Je! Wameithibitisha Biblia Kuwa Bandia?
JE! KWA kweli wanasayansi na wachambuzi wa Biblia wamethibitisha kwamba Biblia ina makosa na hadithi za kutungwa tu? Kabla wewe hujakubali kwamba wamethibitisha hivyo, wapaswa kukumbuka kwamba ingawa wanachuo wengi hutokeza maoni yao kwa njia ya uhakika na ya kimamlaka, si sikuzote wao huwa wakisema yaliyo sawa. Mara nyingi mawazo yao hutegemea misingi isiyo imara.
Dhana Zenye Mashaka
Kwa kielelezo cha taarifa yenye kusikika kuwa yenye mamlaka, fikiria vile S. R. Driver alivyosema kuhusu kitabu cha Danieli. Kulingana na mapokeo, kitabu hiki kimeonwa kuwa kiliandikwa na Danieli mwenyewe katika Babuloni katika karne ya sita K.W.K. (Danieli 12:8, 9) Lakini Driver alidai kwamba kiliandikwa muda mwingi baada ya hapo. Kwa nini? “Uthibitisho” mmoja uliotolewa ni kwamba kitabu hicho kina maneno ya Kigiriki, na Driver alikazania hivi: “Yaweza kushikiliwa kwa uhakika kwamba maneno haya yasingaliweza kutumiwa katika Kitabu cha Danieli kama yasingaliandikwa baada ya kuenea kwa maongozi ya mawazo ya Kigiriki katika Esia kupitia ushindi mbalimbali wa Aleksanda Mkuu.” Aleksanda alifanya ushindi wake mbalimbali karibu 330 K.W.K.
Taarifa ya Driver imesemwa kwa uhakika kabisa. Hata hivyo, ili aiunge mkono, yeye ataja maneno matatu tu ya Kigiriki, yote hayo yakiwa ni majina ya vyombo vya kimuziki. (Danieli 3:5) Kwa maana Wagiriki walikuwa na shughuli za ukaribu pamoja na Esia ya magharibi kuanzia mapema katika historia iliyoandikwa, mtu yeyote awezaje kukazania kihalali kwamba vyombo vya kimuziki vyenye majina ya Kigiriki havikutumiwa katika Babuloni katika karne ya sita K.W.K.? Lo, ni msingi dhaifu kama nini wa kutia shaka kuhusu wakati wa kuandikwa kwa kitabu cha Danieli na kuhusu mwenye kukiandika!
Kielelezo kingine ni kuhusu jinsi vile vitabu vitano vya kwanza vya Biblia huchukuliwa. Kulingana na mapokeo, hivi husemwa kwamba kwa sehemu kubwa viliandikwa na Musa karibu 1500 K.W.K. Hata hivyo, wachambuzi hudai kwamba wao huona namna tofauti za uandikaji katika vitabu hivyo. Pia, wao huona kwamba nyakati fulani Mungu hutajwa kwa jina lake, Yehova, na nyakati fulani kwa neno la Kiebrania “Mungu.” Kutokana na maoni kama haya, wao hufikia kukata shauri kwamba kwa kweli vitabu hivi vya Biblia ni mchanganyo wa hati zilizoandikwa nyakati tofauti na zikaungwa pamoja muda fulani baada ya 537 K.W.K. ili ziwe namna zilivyokuja kuwa mwishowe.
Nadharia hii huaminiwa na wengi, hata hivyo hakuna mtu ameeleza ni kwa nini Musa hangeweza kutaja Muumba kwa njia zote mbili, kuwa Mungu na kuwa Yehova pia. Hakuna mtu amethibitisha kwamba yeye hangeweza kuandika kwa namna tofauti-tofauti akiwa anazungumzia habari zilizo tofauti, akiandika katika nyakati tofauti za maisha yake, au akitumia vyanzo vya mapema kidogo. Zaidi ya hilo, kama vile John Romer alivyosema katika kitabu chake Testament—The Bible and History: “Jambo la msingi lenye kuikataa njia yote hii ya kuchanganua mambo ni kwamba mpaka leo hii hakujapatikana hata kijipande kimoja cha maandishi ya kale chenye kuthibitisha kwamba kulikuwako namna mbalimbali za maandiko tofauti-tofauti yaliyounganishwa pamoja kama vile zisemavyo nadharia zenye kupendwa sana na wanachuo wa ki-siku-hizi.”
Dhana moja ya msingi kuhusu wachambuzi wengi wa Biblia yaelezwa na Cyclopedia ya McClintock na Strong: “Wachunguzi . . . huanza kwa dhana ya kuchukua kwamba mambo hakika ya historia yenye kuhusiana na masimulizi ni yale yaliyo ya hakika kabisa kulingana na asili ya maumbile, yenye kufanana na mambo mengine ya uhakika ambayo sisi twayajua. . . . Je! jambo fulani lisilowezekana kulingana na sheria zijulikanazo za Asili ya Maumbile lataarifiwa na mwandikaji kuwa lilitukia kwa uhakika? Ikiwa ndivyo . . . tukio hilo lenye kusemekana halikutukia.”
Hivyo, wengi huchukua kwamba miujiza isingeweza kuwa ilitukia, kwa maana ni ya hali izidiyo ile ambayo yawezekana kwa kiwango cha sheria za asili ya maumbile. Vivyo hivyo, wao huchukua kwamba ni lazima unabii wenye kuhusu muda mrefu ujao uwe usioweza kutimia, kwa maana wanadamu hawawezi kuona mbali katika wakati ujao. Ni lazima muujiza wowote uwe ni hekaya tu au hadithi ya kutungwa. Ni lazima unabii wowote uliotimizwa kwa uwazi uwe uliandikwa baada ya huo kutimizwa.a Kwa sababu hiyo, watu fulani hubisha kwamba unabii wa kitabu cha Danieli ulitimizwa kufikia karne ya pili K.W.K. na kwa hiyo ni lazima kitabu hicho kiwe kiliandikwa wakati huo.
Lakini dhana ya aina hii yategemea namna moja ya imani: kwamba Mungu hayupo, au ikiwa yupo, yeye hajiingizi kamwe katika historia ya kibinadamu. Kwa uhakika, maana yote ya Biblia ni kwamba Mungu yupo na ni mtendaji katika historia ya kibinadamu. Ikiwa hiyo ni kweli—na ushuhuda waonyesha ni kweli—sehemu kubwa ya msingi wa uchambuzi wa ki-siku-hizi wa Biblia yaonyeshwa kuwa isiyofaa kitu.
Je! Sayansi ya Ki-Siku-Hizi Imeionyesha Biblia Kuwa Yenye Makosa?
Ingawa hivyo, namna gani lile dai la kwamba sayansi imeonyesha kwamba hatuwezi kuiamini Biblia? Ukweli ni kwamba, wakati ambapo Biblia hugusia habari za kile tukiitacho sayansi, muda mwingi yale isemayo huwa hayakosi kupatana na yale ambayo wanasayansi wa ki-siku-hizi hufundisha.
Kwa kielelezo, Biblia hutoa amri zenye kutumika kwa mafaa sana kuhusu kanuni za afya na magonjwa ya kuambukiza. Kitabu Manual of Tropical Medicine chaeleza hivi: “Hakuna mtu awezaye kushindwa kuvutiwa na hatua za tahadhari nyingi kuhusu kanuni za afya zilizokuwa katika kipindi cha Musa. . . . Ni kweli kwamba magonjwa yalipangwa katika vikundi-vikundi vilivyo rahisi kueleweka—[yaani] katika kikundi cha kasoro zenye kutokea pale mwanzoni zikiwa kali-kali, zilizoitwa ‘tauni’; na kasoro zenye kuendelea muda wote, zikiwa na namna fulani ya mtoko-toko, wenye kuitwa ‘ukoma’—lakini zile sheria thabiti sana za kuzuilia mtu akiwa mahali pake peke yake zilileta manufaa kubwa.”
Fikiria, pia, taarifa ya Biblia: “Mito yote huingia baharini, walakini bahari haijai; huko iendako mito, ndiko irudiko tena.” (Mhubiri 1:7) Hili lasikika kama lile elezo ambalo lapatikana leo katika vitabu vya masomo kuhusu ile kawaida yenye kujirudia-rudia daima ya kufanyika kwa maji. Mito hupelekea maji ndani ya bahari, ambamo maji hayo hugeuka kuwa mvuke na kuchukuliwa kwa namna ya mawingu na kurudishwa juu ya bara, kisha huanguka yakiwa mvua au theluji na kutiririka mbio ndani ya mito.
Vivyo hivyo, maamuzi yenye kufikiwa na sayansi kwamba milima huinuka na kuanguka na kwamba wakati mmoja milima ya leo ilikuwa chini ya bahari za kale yapatana na maneno ya kishairi ya mtunga zaburi: “Maji yalikuwa yakisimama juu ya milima yenyewe. Milima ilizidi na kupanda, nyanda za mabonde zikazidi na kushuka—hadi mahali ambapo wewe umeiwekea msingi.”—Zaburi 104:6, 8, NW.
Mwandikaji mmoja alikazania hivi: “Waandikaji wote wa Agano la Kale waliichukua Dunia kuwa sahani tambarare, na nyakati fulani walitaja nguzo ambazo zilisemwa kuwa zaitegemeza.” Ingawa hivyo, hii si kweli. Isaya alinena juu ya yule “anayeketi juu ya duara ya dunia.” (Isaya 40:22) Na Ayubu alisema hivi juu ya Mmoja huyu: “Yeye hutandaza kaskazi juu ya nafasi isiyo na kitu, na kuutundika ulimwengu pasipo kitu.” (Ayubu 26:7) Lile elezo la kwamba dunia ni gimba la mviringo lenye kuning’inia katika anga bila tegemezo lionekanalo lasikika kuwa la ki-siku-hizi sana.
Mageuzi
Namna gani upingano ulio kati ya Biblia na nadharia ya mageuzi?b Encyclopoedia Britannica yaripoti hivi: “Nadharia ya mageuzi yakubaliwa na idadi kubwa zaidi ya wanasayansi.” Lakini Biblia yafundisha, kwa lugha yenye usahili wa kutosha kuweza kueleweka katika kipindi cha kabla ya sayansi, kwamba uhai ulitokea kwa kuumbwa moja kwa moja na Mungu na kwamba zile aina za msingi zilizo tofauti-tofauti za uhai hazikutokea kwa mageuzi bali ziliumbwa.—Mwanzo 1:1; 2:7.
Wanamageuzi hawatofautiani na wachambuzi wa Biblia. Wao wana masadikisho imara na hueleza maoni yao kimamlaka. Lakini kuna wachache walio wanyofu vya kutosha kukiri kwamba nadharia ya mageuzi ina udhaifu mbali-mbali. Mmoja aonyesha wazi hivi: “Kiolezo cha Darwin cha mageuzi . . . , ambacho kwa msingi ni nadharia iliyopita katika hatua mpya za mabadiliko katika muda wa historia,... haiwezekani kuthibitishwa kuwa kweli kwa kufanyiwa majaribio ya uhakikisho au kwa uchunguzi wa moja kwa moja kama ilivyo kawaida katika sayansi... Zaidi ya hilo, nadharia ya mageuzi hushughulika na mfululizo wa matukio yasiyo na mengine ya kufanana nayo, asili ya uhai, asili ya vitu vyenye akili na kadhalika. Matukio yasiyo na mengine ya kufanana nayo hayawezi kufanywa yatukie tena na hayawezi kupasishwa namna yoyote ya uchunguzi wa majaribio ya uhakikisho.” (Evolution: A Theory in Crisis, kilichotungwa na Michael Denton) Mwingine anena juu ya “uhakika wa mageuzi.” Hata hivyo, yeye aonyesha ugumu fulani mkubwa katika kuthibitisha “uhakika” huu: “Utafutapo viunzi kati ya vikundi vile vikubwa-vikubwa vya wanyama, huwa havipatikani kamwe.”—The Neck of the Giraffe, kilichotungwa na Francis Hitching.
Wao Waweza Kujua Mambo Kadiri Gani?
Sehemu kubwa ya ushuhuda wa mageuzi hutolewa na wanajeolojia na wanapalontolojia—wanasayansi ambao huchunguza zamani za kale za dunia. Matatizo yenye kukabiliwa na wanasayansi hawa si tofauti na tatizo lenye kukabiliwa na wananyota. Kwa msaada wa vyombo vya aina tofauti, wananyota hutazama mtupo wa nuru itokayo mbali ajabu kwenye nyota, sayari, magalaksi, na magimba ya anga za nje kama vile kwasari. Kwa kutumia vizuri habari zilizopo kwa kadiri wawezavyo, wao husitawisha nadharia kuhusu mambo ya akili nyingi kama vile umbile la nyota na asili ya ulimwengu wote mzima. Ni mara haba wao huwa na fursa ya kuchunguza nadharia zao, lakini wafanyapo hivyo, mara nyingi huzikuta kuwa hazitoshelezi au ni zenye makosa kabisa.
Mwananyota wa redio Gerrit Verschuur aliandika hivi: “Uchunguzi wa ndani sana uliofanywa hivi majuzi na United States kuhusu sayari ulifunua ukosefu mkubwa sana wa maarifa halisi kuhusu vitu vilivyo katika ulimwengu (kosmosi). Kwa kuitazama karibu tukiwa kule juu, ikaonekana kwamba kumbe [sayari] Mars ni tofauti kabisa na vile tungaliweza kuwazia kutoka duniani. . . . Hakuna mwananyota aliyetazamia kwamba mishipi ya [sayari] Jupiter ingekuwa ina umbo la kuvutia jinsi ile . . . [Sayari] Saturn ndiyo iliyoshangaza kwa kadiri kubwa zaidi wakati kamera za Voyager zilipoonyesha wazi kuwa imezungukwa na duara zenye kujisokota, miezi yenye umbo la chura mwenye kuruka kwa kutanua miguu na duara ndogo-ndogo zaidi ya 1,000. . . . Hali ya kushangaza ionwayo katika anga yaonekana kuwa ndiyo ile ile ionwayo katika vitu vya uchunguzi wa maabara ambavyo hupigwa picha kwa darubini zenye kuongezewa ukubwa wakati wote. Kila mtazamo wa karibu zaidi hufunua habari zisizotazamiwa kabisa ambazo hutushangaza sana na kubadili imani zetu za hapo kwanza.”
Wanajeolojia, wanapalontolojia, na wengine ambao huandaa sehemu kubwa ya “uthibitisho” wa mageuzi huhangaikia, kama wananyota, matukio na vitu vya mbali sana—si umbali wa mwendo bali wa miaka. Sawa na vile wanaanga hutegemea kupata habari kutokana na mtupo wa nuru inayosafiri miendo mirefu kwa kadiri isiyowazika, wanasayansi hawa wengine hulazimika kutegemea vidalili vilivyobakia kiaksidenti kutokana na zamani za kale sana za muda wa sayari yetu. Hali moja na wananyota, pasipo shaka ni lazima wao pia wawe hukosea katika maamuzi yao.
Je! Wewe Waweza Kuiamini Biblia?
Kwa hiyo, watu wenye kufikiri hawahitaji kushangazwa mno na maoni ya wanachuo hivi kwamba wasiweze kuiamini Biblia. Hata hivyo, jambo hilo lenyewe tu halithibitishi kwamba wewe waweza kuiamini. Ili uiamini, wahitaji kufanya jambo ambalo wachambuzi wengi wa Biblia hawajafanya—kujifungulia Biblia wewe mwenyewe, na uisome kwa akili iliyofunguka ili kupokea mawazo mapya. (Matendo 17:11) Miaka kadhaa iliyopita, mwandishi wa hati aliye Mwaustralia, aliyekuwa mchambuzi wa Biblia, aliungama hivi: “Kwa mara ya kwanza katika maisha yangu nilifanya jambo ambalo kwa kawaida huwa ndio wajibu wa kwanza wa mwandishi wa habari: kuchunguza kama habari zangu ni za uhakika. . . . Nami nilishangaa mno, kwa sababu mambo niliyokuwa nikisoma [katika masimulizi ya Gospeli] hayakuwa hadithi za mapokeo tu wala hayakuwa hadithi za kutungwa tu kuhusu maumbile. Yalikuwa katika hali ya kuripoti habari. Kusimulia maajabu ambayo mtu amejionea yeye mwenyewe au akaambiwa. . . . Kuripoti habari kwapasa kufanywe kwa njia yenye ladha, na ladha hiyo imo katika zile Gospeli.”
Sisi twakutia moyo ufuate kielelezo chake. Jisomee Biblia wewe mwenyewe. Ufikiriapo hekima ya kina kirefu iliyo katika Biblia, jinsi unabii wayo hutimizwa, na jinsi ilivyo na muungamano wenye kustaajabisha, utang’amua kwamba huo si mkusanyo wa hadithi za kisayansi zilizo za kutungwa tu. (Yoshua 23:14) Ujioneapo mwenyewe jinsi hekima ya Biblia yaweza kubadili maisha yako yawe bora, hutakuwa na shaka lolote kwamba Biblia ni Neno la Mungu. (2 Timotheo 3:16, 17) Ndiyo, wewe waweza kuiamini Biblia!—Yohana 17:17.
[Maelezo ya Chini]
a Wanafunzi wengi wa Biblia wang’amua kwamba nadharia hii ni yenye kosa kwa kuwa Maandiko ya Kigiriki, yaliyoandikwa katika karne ya kwanza W.K., yana kumbukumbu la maandishi ya utimizo wa unabii mwingi wa Maandiko ya Kiebrania ambayo yaweza kuthibitishwa kwamba yaliandikwa karne kadhaa mapema. Kwa kielelezo, utimizo wa karne ya kwanza wa maelezo yote ya Danieli 9:24-27 umeandikwa ama katika Maandiko ya Kigiriki ama na wanahistoria wa mambo ya kilimwengu.
b Ili kupata zungumzo kamili la pambano baina ya mageuzi na uumbaji, ona kitabu Life—How Did It Get Here? By Evolution or by Creation? kilichotangazwa kwa chapa katika 1985 na Watch Tower Bible and Tract Society of New York.
[Picha katika ukurasa wa 7]
Ni jambo gumu kwa wanapalontolojia kutambua yaliyotukia zamani za kaie sana sawa na vile ilivyo vigumu kwa wananyota kutambua umbile la vitu vilivyomo katika majimbo ya mbali sana ya anga ya juu