Maswali Kutoka kwa Wasomaji
■ Kwa sababu gani Mashahidi wa Yehova wamewatenga na ushirika kwa sababu ya uasi-imani watu fulani ambao bado wanadai wanaamini Mungu, Biblia, na Yesu Kristo?
Wale wanaotokeza kipingamizi hicho wanaonyesha kwamba matengenezo mengi ya kidini yanayodai kuwa ni ya Kikristo yanaruhusu watu wawe na maoni ya kutokubaliana. Hata makasisi fulani hawakubaliani na mafundisho ya msingi ya kanisa lao, na bado wanabaki katika msimamo mzuri. Katika karibu madhehebu zote za Jumuiya ya Wakristo kuna wale wanaofasiri Maandiko kulingana na hali za sasa na wale wanaoyafasiri kwa uhalisi kabisa, nao wanatofautiana sana maoni juu ya kuongozwa kwa Maandiko na roho ya Mungu.
Lakini, mifano hiyo haituwekei mfano wa kwamba hata sisi tuwe tukifanya hivyo. Kwa sababu gani? Nyingi za madhehebu hizo zinaruhusu maoni yenye kuachana sana kati ya makasisi na watu wa kawaida kwa sababu wanajisikia kwamba hawawezi kuwa na uhakika ni upi ulio ukweli wa Biblia. Wao ni kama waandishi na Mafarisayo wa siku za Yesu ambao hawakuweza kusema kama watu wenye mamlaka, kama vile Yesu alivyosema akifundisha. (Mathayo 7:29) Tena, kwa kadiri ambavyo wanadini wanaamini kwamba ni sawa kuchangamanisha mafundisho ya imani mbalimbali, wao wanawekwa chini ya wajibu wa kutokujali sana hata ikiwa imani hizo zinatofautiana sana.
Lakini maoni hayo hayana msingi katika Maandiko. Yesu hakufuata maoni mamoja na madhehebu za dini ya Kiyahudi. Wayahudi wa madhehebu hizo walidai kuwa walimwamini Mungu wa uumbaji na kuyaamini Maandiko ya Kiebrania, hasa Sheria ya Musa. Hata hivyo, Yesu aliwaambia wanafunzi wake ‘wajilinde na mafundisho ya Mafarisayo na Masadukayo.’ (Mathayo 16:11, 12; 23:15) Angalia pia jinsi mtume Paulo alivyosema mambo kwa mkazo mwingi: “Lakini ijapokuwa sisi au malaika wa mbinguni atawahubiri ninyi injili yo yote isipokuwa hiyo tuliyowahubiri, na alaaniwe.” Halafu Paulo akayarudia maneno hayo kutia mkazo,—Wagalatia 1:8, 9.
Kufundisha maoni ya mgawanyiko au yaliyo kando hakupatani na Ukristo wa kweli, kama vile Paulo anavyoonyesha wazi kwenye 1 Wakorintho 1:10: “Ndugu, nawasihi, kwa jina la Bwana wetu Yesu Kristo, kwamba nyote mnene mamoja; wala pasiwe kwenu faraka, bali mhitimu katika nia moja na shauri moja. Kwenye Waefeso 4:3-6 alisema tena kwamba Wakristo wanapaswa “kujitahidi kuuhifadhi umoja wa [r]oho katika kifungo cha amani. Mwili mmoja, na [roho moja], kama mlivyoitwa katika tumaini moja la wito wenu. Bwana mmoja, imani moja, ubatizo mmoja. Mungu mmoja, naye ni Baba wa wote.”
Je, umoja huo ungepatikana na kudumishwa huku kila mtu akijichunguzia Maandiko yeye peke yake, kukata mashauri kwa njia yake mwenyewe kisha kuyafundisha? Hata kidogo! Kwa kusudi hilo Yehova Mungu aliandaa “wengine kuwa mitume, wengine kuwa manabii, wengine kuwa waevanjeli, wengine kuwa wachungaji na walimu . . . mpaka sisi sote tuufikie umoja katika imani na katika maarifa sahihi ya Mwana wa Mungu, kufikia mtu mzima.” Ndiyo, kwa msaada wa wahudumu hao, umoja wa kundi—muungano katika fundisho na utendaji—ungeweza kuwapo na ungekuwapo.—Waefeso 4:11-13, NW.
Kwa wazi, msingi wa kushirikiana kwa njia yenye kukubaliwa pamoja na Mashahidi wa Yehova hauwezi kutegemea kuamini tu Mungu, Biblia, Yesu Kristo, na kadhalika. Papa wa Katoliki ya Roma, na pia Askofu Mkuu wa Canterbury wa kanisa Anglikana, wanadai kuwa wanaamini hayo, hata hivyo wao hawashirikiani katika ushirika mmoja. Vivyo hivyo, mtu kudai tu kwamba anaamini mambo hayo hakungempa ruhusu ya kujulikana kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova.
Ili awe na ushirika unaokubaliwa pamoja na Mashahidi wa Yehova, anatakwa akubali ujumla wote wa mafundisho ya kweli ya Biblia, kutia na imani zile za Kimaandiko zinazofuatwa na Mashahidi wa Yehova peke yao. Kama zipi?
Kwamba lile suala kuu lililo mbele ya wanadamu ni juu ya kama Yehova anastahili kuwa na enzi kuu, na hiyo ndiyo sababu imefanya aruhusu uovu uwepo kwa muda mrefu sana. (Ezekieli 25:17) Kwamba Yesu Kristo alitangulia kuwako kabla hajawa mwanadamu, na ni mdogo kuliko Baba yake wa kimbingu. (Yohana 14:28) Kwamba kuna “mtumwa mwaminifu mwenye akili” duniani leo ‘aliyekabidhiwa faida zote za kidunia za Yesu,’ na mtumwa huyo anashirikiana na Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova. (Mathayo 24:45-47) Kwamba mwaka 1914 ulikuwa alama ya mwisho wa Majira ya Mataifa na kusimamishwa kwa Ufalme wa Mungu katika mbingu, na pia wakati wa Kristo kuwapo kama ilivyotabiriwa. (Luka 21:7-24; Ufunuo 11:15–12:10) Kwamba ni Wakristo 144,000 tu watakaopokea thawabu ya kimbingu. (Ufunuo 14:1, 3) Kwamba Har–Magedoni, inayomaanisha pigano la siku ile kuu ya Mungu Mwenye nguvu zote, iko karibu. (Ufunuo 16:14, 16; 19:11-21) Kwamba itafuatwa na Utawala wa Mileani ya Kristo, ambao utarudisha paradiso ya duniani pote. Kwamba wa kwanza kuifurahia watakuwa “mkutano mkubwa” wa sasa wa “kondoo wengine” wa Yesu.—Yohana 10:16; Ufunuo 7:9-17; 21:3,4.
Je! tuna mfano wa Kimaandiko kutuongoza tuwe na msimamo huo wenye vizuizi vigumu? Hakika tunayo! Paulo aliandika hivi juu ya watu fulani katika siku zake: “Neno lao litaenea kama donga-ndugu. Miongoni mwa hao wamo Himenayo na Fileto, walioikosa ile kweli, wakisema ya kwamba kiyama imekwisha kuwapo, hata kuipindua imani ya watu kadha wa kadha.” (2 Timotheo 2:17, 18; ona pia Mathayo 18:6.) Hakuna jambo la kuonyesha kwamba watu hao hawakuamini Mungu, Biblia, na dhabihu ya Yesu. Hata hivyo, kuhusiana na jambo hilo moja la msingi, vile walivyokuwa wakifundisha juu ya wakati ambao ufufuo unatukia, ilifaa Paulo akawabandika jina waasi-imani, ambao Wakristo waaminifu hawangeshirikiana nao.
Vivyo hivyo, mtume Yohana aliwaita wapinga-Kristo wale ambao hawakuamini kwamba Yesu alikuwa amekuja katika mwili. Huenda ikawa waliamini Mungu, Maandiko ya Kiebrania, Yesu akiwa Mwana wa Mungu, na mambo kama hayo. Lakini wao hawakukubali jambo hili, kwamba Yesu kweli alikuwa amekuja katika mwili, na hivyo wakaitwa “mpinga Kristo. Yohana anaendelea kusema hivi juu ya wale wenye kushika maoni hayo tofauti: “Mtu akija kwenu, naye haleti mafundisho hayo, msimkaribishe nyumbani mwenu, wala msimpe salamu. Maana yeye ampaye salamu azishiriki kazi zake mbovu.”—2 Yohana 7,10,11.
Kwa kufuata vielelezo kama hivyo vya Kimaandiko, ikiwa leo Mkristo (anayejidai kuwa anaamini Mungu, Biblia, na Yesu) anaendeleza mafundisho ya uwongo bila kutubu, huenda ikahitajiwa kabisa aondoshwe katika kundi. (Ona Tito 3:10, 11.) Bila shaka, ikiwa ni jambo tu la kwamba mtu huyo ana mashaka au hana habari juu ya wazo fulani, wahudumu wanaostahili watamsaidia kwa upendo. Hilo linapatana na shauri hili: “Endeleeni kuonyesha rehema wengine wenye mashaka; waokoeni kwa kuwanyakua kutoka motoni.” (Yuda 22, 23) Kwa hiyo, kundi la kweli la Kikristo haliwezi kushtakiwa kikweli kuwa linashikilia maoni yalo lenyewe kwa ukatili, bali ni kwamba linauthamini sana umoja ambao linatiwa moyo katika Neno la Mungu liwe nao, na linajitahidi kuuendeleza.