Biblia Ni Neno la Mungu
JE! NI KWELI kwamba, sayansi ya uchambuzi wa hali ya juu zimeshirikiana zikaweza kuiachisha Biblia kuwa Neno la Mungu, kama ilivyokuwa hapo kwanza? Huenda mtu akafikiri hivyo kwa urahisi. Hata viongozi wa kidini wanakuwa na moyo wa kusema katika maandishi kwamba Biblia haipatani na sayansi, nao uchambuzi wa hali ya juu unaheshimika sana hivi kwamba unafundishwa katika vyuo vya kidini. Lakini mambo ya hakika yanaonyesha nini?
Biblia na Uchambuzi wa Hali ya Juu
Kwa habari ya uchambuzi wa hali ya juu, uhakika ni kwamba, mpaka sasa hakuna uthibitisho kamili ambao umepata kutokezwa wa kuhakikisha mawazo yao. Hakuna yo yote ya maandishi yaliyotajwa kuwa msingi wa kuchambua Pentateuko au kitabu cha Isaya yameweza kupatikana. Na visehemu vya kale vya kitabu cha Danieli vimechimbuliwa vikidokeza kwamba kitabu hicho kiliheshimiwa sana miaka michache tu baada ya wakati ule ambao wachambuzi wa hali ya juu wanadai ndipo kilipoandikwa!
Profesa wa dini anatangaza hivi: “Haiwezi kuthibitishwa katika kisa fulani cho chote kwamba vitabu vya Kibiblia vilitokea kwa njia ya udanganyifu kama inavyoelezwa na shule ya uchambuzi wa hali ya juu. Ni jambo moja shule hiyo kudai hivyo, hali ni jambo jingine lililo tofauti kabisa kwao kuthibitisha dai lao.” (Biblical Criticism, cha Wick Broomall) Mchimbuzi wa vitu vya kale, W. F. Albright, anaongeza hivi: “Haiwezi kukaziwa sana kwamba hakuna ushuhuda hata mmoja wa wakati wa kale katika Mashariki ya Karibu wa kuthibitisha kwamba habari za kutungwa ziliingizwa katika hati au vitabu.” (From the Stone Age to Christianity, cha W. F. Albright) Ni kweli kwamba uchambuzi wa hali ya juu unaendelea kusitawi. Lakini hiyo ni kwa sababu unapatana sana na fikira za kilimwengu leo, si kwa sababu imekwisha kuthibitishwa.
Biblia na Sayansi
Basi, je, sayansi imekanusha Biblia kwa njia fulani-fulani? Nyakati nyingine imeonekana kama kwamba imefanya hivyo. Kwa mfano, katika karne ya 18 ufahamu ulipoongezeka juu ya jinsi dunia yetu ilivyo, ilionekana wazi kwamba sayari yetu ni ya kale sana. Wakati huo, wanadini wengi walisisitiza kwamba, kulingana na Biblia, dunia ilikuwa na umri wa miaka 6,000 tu. Ilionekana kama kwamba huo ulikuwa mfano wenye kuonyesha wazi kwamba fundisho moja la Biblia lilikuwa likikanushwa. Hata hivyo, hakuna mahali ambapo Biblia inasema umri wa dunia. Tatizo hilo lilitokea kwa sababu ya wanadini hao kuwa na ufahamu wenye makosa.
Maneno ya kwanza kabisa ya Biblia ni: “Hapo mwanzo Mungu aliziumba mbingu na nchi.” (Mwanzo 1:1) Maneno hayo, kwamba kulikuwa na mwanzo, yanapatana na maoni ya kisayansi ya sasa. Basi, kulingana na Biblia, kulikuwa na kipindi ambapo dunia ilikuwa “ukiwa, tena utupu,” isiyokaliwa na isiyokalika. (Mwanzo 1:2) Wanajiolojia (wataalamu wa ardhi) wanaojaribu kuvumbua jinsi dunia ilivyokuwa hapo kwanza wanadokeza kwamba wakati mmoja ilikuwa isiyokaliwa na isiyokalika. Halafu, Biblia inaeleza jinsi bahari na mafungu ya ardhi yalivyoumbika. Mimea ilitokea, halafu viumbe wa baharini, ndege, na, mwishowe, wanyama wa nchi kavu. Mwishowe, mwanadamu mwenyewe akatokea. Kwa ujumla, hayo yanafanana sana na yale ambayo wanasayansi wamevumbua kwa kuchimba ndani ya tabaka la kale la dunia, hata wakauvumbua utaratibu ule wa kawaida wa jinsi vitu vilivyo hai vilivyotokea kwa kufuatana.—Mwanzo 1:1-28.
Hiyo si kusema kwamba Biblia inapatana kabisa na mambo yaliyoandikwa katika vitabu vya masomo ya kisayansi. Lakini kuna mambo mengi sana ambayo inakubaliana na sayansi hivi kwamba tunalazimika kujiuliza hivi: ‘Wale waandikaji wa kwanza wa Biblia walijuaje mambo mengi hivyo?’ Kwa kuwa siku zao zilikuwa zile zinazoonwa za kishamba kulingana na maarifa ya kisayansi, ni kwamba tu mtu fulani aliwaambia—uthibitisho wenye nguvu wa kwamba kweli Biblia ni Neno la Mungu. Katika visa ambavyo zipo bali za kutokupatana kati ya nadharia za wanasayansi na Biblia, je, tujichukulie tu kwamba Biblia imekosea na kwamba wanasayansi ndio wanaosema kweli sikuzote? Kuna mifano mingi ya mbele inayoonyesha kwamba sayansi inaweza kukosea mara kwa mara.
Bila shaka, nadharia ya mageuzi inatokeza wazo kuu la kutokukubaliana na Biblia. Jambo linalostahili kuangaliwa juu ya nadharia hii ni jinsi ilivyofuatwa sana upesi na wanasayansi baada ya kuchapishwa kwa kitabu cha Darwin The Origin of Species. Ilikubaliwa muda mrefu kabla haujpatikana wakati wa kuchunguza ukweli wa mawazo ya msingi ya kitabu hicho au kabla ya kutafuta mambo ya kuyathibitisha kwa kuyalinganisha masalio yaliyochimbuliwa katika ardhi ya vitu vilivyokuwa hai zamani. Kwa sababu gani? Mwanamageuzi Hoimar v. Ditfurth anaungama hivi: “Sayansi inafafanuliwa kuwa jaribio la kuona ni kwa kadiri gani mwanadamu na asili anaelezeka bila kuyategemea maelezo yanayohusu miujiza.” (The Origins of Life, cha H. v. Ditfurth) Basi, je, inashangaza kwamba wanasayansi wameishughulikia sana nadharia ya mageuzi, wakatumia wakati na jitihada nyingi wakijaribu kuithibitisha kuwa kweli na kutumia wakati na jitihada chache sana kujaribu kuona kama inaweza kuthibitishwa kuwa si ya kweli? Njia ile nyingine moja tu ya kueleza mambo, yaani uumbaji, ingekuwa ni muujiza—ambayo si yenye kufikirika kwao.
Ingawa hivyo, kwa kweli mtu ye yote asiyechukia miujiza bila msingi mzuri ataona uumbaji kuwa njia yenye sababu nzuri sana za kusaidia kuyafahamu mambo ambayo wanasayansi wameshindwa kueleza, kama vile chanzo cha kanuni ya uhai, hali ya mtu kuwa na fahamu, akili, na hali ya kiadili ya .mwanadamu.
Kitabu Chenye Uwezo
Biblia yenyewe inaonya kwamba kutakuwa na uhitilafiano kati ya hekima ya ulimwengu iliyopokewa na mafundisho ya Biblia yenyewe. (1 Wakorintho 1:22, 23; 3:19) Kwa kuwa maarifa yanayotegemea uchunguzi na falsafa za kibinadamu yanakosa sana uhakika, uhitilafiano huo haupasi kutushangaza. Wala haitupasi kusumbuka ikiwa nadharia fulani zinazofuatwa na wengi zinapingana na Biblia. Biblia yenyewe inatuelekeza tutafute pande nyingine uthibitisho wa dai layo kwamba hiyo kweli ni Neno la Mungu.
Kwa mfano, Biblia inadai kuwa kitabu cha unabii. (2 Petro 1:19-21) Wachambuzi wa hali ya juu wanadai kwamba unabii huo uliandikwa baada ya matukio yenyewe kutendeka, lakini mara nyingi hilo linakuwa jambo lisilowezekana. Unabii mwingi unaomhusu Yesu uliotolewa karne nyingi kabla ya yeye kuzaliwa ulitimizwa kwa ukamili kabisa. (Ona, kwa mfano, Isaya 53:1-12; Danieli 9:24-27.) Unabii wa Yesu mwenyewe juu ya uharibifu wa Yerusalemu ulitimizwa barabara. Na unabii ambao yeye na mtume Paulo walitoa juu ya siku za mwisho unalingana barabara na matukio unayosoma katika magazeti ya habari ya asubuhi ya leo. (Mathayo 24; Marko 13; Luka 21; 2 Timotheo 3:1-5) Kwa kuwa wanadamu wanapojaribu kuutabiri wakati ujao wanakosea sana, unabii wa Biblia ni uthibitisho wenye nguvu kwamba umetoka kwa Chanzo cha juu zaidi.
Ushuhuda mwingine wenye nguvu unaonekana katika maneno ya Biblia yenyewe: “Neno la Mungu li hai, tena lina nguvu.” (Waebrania 4:12) Uwezo huo umeonyeshwa muda wote wa historia na watu kadha ambao wametaabika na kufa wakiitetea haki ya kusoma Biblia au kuelezana na wengine mambo yaliyomo. Hakuna kichapo kingine ambacho kimepata kuwa na matokeo mema hivyo kwa watu wakati kinaposomwa kwa roho ya unyenyekevu na akili. Inabadili watu wenye kupenda vita wawe wenye kuamanika na inaweza kugeuza kabisa utu wa mtu. (Mika 4:3, 4; Waefeso 4:24) Kwa mfano, angalia jinsi Biblia ilivyomsaidia Luiz.
Katika gereza la Brazili alimokuwa amewekwa, Luiz alijulikana kuwa mtu hatari mno, Halafu, mmoja wa Mashahidi wa Yehova alipokuwa akihudumia wengine wa wafungwa wenzi wa Luiz, alipata nafasi ya kusema na Luiz. Maneno ya Biblia yalimgusa sana Luiz hata akabadilika baada ya muda mfupi. (Wakolosai 3:9, 10) Hapo kwanza, hakuna mtu aliyekuwa amethubutu kumrudishia maneno ya kumjibu, lakini sasa alikuwa akitendea kila mtu kwa fadhili na hata kuwapa wakuu wa gereza heshima iliyowastahili. Miaka mitano baada ya Biblia kuanza kuugeuza utu wa Luiz yeye mwenyewe anawaeleza wafungwa wale wengine mambo ambayo amejifunza na hata anaruhusiwa kuhubiri nje ya gereza.
Halafu, mfikirie Wayne. Wayne aliishi maisha ya kufuata sana anasa katika United States, hasa katika ukosefu wa adili na matumizi ya dawa za kulevya. Alipooa, mwenendo wake mbaya mwishowe ukamfanya mke wake pia aanze matendo ya ukosefu wa adili. Maisha yao ya kinyumbani yalikuwa mabaya sana. Walipokaribia kutalikana, mmoja wa Mashahidi wa Yehova alipata nafasi ya kumwonyesha Wayne vile Biblia inavyosema juu ya mtu kujali madaraka yake na kuonyesha upendo katika jamaa. (Waefeso 4:22-24; 5:22-28) Alisaidiwa atambue baadhi ya mambo yaliyoanzisha matatizo yake. (Ona 1 Wakorintho 15:33.) Na, hatimaye, aliweza kubadili njia yake ya kufikiri. Jambo hilo likamsaidia mkeye pia abadilike. Na sasa jamaa ya vijana hao ni mfano mzuri wa watu walioridhika—shukrani kwa Biblia.
Mwishowe chukua kisa cha Elena. Yeye alikuwa kijana Mwargentina mwenye kusumbuliwa na hali ya kushuka moyo. Alipomwendea daktari wa magonjwa ya akili akapate msaada, daktari huyo alimwambia kwamba alihitaji kufanya-fanya ngono na watu wo wote ili atatue matatizo yake. Kijana huyo wa kike akaingilia sana ukosefu wa adili, upashanaji habari na mashetani, na kutumia sana tumbaku. Alitoa mimba mara mbili. Lakini Mashahidi wa Yehova walipendezwa na Elena wakaweza kumsaidia atumie Biblia katika maisha yake. Hatua kwa hatua, maneno ya Biblia yakamwezesha aache mazoea yake mabaya na kupata kumjua Muumba, Yehova Mungu, na Mwanaye, Yesu Kristo. Akisema juu ya watu hao wawili, sasa Elena anasema: “Mimi sikufanya jambo la kunistahilisha yo yote ya mambo mema ninayopokea kutoka kwao, na kwa sababu hiyo najisikia nikitaka kuendelea tu kueleza jinsi walivyo na rehema na upendo kwetu sisi.”
Kama vile mifano michache hii inavyoonyesha, Biblia inaweza kuingiza ndani ya maisha zetu kani yenye kutufaidi sana. Luiz, Wayne, na Elena walisaidiwa wakati Mashahidi wa Yehova walipowafahamisha Biblia na kuwaonyesha kutumia yanayosemwa nayo. Mashahidi hao ni zaidi ya milioni tatu ulimwenguni leo, na wengi wao walikuwa katika hali kama hizo lakini wote wameruhusu Biblia ifanye mabadiliko makubwa katika maisha zao. Matokeo yakawa nini?
Wakristo hao milioni tatu wanakuwa jamii ambamo matatizo yale makubwa yanayotisha wakati ujao wa wanadamu yamekwisha kuanza kutatuliwa. Wao hawagawanywi na mambo ya kutukuza taifa wala kabila. Bali, kwa msaada wa Biblia wanafanya bidii kushinda hali za ubaguzi wa kitaifa na kiuchumi. Nao wamejifunza kuishi pamoja kwa amani, na hiyo ni hatua ya kwanza ya utimizo wa unabii mmojapo wa Biblia ulio wa kustaajabisha zaidi.—Isaya 11:6-9.
Kuwako kwa kikundi cha watu hao ni uthibitisho wenye nguvu kwamba kweli Biblia ni Neno la Mungu. Sisi tunakualika upate kuwajua Wakristo hawa ili ujionee mwenyewe uthibitisho huo. Mashahidi wa Yehova watafurahia sana kukusaidia ufanye hivyo.
[Blabu katika ukurasa wa 5]
Hakuna kabisa uthibitisho halisi wa madai ambayo uchambuzi wa hali ya juu unaifanyia Biblia
[Blabu katika ukurasa wa 6]
Biblia haitegemei sayansi wala falsafa za kisasa ili kuthibitisha kwamba hiyo ni Neno la Mungu
[Picha katika ukurasa wa 7]
Biblia inabadili watu