Je! Wewe Unaweza, Kukubali Nidhamu?
‘SIKU hizi wazazi wanapiga Tam Tam tu (ngoma ya kuchezea dansi), si watoto wao.’ Elezo hilo lilisikiwa likisemwa na wasichana wa shule katika chuo kimoja cha Afrika. Walimaanisha nini? Kwamba nidhamu imekuwa jambo la kizamani. Wazazi hawataki kuitoa, na watoto wanafurahi sana kutokupokea nidhamu.
Je, ni mielekeo ya hekima? Kulingana na kamusi, nidhamu hasa ni “mazoezi yanayosahihisha, kurekebisha, au yanayokamilisha nguvu za akili au tabia ya kiadili.” Je, kweli mtu ye yote anaweza kuendelea vizuri bila aina hiyo ya nidhamu? Kwa sababu gani wasichana hao wa shule wa Afrika—na wazazi wao—wanafikiri kwamba wanaweza kuendelea vizuri bila nidhamu?
Kwa kweli, mwelekeo usio wa maoni mazuri juu ya nidhamu hauonyeshwi na wasichana wa shule wa Afrika na wazazi wao tu. Inaonekana kwamba walio wengi leo wanaliona shauri lo lote au nidhamu kuwa ni kuingilia uhuru wao bila ruhusa, kukatiza haki zao. Lakini, mwelekeo wa nanma hiyo haukutokea katika karne 20 tu. Maelfu ya miaka iliyopita, Mungu mwenyewe aliona kwamba “mawazo ya moyo wa mwanadamu ni mabaya tangu ujana wake.” (Mwanzo 8:21) Akionyesha matokeo ya kuwako kwa maelfu ya miaka ya mwelekeo huo mbaya, mtume Paulo aliandika: “Watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda fedha, wenye kujisifu, wenye kiburi, wenye kutukana, wasiotii wazazi wao, wasio na shukrani, wasio safi, wasiopenda wa kwao, wasiotaka kufanya suluhu, wasingiziaji, wasiojizuia, wakali, wasiopenda mema, wasaliti, wakaidi, wenye kujivuna.” (2 Timotheo 3: 2-4) Si ajabu kwamba nidhamu haipendwi na watu wengi!
Kweli Nidhamu Ni Mbaya Sana?
Je, kweli Mkriso anahitaji nidhamu? Basi, Yesu alisema kwamba ile njia ya uzima “imesonga.” (Mathayo 7:13, 14) Ni rahisi kuwaya-waya na kuiacha. Kwa hiyo je, halingekuwa jambo la hekima kukubali nidhamu, mazoezi kama vile kamusi inavyoyaita? Fikiria kisa cha msafiri anayewaya-waya bila kutazamia na kuiacha njia yake kisha anajikuta akiwa karibu sana na eneo la hatari. Ikiwa mtu asiyemjua angemwonyesha jinsi ya kurudia njia yake, yeye angeitikiaje? Je, angeukataa msaada huo kwa hasira, akisisitiza ya kwamba ana haki ya kwenda anakotaka? Je, angemshtaki yule mtu mwenye urafiki asiyemjua kuwa anajidukiza katika haki zake? Ni vigumu. Angeshukuru kwa msaada aliotolewa.
Kwa hiyo Mkristo mwenye hekima anashukuru anapotolewa msaada kwa kupewa nidhamu yenye ufadhili. Maneno ya nabii ni ya kweli hata umri au ujuzi wetu maishani uwe nini: “Ee [Yehova], najua ya kuwa njia ya wanadamu haimo katika nafsi yake; kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa wanadamu.” (Yeremia 10:23) Kwa hiyo, sisi sote tunahitaji nidhamu.
Walikataa Nidhamu
Mtu mmoja aliyekataa nidhamu alikuwa Kaini, aliyemwonea wivu Habili ndugu yake. Alipoona kwamba Kaini alikuwa akianza kuwaya-waya kuiacha njia inayofaa, Yehova mwenyewe alimwonya kwa upole, akamuuliza: “Kwa nini una ghadhabu? na kwa nini uso wako umekunjamana? Kama ukitenda vyema, hutapata kibali? Usipotenda vyema dhambi iko, inakuotea mlangoni, nayo inakutamani wewe, walakini yapasa uishinde.” (Mwanzo 4:6, 7) Lakini Kaini hakusikiliza. Alimwua Habili ndugu yake na hivyo akaanzisha uuaji katika historia ya kibinadamu.—Mwanzo 4:8-16.
Katika siku za Samweli, wana wa Eli pia hawakukubali nidhamu. Baba yao alikuwa ndiye kuhani mkuu kwenye patakatifu pa Yehova, lakini wanaye walitumia cheo chao kuiba matolea na kushawishi wanawake wafanye uasherati pamoja nao. Baba yao aliwakemea—kwa unyonge kidogo—lakini wao hawakusikiliza. Matokeo yakawa nini? Kukataa nidhamu kulifanya wauawe katika pigano, naye Eli akafa kwa kushtuliwa na habari hizo—1 Samweli 2:12-17, 22-25; 3:11-18; 4:1-4, 10-18.
Lakini Wengine Walisikiliza
Lakini, wengine walikubali nidhamu. Daudi mfalme na mwanaume wa vita, alifanya uhalifu mbaya sana aliposababisha kifo cha Uria, mwanamume ambaye yeye alikuwa amefanya uzinzi na mke wake. Lakini Daudi alilikubali kemeo ambalo Mungu alipeleka kupitia nabii Nathani, na hivi Yehova hakumkataa yeye. (2 Samweli 12:1-14) Ndiyo, nidhamu inaweza kutusaidia tupone hata kutokana na dhambi zilizo nzito sana.
Ayubu alishauriwa na kijana Elihu na angaliweza kulikataa shauri hilo kwa hasira. Ingawa Ayubu alikuwa ameumizwa sana na Shetani, yeye alikuwa amekataa ‘kumlaani Mungu kisha afe.’ Kwa sababu ya kutenda, angaliweza kukosa kuona sababu ya kulisikiliza shauri la kijana huyo. Ingawa hivyo, Ayubu alilisikiliza na akajua kwamba, ijapokuwa alikuwa na ukamilifu, mwelekeo wake wa akili ulihitaji rekebisho fulani. Ndipo alipopata pendeleo la kupokea mashauri kutoka kwa Yehova mwenyewe na mwishowe akathawabishwa kwa kupewa baraka nyingi. (Ayubu 2:9, 10; 32:6; 42:12-16) Hivyo, nidhamu inaweza kusaidia hata wale walio na kumbukumbu za kutokeza za uvumilivu na uaminifu.
Mtume Petro, pia, alipokea nidhamu. Kumbuka, Petro alikuwa mtume wa Yesu Kristo, shahidi wa njozi ya kugeuka sura kwa Yesu, na ndiye Kristo aliyemkabithi “funguo za Ufalme.” (Mathayo 16:18, 19) Hata hivyo, katika pindi moja mtume Paulo, ambaye kwa kulinganishwa alikuwa mfuasi mpya wa Yesu alimtia nidhamu hadharani Petro kwa sababu ya mwenendo wake katika kundi la Antiokia. Ni wazi kwambu Petro aliikubali nidhamu hiyo, kwa maana baadaye yeye alinena juu ya “ndugu yetu mpenzi Paulo.” (2 Petro 3:15; Wagalatia 2:11-14) Kwa hiyo, Mkristo mwenye mapendeleo mengi, pia, anaweza kutazamia kupokea nidhamu.
Wakristo wa Kisasa na Nidhamu
Katika kundi, hatupaswi kushangaa tukipokea shauri kutoka kwa mtu ye yote aliyekomaa. Lakini wale hasa waliokabidhiwa daraka la kuchunga faida zetu ni wazee waliowekwa rasmi. Wachungaji hao wa kiroho ndio wanaambiwa hivi na Biblia: “Fanya bidii kuijua hali ya makundi yako; na kuangalia sana ng’ombe zako.”—Mithali 27:23.
Tunaweza kusaidika tukubali nidhamu tukitambua kwamba upendo wa kweli, na pia ushujaa, vinahitajiwa ili wazee watoe shauri. Wazee wanajibiwa vikali mara nyingi wanapojaribu kusaidia. Kwa mfano, mzee mmoja Mwafrika alisema na mwanamke aliyekuwa amekuwa Mkristo kwa muda mrefu, akimwonya kwamba alikuwa akijihusisha na jambo fulani lisilo la Kikristo. Ilikuwa vigumu kutoa shauri hilo, na ugumu wenyewe uliongezeka wakati mwanamke huyo alipoudhika. Hatimaye, shauri hilo lilikataliwa kisha yule aliyepewa shauri hilo akakata kabisa uhusiano wake na mzee aliyekuwa amejaribu kumsaidia. Mwanamke huyo angalikuwa mwenye hekima zaidi kama angalikumbuka kwamba ‘jeraha utiwazo na rafika ni amini.’—Mithali 27:6.
Nidhamu inaweza kutusaidia tutumie mithali nyingine ya Biblia: “Mwenye busara huyaona mabaya na kujificha; bali wajinga huendelea mbele wakaumia.” (Mithali 22:3) Maneno hayo yangalimsaidia mwanamume Mkristo katika nchi ile ile. Yeye aliingia katika tabia ya kwenda-kwenda kwenye mikahawa ya watu wote bila mke na watoto wake. Wengine walifadhaishwa na jambo hilo kwa sababu katika eneo hilo wasichana wenye kutumikia watu katika mingi ya mikahawa walikuwa malaya wenye kutafuta watu kwa shughuli yao. Kwa hiyo wazee wa kule walisema mara kadha na mwanamume huyo juu ya jambo hilo. Lakini yeye alikataa shauri alilopewa, kwa ukali mara nyingi. Mwishowe, alianguka katika mtego wa uasherati. Angalikuwa mwenye hekima zaidi kama angalitii shauri hilo lenye kusudi zuri!
Kama tutasahaulia mbali kwa kitambo maoni yetu yenyewe na kujaribu kuona mambo kama Yehova ayaonavyo, tutakubali nidhamu kwa upesi zaidi. Ni kweli kwamba nidhamu inaweza kuwa inatukumbusha hali zetu wenyewe za kutokukamilika kwa njia isiyofurahisha. Inaweza kutufanya tujisikie tumepoteza kidogo heshima yetu. Lakini ebu fikiria jinsi Yehova anavyofurahi wakati watumishi wake wanapotenda kwa hekima na kuepuka kutumbukia katika dhambi. “Mwanangu, uwe na hekima,” Neno lake linasema “na kunifurahisha moyo wangu; ili nipate kumjibu anilaumuye.” (Mithali 27:11) Tukiweza kukimeza kiburi chetu na kukubali nidhamu inayotolewa, tutakuwa kati ya wale ambao wanampa Yehova jibu kwa mashtaka anayofanyiwa na Shetani.
Nidhamu Inazaa Matunda Mema
Kama vile tumeona, sisi sote tunahitaji nidhamu. Inahitajiwa na wanaume na wanawake, vijana na wazee, wale ambao wamekaa katika ukweli kwa muda mrefu na wapya zaidi. Kwa hiyo, inatupasa tutazamie nidhamu, hata kuitafuta. Jifunze neno la Mungu na uone linasema nini kukupa mashauri wewe. (2 Timotheo 3:16, 17) Hudhuria mikutano na usikilize kwa makini uone ni mambo gani yanayokuhusu wewe. (Waebrania 10:24, 25) Wewe binafsi ukipewa nidhamu ya kimaandiko yenye upendo, kwa vyo vote ikubali katika roho ambayo imetolewa. Yatumie kwa faida mazoezi yo yote ya kukusahihisha yanayotoka kwa Yehova.
Paulo aliwaambia Waebrania hivi: “Kila adhabu wakati wake haionekani kuwa kitu cha furaha, bali cha huzuni; lakini baadaye huwaletea wao waliozoezwa nayo matunda ya haki yenye amani.” (Waebrania 12:11) Hivyo, ingawa huenda nidhamu ikaumiza nyakati nyingine, ina matokeo mazuri. Kukubali nidhamu kunaweza kutusaidia tuwe kati ya wale wanaofurahisha Yehova. Nidhamu itatusaidia ‘twende kwa ukamilifu, tutende haki, na kusema kweli kwa moyo wetu.’ (Zaburi 15:1, 2) Basi, acheni sisi sote tuikubali nidhamu.