Wale Wanyama wa Kitabu cha Ufunuo—Sababu Gani Usome Habari Zao?
UFUNUO! Hilo ni moja la majina yenye kuvuta akili ambalo kitabu cha mwisho cha Biblia kimepewa. Kitabu hicho kimejawa na masimulizi yenye uhai mwingi kuhusu viumbe, na yenye kutokeza zaidi kati ya hayo ni yale ya joka na . wanyama-mwitu watatu. Watu wengine wanawaona wanyama hao kuwa wa kuogopesha sana. Wengine wanayapuuza kuwa ni mambo tu yaliyowaziwa na mwanamume mzee. Basi, kwa sababu gani wewe usome juu ya wale wanyama wa kitabu cha Ufunuo? Kwa sababu furaha yako inahusika.
Ni kweli kwamba mtume Yohana alikuwa mwanamume mzee wakati alipoandika kitabu cha Ufunuo karibu miaka 1,900 iliyopita. Hata hivyo, je, hiyo inamaanisha kwamba wanyama kinachosimulia walikuwa ni mauzauza ya akili ya mtu mzee tu? Hapana, na siye Yohana aliyekuwa mzee wa kwanza kupata njozi kama hizo. Mwanamume jina lake Danieli aliona pia njozi za wanyama katika umri wa uzee wake, na njozi hizo zilithibitika kuwa unabii sahihi wa mbadiliko katika serikali ya kibinadamu. (Danieli, sura 7 na 8) Zaidi ya hilo, Yesu Kristo mwenyewe alimwona Danieli kuwa ameongozwa kwa roho ya Mungu, akamwita nabii na kutaja maneno ya maandishi yake.—Mathayo 24:15.
Yesu alionyesha kwamba mitume wake wangepokea maagizo zaidi ya kimungu baada ya yeye kufa. (Yohana 16:12, 13) Na kwa 1 kuwa sehemu nyingi za kitabu cha Ufunuo „ zimetimizwa kwa njia nzuri sana, tunaweza kuwa na uhakika kwamba njozi za mtume Yohana za wale wanyama wa kitabu cha Ufunuo ziliandikwa kwa uongozi wa roho ya Mungu pia.—2 Timotheo 3:16.
Utangulizi wa kitabu cha Ufunuo unasema: “Ufunuo kupitia Yesu Kristo, ambao Mungu alimpa . . . Naye alimtuma malaika wake akautoa katika ishara kupitia kwake kwa mtumwa wake Yohana.” (Ufunuo 1:1, NW) Kwa hiyo, mifano katika kitabu cha Ufunuo, kutia wale wanyama, ni usemi wa mfano, si halisi. Hakuna haja ya kuogopa kusoma juu yao. Wanyama hao wa mfano wanawapa Wakristo maarifa ya maana sana, na kuwawezesha kuhifadhi uhusiano wao na Mungu. Kwa hiyo, mtume Yohana angeweza kuandika hivi: “Mwenye furaha ni yeye asomaye kwa sauti kubwa na wale wanaoyasikia maneno ya unabii huu, na wanaoyashika mambo yaliyoandikwa humo; kwa maana wakati uliowekwa u karibu.”—Ufunuo 1:3, NW.