“Yule Neno Alikuwa Pamoja na Mungu, na Yule Neno Alikuwa . . . ”?
NI VIFUNGU vichache katika Biblia vimefikiriwa sana katika makanisa ya Jumuiya ya Wakristo kuliko andiko la Yohana 1:1. Maneno ya andiko hilo katika tafsiri nyingi za Biblia yanafanana na yale ya Tafsiri ya Union Version: “Hapo mwanzo kulikuwako Neno, naye Neno alikuwako kwa Mungu [ὁ θεός], naye Neno alikuwa Mungu [θεός].”
Wengi wanaoukubali Utatu wanaonyesha kifungu hicho kuunga mkono fundisho lao. Hata hivyo, mstari huo umefasiriwa kwa njia tofauti katika tafsiri fulani, wenye kutafsiri wakikiri kwamba Kigiriki cha kwanza kinafunua tofauti fulani iliyofichika katika fasiri mfano wa ile iliyotajwa juu.
Mwaka 1984 kulitokea katika Kiingereza tafsiri moja iliyofanywa kutoka Kijeremani na mwanachuo Ernst Haenchen (Das Johannes-evangelium. Ein Kommentar). Inafasiri Yohana 1:1 hivi: “Hapo mwanzoni alikuwako Logos, na Logos alikuwa pamoja na Mungu, na wa kiungu [wa jamii ya waungu] alikuwa Logos.”—John 1. A Commentary on the Gospel of John Chapters 1-6, kilichotafsiriwa na Robert W. Funk, ukurasa 108.
Kinapolinganisha Mwanzo 1:1 na mstari wa kwanza wa Injili ya Yohana, kitabu hicho cha maelezo kinasema hivi: “Hata hivyo, Yohana 1:1 linaeleza juu ya kitu fulani kilichokuwa kimekwisha kuwako katika wakati wa zamani kabisa; jambo la kustaajabisha ni kwamba kitu hicho si ‘Mungu.’ . . . Kwa njia hiyo Logos (nasi hatuna neno ama katika Kijeremani ama Kiingereza linalolingana na maana mbalimbali za neno hilo la Kigiriki) anainuliwa juu mno mpaka kufanya hivyo kunakaribia kuwa jambo lenye kuudhi. Neno hilo linavumilika kwa sababu tu maneno yanaendelea kusema ‘na Logos alikuwa katika kuwapo kwa Mungu,’ ndiyo kusema, katika muungano wa uhusiano wa kindani, wa kibinafsi pamoja na Mungu.”
Je! inasikika kama mwanachuo Haenchen alitambua katika Kigiriki tofauti fulani kati ya Mungu na Logos, au Neno? Maneno ya mtungaji yanayofuata yanakaza fikira juu ya uhakika wa kwamba katika ile lugha ya kwanza hakuna neno la kudhihirisha kitu kinachosemwa lililotumiwa pamoja na neno theos, au mungu, katika kile kifungu cha mwisho cha maneno. Mtungaji huyo anaeleza hivi:
“Ili kuepuka kuelewa vibaya, inaweza kuongezewa hapa kwamba maneno haya θεός [the·osʹ] na ὁ θεός [ho the·osʹ] (‘mungu, wa kiungu’ na ‘Mungu’) hayakuwa neno moja katika kipindi hicho. Kwa hiyo Philo ameandika hivi: λόγος [Logos] maana yake ni θεός (‘wa kiungu’) wala si ὁ θεός (‘Mungu’) kwa kuwa logos si Mungu katika ile maana yenyewe kabisa. . . . Kwa namna inayofanana na hiyo, Origen, pia, anafasiri hivi: Huyo mwandikaji wa Injili hasemi kwamba logos ni ‘Mungu,’ bali anasema tu kwamba logos ni ‘wa kiungu.’ Kwa kweli, kulingana na mtungaji wa ule wimbo wa kidini [katika Yohana 1:1], sawa na kulingana na yule mwandikaji wa Injili, Baba peke yake ndiye aliyekuwa ‘Mungu’ (ὁ θεός; linganisha 17:3); ‘Mwana’ alikuwa mdogo kwake (linganisha 14:28). Lakini hilo ni jambo linalodokezwa tu katika kifungu hicho kwa sababu hapo mkazo ni juu ya ukaribiano wa mmoja na mwenzake.”
Halafu Haenchen anasema: “Katika imani ya Wayahudi na Wakristo ya Mungu mmoja tu iliwezekana sana kusema juu ya waungu waliokuwako kandokando na wakiwa chini ya Mungu lakini ambao hawakulingana naye. Flp 2:6-10 linathibitisha hivyo. Katika kifungu hicho Paulo anaonyesha mtu wa kiungu aliye hivyo tu, wala si zaidi ya hapo, ambaye baadaye akawa mwanadamu Yesu Kristo. . . . Hivyo, katika Wafilipi na pia Yohana 1:1 unaohusika si uhusiano wa usemi kati ya wawili walio katika mmoja, bali ni muungano wa kibinafsi wa watu wawili.”—Kurasa 109, 110.
Kwa hiyo, badala ya kusema kwamba Logos (Yesu) alikuwa pamoja na Mungu na alikuwa Mungu, andiko la Yohana 1:1 linaeleza kwamba Logos alikuwa pamoja na Mungu Mwenye Nguvu Zote na alikuwa wa kiungu, au alikuwa kimungu.