Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w86 4/1 kur. 3-4
  • Biblia Ni Neno la Mwanadamu Tu?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Biblia Ni Neno la Mwanadamu Tu?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Je! Ni ya Maana?
  • Kuamini Kumeenda Wapi?
  • Biblia Ni Neno la Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
  • “Agano la Kale” Ni Lenye Kusadikika Kadiri Gani?
    Biblia—Neno la Mungu au la Binadamu?
  • Biblia Iliandikwa Wakati Gani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2011
  • Kwa Nini Uisome Biblia?
    Biblia—Neno la Mungu au la Binadamu?
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
w86 4/1 kur. 3-4

Biblia Ni Neno la Mwanadamu Tu?

WILLIAM TYNDALE alitoa uhai wake akijaribu kuifanya ipatikane kwa kila mtu. Martin Lutheri alitumia jitihada kubwa sana kuitafsiri katika Kijeremani. Kwa wafuasi wa John Calvin, hiyo ilikuwa ndiyo “kanuni na kiwango cha ukweli wote.” Ndiyo, kuna wakati ambao ni watu wachache waliokuwa wakitia shaka juu ya kama Biblia ni Neno la Mungu. Hiyo ilikuwa pia imani ya Kanisa Katoliki la Kiroma.

Ingawa hivyo, mambo ni tofauti sana leo. Biblia, ambayo ndiyo kitabu kinachouzwa kwa wingi zaidi katika historia, inasomwa na watu wachache, kisha ni wachache hata zaidi wanaoifuata. Mtungaji James Barr, akitoa maoni yaliyo ya watu wengi, alisema: “Usimulizi wangu wa kufanyizwa kwa mapokeo ya kibiblia ni usimulizi wa kazi ya kibinadamu. Ni maneno ya mwanadamu juu ya anayoamini... Jina ambalo lingeifaa Biblia kuitwa lingekuwa Neno la Israeli, Neno la Wakristo fulani mashuhuri.”​—The Bible in the Modern World, cha James Barr.

Kwa sababu gani kumetokea badiliko? Je, Biblia ni Neno la Mungu au neno la wanadamu fulani? Je, hata ni ya maana katika karne hii ya 20?

Je! Ni ya Maana?

Kwa kujibu kwanza lile ulizo la mwisho, ndiyo, ni ya maana. Kwa sababu gani? Biblia inaelezwa kuwa ‘taa ya miguu yetu, na mwanga wa njia yetu.’ (Zaburi 119:105) Leo, tunauhitaji kweli kweli mwanga huo. Sayari yetu iliyo ya kupendeza sana inaharibiwa. Mamilioni mengi ya watu wanakaa na njaa. Si watu wengi walio na uhakika juu ya wakati ujao, na kuna tisho la kama wanadamu hata wataendelea kuwako. Biblia ina toleo la kutupa mwongozo tuzipite nyakati hizi zenye hila tukaufikie wakati ujao ulio salama na wenye furaha. Ikiwa hiyo ni Neno la Mungu kweli kweli, ndiyo tunayohitaji hasa.

Kwa hiyo mbona watu wamekuja kuitilia shaka? Jibu la ulizo hilo litatusaidia tuamue kama kitabu hicho ni Neno la Mungu kweli kweli au sivyo kilivyo.

Kuamini Kumeenda Wapi?

Katika karne za 17 na 18, kule kuaminiwa kwa Biblia na watu wa karibu kila mahali kuliendelea kubadilishwa na maoni yenye kuwa tofauti. Katika Ulaya ilisitawi roho ya kutilia mambo mashaka na kuyaona kwa njia za kilimwengu. Mifumo ya serikali, uchumi, maumbile, dini, kila kitu kilitiliwa shaka. Hata Biblia haikuponyoka kutiliwa mashaka hayo.

Mashaka juu ya kitabu hicho yalisemwa wazi katika karne ya 17 na Pierre Bayle, aliyekuwa Mkatoliki hapo kwanza, naye aliutilia shaka ukweli wa Biblia katika mambo ya kihistoria na tarehe. Wengine walifuata fikira zake, na katika karne ya 19, hali ya kutia-tia mashaka juu ya mambo ikasitawi sana katika shule ya uchambuzi wa hali ya juu. Wenye uchambuzi huo wanasisitiza kwamba Biblia haiko jinsi inavyoonekana kuwa. Kulingana na wao, si Musa aliyeandika Pentateuko (vitabu vitano vya kwanza). Bali, ilikusanywa badaye kidogo katika historia ya Kiyahudi kutokana na maandishi kadha yaliyoandikwa karne nyingi baada ya siku za Musa. Wanasema kwamba pasipo shaka unabii wo wote unaosemwa kuwa ulitimia uliandikwa baada ya kutimia. Kwa hiyo, kitabu cha Isaya kiliandikwa na watu kadha kwa muda wa mamia ya miaka. Na kitabu cha Danieli kiliandikwa karibu na mwaka 165 K.W.K.

Matokeo ya uchambuzi wa hali ya juu yanaonwa katika kisa cha mwanachuo wa Biblia aliye Mjeremani, David Friedrich Strauss: “Je! bado sisi ni Wakristo? Hapana, akasema Strauss, angalau si wale kati yetu ambao wamejihusisha sana na Uchambuzi wa Hali ya Juu, kwa maana hatuwezi tena kuikubali Biblia kuwa Neno la Mungu​—Religion and the Rise of Scepticism, cha Franklin L. Baumer.

Kizazi kipya cha nyukilia kimetokeza pia mavumbuzi mapya katika sayansi. Mengine kati ya hayo yakaiunga mkono Biblia, lakini mengine yakaelekea kupingana nayo. Kwa hiyo, watu wengi waliongozwa kuamini kwamba Biblia imechakaa. Maoni hayo yalitiliwa mkazo katikati ya karne ya 19 wakati ambapo nadharia ya mageuzi ilianza kufuatwa na watu wengi​—nadharia inayopingana kabisa na simulizi ya uumbaji katika kitabu cha Mwanzo. Nadharia hiyo ilifuatwa kwa hamu nyingi na wanasayansi, na leo inakubaliwa na makasisi wengi na kufundishwa kuwa jambo hakika katika shule nyingi.

Je, yote hayo yanamaanisha kwamba kwa njia fulani sayansi imeikanusha Biblia? Au uchambuzi wa hali ya juu umeonyesha kwamba Biblia si Neno la Mungu?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki