Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w85 10/15 kur. 15-20
  • “Taifa” Linalolisha Mamilioni ya Watu Wenye Njaa

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Taifa” Linalolisha Mamilioni ya Watu Wenye Njaa
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • ‘Kutegemea Nguvu za Yehova’
  • Kuijaza Mazao “Nchi Yenye Kuzaa”
  • Mwendo wa “Leviathani” Wakomeshwa
  • Wokovu kwa Wanaochagua Nuru
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
  • Mkono wa Yehova Wainuliwa
    Unabii wa Isaya I—Nuru kwa Wanadamu Wote
  • Ambayo Kuzaliwa kwa Taifa hilo Kumemaanisha kwa Wanadamu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
w85 10/15 kur. 15-20

“Taifa” Linalolisha Mamilioni ya Watu Wenye Njaa

1, 2. (a) Ni uhitaji gani wa kweli unaopasa kuonwa na wakaaji wa dunia? (b) Ni taifa gani tunaloweza kutegemea katika jambo hilo?

PASIPO shaka mamilioni ya watu wa dunia hii wanaona njaa wakitaka “chakula” kitakachowalisha wapate uzima usiokoma hapa duniani, wakati dunia itakapogeuzwa iwe paradiso kila mahali. Lakini wamwendee nani au waende wapi? Jamhuri ya Israeli haifanyi jaribio la kutimiza unabii wa Biblia katika Isaya 27:6 juu ya kujaza dunia “mazao” ili wanadamu wapate faida yenye kudumu.

2 Taifa la Israeli katika karne ya kwanza ya Wakati wa Kawaida wetu lilipoteza kazi liliyopewa kubariki wanadamu wote. Hivyo ni mabaki madogo tu ya Wayahudi wa asili walioambiwa na Masihi maneno haya: “Mimi nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani. Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, kuwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu . . . Na, tazama! mimi nipo pamoja na ninyi siku zote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mathayo 28:18-20, NW) Lakini namna gani karne 19 baadaye? Ni nani katika wakati wetu wanaofikiria kutimiza Isaya 27:6? Na wewe na wapendwa wako mnahusikaje?

3. Ni akina nani katika karne yetu waliopatwa na “hasira kali” ya Mungu inayotajwa katika Isaya 27:4?

3 Ingawa kufikia wakati huu wetu ni miongo mingi ya miaka imepita tangu wakati wa matukio yenyewe, inatufaa tuchunguze kwa ufupi mambo fulani yaliyotendeka katika miaka ya Vita ya Ulimwengu ya Kwanza. Wakati huo Yehova Mungu alikuwa na sababu inayofaa kuyaonea “hasira kali” mataifa ya Jumuiya ya Wakristo kwa maana yalijitia katika pigano hilo lililomwaga damu. (Linganisha Isaya 27:4, NW.) Yalifanya hivyo badala ya kuachilia enzi zao za kitaifa kwa Mungu Aliye Juu Zaidi wakati Ufalme wake uliposimamishwa katika mbingu mwaka 1914 ukiwa mikononi mwa Mwanaye aliyetukuzwa, Yesu Kristo. Waliongeza kuni kwenye hasira kali yake kwa kuwatesa mabaki ya Israeli wa kiroho, wakiwazuia kwa makusudi hao Wanafunzi wa Biblia walio Wakristo wasiutangaze kwa uhuru Ufalme wake uliosimamishwa. Lakini, kwa kweli wengi wa mabaki ya Israeli wa kiroho walijiachilia washindwe na mikazo ya kilimwengu, hivyo wakawa hawatekelezi vizuri daraka lao la kuwa wachaguliwa waliotolewa katika huu mfumo wa mambo ya kilimwengu. Wakati huo hawakuliona suala la kutokuwamo kabisa katika mapigano ya ulimwengu huu, kwa hiyo wakaja chini ya hatia ya damu, na kwa muda fulani walistahili pia kupatwa na kiasi fulani cha “hasira kali” ya Mungu.

4. “Hasira kali” ya Mungu ilikuwa na matokeo gani juu ya watumishi wake Wakristo, na tunaweza kujifunza somo gani kutokana na jambo hilo?

4 Kama wewe ungaliishi wakati huo, unafikiri ungalitenda namna gani kwa sababu ya mikazo hiyo ya wakati wa vita? Inakupasa ufikirie mambo kama hayo, kwa maana kwa kufanya hivyo huenda ukaimarisha azimio lako juu ya jambo ambalo ungefanya ukikabiliana na mikazo yo yote ya wakati ujao. Wakati huo huenda ingalielekea kuwa kama wakati ulifika wa kuacha kuutangaza Ufalme na kupumzika. Wengi walielekea kutenda hivyo, wakajisikia kwamba iliwapasa kungoja bila kufanya lo lote ili wapate utukuzo wa mapema wakawe pamoja na Yesu Kristo aliyetawazwa. (Luka 22:28-30) Hata hivyo, ile nidhamu waliyopewa Wakristo wa kweli wa kipindi hicho kwa kupokea kiasi fulani cha “hasira kali” ya Yehova haikupita bure, kwa hiyo ilizaa matunda. Iliwatia nguvu kwa ajili ya kazi iliyokuwa ikija ya kuitangaza siku ya kisasa cha Mungu wetu juu ya yule ambaye nabii Isaya anamwita “Leviathani” katika Isaya 27:1 (NW), ambapo tunasoma hivi:

5. Katika nyakati za kisasa, Yehova amegeuzaji fikira zake kumwelekea ‘Leviathani’ anayetajwa katika Isaya 27:1?

5 “Katika siku hiyo Yehova, kwa upanga wake mgumu ulio mkuu na wenye nguvu, atageuza fikira zake kwenye Leviathani, yule nyoka anayenyiririka, hata kwenye Leviathani, yule nyoka mwenye kupotokapotoka, na yeye kwa uhakika ataua lile dubwana la bahari lililo katika ile bahari.”

Huko nyuma katika nyakati za kale, Yehova alielekeza fikira zake kwenye watekaji wa watu wake. Kama vile tumeona hapo kwanza, kati ya watekaji hao ilikuwako milki ya Babuloni, na pia Misri na Ashuru. (Isaya 27:12,13) Je! wewe unaweza kuona matumizi ya kisasa ya maneno hayo ya mfano yaliyo katika Isaya 27:1? Katika kipindi kile cha karibu-karibu na Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, watu wa Mungu hawakuwa wametekwa na taifa au milki yo yote moja. Lakini Yehova alihitaji kuelekeza fikira kwenye Leviathani mmoja wa mfano, yaani, Shetani Ibilisi. Yeye anajinyiririsha kwa ulaghai katika bahari ambayo ni wanadamu na kutumia vitu vilivyopo duniani ili kuwatia hatarini au kuwafungia njia watumishi wa Mungu.​—Linganisha Ufunuo 17:15.

6, 7. (a) Ni nini katika nyakati za kisasa kikawa kama “vichaka vya miiba na magugu”? (b) Tunaweza kutazamia nini wakati ujao kuyahusu?

6 Mwaka 1919, wakati mabaki ya Israeli wa kiroho walipoanza tena kuuhubiri Ufalme kwa shauku, huo ndio uliokuwa wakati wa Yehova kusema:

“Hakuna hasira kali niliyo nayo mimi. Ni nani atakayenipa vichaka vya miiba na magugu katika pigano? Mimi nitavikanyaga vitu hivyo. Nitaviwasha moto vitu hivyo wakati ule ule mmoja.”​—Isaya 27:4, NW.

7 Baada ya kumalizika kwa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, Ushirika wa Mataifa ulisimamishwa kwa kuukataa Ufalme wa Mungu mikononi mwa Kristo. Tunaweza kulinganisha jambo hilo na kuweka “vichaka vya miiba na magugu” katika njia anayopitia Yehova Mungu, ili viwe kizuizi au kipingamizi asipite. Sasa tengenezo la Umoja wa Mataifa limechukua mahali pa Ushirika huo. Kwa kutumia Umoja wa Mataifa, yale mataifa mbalimbali yaliyo wanachama yanafunua azimio lao la kuuzuia Ufalme wa Kristo unaotangazwa na kwamba yanakusudia kuhifadhi enzi yao wenyewe ya ulimwengu. Katika “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” kwenye Har–Magedoni, yeye atavikanyaga “vichaka vya miiba na magugu” yote, aviponde na mwishowe afanye kana kwamba anavichoma moto, vibaki majivu matupu. Kwa njia hiyo ataonyesha ni nani hasa aliye Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote. Basi, unaweza kuona kwamba hata kama wewe hukuwa hai kati ya Wakristo wapakwa mafuta huko nyuma karibu na Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, huenda ukapatwa na mambo​—upate faida au upate hasara​—katika matokeo ya mwisho ya matukio yenye ulinganifu wa Isaya 27:1.​—Ufunuo 16:14-16; 17:1–18:4.

‘Kutegemea Nguvu za Yehova’

8. Leo mataifa mengi yanategemea nini?

8 Wanachama wa Umoja wa Mataifa wanategemea nguvu zao wenyewe na kutumaini ngome yao iliyofanywa na wanadamu. Hata hivyo, uhakika walioweka katika ngome hiyo umekuwa hauna nguvu za kutosha kuwazuia wasivumbue silaha iliyo hatari zaidi ya zote, silaha iliyo upeo wa silaha zote za kivita, yaani, lile kombora la nyukilia. Inaelekea kwamba si Umoja wa Mataifa unaowazuia kutumia kombora la nyukilia, bali ni woga wa kwamba taifa moja likitumia kombora hilo, yale mengine pia yatalitumia yajilipize kisasi.

9, 10. Kwa sababu gani ni jambo la hekima tutegemee “ngome” nyingine?

9 Ingawa hivyo, kama tulivyoona, jambo hasa linalotisha kukatiza uhai wa mataifa ni “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi.” Mataifa yanaweza kutumainia kufanya nini dhidi ya Mungu Mwenye Nguvu Zote, Yule aliyetia uwezo ule wa kuogofya ndani ya kiini cha kila atomi ya tungamo? Huenda ukawa unasadiki sana kwamba Muumba ni mwenye uwezo mwingi zaidi ya mataifa yakiwa pamoja na silaha zao zote. Wale wanaothamini uhakika huo​—na Mashahidi wa Yehova wanauthamini​—wana njia moja tu ya kufuata. Hiyo imeonyeshwa katika maneno yanayoendelea kusemwa na Yehova

“Ama sivyo na ategemee ngome yangu, na afanye amani pamoja na mimi: amani na aifanye pamoja na mimi.” (Isaya 27:5, NW)

Hakuna shirika lo lote linalotumiwa na wanadamu lililo ngome ya kukimbilia ili kupata usalama au kuzuia vita duniani, na hakika hakuna lo lote lililo ngome ya kukimbiliwa na jamaa za dunia zikakae salama.

10 Inaelekea unajua kwamba watu wengi leo wanajiingiza katika majadiliano makali na vyama vinavyohusika na silaha za nyukilia na upunguzaji wa zana za vita. Sikitisho ni kwamba wanapofanya hivyo fikira zao zinaondoshwa kwenye ukweli wa kwamba vita isiyoepukika ya Mungu Mwenye Nguvu Zote kwenye Har–Magedoni ndiyo inayotisha kuletea mataifa yote uharibifu. Ukithamini ukweli huo, mwendo wa hekima unaopaswa kuchukua ni kwenda upande wa Yehova. Watu wote wanaotafuta usalama wanapaswa kutegemea “ngome” yake, yaani, kuwa kwake na nguvu zisizoweza kwisha. Tengenezo zima la Shetani Ibilisi halitaweza kumshinda Mkristo ambaye ameitegemea “ngome” hiyo.

11. Tunaweza kutumiaje maneno ya Yesu kwenye Luka 14:31-33 tunapoitegemea “ngome” ya Mungu?

11 Yehova na majeshi yake yaliyo chini ya Kapteni, Yesu Kristo, ni kama sasa wako mwendoni wakipiga miguu. Wakiwa wangali Kapteni, Yesu Kristo, ni kama sasa wako mwendoni wakipiga miguu. Wakiwa wangali mbali, mwendo wa akili, hata wa hekima halisi ambao ni lazima mtu achukue, ni kupeleka mapema ujumbe wa amani na kutafuta amani kwa kuona kwamba mambo yamemzidia. Kapteni asiyeshindika wa vikosi vya Yehova alishauri mwendo huo ufuatwe alipokuwa hapa chini duniani. (Luka 14:31-33, NW) Nawe ukichunguza kwa uangalifu aliyoyasema Yesu katika andiko hilo, utaona kwamba alitaja mwelekeo wetu kuhusu “mali” zetu. Tuwe tunaishi katika nchi fulani iliyokwisha kuendelea na yenye usitawi au katika nchi ambayo sasa ndio inaendelea, ambako mtu anatoa jasho kweli kweli ndio apate usalama wa kifedha, inatupasa tuyachunguze maoni yetu kindani. Jiulize hivi: Je! Kweli mimi ninategemea nguvu za Yehova ziwe ndizo ngome yangu, au ninaacha “mali” ziwe na umaana ulio mkubwa sana? Kuhusiana na jambo hilo, tafadhali soma Luka 12:15-21.

12. Kuna ushuhuda gani kwamba watu wengi leo wanaendelea kutegemea nguvu za Yehova?

12 Katika sehemu zote za dunia, maelfu mengi ya Mashahidi wa Yehova wamekwisha kwenda upande wa Yehova bila kuwa na mashaka, wakatafuta amani naye. Wengi wanapanga mambo yao ili watumie saa nyingi kila mwezi kwenye utendaji wa kufanya wanafunzi. Kila mmoja anayejitahidi kweli kweli kumtumikia Yehova yu katika hali ya kuweza kupata ile “amani ya Mungu” iliyoahidiwa, inayopita wazo na ufahamu wote wa kibinadamu. (Wafilipi 4:7) Kukiwa kungali na wakati, wao wanaendelea kusaidia wengine waingie katika mpango huo wenye kuamanika wa Yehova Wa vikosi. Katika maisha yako wewe umeipa nafasi gani kazi hiyo yenye kuokoa uhai?

Kuijaza Mazao “Nchi Yenye Kuzaa”

13. Andiko la Isaya 27:6 linaonyesha ni nini kingeweza kutazamiwa katika wakati wetu?

13 Taifa la Israeli wa kiroho lingetimiza daraka gani kuhusiana na ulimwengu liliporudishwa kwenye kibali cha kimungu baada ya Vita ya Ulimwengu ya Kwanza? Tunaonyeshwa jambo hilo katika maneno haya yenye kutia moyo ya Isaya 27:6:

“Katika siku zinazokuja Yakobo atatia mizizi, Israeli atachanua maua na kwa kweli achipuke; nao wataujaza mazao kweli kweli uso wa ile nchi yenye kuzaa.”

Chunguza ukweli wa maneno hayo leo. Kufanya hivyo kutakuongezea sababu ya kuwa mmoja wa watu wa Mungu. Au, ikiwa tayari ndivyo ulivyo, kutakuongezea sababu ya kuazimia kwa imara zaidi ubaki kati ya waabudu wa kweli hata yakitokea majaribu au matatizo gani.

14. Maneno ya Isaya 27:6 yametimizwaje juu ya watu wa Mungu?

14 Hali kama iliyotabiriwa katika unabii wa Isaya 27:6 imezidi kupatikana kati ya waabudu wa Yehova tangu mwaka 1919, wakati ambao mkusanyiko mkuu wa kwanza wa Mashahidi wa Yehova ulifanywa Cedar Point, Ohio. Kwa mfano, haukupita muda mrefu baada ya hayo kwamba Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi ikaanza kuchapa gazeti jipya layo, The Golden Age, ambalo sasa linaitwa Amkeni! Ilikuwa ni kama kwamba Yuda wa kiroho alikuwa akitia mizizi wakati huo.

15. Waabudu wa kweli walitokezewa taraja gani la kusisimua kuanzia mwaka 1918?

15 Hivyo katika ile miaka ya mwanzo-mwanzo wa kuachiliwa huru na kurudishwa katika kibali cha Yehova, Wakristo wa kweli walianza kuchanua maua kama “upandaji wa Yehova.” (Isaya 61:3, NW) Mwaka 1918, ule mwaka wa mwisho wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, hotuba ile yenye kustaajabisha “Mamilioni Wanaoishi Sasa Huenda Wasife Kamwe” ilitolewa mbele ya watu wote na J. F. Rutherford. Kwa kuwa wakati huo ni wachache tu kati ya wanafunzi waliozaliwa kwa roho wa yule Mfalme mwenye kutawala, Yesu Kristo, waliokuwa wamebaki duniani waifanye kazi iliyowakalia waliyoagizwa rasmi na Mungu, je, hotuba hiyo ilikadiria mambo kupita kiasi?

16. (a) Mabaki walitendaje kwa sababu ya mataraja yaliyokuwa mbele yao? (b) Ni “mazao” gani waliyofurahia, na matokeo yakawa nini?

16 Yehova angetumiaje Wakristo hao kuujaza ‘mazao uso wa ile nchi yenye kuzaa’? Mabaki ya Israeli wa kiroho walichukua hatua ya kwanza, lakini namna gani “mazao” ambayo yangejazwa katika ile nchi yenye kuzaa? Mabaki waliyaona “mazao” hayo, ambayo yalikuwa ni pamoja na zile habari njema za Ufalme wa Yehova uliosimamishwa ukiwa mikononi mwa Kristo, kuwa yenye ladha nzuri sana na yenye kujenga mwili hata wakataka kuwagawia wanadamu wenzao. Yehova alikuwa ametabiri kwamba mnyonge angekuwa elfu na mdogo taifa hodari, na basi ikawa kwamba Mungu hakukosea hesabu. (Isaya 60:22) Baada ya muda mfupi “mkutano mkubwa” wa “kondoo wengine” wa yule Mchungaji Mwema, Yesu Kristo, ulijiunga na mabaki ya Israeli wa kiroho.​—Ufunuo 7:9-17; Yohana 10:16.

17, 18. Wewe unaweza kushuhudia nini juu ya ‘kuujaza mazao uso wa ile nchi yenye kuzaa’?

17 Huenda wewe ukawa unajua jinsi hali ya Ukristo wa kweli ilivyo leo. Sasa Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi ina matawi 94 duniani pote. Sasa makundi yenye kutenda ya Mashahidi wa Yehova yaliyoundwa kwa namna ya tengenezo ni karibu 48,000, nayo yanapatikana katika nchi 203. Sifa yote inamwendea yule Mungu wa kweli, na maendeleo hayo yenye kusifika yanatetea ukweli wa Neno lake lisilokosea, ijapokuwa “ule mwisho,” kama ulivyotabiriwa katika Mathayo 24:14, haujafika.

18 Ndiyo, kuna Wakristo karibu milioni tatu wanaofanya kazi pamoja na Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi duniani pote. Mamilioni hayo ni wale hasa wa “kondoo wengine” wa Kristo, ambao wamekuwa wakiendesha sehemu ile ngumu ya kazi ya kutoa ushuhuda ulimwenguni pote, nayo ‘furaha ya Yehova imekuwa ndiyo nguvu au ngome yao.’ (Nehemia 8:10, NW) Kwa hiyo, kila mmoja wetu leo ana nafasi ya kushibishwa kiroho na kushiriki ‘kuujaza mazao uso wa ile nchi yenye kuzaa.’

19. Ni nini ambalo huenda ukafurahia juu ya ile “nchi yenye kuzaa,” na unalionaje jambo hilo?

19 Tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova hataruhusu kamwe “mazao” ya sasa ya ile “nchi yenye kuzaa,” lile shamba la utendaji wa Mashahidi wake, yaharibiwe. Haitakuwa kamwe kwamba kazi ya mashahidi wake wenye kuhubiri ilifanywa bure! Matunda ya kiroho, au “mazao” yaliyositawishwa na Wakristo wa kweli, ni ya kulisha wote wanaotaka kuyatumia. Baadaye, hiyo itatia ndani mabilioni na wanadamu wafu watakaofufuliwa chini ya Utawala wa Mileani wa Yesu Kristo. Wazia hilo laweza kuwa na maana gani kwako wakati ujao! Baadaye, Waisraeli wengi wa asili wa siku zilizopita watafufuliwa. Huenda ikawa wengine wao walihusika katika utimizo wa kwanza wa unabii ulio katika Isaya sura ya 27. Je! Halingekuwa jambo lenye kusisimua ukiwa hai wakati huo, likikuwezesha kueleza jinsi ulivyoshiriki katika kazi kubwa zaidi ya siku hizi ya ‘kuijaza mazao ile nchi yenye kuzaa’?​—Linganisha Ufunuo 22:2, 3.

Mwendo wa “Leviathani” Wakomeshwa

20. Ni jambo gani linalomngoja “Leviathani” huko mbele, na matokeo yatakuwa nini juu ya enzi kuu ya Mungu?

20 Wakati huo Misri ya mfano, iliyo mfumo mbovu wa sasa ambao Shetani Ibilisi ameutawala akiwa mungu wao, hautakuwapo. Yehova atakuwa amekwisha kuelekeza fikira zake kwenye yule Leviathani wa mfano, yule nyoka mwenye kujinyiririsha, mwenye kupotokapotoka, aliyemo katikati ya bahari ambayo ni wanadamu. Yeye na mataifa, na hata miungano ya mataifa, watakwisha. Hatakuwapo awe mpotoaji wa wanadamu ambao Yesu Kristo alifia. (Isaya 27:1) Ndiyo, Shetani Ibilisi atafungwa katika shimo lisilo na mwisho muda wote wa Utawala wa Miaka Elfu wa Yesu Kristo, Mwana wa Daudi ambaye ndiye Mrithi anayestahili wa Ufalme. Wale Waisraeli wa kiroho 144,000 watakuwa warithi washirika mbinguni pamoja na huyo Simba wa mfano wa kabila la Yuda. (Warumi 8:16, 17; Ufunuo 5:5, 9, 10; 7:1-4) Yehova Mungu Aliye Juu Zaidi atakuwa ameondolewa malawama milele akiwa ndiye Bwana Mwenye Enzi Kuu wa ulimwengu wote. Tengenezo la Yehova la ulimwengu wote katika mbingu na dunia litafurahia kupata amani na upatani wenye kudumu. Mpaka wakati usio na kikomo, hata milele na milele, Yehova atalifurahia sana tengenezo lake la ulimwengu wote lililounganishwa kwa umoja.

Wewe Unaweza Kukumbuka?

◻ Ni kwa sababu gani Wakristo wa kweli waliihisi “hasira kali” ya Yehova mapema katika karne hii, nasi tunaweza kujifunza nini kutokana na tukio hilo lililowapata?

◻ Tofauti na mataifa, ni jinsi gani sisi tunaweza ‘kutegemea Yehova kuwa ngome yetu’? (Isaya 27:5)

◻ “Nchi yenye kuzaa” imejazwaje “mazao” katika wakati wetu? (Isaya 27:6, NW)

◻ Ni utimizo gani wa wakati ujao tunaoweza kutazamia kwa uhakika juu ya Isaya 27:1?

[Picha katika ukurasa wa 17]

Watu wengine wanatumainia kwamba wanadamu watalimaliza lile tisho la silaha za nyukilia, lakini wenye hekima kutoka mataifa yote ‘wanaendelea kutegemea ngome ya Yehova’

[Picha katika ukurasa wa 18]

Ongezeko katika Wakristo wanaolishwa vizuri kiroho linaonekana katika mpanuko wa matawi ya Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi

Hispania

Brazili

Kanada

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki