Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g03 12/22 kur. 16-18
  • Nawezaje Kufaulu Kusema Mbele ya Watu?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Nawezaje Kufaulu Kusema Mbele ya Watu?
  • Amkeni!—2003
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kusema Mbele ya Watu
  • Kushinda Woga
  • Madokezo Muhimu
  • Msaada Kutoka kwa Msemaji Mkuu
  • Utulivu
    Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
  • Kuwatazama Wasikilizaji
    Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
  • Sanduku La Swali
    Huduma Yetu ya Ufalme—2000
  • Sababu Gani Wewe Unataka Kutoa Hotuba ya Biblia?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—2003
g03 12/22 kur. 16-18

Vijana Huuliza . . .

Nawezaje Kufaulu Kusema Mbele ya Watu?

“Nilifikiri watu walitambua makosa yangu yote na wasiwasi wangu. Sikukazia fikira yale niliyosema. Nilidhani wanacheka kimoyomoyo.”—Sandy.a

UKUMBI wa shule umejaa pomoni. Unasikia ukiitwa kupitia vipaza-sauti na watu wote wanakutazama kwa ghafula. Hatua chache kuelekea jukwaani zinaonekana kuwa mbali sana. Mikono yako inalowa jasho, miguu yako inalegea, na mdomo wako unakauka kabisa. Kisha, tone la jasho linatiririka usoni. Aibu iliyoje! Unahisi kana kwamba unaenda kuchinjwa.

Kusema kweli, wengi wetu huogopa kusema mbele ya watu. (Yeremia 1:5, 6) Watu fulani hata wamesema kwamba ni afadhali wafe kuliko kusema mbele ya watu! Hata maoni yako yawe nini, kuna sababu nzuri za kukuchochea ufanye maendeleo ya kusema mbele ya watu. Hebu tuchunguze baadhi ya sababu hizo na tuone jinsi unavyoweza kuwa msemaji mzuri.

Kusema Mbele ya Watu

Tangazo moja kuhusu mtaala wa kusema mbele ya watu lilisema hivi: “Kusema mbele ya watu ni ustadi ambao kila mtu anahitaji.” Naam, huenda ukahitajika kusema mbele ya watu siku moja. Shule nyingi huwasaidia wanafunzi kusema mbele ya watu. Msichana mmoja anayeitwa Tatiana anaeleza: “Pindi nyingi nilihitajika kusema mbele ya wanafunzi wenzangu darasani.” Mara nyingi wanafunzi wanapaswa kuwa tayari kuzungumzia mambo mbalimbali kama vile kutoa ripoti, kuchambua kitabu, kuwaeleza wengine habari fulani kupitia video au kaseti, na kushiriki mijadala.

Unapoanza kufanya kazi, huenda ukaombwa kuwafundisha wafanyakazi wenzako, kuzungumza na wateja, au kutoa taarifa ya kifedha mbele ya kamati ya usimamizi. Kwa ujumla ustadi wa kusema mbele ya watu ni muhimu katika kazi mbalimbali kama vile uandishi wa habari, usimamizi, uhusiano na umma, na uuzaji.

Vipi ukiamua kuwa kibarua au karani? Kusema mbele ya watu kunaweza kukusaidia upate kazi. Unapopata kazi, uwezo wako wa kusema mbele ya watu unaweza kukusaidia. Baada ya kumaliza shule, Corrine alifanya kazi akiwa mhudumu hotelini kwa miaka mitatu. Anasema: “Ikiwa unajua kusema vizuri, watu wanakuona kuwa umekomaa na kwamba unaweza kushughulikia madaraka mengi. Unaweza hata kupata kazi nzuri zaidi, mshahara mnono zaidi, au hata uheshimiwe zaidi.”

Pia, kusema mbele ya watu ni sehemu ya ibada ya vijana Wakristo. (Waebrania 10:23) Taneisha anasema, “ni muhimu kuzungumza waziwazi. Tuna pendeleo la kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu.” (Mathayo 24:14; 28:19, 20) Vijana Wakristo hawawezi kuacha “kusema juu ya mambo ambayo [wameyaona] na kuyasikia” kutanikoni na katika utumishi.—Matendo 4:20; Waebrania 13:15.

Kwa hiyo, kujifunza kusema vizuri kunaweza kukusaidia katika njia nyingi. Hata hivyo, huenda bado unaogopa kusema mbele ya watu. Je, kuna jambo unaloweza kufanya kushinda wasiwasi huo? Ndiyo.

Kushinda Woga

Mtaalamu wa mfadhaiko na kusema mbele ya watu Dakt. Morton C. Orman anasema: “Si lazima uwe na akili nyingi au mkamilifu ili ufanikiwe. Kusudi la kusema mbele ya watu ni kuwaeleza wasikilizaji jambo la maana.” Kwa hiyo, kazia fikira ujumbe wako, usijifikirie wala kufikiria wasiwasi wako. Watu wengine katika karne ya kwanza walifikiri kwamba mtume Paulo si msemaji mwenye ufasaha, lakini alifanikiwa kwa kuwa sikuzote alisema mambo ya maana. (2 Wakorintho 11:6) Vivyo hivyo, ukizungumzia jambo muhimu ambalo unasadiki kabisa, wasiwasi wako utakwisha.

Msemaji mwingine hodari na mwalimu, Ron Sathoff, anatoa dokezo hili: Usizungumze kana kwamba unaigiza. Jaribu kusema kana kwamba unazungumza na mtu mwingine. Naam, sitawisha uhusiano mzuri na wasikilizaji, usiwaone kama umati, zungumza na mtu mmoja-mmoja kama katika mazungumzo ya kawaida. Pendezwa nao kikweli na uzungumze nao jinsi unavyosema kikawaida. (Wafilipi 2:3, 4) Kadiri unavyozungumza kama kawaida, ndivyo utakavyotulia.

Jambo lingine linalofanya wengi wawe na wasiwasi ni kuogopa kuaibika au kufikiri kwamba wasikilizaji watawachambua. Msemaji mwenye ustadi na mwalimu, Lenny Laskowski, anatukumbusha kwamba kwa kawaida wasikilizaji huwa na maoni mazuri wanapoanza kumsikiliza msemaji. Anasema: “Wanataka ufanikiwe si ushindwe.” Kwa hiyo, uwe na maoni mazuri. Ikiwezekana, wasalimie wasikilizaji wako kabla ya mkutano kuanza. Waone kuwa marafiki wala si maadui.

Pia kumbuka kwamba si vibaya kuwa na wasiwasi. Mtaalamu mmoja anasema hivi: “Tofauti na maoni ya wengi, wasiwasi unaweza kukusaidia unapozungumza.” Kwa nini? Kwa sababu ukiwa na wasiwasi kidogo, hiyo inaonyesha kwamba una kiasi na hivyo hutajiamini kupita kiasi. (Methali 11:2) Wanariadha, wanamuziki, na waigizaji wengi huhisi kwamba wasiwasi kidogo huwasaidia kuwa na matokeo mazuri zaidi, na hilo linawahusu wasemaji pia.

Madokezo Muhimu

Kwa kutumia madokezo yafuatayo na mengineyo, vijana fulani Wakristo wamepata uzoefu na wamefanikiwa kuwa wasemaji wazuri shuleni, kazini, na katika makutaniko yao. Jaribu madokezo yafuatayo ambayo yamewasaidia.

Jade: “Sema kwa maneno yako mwenyewe. Uwe na uhakika kuhusu faida za mambo unayosema. Ukiona hotuba yako kuwa muhimu, wasikilizaji wataiona hivyo pia.”

Rochelle: “Niliona ni muhimu kujirekodi kwenye video. Itakusaidia kuona kasoro zako. Pia jaribu kuchagua habari unayofurahia. Itakuwa rahisi kuizungumzia.”

Margrett: “Mimi huzungumza kwa njia ya kawaida ninapotumia muhtasari badala ya kuandika habari zote. Pia, kuvuta pumzi kabla ya kuzungumza hunisaidia nitulie.”

Corrine: “Usiogope kujicheka unapokosea. Kila mtu hukosea. Fanya tu yale unayoweza.”

Kama ilivyo katika shughuli yoyote, kama vile michezo, sanaa, au muziki, uzoefu na mazoezi mengi yanahitajiwa. Tatiana anasema inafaa kutayarisha habari utakazozungumzia mapema ili uwe na wakati wa kutosha kufanya mazoezi. Usikate tamaa. Anasema: “Kadiri ninavyoendelea kuzungumza mbele ya watu, ndivyo ninavyoweza kutulia zaidi.” Hata hivyo, kuna msaada mwingine ambao hupaswi kusahau hasa ikiwa umepewa mgawo wa kutetea ibada ya kweli.

Msaada Kutoka kwa Msemaji Mkuu

Kabla hajawa mfalme wa Israeli, kijana Daudi tayari alikuwa “msemaji mwenye akili.” (1 Samweli 16:18) Iliwezekanaje? Inaonekana alipokuwa kijana, alikaa nje kwa muda mrefu akichunga kondoo, na alitumia vipindi hivyo kusitawisha uhusiano wa karibu pamoja na Msemaji Mkuu, Yehova Mungu, kupitia sala. (Zaburi 65:2) Uhusiano huo ulimsaidia kusema waziwazi, kwa nguvu, na kwa usadikisho hata chini ya hali ngumu.—1 Samweli 17:34-37, 45-47.

Uwe na hakika kwamba unapoendelea na ibada yako, Mungu atakusaidia kusema kwa usadikisho na kukupa “ulimi wa waliofundishwa,” kama alivyomsaidia Daudi. (Isaya 50:4; Mathayo 10:18-20) Naam, ukitumia fursa za kuboresha ustadi wako wa kusema sasa, unaweza kuwa msemaji mzuri!

[Maelezo ya Chini]

a Baadhi ya majina yamebadilishwa.

[Sanduku katika ukurasa wa 18]

Wanazoezwa Kuwa Wasemaji

Katika makutaniko ya Mashahidi wa Yehova duniani pote, kuna programu ya kila juma ya kutoa maagizo kupitia Biblia inayoitwa Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Wanafunzi hushiriki mazungumzo, hutoa hotuba mbele ya kutaniko na kupokea mashauri yanayowasaidia kufanya maendeleo. Je, programu hiyo ina matokeo? Tafadhali soma maelezo haya ya Chris mwenye umri wa miaka 19.

Anasema: “Kabla sijajiandikisha kwenye shule hiyo, nilikuwa na wasiwasi mwingi nilipokuwa mbele ya watu. Sikufikiri ningeweza kuzungumza mbele ya watu. Lakini wengine kutanikoni walinitia moyo waliponiambia kwamba hata nikiwa na kigugumizi, watafurahia kunisikiliza kwa kuwa wanatambua jitihada zangu. Kisha walinipongeza baada ya kila hotuba. Hilo lilinitia moyo sana.”

Chris amekuwa katika shule hiyo kwa miaka mitano, na sasa anajitayarisha kutoa hotuba yake ya kwanza ya dakika 45. Je, unanufaika na shule hiyo?

[Picha katika ukurasa wa 17]

Kuwa msemaji mzuri kunaweza kukusaidia katika njia mbalimbali maishani

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki