Ukamilifu wa Ayubu—Ni Nani Anayeweza Kuuiga?
“Yeye atanipima katika mizani zilizo sahihi naye Mungu atapata kujua ukamilifu wangu.”—AYUBU 31:6, Biblia ya New World Translation.
1. Kwa sababu gani ni vizuri kufikiria mfano wa Ayubu, na ni maulizo gani yanayotokezwa?
AYUBU alikuwa na uhakika juu ya ukamilifu wake na kwa hiyo akakubali kuchunguzwa na Mungu. Mfano wake unaweza kuwa kitia-moyo kikubwa kwetu leo, hasa wakati huu ambapo Shetani Ibilisi anajaribu sana kuvunja ukamilifu wa wote wanaomtumikia Mungu. (1 Petro 5:8) Kwa kutambua hivyo, mwanafunzi Yakobo alisema ‘tuchukue manabii kama kielelezo cha kupatwa na uovu na kujizoeza subira,’ hasa Ayubu. (Yakobo 5:10, 11, NW) Lakini ni nani anayeweza kuiga ukamilifu wa Ayubu? Je, sisi tunaweza? Ni kwa njia zipi Ayubu alituwekea mfano wa kushika ukamilifu?
2. (a) Jina Ayubu lina maana gani? (b) Ni jambo gani lililotimizwa na mwendo wa Ayubu wa kushika ukamilifu?
2 Jina Ayubu linamaanisha “kitu cha kutendwa uhasama,” na hakika hivyo ndivyo yeye akawa. Lakini wakati Yehova alipomruhusu Shetani afanye kulingana na ombi lake kisha akauondoa ukigo wa ulinzi uache kumzunguka Ayubu, hakuna jambo ambalo Shetani angeweza kufanya auvunje ukamilifu wa Ayubu kwa Mungu. (Ayubu 1:1–2:10) Kwa njia hiyo Ayubu aliandaa jibu la kutolea laumu la Shetani kwamba yeye angeweza kugeuza mtu ye yote aache kumtumikia Mungu. (Mithali 27:11) Kwa mwendo wake wa kushika ukamilifu, Ayubu ni kama alikuwa akitolea ulimwengu mzima tangazo la kwamba, ‘Shetani, wewe ni mwongo mwenye kudharaulika, kwa sababu Yehova ni Mungu wangu, nami nitashika ukamilifu kuelekea yeye hata kutokee nini!’—Ayubu 27:5, NW.
Wale Walio Kama Ayubu
3. Ni nani aliyelindwa mbinguni, na ni maulizo gani yaliyotokezwa juu yake?
3 Ni jambo la maana kuangalia kwamba suala kati ya Yehova na Shetani lilihusu ulimwengu mzima, kutia na makao ya kiroho. “Uzao” ulioahidiwa alikuwa kule mbinguni akiwa amezungushiwa ukigo kwa ulinzi wa Yehova, na kupitia kwake Mungu alinuia kutimiza makusudi Yake makuu. (Mwanzo 3:15) Hata hivyo, wakati ‘ukigo wa ulinzi’ ungeondolewa, je, huyo kweli angeiga ukamilifu wa Ayubu? Je, angeonyesha kwamba mwanadamu mkamilifu, kama alivyokuwa Adamu, angeweza kushika ukamilifu usiopunguka kuelekea Mungu? (1 Wakorintho 15:45) Shetani alifanya matayarisho ya kuutia “uzao” huo kwenye jaribu kali sana ukiisha kutokea duniani.
4. (a) Ni nani akawa ndiye kitu kikuu cha kutendwa uhasama na Shetani, nasi tunajuaje Mungu aliondoa ulinzi wake kwa mtu huyo? (b) Yesu alimwandalia Yehova nini?
4 Yesu Kristo akawa ndiye “uzao” uliopelekwa kutoka mbinguni. Hivyo akawa ndiye hasa wa kuelekezewa fikira na Shetani, ndiyo, kitu kikuu cha kutendwa uhasama na Shetani. Kuonyesha ushuhuda wa kwamba Yehova alikuwa ameondoa ukigo wa ulinzi wake, Kristo alipiga kelele hivi alipokuwa juu ya mti wa mateso: “Mungu wangu, Mungu wangu, mbona umeniacha?” (Mathayo 27:46; Zaburi 22:1) Ingawa alihisi sana kwamba Mungu alikuwa ameondoa ulinzi wake, Yesu alifanya kama Ayubu kwa ‘kutokufanya dhambi, wala hakumwazia Mungu kwa upumbavu.’ (Ayubu 1:22) Yeye alimwiga Ayubu, akashika ukamilifu usiopunguka kuelekea Mungu, na hivyo akathibitisha kwamba ‘hapana mmoja aliyekuwa kama yeye duniani.’ (Ayubu 1:8) Hivyo ni katika Yesu peke yake Yehova Mungu ana jibu kamili na la milele kwa shtaka la uwongo la Shetani la kwamba Mungu hawezi kuweka duniani mwanadamu atakayebaki akiwa mwaminifu kwake chini ya jaribu lililo kubwa zaidi.
5. (a) Shetani anaendelea kufanya nini? (b) Shetani alifanya nini alipoondolewa mbinguni?
5 Bado akitaka jibu zaidi, Shetani anaendelea kuwashtaki ndugu za kiroho wa Yesu, ambao, wakiwa pamoja na Yesu, ndio wanaokuwa “uzao” wa tengenezo la Mungu lililo mfano wa mwanamke. Wakati inapoeleza juu ya kusimamishwa kwa Ufalme mbinguni, Biblia inasema hivi juu ya Shetani: “Ametupwa chini mshitaki wa ndugu zetu, yeye awashitakiye mbele za Mungu wetu”! Lakini, Shetani hashtaki tu na kuachia hapo, bali anatokeza shambulio lenye uhasama! Biblia inaeleza kwamba baada ya yeye kuporomoshwa kutoka mbinguni, “joka [Shetani] akamkasirikia yule mwanamke, akaenda zake afanye vita juu ya wazao wake waliosalia, wazishikao amri za Mungu, na kuwa na ushuhuda wa Yesu.”—Ufunuo 12:7-12, 17.
6. (a) Ni akina nani leo wanaoongoza kazi ya kuhubiri, na ni akina nani wamejiunga nao? (b) Shetani anajaribu kuwafanya nini wote hao?
6 ‘Wazao wa mwanamke waliosalia’ ni Mashahidi wapakwa mafuta wa Yehova waliobaki duniani leo. Wao ndio wanaoongoza “kuwa na ushuhuda wa Yesu,” wakitangaza waziwazi ulimwenguni pote kwamba sasa yeye amekwisha kutawazwa kuwa Mfalme na karibuni ataukomesha mfumo huu wa mambo usio mwadilifu. (Mathayo 24:14; Danieli 2:44) Lakini hawako peke yao hata kidogo! Sasa mkutano mkubwa sana wa watu zaidi ya milioni tatu wamejiunga nao kuwa tengenezo lenye umoja la washika ukamilifu ulimwenguni pote. Washika-ukamilifu wote hao, pia, wamekuwa vitu vya kuletewa mateso yasiyo na mwisho ya Shetani, naye Yehova Baba yao wa kimbingu anafurahia ukamilifu wao.—2 Timotheo 3:12; Mithali 27:11.
7. Kwa sababu gani tunaweza kuwa na tumaini hakika tunapokabili mashambulio ya Shetani?
7 Hakika inafaa kutambua kwa uzito kwamba, kama ilivyokuwa kwa Ayubu, fikira mbovu za Shetani zimeelekezwa juu yetu sisi tunaojaribu kushika ukamilifu kuelekea Mungu. Lakini, hatuhitaji kutiwa kasirani na jambo hilo. Kwa sababu gani? Kwa sababu “Yehova ni mwororo sana katika upendo wenye shauku na ni mwenye rehema,” tena “hatakupungukia wala kukuacha.” (Yakobo 5:11, NW; Kumbukumbu la Torati 31:6, UV) Ndiyo, Yehova atatutegemeza. “Yeye ni ngao kwao waendao kwa ukamilifu,” Biblia inasema. (Mithali 2:7) Ingawa hivyo, hiyo haimaanishi kwamba Yehova hataturuhusu tujaribiwe. Atafanya hivyo, sawa na alivyomruhusu Ayubu ajaribiwe. “Ila Mungu ni mwaminifu,” akasema mtume Paulo, “ambaye hatawaacha mjaribiwe kupita mwezavyo; lakini pamoja na lile jaribu atafanya na mlango wa kutokea, ili mweze kustahimili.”—1 Wakorintho 10:13.
Tunapokuwa Chini ya Jaribu
8. Mfano wa Ayubu unaweza kutufaidije leo?
8 Mfano wa Ayubu wa ukamilifu unaweza kutusaidia hasa tunapokabili majaribu makali. Ayubu alitaabika sana hata akajisikia ni afadhali afe na kufichwa katika Sheoli, kaburi la ujumla la wanadamu. (Ayubu 14:13) Watu fulani wamejisikia ivyo hivyo leo, wakasema kwamba wangeweza kuhusianisha hali yao na ile ya Ayubu wakati alipokuwa akitaabika sana. Labda pindi fulani wewe umejisikia ivyo hivyo. Kwa kweli, kusoma habari za kutaabika kwake kunaweza kuwa kama kupokea kitia-moyo kutoka kwa rafiki ambaye amepitia jaribu lililo kali zaidi ya lile letu wenyewe. Kujua kwamba mtu mwingine amevumilia, naye anafahamu, hakika kunatusaidia sisi pia tuvumilie.
9. Tunafaidiwaje na ushikaji ukamilifu wa wengine?
9 Kwa kuwa anatambua mahitaji yetu, Yehova aliagiza kitabu cha Ayubu kiandikwe ili kitusaidie tushike ukamilifu kama Ayubu. (Warumi 15:4; Yakobo 5:10, 11) Mungu anajua kwamba, kama vile sehemu moja ya mwili inavyotegemea nyingine, ndivyo watumishi wake waaminifu wanavyohitajiana. (1 Wakorintho 12:20, 26) Kumbuka mikusanyiko ile ya karibuni ya “Washika Ukamilifu” iliyohudhuriwa na mamilioni ya wasomaji wa gazeti hili. Wale waliokuwako watakumbuka jinsi walivyojisikia vizuri kuwa katika ushirika wa wengi sana ambao shabaha yao kuu ni kudumisha ukamilifu kwa Mungu. Wahudhuriaji walitiwa moyo sana washike ukamilifu kwa kujua kwamba maelfu mengi waliokuwa karibu nao wanashika ukamilifu pia chini ya majaribu magumu wanapokuwa katika mahali pao pa kazi au shuleni katika mitaa ya kwao wenyewe!—1 Petro 5:9.
10. (a) Ni kwa njia gani mtu anaweza kushindwa kuendeleza maoni yanayofaa? (b) Ayubu alianza kutia shaka juu ya nini?
10 Hata hivyo huenda tukashindwa kudumisha maoni yanayofaa sikuzote, kama vile Ayubu. Mtu anayetaabika sana, na aliye katika hali ya kushuka moyo, huenda akafikiri au kusema, ‘Jamani, mbona Mungu ananifanyia hivi? Mbona anaruhusu jambo hili litukie?’ Huenda hata akafikia hatua ya kuuliza, ‘Kuna faida gani kwamba namtumikia Mungu?’ Kwa sababu ya kutokujua chanzo cha taabu yake, Ayubu alitia shaka juu ya kama kuna faida ya kuwa mwadilifu wakati wa sasa, kwa kuwa watu wema walionekana kuwa wakitaabika sana, na hata zaidi ya wabaya. (Ayubu 9:22) Kulingana na Elihu, Ayubu alisema: “Mimi napata faida gani? Napata faida gani inayozidi ile ambayo ningalipata kama ningalitenda dhambi?” (Ayubu 35:3, An American Translation) Lakini hatuwezi kujiacha tuhangaishwe mno na taabu zetu wenyewe hata tupoteze maoni yanayofaa na kutilia shaka ubora wa kumtumikia Mungu.
11. Elihu alimwandalia Ayubu sahihisho gani zuri?
11 Elihu alimwandalia Ayubu usahihisho uliohitajiwa, akanyoosha mambo kwa kuonyesha kwamba Yehova ametukuka zaidi ya Ayubu. (Ayubu 35:4, 5) Alionyesha kwamba, hata litukie jambo gani, haitupasi kamwe kukata shauri kwamba Mungu hajali na kuwaza kwa njia fulani kwamba tunaweza kumpuuza Yeye kwa sababu ya kumfikiria kuwa mwenye hali fulani za udhalimu. “Ukifanya dhambi kwa kweli,” Elihu akamuuliza Ayubu, “unakuwa umetimiza nini dhidi yake? Nayo maasi yako yakiongezeka kwa kweli, wewe unakuwa umemfanya nini?” (Ayubu 35:6, NW) Ndiyo, ukijaribu kumpuuza Mungu kwa kuziacha njia zake au utumishi wake, unajiumiza mwenyewe tu, wala si Mungu.
12. Ushikaji ukamilifu wetu unamhusuje Mungu?
12 Kwa upande mwingine, Elihu alionyesha kwamba sisi hatuwi tunampa Yehova faida ya kibinafsi tukitenda yanayofaa. Bila shaka, Mungu anafurahi sana tukishika ukamilifu. Hata hivyo, yeye hategemezwi kwa vyo vyote na ibada yetu, kama inavyoonyeshwa na ulizo ambalo Elihu alimuuliza Ayubu: “Ikiwa umetenda yanayofaa kweli kweli, unakuwa umempa nini, au yeye anakuwa amepokea nini kutoka mkono wako mwenyewe?” (Ayubu 35:7, NW) Mungu alitupa sisi uhai, na kwa sababu yake tunapumua na kwenda na kuwapo. Kila kitu ni chake! (Matendo 17:25; 1 Mambo ya Nyakati 29:14) Hivyo uovu wala uadilifu wetu hauwezi kuwa na matokeo ya kibinafsi juu ya Mungu.—Ayubu 35:8.
Tunaposahihishwa
13. (a) Ayubu alitendaje juu ya sahihisho alilopewa? (b) Sisi sote tuna tatizo gani?
13 Ayubu alitendaje alipopewa sahihisho, kwanza na Elihu kisha na Yehova mwenyewe? Alilikubali, akatubu “katika mavumbi na majivu.” (Ayubu 42:6) Ndiyo, Ayubu alijinyenyekeza, akakubali kosa lake. Na je, sisi hatuvutiwi na unyenyekevu wa namna hiyo? Lakini namna gani sisi? Ingawa huenda ikawa sisi ni washika-ukamilifu walio thabiti kama Ayubu, sisi sote tunaelekea kufanya makosa na kupoteza usawaziko kwa njia moja au nyingine. (Yakobo 3:2; Wagalatia 2:11-14) Tufanye nini tukionyeshwa kosa letu au hali ya kutokukamilika, hata ikiwa tumeonyeshwa na mtu wa umri mdogo kama Elihu?—Ayubu 32:4.
14. (a) Ni elekeo gani lililo la kawaida wakati mtu anaposahihishwa? (b) Ni jambo gani linaloweza kuhusika katika kutokeza makosa au maamuzi yasiyofaa, na ni mfano gani ambao Ayubu aliweka aliposahihishwa?
14 Si jambo jepesi sikuzote kukubali sahihisho. (Waebrania 12:11; Mithali 3:11, 12) Tuna elekeo la kujaribu kujitetea. Kama vile Ayubu, huenda ikawa hatukusema au kufanya ubaya wo wote kwa makusudi. Huenda ikawa kusudio letu lilikuwa zuri. Lakini huenda ikawa tulinena bila maarifa kamili, kwa kukosa ufahamu au bila hisia. Labda maelezo yetu yalionyesha hali ya majivuno ya kikabila au kujiona kwamba taifa letu ni bora kuliko la wengine, au kushikilia sana jambo fulani lisiloungwa mkono na Maandiko. Huenda ikawa tutajulishwa kwamba tuliyosema ni maoni ya kibinafsi tu na kwamba yameumiza wengine kwa kiasi cha kuhatirisha hali yao ya kiroho. Tunaposahihishwa, je, tutakuwa kama Ayubu tukubali ‘tulisema maneno tusiyoyafahamu’ na ‘kutubu’?—Ayubu 42:3, 6.
Kumtumaini Mungu, Wala si Mali
15. Tunajuaje kwamba tumaini la Ayubu halikuwa katika mali zake?
15 Bildadi alitia shaka juu ya chanzo ambacho Ayubu alitumainia, akidokeza kwamba yeye alikuwa amemsahau Mungu na kwamba alikuwa ameweka tumaini lake mahali pengine. (Ayubu 8:13, 14) Hata hivyo, ingawa Ayubu alikuwa amebarikiwa kwa vitu vingi vya kimwili, tumaini lake halikuwa katika vitu hivyo. Ukamilifu wake haukutikisika hata kidogo alipopoteza mali zake zote. (Ayubu 1:21) Alipokuwa akimaliza kujitetea, Ayubu alisema: “Ikiwa nimeifanya dhahabu kuwa tumaini langu, na kuiambia dhahabu safi, Wewe u tegemeo langu; kama nilifurahi kwa kuwa mali yangu yalikuwa mengi, na kwa sababu mkono wangu umepata vitu vingi . . . hilo nalo lingekuwa uovu wa kuadhibiwa na waamuzi; kwani [ningemkana] Mungu aliye juu.”—Ayubu 31:24-28.
16. (a) Inatupasa tujichunguzeje wenyewe? (b) Mungu anawatolea ahadi zipi wale wanaomtumaini yeye?
16 Namna gani sisi? Sisi tunaweka wapi tumaini letu—katika Yehova au katika mali za kimwili? Kama tungepimwa katika mizani iliyo sahihi, kama vile Ayubu alivyotaka afanywe, je, Mungu angejua kwamba sisi tuna ukamilifu katika jambo hilo? Je, kweli hangaikio letu kuu maishani ni lile la kumwandalia Yehova mwendo wa kushika ukamilifu ili autumie kujibu malaumu ya Shetani? Au sisi tunahangaikia hasa kutosheleza tamaa zetu za kutaka anasa na mali? Ingekuwa vizuri kama nini tukiwa kama Ayubu na kuufurahisha moyo wa Yehova kwa kumtumaini Yeye, tusipojihesabia sisi wenyewe au vitu vya kimwili tulivyo navyo umaana usiostahili! Tukimtumaini Yehova, tuweke faida zake kwanza, yeye anaahidi hatatuacha kamwe wala kutuondoka.—Mathayo 6:31-33; Waebrania 13:5, 6.
Maadili Katika Ngono
17. Ni vidokezo gani ambavyo “wafariji” wa Ayubu walitokeza, lakini Ayubu alisema nini juu ya mwenendo wake wa kiadili?
17 Wafariji wa uwongo wa Ayubu hawakumshtaki juu ya mwenendo mbaya wa ngono kwa njia ya moja kwa moja, lakini walidokeza-dokeza kwamba alikuwa na hatia ya kosa fulani la siri ambalo Mungu alikuwa akimwadhibia. Kwa kuwa alikuwa mtu mwenye mali nyingi, akiwa ndiye “mkuu sana kuliko watu wote wa upande wa mashariki,” hakika Ayubu alitokewa na nafasi za kumwezesha kufanya ngono nje ya mpango wa ndoa kama angalitaka. (Ayubu 1:3; 24:15) Watumishi wengine wa Mungu, wa kabla na baada ya wakati wa Ayubu, waliangukia vishawishi vya ngono. (Mwanzo 38:15-23; 2 Samweli 11:1-5) Lakini, Ayubu alijitetea kuwa hakuwa na mipango ya ujanja ya kutenda kosa hilo, akitangaza hivi: “Nilifanya agano na macho yangu; basi nawezaje kumwangalia msichana? Kama moyo wangu ulishawishwa kwa mwanamke, nami nimeotea mlangoni pa jirani yangu . . . hilo lingekuwa kosa kuu; naam, lingekuwa ni uovu wa kuadhibiwa na waamuzi.”—Ayubu 31:1, 9-11.
18. Kwa sababu gani ni vigumu sana kudumisha maadili ya ngono, hata hivyo ni kwa sababu gani sisi tutakuwa wenye furaha tukiyadumisha?
18 Labda hakuna njia nyingine ambayo kwayo Shetani amefanikiwa sana kubomoa ukamilifu wa watumishi wa Mungu kama vile alivyofanikiwa kwa kuwashawishi wafanye uasherati. (Hesabu, sura ya 25) Je, wewe unaweza kuiga ukamilifu wa Ayubu kwa kupinga sana vishawishi vyote vya kuwa na mwendo mbaya wa ngono? Huo ni mwito mkubwa wa ushindani, hasa katika ulimwengu huu ambamo ukosefu wa adili unapatikana sana. Lakini fikiria ni vizuri kama nini, wakati unapoombwa utoe hesabu, kuweza kusema kwa uhakika kama vile Ayubu alivyofanya: “Mungu atapata kuujua ukamilifu wangu”!—Ayubu 31:6.
Kinachoweza Kutusaidia
19. Ni jambo gani linalohitajiwa sana litusaidie kushika ukamilifu?
19 Si jambo jepesi kuiga ukamilifu wa Ayubu, kwa kuwa leo Shetani anajaribu kwa bidii kuvunja ukamilifu wetu kama alivyojaribu kuuvunja wa Ayubu. Basi, inahitajiwa kwamba tuvae suti kamili ya silaha kutoka kwa Mungu. (Waefeso 6:10-18) Jambo hilo linahusu kuwa watu wenye kushikilia mambo ya Mungu, kama Ayubu, kufikiria daima kumpendeza Yeye katika lo lote ambalo sisi au jamaa zetu tunafanya. (Ayubu 1:5) Hivyo funzo la Biblia, ushirika wa kawaida pamoja na waamini wenzetu, na tangazo la waziwazi la imani yetu ni mambo yanayohitajiwa sana.—2 Timotheo 2:15; Waebrania 10:25; Warumi 10:10.
20. (a) Ni tumaini gani linaloweza kututegemeza wakati wa majaribu? (b) Ni thawabu gani ya kushika ukamilifu iliyotajwa na mtunga zaburi tunayoweza kupokea?
20 Lakini jambo hasa linaloweza kututegemeza zaidi wakati wa jaribu ni lile lililotegemeza Ayubu, tumaini lake hakika la kwamba maisha siyo aya haya tu. “Mtu hodari akifa, je, anaweza kuishi tena?” Ayubu akauliza. Na kwa kujibu alisema hivi: “Wewe utaita, nami nitakujibu.” (Ayubu 14:13-15, NW) Kuwa na uhakika kamili uo huo kwamba Yehova atafufua watumishi wake waamini kunaweza pia kutusaidia tukabili jaribu lo lote ambalo huenda Shetani akaweka juu yetu. (Waebrania 6:10) Zamani za kale mtunga zaburi wa Biblia aliandika hivi: “Nami katika ukamilifu wangu umeitegemeza, umeniweka mbele za uso wako milele.” (Zaburi 41:12) Huo na uwe ndio wakati ujao wenye furaha wa kila mmoja wetu—kuja kutegemezwa na Yehova na kuhifadhiwa naye milele kwa sababu ya kuwa watumishi wake washika ukamilifu!
Unaweza Kujibu?
◻ Ni akina nani wamethibitika kuwa kama Ayubu, na ni ulinganifu wa mambo gani unaoweza kufanywa kati yao na Ayubu?
◻ Tunaweza kujifunza nini kutokana na alivyotenda Ayubu akiwa katika majaribu?
◻ Ayubu aliitikiaje sahihisho, nasi tunaweza kujifunza nini kutokana na jambo hilo?
◻ Ni mfano gani bora ambao Ayubu aliandaa kuhusu vitu vya kimwili na maadili yanayohusu ngono?
◻ Ni jambo gani linaloweza kutusaidia kudumisha ukamilifu kama Ayubu?
[Picha katika ukurasa wa 17]
Wewe umepata kutia shaka kama Ayubu juu ya faida ya sasa ya kushika ukamilifu?