Biblia—Kitabu kwa Ajili ya Wanadamu Wote
“TAZAMA, mkutano mkubwa sana ambao hapana mtu awezaye kuuhesabu, watu wa kila taifa, na kabila, na jamaa, na lugha, wamesimama mbele ya kile kiti cha enzi.”
Huo ni mkutano wa aina gani? Nao wanafanya nini?
“Wana matawi ya mitende mikononi mwao,” maelezo yanaendelea kusema. “[Wanalia] kwa sauti wakisema, Wokovu una Mungu wetu aketiye katika kiti cha enzi, na Mwana-Kondoo.” Hapana, wao si mkutano wa watu wenye ghasia wanaodai jambo fulani au kuandamana kwa kusudi fulani. Bali, ni mkutano wenye furaha na nderemo ambao umetoka sasa hivi kupita katika tukio la kusisimua sana. “Hao ndio wanatoka katika dhiki ile iliyo kuu, . . . Hawataona njaa tena, wala hawataona kiu tena, . . . na Mungu atayafuta machozi yote katika macho yao.”
Ujumbe kwa Ajili ya Wanadamu Wote
“Mkutano mkubwa” huo wa kimataifa umeonyeshwa ulivyo katika kitabu cha mwisho cha Biblia, Ufunuo, sura ya 7, mistari 9 mpaka 17. Kwa njia ya picha, tunaonyeshwa mbele kwenye wakati ambao wanadamu hawatagawanywa tena na kabila, lugha, wala taifa bali wataungana katika amani na upatano na kufurahia uhuru wa kweli usio na woga wala ukosefu wa vitu. Huo wenyewe ni ujumbe usio na kifani ambao Biblia inatolea wanadamu wote.
Lakini, huenda ukauliza, ni kwa njia gani ujumbe huo hauna kifani? Je! si watu katika sehemu zote za ulimwengu wamekuwa wakiongea juu ya amani na umoja? Kwa kweli wamekuwa wakifanya hivyo. Katika kizazi hiki chenye msukosuko wa kimataifa, unaozidishwa na mapambano ya kisiasa, kikabila, kiuchumi na kidini, ni mtu gani mwenye akili nzuri hangehangaikia amani ya ulimwengu? Lakini muda mrefu kabla hakujawa na mapambano hayo ya kimataifa, na muda mrefu kabla kuhifadhiwa kwa uhai wa wanadamu hakujawa jambo la kuhangaikiwa, Biblia ilizungumza juu ya wanadamu wote kufurahia amani na umoja chini ya serikali moja, Ufalme wa Mungu.
Maoni Yanayohusu Ulimwengu Wote Tangu Hapo Mwanzo
Tangu mwanzo wake, Biblia inaonyesha maoni yanayohusu ulimwengu wote inapotaja wakati ujao wa wanadamu. “Zaeni, mkaongezeke, mkaijaze nchi, na kuitiisha” ndiyo amri ya kwanza ambayo Muumba, Yehova Mungu, aliwapa Adamu na Hawa. (Mwanzo 1:28) Adamu na Hawa hawangekuwa babu na nyanya wa kabila au taifa fulani moja tu. Bali, wangekuwa wazaa jamii ya kibinadamu. Mtume Paulo alishuhudia jambo hilo alipowapelekea Wagiriki katika Athene ujumbe wa Biblia. Aliwaambia kwamba Mungu “alifanya kila taifa la wanadamu kutoka katika mmoja, wakae juu ya uso wa nchi yote.”—Matendo 17:26.
Ni lazima tuungame kwamba wazo la jamii nzima ya kibinadamu kuwa ndugu na dada lilikuwapo muda mrefu sana kabla watu kwa ujumla hawajalifikiria. Hata leo, kujapokuwa na maongezi mengi juu ya kuleta amani na udugu wa ulimwenguni pote, je, si kweli kwamba ubaguzi wa kikabila na utaifa unaendelea kuwa kati ya kani zinazosumbua sana wanadamu kwa kuleta migawanyiko mikubwa zaidi? Hata hivyo, Biblia inavipita kwa mbali vizuizi hivyo na vinginevyo. Inasema na watu wa mataifa yote kama kwamba ni jamaa moja kubwa na kuitaja dunia kuwa makao mamoja makubwa kwa ajili ya jamii nzima ya kibinadamu. Katika maana hiyo, Biblia kweli ni kitabu kwa ajili ya wanadamu wote.
Taraja la jamii nzima ya kibinadamu kuishi ikiwa jamaa yenye furaha duniani pote lingalitimizwa kama Adamu na Hawa wangalibaki wakiwa watiifu kwa Yehova Mungu. Lakini mambo hayakuwa hivyo. “Kwa mtu mmoja [Adamu] dhambi iliingia ulimwenguni, na kwa dhambi hiyo mauti; na hivyo mauti ikawafikia watu wote kwa sababu wote wamefanya dhambi,” Biblia inatuambia.—Warumi 5:12.
Kulingana na maelezo hayo, hakuna kabila wala taifa lililo bora wala duni kuliko kabila au taifa jinginelo lote. Hapa tena, Biblia inasema na wanadamu wote bila ubaguzi wala upendeleo. Inaloonyesha tu ni kwamba “wote wamefanya dhambi na hupungukiwa na utukufu wa Mungu.” (Warumi 3:23, NW ) Ingawa huenda watu katika maeneo fulani wakawa na mali nyingi zaidi za kimwili, wakawa na elimu nzuri zaidi, na mambo kama hayo, je, si kweli kwamba kila mahali tunapotazama, tunaona watu wakikabiliwa na matatizo yale yale ya msingi—magonjwa, uzee, kutokamilika, na kifo?
Ahadi ya Kufaidi Wanadamu Wote
Ingawa hali ya kibinadamu ilikuwa imekuwa ya shida kubwa, haikuachwa bila tumaini. Wakati huo wenye kuhitaji hatua ya maana, Yehova Mungu alijihusisha kwa kutoa ahadi. Mungu alimwambia Abrahamu hivi: “Katika uzao wako mataifa yote ya dunia watajibarikia.” (Mwanzo 22:18) Ni kwamba, ahadi hii imekubaliwa na tatu kati ya dini zile kubwa-kubwa za ulimwengu—dini ya Wayahudi, Ukristo, na Uislamu—kuwa sehemu ya imani zao. Ni Biblia peke yake inayofunua hatua-hatua za kutimizwa kwa ahadi hiyo kwa kuandika shughuli ambazo Yehova Mungu alifanya na Abrahamu na wazao wake, kutia na taifa la kale la Israeli.
Lakini hapo ndipo pasipopendwa na watu wengi. Wao wanaona kwamba huo ni mfano mzuri sana wa kupendelea taifa fulani. Kwa sababu hiyo, wanaitupilia mbali Biblia, au angaa sehemu kubwa ya Maandiko ya Kiebrania, kuwa ni mapokeo ya kikabila tu. Lakini je, hiyo ni njia timamu ya kufikiri? Kwa kweli, ni kwa sababu gani Yehova alionyesha uhakika mwingi hivyo na Abrahamu na kumtolea ahadi hiyo?
Biblia inaeleza hivi: “Abrahamu alimwamini Mungu, na kwa imani yake akakubaliwa kuwa mtu mwadilifu; na hivyo Abrahamu akaitwa rafiki wa Mungu.” (Yakobo 2:23, HNWW) Jambo la kupendeza ni kwamba, kitabu kitakatifu cha Kiislamu, Korani, kinaonyesha pia kwamba sababu ya Abrahamu kukubaliwa na Mungu awe rafiki yake ilikuwa imani. “Ni nani mwenye dini bora ila yule anayejitiisha kabisa kwa Allah? Naye ndiye mtenda mema (kwa wengine) na huifuata imani ya Ibrahimu [Abrahamu], yule mnyofu, na Allah alimchukua Ibrahimu awe rafiki.” —SURA 4, mstari 125, kitabu Holy Qur’an, kilichotafsiriwa na M. H. Shakir.
Namna gani Waisraeli? Miaka zaidi ya 400 baada ya Mungu kumtolea Abrahamu ile ahadi, Musa aliwaambia hivi: “[Yehova] hakuwapenda ninyi, wala hakuwachagua ninyi, kwa sababu mlikuwa wengi kuliko mataifa yote, maana mlikuwa wachache kuliko watu wote; bali kwa sababu [Yehova] anawapenda, na kwa sababu alitaka kuutimiza uapo wake aliowaapia baba zenu.”—Kumbukumbu la Torati 7:7, 8.
Kwa hiyo sababu haikuwa kwamba Abrahamu au Waisraeli walikuwa kabila au taifa bora kuliko yale mengine, au kwamba kwa njia yo yote walikuwa watu afadhali kuliko wale wengine. Bali, ni kwa sababu ya upendo wa Mungu na fadhili zisizostahilika alizowaonyesha kwa sababu ya imani na matendo yanayofaa. Mtume Petro alielewesha jambo hilo aliposema hivi: “Mungu hana upendeleo; bali katika kila taifa mtu amchaye na kutenda haki hukubaliwa na yeye.”—Matendo 10:34, 35.
Hivyo, ingawa kwa muda fulani Yehova Mungu alishughulika na taifa la Israeli peke yalo, kwa kweli yeye alikuwa akiifikiria masilahi ya wanadamu wote. Shughuli alizofanya pamoja na Israeli hazikuandikwa katika Biblia ili kuendeleza roho ya utaifa wala kuinua taifa moja juu ya jingine. Bali, “yote yaliyotangulia kuandikwa yaliandikwa ili kutufundisha sisi; ili kwa saburi na faraja ya maandiko tupate kuwa na tumaini.” (Warumi 15:4) Ndiyo, matukio hayo yanakazia upendo na subira ya Mungu katika kuliandaa hatua kwa hatua tumaini la kwamba kwa mara nyingine wanadamu wote wataunganishwa katika amani na upatano. Tumaini hilo litatimizwaje?
Usimamizi kwa Ajili ya Amani
“Ni kulingana na furaha [ya Mungu] njema ambayo alikusudia ndani yake mwenyewe kwa ajili ya usimamizi katika utimilifu wa nyakati zilizowekwa, yaani, kuvikusanya tena vitu vyote pamoja katika Kristo, vitu vilivyomo mbinguni na vitu vilivyo duniani,” Paulo akaeleza. (Waefeso 1:9, 10, NW ) “Usimamizi” huo ni nini?
Neno hilo limetafsiriwa kutokana na neno la Kigiriki oi·ko·no·miʹa, ambalo kwa msingi linamaanisha “njia ya kusimamia jamaa nyumbani.” Hivyo, ingawa wanadamu wamegawanyika kisiasa, kikabila, kiuchumi, na kidini, Mungu amekusudia kuzikomesha kani zote hizi zenye kuleta migawanyiko na kukusanya wanadamu wote watiifu pamoja tena wawe jamaa yenye furaha duniani pote. Atafanyaje hivyo? Atafanya jambo hilo kupitia Ufalme wa Kimasihi ulio mikononi mwa Mwanaye, Yesu Kristo.—Ona Danieli 2:44; Isaya 9:6, 7.
Leo, katikati ya msukosuko na matatizo ya duniani pote, mamilioni ya watu katika sehemu zote za ulimwengu wameuitikia ujumbe wa Biblia unaohusu amani na upatano. Wametokea wakiwa ule “mkutano mkubwa” usiopewa hesabu unaoelezwa katika kitabu cha Ufunuo. Kwa njia ya mfano, wao tayari wanapunga-punga matawi ya mitende mbele ya kiti cha enzi cha Mungu, wakimtolea sifa na utii wao yule “aketiye katika kiti cha enzi,” Yehova Mungu, “na Mwana-Kondoo,” Yesu Kristo.—Ufunuo 7:9, 10.
Je! ujumbe huo unakuvutia wewe? Bila kujali wewe ni kabila, taifa, au lugha gani, kwa kuuchunguza na kuukubali sasa ujumbe wa Biblia, unaweza kujiunga na “mkutano mkubwa” huo wa kimataifa. Ukiwa pamoja nao, unaweza kusema hivi kwa uhakika: “Ziko mbingu mpya na dunia mpya ambazo sisi tunangojea kulingana na ahadi yake, na katika hizo uadilifu utakaa.”—2 Petro 3:13, NW.
Kweli, Biblia inaweza kuwa Kitabu kilichopo kwa ajili yako!
[Picha katika ukurasa wa 5]
Adamu na Hawa ndio waliokuwa wazaa jamii ya kibinadamu
[Picha katika ukurasa wa 7]
Abrahamu, aliyeacha nchi ya kwao, alipata upendeleo wa Mungu kupitia imani na matendo yanayofaa