremia 17:9) Je! anasukumwa na tamaa ya kutukuza Mungu na kufaidi waamini wenzake na wengine? Au anataka kutoa hotuba hizo za Kibiblia kwa sababu kuna umashuhuri unaohusiana na usemaji wa mbele ya watu wote na pia kwa sababu ana tamaa ya kujichongea jina?
Kusudi linalofaa litajidhihirisha kwa njia mbalimbali. Kwanza, litatufanya tutambue kwamba ni kwa msaada wa roho ya Yehova tu tunaweza kulitumia vizuri pendeleo la kusema ukweli wa Mungu tukiwa jukwaani mbele ya watu wote. Basi, tutakuwa na nia inayofanana na ile ya mtume Petro, aliyesema: “Mtu akisema, na aseme kama mausia ya Mungu; mtu akihudumu, na ahudumu kwa nguvu anazojaliwa na Mungu; ili Mungu atukuzwe katika mambo yote kwa Yesu Kristo.”—1 Petro 4:11.
Lazima upendo uwe ndiyo sababu ya kutaka kutoa hotuba ya Biblia. Kwanza, ni lazima tuwe na upendo kuelekea Yehova Mungu, tutamani kumletea yeye utukuzo na kushiriki katika kulitakasa jina takatifu lake. Pili, kusudi letu linapasa kutia ndani upendo kuelekea wasikilizaji wetu, tamaa ya moyo mweupe ya kuwafundisha na kuwachochea kwenye “vitendo vitakatifu vya mwenendo na matendo ya utawa.”—2 Petro 3:11, NW.
Tamaa ya moyo mweupe ya kujenga waamini wenzetu na wengine inapasa pia kuwa ndilo kusudi letu la kutoa hotuba ya watu wote. Jambo hilo litatuzuia tusijaribu ‘kutekenya masikio’ ya wasikilizaji wetu kwa kuwaambia yale tu wanayotaka kusikia. (2 Timotheo 4:3, NW) Tamaa ya kujenga wengine kiroho itatusukuma pia tuepuke kufanya mizaha au kusema mambo yanayokusudiwa tu kufurahisha wasikilizaji au kuwafanya wacheke. Wala hatutatumia maneno yaliyotiwa sukari nyingi kwa kusudi la kujionyesha. Wala hatutaonyesha hekima ya kilimwengu kwa kujitahidi kufanya wasikiaji watushangae. Bali, tukiwa na kusudi linalofaa la kusema mbele ya watu wote, tutafuata mfano wa mtume Paulo, ambaye alionyesha ‘dalili ya roho na ya nguvu, ili imani ya wasikiaji wake isiwe katika hekima ya wana-damu, bali katika nguvu za Mungu.’—1 Wakorintho 2:3-5.
Mambo Matatu ya Msingi
Kutoa hotuba ya Kibiblia ya watu wote kunahusiana na hali ya akili na moyo. Basi, zaidi ya kuwa ni lazima wasemaji Wakristo wawe na nia inayofaa, ni lazima pia wawe na jambo lenye mafaa la kusema. Hiyo inataka wafikirie mambo matatu ya msingi. Hayo ni Maandiko, mambo hakika, na usadikishi unaotumia sababu zenye utimamu.
Kwanza, ni lazima ikumbukwe kwamba kwa wazi wazo kuu la hotuba ya Kibiblia ya watu wote linapasa kuonyeshwa na maandiko yanayotumiwa na msemaji. Ukipewa pendeleo la kutoa hotuba kama hiyo, inakupasa uijue vizuri habari yako na kuyatumia inavyofaa. Siku ya Pentekoste, 33 W.K., mtume Petro alitaja-taja Maandiko ili kuunga mkono maneno yake. (Matendo 2:14-41) Waberoya waliridhika kwamba Paulo alikuwa ametegemeza sana maneno yake juu ya msingi wa Maandiko. (Matendo 17:10, 11) Naye Apolo ‘alionyesha kwa maneno ya maandiko ya kuwa Yesu ni Kristo,’ Masihi aliyekuwa ametamaniwa kwa muda mrefu.—-Matendo 18:28.
Bila shaka, mtu anapewa msingi wa Kimaandiko wa hotuba ya watu wote katika muhtasari unaotolewa na Sosaiti yetu. Hata hivyo, msemaji anaweza kutumia maandiko ya ziada na mengine yanayolingana na yale yaliyoonyeshwa, mradi yanatumika kwa usawa ule ule na kwamba hayatumiwi kupita kiasi. Katika jambo hilo, ni lazima mhudumu Mkristo awe mwangalifu ayaeleze kulingana na nuru ya kiroho inayoendelea kuongezeka. Kwa mfano, huenda msemaji akatumia 1 Wakorintho 2:9 kwa njia isiyo sahihi kuhusiana na Paradiso ya kidunia ya wakati ujao, hali habari zinazozunguka (mstari 7 na 10) zinaonyesha kwamba andiko hilo linahusu mambo yale ya ndani zaidi ya hekima ya Mungu.
Pili, inafaa kufikiria mambo hakika yanayotumiwa ili kuunga mkono maneno yaliyonenwa na msemaji wa watu wote. Uangalifu unapasa utumiwe ili mambo yanayotolewa yasiwe yanaweza kutiliwa mashaka halali au kufanyiwa ubishi. Hasa uangalifu unahitajiwa ikiwa jambo fulani linaelekea kuchochea kwa urahisi maoni ya kutokubaliana na yaliyosemwa. Ni jambo la hekima—tena linahitajiwa kabisa—kuhakikisha kwamba yanayosemwa ni ya kweli. Kwa sababu hiyo, sikuzote inakuwa vizuri zaidi mtu aweze kuelekeza kwenye vyanzo vinavyotegemeka vya habari kwa kuwa huenda ikatukia kwamba maneno fulani yanatiliwa mashaka. Siku ya Pentekoste, Petro alionyesha mambo hakika yaliyojulikana sana na watu. Ndivyo pia alivyofanya mtume Paulo katika Areopago, au Kilima Mars, katika Athene.—Matendo 2:22; 17:22, 23, 28.
Tatu, ni wazi kabisa kwamba kuna uhitaji wa sadikisho lenye sababu zenye utimamu. Msemaji wa watu wote aliye Mkristo anahitaji kufikiri pamoja na wasikilizaji wake kwa kuwapa sababu. Hivyo tunasoma kwamba Paulo “akaanza kusemezana pamoja na Wayahudi na watu wale wengine walioabudu Mungu akiwatolea sababu katika sinagogi na pamoja na wale waliopatikana katika soko kila siku.” (Matendo 17:17, NW) Katika hotuba ya watu wote, sababu zinazotolewa katika kusema mambo zinapasa kuwa zenye utimamu, rahisi kufahamika, zenye kuelezwa waziwazi, nyepesi kueleweka. Msaada mkubwa katika jambo hilo ni matumizi ya viunzi vinavyoonyesha uhusiano kati ya mambo ambayo yamekwisha kusemwa na yale yanayoyafuata.
Basi, ukipewa pendeleo la kuwa msemaji wa watu wote, hakikisha kwamba una nia ya akilini inayofaa kuelekea hotuba ya Kibiblia. Moyoni mwako uwe na upendo kuelekea Muumba wako na wanadamu wenzako. Kusanya kisha utokeze maandiko na mambo hakika kwa kutumia sadikisho lenye sababu zilizo na utimamu. Ndipo mithali hii itakapokuhusu wewe: “Ulimi wa mwenye haki ni afya.” (Mithali 12:18) Zaidi ya hilo, kutoa hotuba nzuri za Kibiblia zinazotukuza Mungu ni njia moja ya ‘kuokoa nafsi yako na wale wakusikiao pia.’—1 Timotheo 4:16.