Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w86 4/15 kur. 28-30
  • Wewe Utachagua Kazi Gani ya Maisha?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Wewe Utachagua Kazi Gani ya Maisha?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Sababu Inayowafanya Waichague Huduma ya Wakati Wote
  • Kutoa Ushuhuda kwa Kutumia Mashua
  • Kuupendekeza Utumishi wa Wakati Wote
  • Upainia Uliongoza Kwenye Mapendeleo Makubwa Zaidi
  • Wewe Utatumiaje Maisha Yako?
  • Wakumbuke Watumishi wa Wakati Wote
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2014
  • Utumishi wa Painia—Je, Wakufaa Wewe?
    Huduma Yetu ya Ufalme—1998
  • Baraka za Huduma ya Painia
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Shangwe za Utumishi wa Wakati Wote
    Huduma Yetu ya Ufalme—2002
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
w86 4/15 kur. 28-30

Wewe Utachagua Kazi Gani ya Maisha?

JE! WEWE ni mtu mchanga aliye shuleni? Ikiwa ndivyo, inaelekea una baraka ya kuwa na majaliwa yanayoambatana na ujana, afya nzuri na nishati na nguvu nyingi. Mbele yako una maisha marefu kama barabara isiyopata kusafiriwa. Utayatumiaje katika miaka ya mbele?

Unapofikiri juu ya wakati ujao wako, bila shaka akili yako inajawa na maulizo mengi. Je, niende kwenye chuo kikuu, na kutafuta kazi na maisha nikiwa daktari, msomi wa sheria, au mwanasayansi? Je, ndoto ya kupanda ngazi ya kikazi nikapate mafanikio ya kifedha na heshima kati ya watu inanivutia? Je, ningekuwa mtu mashuhuri katika sanaa za kuigiza michezo au kuchora? Au, mimi kijana niliyejitoa kwa Yehova Mungu, napaswa kuichagua huduma ya wakati wote iwe ndiyo kazi yangu ya maisha, hivyo ‘nimkumbuke Muumba wangu katika siku za ujana wangu’?—Mhubiri 12:1.

Mara nyingi magazeti ya habari mbalimbali yanaonyesha maisha ya watu mashuhuri kuwa ya kusisimua na ya kuvutia sana, lakini wewe unajua nini juu ya maisha ya mhudumu wa wakati wote? Je, yanakosa upendezi au ni ya kuchosha? Au ni ya kupendeza na kusisimua kweli kweli? Kufikiria maono fulani yaliyotokea katika maisha ya kweli ya wale ambao wamekuwa katika huduma ya wakati wote muda wa miaka mingi kunaweza kukusaidia ufanye uamuzi.

Sababu Inayowafanya Waichague Huduma ya Wakati Wote

Wakati vita ilipokuwa ikiwaka sana katika Vietnam, Harry alikuwa akihudhuria Chuo Kikuu cha Hawaii, akisomea kuwa mwalimu wa historia. Alikuwa pia akijifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Yeye alihusika kama wengi wa wanadarasa wenzake katika mawazo ya kutaka mapinduzi makubwa ya utawala yaliyokuwa kawaida ya wanafunzi wakati huo, kisha akaanza kutumia dawa za kulevya, na kuiona dawa ya LSD kuwa ya kusisimua zaidi. Asubuhi moja aliamka katika jengo alimokuwa akiishi akakuta sakafu imetapakawa na chupa za pombe, vipande vya sigareti, na wanaume na wanawake. Harry hakuweza kukumbuka sana ilivyokuwa ila kwamba kulikuwa kumetokea ubishi pamoja na polisi kwamba waonyeshe cheti chao cha kufanya ukaguzi kabla hawajaanza upekuzi wao, kisha mwenye jengo hilo akatisha kuwafukuza. Mambo yalipofikia hapo ndipo yeye alipoamua ama aache kujifunza Biblia ama asafishe maisha yake. Alitumia hekima akachagua kusafisha maisha yake.

Harry alipoendelea kuongeza maarifa yake ya Biblia, aliacha kuvutiwa na elimu ya chuo kikuu na kazi ya maisha ya ualimu. Akaondoka chuoni, akatafuta kazi ya kibarua, akabatizwa, na baada ya muda mfupi akastahili kuwa painia—mhubiri wa wakati wote. Hivyo Harry akaanza kazi mpya ya maisha, yenye kujawa na mambo yenye matatizo, mafaa na upendezi.

Walipokwisha kuwa mapainia wa pekee, Harry na mkeye waligawiwa kuwa wamisionari Belau kwenye “visiwa vyenye miamba” ya kupendeza katika Pasifiki ya Magharibi ambako wangali wanatumikia. Maisha ya umisionari yakoje katika visiwa hivyo?

Kutoa Ushuhuda kwa Kutumia Mashua

Ushuhuda mwingi katika visiwa vya Micronesia unafanywa kwa kusafiria mashua na miguu. Harry na mkeye, Rene, wanaikumbuka mara ya kwanza wao kutoa ushuhuda kwa mashua katika kisiwa cha mbali kidogo. “Tulikaa katika nyumba iliyokuwa maili nyingi upande wa juu wa mto wenye kupindika-pindika uliojipota-pota kupitia vichaka vya mikandaa na msitu uliosongamana sana hivi kwamba tulichoweza kuona juu yetu ni rangi ya kijani kibichi tu,” anakumbuka. “Tulipokuwa tukitoka mahali pa makao yetu, tulikuwa tukisafiri mtoni, tunasimama kuwahubiri watu walioishi kandokando ya kingo za mto. Jioni moja kabla tu ya giza kuingia, tulikuwa tukitoka utumishi wa shambani na kupanda kutoka mtoni kwenda nyumbani kwetu usiku huo. Kwa ghafula Rene akapiga ukelele. Mimi nilizunguka haraka nikaona maji yakitikisika haraka na mkia mrefu wa kiumbe wa majini ukiingia mtoni. Alikuwa ni mamba wa maji ya chumvi—akiwa ni wa aina ile kubwa zaidi ulimwenguni. Tunashukuru kwamba tulifika nyumbani salama salimini. Ingawa ulikuwa wakati wa kuogea mtoni, baada ya kumwona mamba huyo mkubwa sana tuliwaza ilikuwa salama zaidi kufunga ndoo kwa kamba na kuyavuta maji ya kuogea ndani ya mashua yetu.”

Kwa kuwa vijiji na nyumba nyingi haziwezi kufikiwa kwa kutumia gari wala kwa mashua, wamisionari wanatumia saa nyingi wakipiga miguu kupitia vijia vya msituni vyenye minazi kandokando na mazingira ya kupendeza macho ili kuwafikia watu wanyenyekevu wenye urafiki. Harry anasema: “Mara nyingi watu hao wanaokaa peke yao wanaonyesha ukaribishaji. Wanapanda mnazi, wanachuma nazi, wanaikata ile sehemu ya juu kwa kishoka, na kukupa maji yake unywe kwa mdomo bila kutumia kikombe. Yanaburudisha sana, ni yenye ladha nzuri na yenye kujenga mwili.”

Jitihada za kuhubiri za wamisionari katika Belau zimethawabishwaje? Sasa wana kundi lenye Wakristo wa kweli 42. Kwa wastani, kumi kati yao walikuwa katika huduma ya wakati wote kila mwezi mwaka uliopita, na watu 193 walihudhuria Ukumbusho wa kifo cha Kristo mwaka 1985.

Baada ya kuwa katika utumishi wa wakati wote miaka 17, sasa Harry anajisikiaje juu ya uamuzi alioufanya kutumia maisha yake katika utumishi wa Yehova kwa ukamili? “Kama mimi nisingaliupata ukweli wa Mungu miaka 17 iliyopita, ningalipoteza wakati na maisha yangu kufuatia mambo ya kilimwengu,” anasema. “Singalipata amani ya akili wala usalama ambao nimeupata wakati wa miaka yangu ya kuwa painia na mmisionari, nikiwa mseja kwa miaka mingi na pia baadaye nikiwa pamoja na Rene ambaye nimeshiriki naye miaka minane iliyopita katika umisionari.”

Kuupendekeza Utumishi wa Wakati Wote

Milton alikuwa akihudhuria shule ya sekondari katika Hawaii. Ingawa wengine walikuwa wakimtia moyo ajitahidi kufikia kazi ya maisha yenye usalama wa kifedha, dada yake na kaka zake wawili walikuwa tayari katika upainia wa wakati wote. Mifano yao ilimtia moyo hata yeye afikirie kuingia katika huduma ya wakati wote. Zaidi ya hivyo, alisikia hotuba juu ya baraka za utumishi wa wakati wote na jinsi Yehova atakavyotuandalia mahitaji yetu ya kimwili tukimtumaini na kumtanguliza katika maisha zetu. Milton anasimulia hivi: “Jambo hilo lilinisukuma nichague huduma ya wakati wote kuwa kazi yangu ya maisha. Kwa hiyo kabla sijamaliza shule ya sekondari, nilibatizwa na nikaingia utumishi wa wakati wote.”

Milton alipoanza kupainia, mapainia katika kundi lao walikuwa chini ya kumi. Basi alifanya nini? “Nilikaribisha ndugu vijana wafanye kazi nami katika utumishi wa shambani,” anasema. “Matokeo yakawa kwamba wengi wao walijiunga nami baadaye katika utumishi wa wakati wote.”

“Shemeji yangu wa kiume alikuwa mzee na painia,” Milton anaendelea kusema. “Tulikuwa katika kundi moja na tulishirikiana kuwatia wengine moyo wapainie. Ikaamuliwa kwamba mimi ningewatia moyo vijana-matineja, naye angewatia moyo wake wenye shughuli za kinyumbani. Baada ya miezi kadha, walikuwako wahudumu 25 wa wakati wote kundini. Mwangalizi wa mzunguko alipokuja, alikaribisha kumi kati yao wafanye maombi ya upainia wa pekee na kuhamia makundi ya karibu. Halafu tukauzungumza mradi wa kusaidia kumi zaidi waingie katika utumishi wa painia ili wajaze nafasi za wale waliokuwa wametumwa nje. Kufikia ziara ya mwangalizi wa mzunguko iliyofuata, wengine 15 walikuwa wamechukua utumishi wa wakati wote. Sasa tukawa tuna mapainia 30. Halafu tena mwangalizi wa mzunguko akaomba kumi kati yao wahamie makundi mengine. Hapo tena tukaanza kupanga kupata wengine wa kujaza nafasi za walioondoka. Kabla ya ziara ya mwangalizi wa mzunguko iliyofuata, wengine 20 wakafanya maombi ya utumishi wa painia! ”

Roho ya painia yenye kuambukia imewaingia vijana pia. Kufikia wakati ambao walihitimu kwenda shule ya sekondari, karibu wote walikuwa wamejiwekea mradi wa kufanya utumishi wa wakati wote. Dada mmoja aliamua kufanya upainia akiwa na umri wa miaka 13. Alisema: “Hilo ndilo lililoelekea kuwa jambo la asili kufanya.” Yeye na vijana wengine kundini hawakufikiria tena kwa uzito jambo jingine lo lote. Ushuhuda wa kikundi ukapangwa uwe ukifanywa baada ya shule, na mwishowe wanafunzi 60 kutoka shule tatu mbalimbali wakawa wakiunga mkono utendaji huo pamoja na mapainia. Wakati wa miezi ya kiangazi, ilitia moyo sana kuona hesabu inayofikia 130 wakikusanyika kwa ajili ya ushuhuda wa kikundi!

Upainia Uliongoza Kwenye Mapendeleo Makubwa Zaidi

“Mwaka 1974,” anakumbuka Milton, “nilialikwa nikubali kazi ya misionari katika mgawo uliokuwa kilometa 6,440 kutoka nyumbani —visiwa vya Belau katika Micronesia.” Tatizo moja lililochukua muda mwingi ili kulizoea lilikuwa “kutembea miendo mirefu kwa kupita kati ya mimea mibichi ya tropiki na kusafiri kwa mashua.”

Siku moja yenye joto jingi, baada ya kutembea muda wa saa nyingi katika njia zenye mavumbi-mavumbi, Milton anakumbuka kwamba “tulikuwa tumechoka sana tulipofikia nyumba ya jamaa yenye kupendezwa. Mama alituma mwanaye ateremke mtoni. Akarudi akiwa na tunda kubwa sana la tikiti lililotiwa baridi na maji ya mtoni. Tulikula zaidi ya nusu, na wee, liliburudisha kama nini! ”

Mwaka mmoja baada ya kuwa katika mgawo wake wa umisionari, Milton alitamani kuona miradi mitatu ikitimizwa katika Belau, yaani, mwishowe ndugu wa hapo wachukue madaraka ya kundi, vijana waingie utumishi wa wakati wote, na kundi lijijengee Jumba la Ufalme lao wenyewe. Sasa yeye anaeleza; “Baada ya kukaa hapa miaka kumi, sala zangu za kuiona miradi yote mitatu ikitimizwa zinaendelea kujibiwa.”

Je, Milton anaona alifanya uchaguzi unaofaa miaka 14 iliyopita alipoingia utumishi wa wakati wote uwe kazi yake ya maisha? “Jambo moja ambalo nimejifunza kutokana na miaka yangu yote katika utumishi wa wakati wote ni hili: Tukiwa na nia, Yehova atatutumia katika wakati unaofaa,” ndivyo anavyojibu. “Haitupasi kamwe kuacha kujitoa kwa nia katika utumishi wake. Hutajuta kamwe kwamba ulifuatia maisha ya kumtumikia Yehova ukiwa mhudumu wa wakati wote.”

Wewe Utatumiaje Maisha Yako?

Ninyi vijana, mtatumiaje wakati ujao wenu? Kwa faida yenu wenyewe, au kwa ajili ya Yehova kabisa? (Warumi 14:8) Fikiria sasa kwa sala utumishi wa wakati wote katika ujana wako. Iga Yesu kwa kuishi sehemu iliyobaki ya maisha yako “kwa ajili ya mapenzi ya Mungu.” (1 Petro 4:2, NW ) Kufanya hivyo kutakuwa ulinzi usipatwe na tamaa za makuu, kazi za maisha, na mashirika ya kilimwengu yenye kudhuru. Changanua hali zako na ujiwekee tarehe fulani ya wazi iwe mradi wako wa kuingia utumishi wa wakati wote. Jitahidi kuufikia mradi huo. Sali upate msaada wa Yehova ili uufikie.—Waefeso 6:18.

Uchaguzi wa kufanya upainia uwe kazi ya maisha ungeweza kukuongoza kwenye mapendeleo mengi mazuri ya utumishi kwa kadiri usiyotazamia. Maisha yako yatajawa na furaha, usalama, na upendo. Yatakuwa ya kusisimua, ya kupendeza, na kuridhisha. Juu ya yote, yatakuwa maisha yenye kumpendeza Yehova.—Mithali 27:11.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki