Maisha na Huduma ya Yesu
Huruma kwa Mwenye Ukoma
WAKATI Yesu na wanafunzi wake wanne wanapotembelea miji ya Galilaya, habari juu ya ajabu anazofanya zinaenea sehemu zote za wilaya. Habari za matendo yake zinafikia mji mmoja ambako kuna mwanamume mwenye ugonjwa wa ukoma. Tabibu Luka anaeleza kuwa mtu huyo alikuwa “amejaa ukoma.” Ugonjwa huo wa kuogopesha sana, ukiwa katika hatua zake za kukolea, unaumbua pole kwa pole sehemu mbalimbali za mwili. Kwa hiyo mwenye ukoma huyo yu katika hali ya kusikitikiwa.
Wakati Yesu anapofika mjini, mwenye ukoma anamkaribia. Kulingana na sheria ya Mungu, mwenye ukoma anapaswa kupaaza sauti ya kuonya akisema, “Ni najisi, ni najisi! ” ili alinde wengine wasimkaribie mno na kuwa katika hatari ya kuambukiwa. Sasa mwenye ukoma huyo anaanguka kifudifudi, na kumwomba Yesu hivi: “Bwana, ukitaka, waweza kunitakasa.”
Lo, mtu huyo ana imani na Yesu kweli kweli! Hata hivyo, hakika ugonjwa wake wa kusikitisha unamfanya aonekane vibaya sana! Yesu atafanya nini? Wewe ungefanya nini? Kwa kuvutwa na huruma, Yesu ananyoosha mkono na kumgusa mtu yule, akisema: “Nataka; takasika.” Halafu ukoma unatoweka na kumwacha mara hiyo.
Je, wewe ungependa mtu mwenye huruma kama huyo awe mfalme wako? Njia ambayo Yesu anamtendea mwenye ukoma huyo inatoa uhakika wa kwamba wakati wa utawala wa Ufalme wake unabii huu wa Biblia utatimizwa: “Atamhurumia aliye dhaifu na maskini.” Ndiyo, hapo ndipo Yesu atakapoitimiza tamaa ya moyo wake ya kusaidia wote wenye kutaabishwa.
Hata kabla ya kumponya mwenye ukoma, huduma ya Yesu imekuwa ikitokeza msisimuko mkubwa kati ya watu. Kwa kutimiza unabii wa Isaya, sasa Yesu anamwagiza hivi mtu huyo aliyeponywa: “Angalia, usimwambie mtu neno lolote.” Halafu anamwagiza hivi: “Enenda zako ukajionyeshe kwa kuhani, ukatoe alivyoamuru Musa kwa kutakasika kwako, iwe ushuhuda kwao.”
Lakini mtu huyo anafurahi sana hivi kwamba anashindwa kunyamaza asieleze wengine habari za muujiza huo. Anaenda zake na kuanza kuzieneza kila mahali. Anaongea sana habari hizo, na inaonekana anafanya watu wapendezwe sana na kuingiwa na hamu nyingi hivi kwamba Yesu anakuwa hawezi kuingia mji kwa njia ya waziwazi. Hivyo Yesu anakaa mahali pa upweke-upweke ambako hakuna mtu anayeishi, na watu wa kutoka kila mahali wanakuja huko kumsikiliza na kuponywa magonjwa yao. Luka 5:12-16; Marko 1:40-45; Mathayo 8:2-4; Mambo ya Walawi 13:45; 14:10-13; Zaburi 72:13; Isaya 42:1, 2.
◆ Ukoma unaweza kuwa na matokeo gani, na mtu mwenye ukoma alipaswa kutoa onyo gani?
◆ Mwenye ukoma mmoja alimsihije Yesu, nasi tunaweza kujifunza nini kutokana na itikio la Yesu?
◆ Mtu aliyeponywa alikosaje kumtii Yesu, na matokeo yalikuwa nini?