Usizishiriki Dhambi za Wengine
“Mimi sikuketi na watu wasiosema ukweli; nami siingii niwe pamoja na wale wanaoficha jinsi walivyo.”—ZABURI 26:4, NW.
1. Ni kwa sababu gani Yuda alibadili kusudi lake la kuandikia Wakristo wenzake?
KARNE kumi na tisa zilizopita, mwanafunzi Yuda alikuwa amekusudia kuandikia waamini wenzake juu ya ‘wokovu ambao wao kwa ujumla walikuwa nao.’ Lakini aliuona uhitaji mkubwa wa kuwahimiza ‘wafanye vita vikali kwa ajili ya ile imani ambayo ilitolewa mara moja kwa wakati wote kwa wale watakatifu.’ Kwa sababu gani? Kwa sababu ‘watu fulani wasiomwogopa Mungu’ walikuwa wamejipenyeza kisiri ndani ya kundi na walikuwa ‘wakigeuza fadhili zisizostahilika za Mungu wetu kuwa kisababu cha mwenendo mpotovu.’—Yuda 3, 4, NW.
2. Ingawa inaburudisha kuzungumza wokovu, nyakati nyingine ni lazima jambo gani lifikiriwe kwa sala?
2 Inaburudisha kama nini kuzungumza wokovu walioushiriki wote kwa ujumla! Kuutafakari ujumbe huo kunaleta uradhi mkubwa, nasi tunafurahi sana tunapozitazamia baraka zote zitakazoletwa na wokovu huo. Hata hivyo, ziko nyakati ambapo, badala ya kusema juu ya wokovu, tunakabiliwa na uhitaji wa kufikiria mambo mengine mazito. Hayo yasiporekebishwa, yanaweza kuibomoa imani yetu na kutufanya tuondoke katika shindano la mbio ya uzima. Kama vile onyo la Yuda juu ya kuepuka mwenendo wenye kosa lilivyotolewa kwa uthabiti na mkazo mwingi, vivyo hivyo inakuwa lazima nyakati nyingine Wakristo wafikirie kwa sala mashauri ya Kimaandiko yanayotajwa kwa kutoboa mambo waziwazi.
Dhambi Zetu Wenyewe
3. Kwa sababu gani tunahitaji nidhamu, nayo ipokeweje?
3 Mtunga zaburi Daudi alisema: “Mimi naliumbwa katika hali ya uovu; mama yangu alinichukua mimba hatiani.” (Zaburi 51:5) Sisi sote tumezaliwa tukiwa watenda dhambi. (Warumi 5:12) Mtume Yohana aliandika hivi: “Tukisema kwamba hatuna dhambi, twajidanganya wenyewe, wala kweli haimo mwetu.” (1 Yohana 1:8) Kwa kuwa sisi ni watenda dhambi, kuna nyakati ambazo tunahitaji nidhamu ili turekebishe mwendo wetu. Nidhamu hiyo inatoka kwa Yehova kupitia Neno lake, Biblia, na tengenezo lake. Nidhamu yake inaturekebisha na kutusaidia tutembee kwa kunyooka mbele zake. Ni kama vile mtume Paulo alivyoonelea: “Kila adhabu [nidhamu, NW] wakati wake haionekani kuwa kitu cha furaha, bali cha huzuni; lakini baadaye huwaletea wao waliozoezwa nayo matunda ya haki yenye amani.” (Waebrania 12:11) Kwa sababu ya matunda yenye kuamanika yanayotokana na nidhamu hiyo, hakika tunapaswa kuipokea kwa shukrani.
4. Ni wakati gani inafaa nidhamu itolewe, nayo inaweza kuwa na matokeo gani?
4 Huenda tukapewa nidhamu inayotoka kwa Yehova mara tu tunapoanza kufuata mwendo ambao ungeweza kutuongoza kwenye kosa kubwa zaidi. (Wagalatia 6:1) Nyakati nyingine, huenda nidhamu hiyo ikatujia baada ya sisi kuingia sana katika mwendo wenye kosa. Huenda ikawa lazima nidhamu hiyo iwe kali, kama wakati mtume Paulo alipowahimiza Wakorintho kwa uthabiti wamchukulie hatua mwasherati mmoja katika kundi. (1 Wakorintho 5:1-5) Vyo vyote iwavyo, nidhamu hiyo inatolewa ili mtenda kosa aweze kutubu, ageuke, na kuondoka bila kuyumbayumba katika tamaa zenye dhambi zinazoingiza mtu ndani ya kosa zito. (Linganisha Matendo 3:19.) Watumishi wa Yehova wanashukuru kwa kupewa nidhamu ya namna hiyo, sawa na vile mtu yule aliyekemewa katika kundi la Korintho wa kale alivyofaidika, na inaonekana alirudishwa pia awe na ushirika wenye upendo pamoja na kundi.—2 Wakorintho 2:5-8.
5. Kwa kawaida Wakristo wanaohusika katika dhambi nzito wanafanya nini?
5 Wingi mkubwa wa wale waliojiweka wakfu kwa Yehova wanaujua sana uhitaji wa kutembea kwa njia iliyonyooka mbele za Mungu. Ikitukia kwamba wamehusika katika dhambi nzito, wao wanauacha upesi mwendo huo mbaya, wanawaendea wazee waliowekwa rasmi, na kuonyesha ushuhuda wa toba ya kweli. (Yakobo 5:13-16) Uhakika wa kwamba ni wachache kati ya Mashahidi wa Yehova wanaotengwa na ushirika kila mwaka unashuhudia kwamba wao wanachukia yaliyo mabaya na kutamani kutenda yaliyo mema.—Zaburi 34:14; 45:7.
Dhambi za Wengine
6, 7. Watu fulani wanaotenda kosa wanajaribu kuwavutaje wengine?
6 Hata hivyo wengine ambao inaelekea kuwa wanapenda mambo yanayofaa wanaonekana kuwa wameruhusu mioyo yao iwadanganye, kwa maana hawaonyeshi kuwa wanachukia yaliyo mabaya. (Zaburi 97:10; Amosi 5:15) Matokeo ni kwamba wanahusika katika kutenda mambo yenye dhambi na hawaendelezi pigano la kutenda yanayofaa. Nyakati nyingine, huenda hata wakafikia hatua kubwa kuliko hiyo, wakitafuta kuhusisha wengine katika mwendo wao wenye dhambi. Ni jambo la maana kama nini tukatae madokezo yao!—Linganisha Mithali 1:10-15.
7 Nyakati nyingine wale wanaoelekea kutochukia mabaya wanasema maneno yaliyo laini sana mpaka hamu ya kutenda yasiyofaa inasitawi mioyoni mwa wale wanaowasikiliza. Huenda wakawatia moyo wajiingize katika mwenendo usio wa adili au katika kitendo fulani kinachoukaribia mwenendo unaokataliwa na Mungu. Au huenda mtu akahimizwa ahusike katika hali inayoweza kumtia katika hatari ya kiroho. Wale wanaojaribu kubembeleza wengine kwa njia hiyo huenda wakadai kwamba Yehova ni Mungu mwenye upendo atakayeturehemu tutendapo dhambi. Hila hiyo ya moyo inaweza kusababisha madhara ya daima. (Yeremia 17:9: Yuda 4) Hakika inatupasa ‘tuzuie mguu wetu usiende katika mapito yao’!—Mithali 1:15.
Kuzishiriki Dhambi za Wengine
8. Ni maulizo gani yanayohitaji kufikiriwa?
8 Lakini namna gani tukitambua kwamba mwendo fulani tunaodokezewa tufuate haufai? Je! kuukataa tu kunaonyesha bila shaka lo lote kwamba sisi hatuna daraka zaidi katika jambo hilo? Ikiwa tunajua kwamba wenye kudokeza kwamba sisi tutende kosa wanalitenda wao wenyewe, inatupasa tufanye nini?
9. Kwa sababu gani huenda wengine wasiripoti makosa yaliyofanywa na wengine, lakini kwa sababu gani hilo ni jambo zito?
9 Huenda wengine wanaojua habari za kosa lililotendwa wakawa na maelekeo ya kunyamaza wasiwaambie wale walio na daraka la kwanza la kutunza usafi wa kundi. Kwa sababu gani? Labda hawataki kuonwa kuwa wahaini. Au, kwa sababu ya kujidanganya kwamba wakisema wanakuwa wasio washikamanifu, huenda wakakaa kimya au wakawaambia wale tu wanaoahidi kuitunza habari hiyo iwe siri. Kufanya hivyo ni jambo zito sana. Kwa sababu gani? Kwa sababu kunaweza kufanya mtu azishiriki dhambi za wengine.
10, 11. (a) Mtume Yohana alisema nini juu ya kuzishiriki dhambi za wengine? (b) Ikiwa tumejua kwamba mshiriki wa kundi amefanya kosa, tunaweza kujiuliza nini?
10 Mtume Yohana alionyesha kwamba inawezekana kushiriki dhambi za mtu mwingine. Aliandika hivi: “Kila apitaye cheo, wala asidumu katika mafundisho ya Kristo, yeye hana Mungu. . . . Mtu akija kwenu, naye haleti mafundisho hayo, msimkaribishe nyumbani mwenu, wala msimpe salamu. Maana yeye ampaye salamu azishiriki kazi zake mbovu.” (2 Yohana 9-11) Mwasi-imani mwenye kuacha “mafundisho ya Kristo” hangekuwa mshiriki anayefaa, naye Mkristo mshikamanifu angeepuka kuwa mshiriki katika uovu wake kwa kukataa hata kumpa salamu.
11 Kwa kuwa ndivyo ilivyo kwa habari ya mwasi-imani, hakika hatungetaka kuwa washiriki katika uovu wa wengine ambao tumejua wamefanya vitendo visivyo vya adili. Namna gani, basi, tukijua kwamba mshiriki wa kundi amekuwa mwivi au mlevi? Tukishindwa kumtia moyo atafute msamaha wa Yehova na kuungama dhambi yake kwa wazee, je, sisi tunakuwa kabisa bila lawama? Hapana, kwa maana tuna daraka zito.
Usafi na Ulinzi Unahitajiwa Sana
12. Kwa sababu gani tuhangaikie usafi wa kiroho wa kundi?
12 Ni lazima sisi mmoja mmoja tuhangaikie usafi wa kiroho wa kundi. Jambo hilo lilikaziwa vizuri sana kama nini wakati wahamishwa Wayahudi walipokaribia kuondoka Babuloni katika karne ya sita K.W.K.! Amri waliyopewa na Mungu ilisema: “Nendeni zenu, nendeni zenu, tokeni huko, msiguse kitu kichafu; tokeni kati yake [Babuloni]; iweni safi ninyi mnaochukua vyombo vya [Yehova].”—Isaya 52:11.
13. Yuda alionyeshaje kwamba ni lazima tuhangaikie kulinda watu wa Yehova na watenda makosa?
13 Ni lazima pia tuhangaikie kulinda watu wa Yehova na wale wanaotafuta kuwashawishi waingie katika makosa. “Watu wasiomwogopa Mungu” siku za Yuda walijaribu ‘kugeuza fadhili zisizostahilika za Mungu kuwa kisababu cha mwenendo mpotovu,’ lakini mwanafunzi huyo mshikamanifu alichukua hatua kuonya waamini wenzake na hivyo kuwalinda. Aliwakumbusha juu ya mifano yenye maonyo iliyotokezwa na Waisraeli wasio waaminifu, malaika wasiotii, na wengine. Soma barua yake iliyoongozwa na Mungu, nawe utaona kwamba Wakristo washikamanifu hawawezi kujikalia kitako tu wakati usafi wa kundi unapoelekea kuharibiwa au watu wa Mungu wanapohitaji kulindwa na watu wasiofuata adili wenye makusudio machafu.
14. Mtenda kosa asipoungamia wazee, andiko la Zaburi 26:4 linaweza kutusaidiaje tuamue la kufanya?
14 Hata hivyo, namna gani kama tumemtia moyo mtu aliyetenda kosa atafute msamaha wa Mungu na kuungamia wazee, lakini yeye anaendelea kuahirisha au haoni uhitaji wa kuchukua hatua hizo. Je! tunaweza kuliachilia hivyo jambo hilo? Huenda wengine wakawaza kwamba hawataki kuhusika. Huenda wasitake kupoteza urafiki wa mwenye kukosa. Na huenda wasitake kufikiriwa kuwa watu wanaofunua siri kwa kuwaambia wazee. Lakini ni kosa kuwaza hivyo. Mtunga zaburi Daudi alisema: “Mimi sikuketi na watu wasiosema ukweli; nami siingii niwe pamoja na wale wanaoficha jinsi walivyo.” (Zaburi 26:4, NW) Hakika, basi, sisi hatungetaka kuwa washiriki wa makosa ya “wale wanaoficha jinsi walivyo.”
15. Andiko la Mambo ya Walawi 5:1 linaonyesha tuna daraka la kufanya nini tukiisha kumpa mwenye kukosa wakati unaotosha wa kuwafikia wazee awaeleze kosa lake?
15 Basi, baada ya sisi kumpa mtu yule kiasi kinachotosha cha wakati awafikie wazee kuwaeleza kosa lake, ni daraka letu mbele za Yehova kutoishiriki dhambi yake. Tunahitaji kuwajulisha waangalizi wenye madaraka kwamba mtu huyo amefunua kosa zito linalostahili kuchunguzwa nao. Jambo hilo lingepatana na andiko la Mambo ya Walawi 5:1, linalosema: “Na mtu awaye yote akifanya dhambi, kwa kuwa ameisikia sauti yenye kuapisha, naye akawa ni shahidi, kwamba aliona au kujua, asipolifunua neno lile, ndipo atakapochukua uovu wake mwenyewe.” Bila shaka, ni lazima tuepuke kutenda haraka haraka kwa kudhania tu kwamba kosa limefanywa.
16. Ni jambo gani lililo la maana kuliko ushikamanifu kwa rafiki anayekataa kufunulia wazee waliowekwa rasmi kosa lake zito?
16 Katika ulimwengu wa leo, ni zoea la kawaida kufunika makosa ya wengine. Watu wengi wanakuwa mabubu kama jiwe kwa habari ya kufunua makosa yaliyotendwa na wengine ili yajulikane na wanaopaswa kuyajua. Mtu anatakwa awe na nguvu za utu wa Kikristo ndipo aweze kuwajulisha wazee waliowekwa rasmi juu ya dhambi nzito ya mwamini mwenzake. Lakini ikiwa tunataka kupata upendeleo wa Yehova, ni lazima tuepuke kuacha urafiki wa kibinafsi utupofushe kujifanya hatuoni kosa la mtu mwingine. Uhusiano wetu na Mungu ni wa maana kubwa kuliko ushikamanifu kwa rafiki aliye na hatia ya kutenda kosa zito na mwenye kukataa kuwafunulia jambo hilo wazee waliowekwa rasmi.
Tatizo Linalopasa Kufikiriwa na Wote
17. Ni jambo gani linaloonyesha kwamba vijana fulani walio miongoni mwetu wanahitaji kujihadhari wasizishiriki dhambi za wengine?
17 Nyakati nyingine tatizo la kuzishiriki dhambi za wengine linakuwa kati ya vijana fulani walio miongoni mwetu. Wanakaa wamenyamaza na kukataa kuambia wale wanaopaswa kujulishwa wakati wengine wanapofanya mambo ambayo yangeweza kuliharibu kundi na kulifanya lipoteze upendeleo wa Yehova. Ni jambo la kawaida sana katika mifumo ya shule za kilimwengu kufunika makosa ya wengine. Lakini wakati maoni hayo yanapoenea na kulifikia kundi, matatizo mengi yanaweza kutokea. Hata kumekuwa na ripoti zenye kuonyesha kwamba vijana wanaungana pamoja ili waingie katika mwenendo mbaya huku wakiapishana kwamba kila mmoja wao atatunza siri. ili wazee na wazazi wasijue utendaji huo. Kujiachilia wafuate mkazo huo wa vijana wa rika lao na tamaa ya kutaka wakubaliwe na kikundi chao kumewaletea maumivu mengi ya moyoni vijana hao, wazazi wao, na wengine kundini wakati makosa yao yamefichuliwa. Ni lazima tukumbuke kwamba hakuna jambo lililofichwa ambalo halitafunuliwa, na moja la madaraka yetu ya msingi mbele za Yehova ni kusaidia kutunza usafi wa tengenezo lake.—Luka 8:17.
18. Inawapasa wazazi Wakristo wafanye nini watoto wao wakikosa?
18 Watumishi wote wa Yehova wanapaswa kujiangalia sana wasizishiriki dhambi za wengine. Wazazi wengine wanajaribu kutetea mwenendo mbaya wa watoto wao, wakijitahidi kuwakinga. Lakini haiwapasi wazazi Wakristo kufuata mwelekeo wa kwamba kila mtu anawaonea watoto wao wakati wanapokosa. Badala ya hivyo, wazazi wanaoogopa Mungu wanapaswa kusaidia wazao wao wanaotenda makosa wapokee, wakubali, na wafaidike kutokana na nidhamu yo yote inayohitajiwa ambayo imeonyeshwa katika Neno la Mungu.
19. (a) Kwa habari ya dhambi nzito, waume na wake Wakristo walio wenzi wa ndoa wanahitaji kujiangalia na nini? (b) Ni lazima wazee wafanye nini mmoja wao au mtumishi wa huduma akitenda dhambi nzito?
19 Pia waume na wake Wakristo wanahitaji kujiangalia ili wasivunje sheria za Mungu kwa kufunika dhambi nzito za wenzi wao. Inawapasa wakumbuke kisa cha Anania na Safira, waliotunga hila lakini ikawa kazi bure walipojaribu kufunika dhambi nzito. (Matendo 5:1-11) Ni lazima wazee pia au watumishi wa huduma wawe chonjo wasilindane wao kwa wao ikiwa mmoja wao ametenda dhambi nzito ambayo ingeweza kufanya atengwe na ushirika. Imewapasa waifuate kanuni iliyoonyeshwa na Paulo, aliyeandika hivi: Usimwekee mtu mikono kwa haraka, wala usizishiriki dhambi za watu wengine. Ujilinde nafsi yako uwe safi.”—1 Timotheo 5:22.
Hekima ya Kuendeleza Hali ya Kutolaumika
20. Badala ya kufunika au kushiriki dhambi kubwa za wengine, inatupasa tufanye nini?
20 Haiwapasi watumishi wa Yehova washiriki wala waige njia mbaya za ulimwengu huu. Alipokuwa akimwandikia Gayo, mtume Yohana alisema: “Mpenzi, usiuige ubaya, bali uige wema. Yeye atendaye mema ni wa Mungu, bali yeye atendaye mabaya hakumwona Mungu.” (3 Yohana 11) Ni vizuri kama nini kuongozwa na Neno la Mungu lililo hakika na hivyo kufanya mema! Basi, badala ya kufunika au kushiriki dhambi kubwa za wengine, azimio letu limepasa liwe kung’aa kama vimulikaji, tukiwa watu wasio na lawama wala hatia. (Wafilipi 2:14, 15) Kila mtumishi wa Mungu ana daraka la kutunza usafi wa kundi, huku yeye binafsi akibaki bila waa. (2 Petro 3:14) Lakini namna gani kama unafadhaika kwa sababu unatia shaka juu ya kama jambo fulani lililotendwa na mtu fulani lilifaa? Inakupasa ujione huru kusema na wazee upate mwongozo juu ya mwendo unaofaa kufuatwa.
21. (a) Upendo alio nao Kristo kwa kundi lake unakuwaje mfano kwetu? (b) Kwa habari ya makosa ya wengine, inatupasa sisi tubebe daraka gani?
21 Upendo wetu kwa tengenezo la Yehova unapasa kuwa kama ule ambao Yesu Kristo alimwonyesha bibi-arusi wake wa kiroho, lile kundi. Yeye alilipenda “[kundi], akajitoa kwa ajili yake; ili makusudi alitakase na kulisafisha kwa maji katika neno; apate kujiletea [kundi] tukufu, lisilo na ila wala kunyanzi wala lo lote kama hayo; bali liwe takatifu lisilo na mawaa.” (Waefeso 5:25-27) Vivyo hivyo, upendo wetu kwa tengenezo la Yehova unapasa utusukume kufanya yote tuwezayo tutunze usafi walo. Tusifanye kamwe jambo lo lote limvunjie heshima Mungu wala tengenezo lake wala tusiachilie makosa ya wengine kundini. Bali, acheni tuwatie moyo watenda makosa wanyooshe mwenendo wao na kutafuta msaada wa wazee. Wakishindwa kufanya hivyo katika muda unaotosha, sisi na tuchukue daraka letu la kuwajulisha waangalizi waliowekwa rasmi. Kwa njia hiyo, tutaepuka kuwa washiriki katika dhambi za wengine na kuchukua lawama fulani kwa mwenendo wao mbaya.
22. (a) Ili tuje tupate wokovu, ni lazima tufanye nini? (b) Ni maulizo gani yanayobaki yafikiriwe?
22 Wokovu ambao sisi kwa ujumla tunaushiriki ni hazina isiyoweza kuwa na kifani. Ili tuufikie ni lazima tuendelee kutembea mbele za Yehova kwa njia iliyonyooka. Basi, acheni tusaidiane kufanya hivyo, bila kuzishiriki kamwe dhambi za wengine. Yehova ameandaa kwa upendo mpango wa kitengenezo ili kutusaidia katika jitihada hizo, nao wazee waliowekwa wanashiriki sehemu ya maana katika mpango huo. Lakini wao wanafuataje mfano wa Yehova na Mwanaye, yule Mchungaji Mwema? Ni usaidizi gani ambao wazee wanaweza kutupa sisi tunaposonga kwenye njia ya uzima? Makala inayofuata itajibu maulizo hayo.
Wewe Unaweza Kukumbuka?
◻ Inakupasa uioneje nidhamu?
◻ Mwamini mwenzako akikuambia kwamba ametenda dhambi nzito, inakupasa umhimize afanye nini?
◻ Imekupasa ufanye nini ukijua kwamba mtenda kosa hakuwaungamia dhambi yake wazee waliowekwa rasmi?
◻ Tuwe wazee, waume na wake, au watoto, tunaweza kuepukaje kuzishiriki dhambi za wengine?
[Picha katika ukurasa wa 19]
Mtume Yohana alitoa onyo la kujihadhari na kuzishiriki dhambi za wengine