Kusali Mbele ya Wengine Kwa Moyo Mnyenyekevu
ILIKUWA siku ya kupendeza katika historia ya Kiisraeli. Mfalme Daudi alikuwa amepanga Sanduku la Yehova liletwe liingizwe katika mji mkuu mpya, Yerusalemu. Kwa shangwe, yeye alimsifu Yehova mbele ya watu wote, akamalizia sala ya kutoka moyoni kwa maneno haya: “Na awe mbarikiwa Yehova Mungu wa Israeli kutoka umilele mpaka umilele.” Wakiwa na mioyo iliyojaa, wenye kusikiliza “walisema ‘Amin’ na kumpa Yehova sifa.”—1 Mambo ya Nyakati 16:36, The Bible in Living English
Katika nyakati za kale, lilikuwa jambo la kawaida sana mtu mwenye kustahili kati ya watu wa Mungu kuwakilisha wengine katika sala kwa njia hiyo. Na watumishi wa Yehova leo wana zoea lile lile. Mikutano ya kundi, makusanyiko, nyakati za jamaa kula, na mafunzo ya nyumbani ya Biblia ni baadhi ya pindi ambapo wanaume Wakristo—na nyakati nyingine wanawake—wanakuwa na pendeleo la kuwakilisha wengine katika sala. (1 Wakorintho 11:4, 5) Matokeo yanakuwa nini? Kama ilivyokuwa katika siku za Daudi, wale wanaosikiliza na kusema “Amin” wanajengwa na kujisikia kwamba uhusiano wao na Yehova umetiwa nguvu.
Kuwakilisha wengine katika sala ni daraka zito. Ni lazima yule anayesali aeleze mawazo yanayoonyesha vya kufaa mambo yaliyo katika mioyo ya wenye kusikiliza. Sala yake inaleta matokeo fulani juu ya hali yao ya kiroho. Kwa hiyo, ingefaa wale wanaofurahia pendeleo hilo waonyeshe maoni yaliyo katika ombi la Daudi: “Sala yangu ipae mbele zako kama uvumba.”—Zaburi 141:2.
Tunaweza kutayarishaje sala zetu ili ziwe na harufu tamu kama uvumba mbele za Yehova? Ni kwa kutangulia kufikiria tutakayoyasema kulingana na uongozi ambao Yehova ameandaa. Biblia ina sala nyingi sana zilizo mifano mizuri na pia mashauri mengi bora juu ya habari ya sala. Kuzifikiria habari hizi kutatufundisha kanuni za maana zinazosaidia sana tunaposali kwa kusikiwa na wengine na kwa ajili yao.
Kwa Moyo Mnyenyekevu
Moja ya kanuni hizo ni kwamba Yehova anasikiliza sala zinazotolewa na watu wanyenyekevu. (2 Mambo ya Nyakati 7:13, 14) Mtunga zaburi anatuambia: “Ingawa [Yehova] yuko juu, amwona mnyenyekevu, naye amjua mwenye kujivuna tokea mbali.” (Zaburi 138:6) Ili kuona mfano mmoja, fikiria unyenyekevu wa Mfalme Sulemani katika sala aliyotoa mbele ya watu kwenye wakfu wa hekalu. Muda mfupi tu ulikuwa umepita tangu amalize ujenzi wa moja la majengo yenye fahari nyingi zaidi yaliyopata kuonekana katika dunia hii, lakini jambo hilo halikumtia majivuno. Bali, yeye alisali hivi: “Mungu je! yamkini atakaa na watu duniani? Tazama, mbingu na mbingu za mbingu za mbingu hazikutoshi; siuze nyumba hii niliyoijenga! ”—2 Mambo ya Nyakati 6:18.
Sisi pia tunapaswa kuwa wanyenyekevu, hasa tunaposali kwa ajili ya wengine. Kwa sehemu moja, unyenyekevu unaonyeshwa na namna ya sauti. Bila shaka, inawapasa Wakristo waepuke unyenyekevu wa uwongo au kujisingizia utakatifu. Lakini sala za unyenyekevu hazisikiki kuwa zenye maneno makuu wala za kujionyesha. (Mathayo 6:5) Unyenyekevu unaonyeshwa, pia, na mambo tunayosema. Tukisali kwa unyenyekevu, hatutadai kwamba Yehova afanye mambo fulani. Bali, tutaomba kwamba akubali kutenda kwa njia inayopatana na mapenzi yake.—Linganisha Zaburi 118:25.
Unyenyekevu, pia, utatuongoza tuepuke kutumia sala kuthibitisha jambo fulani au kutolea watu mmoja mmoja mashauri ya kibinafsi. Ama sivyo, tutakuwa tukionyesha roho iliyodhihirishwa na Mfarisayo katika mmoja wa mifano ya Yesu. Yesu alinena juu ya Mfarisayo na mkusanya-kodi waliokuwa wakisali wakati ule ule mmoja hekaluni. Mfarisayo alisema: “Ee Mungu, nakushukuru kwa kuwa mimi si kama watu wengine, wanyang’anyi, wadhalimu, wazinzi, wala kama huyu mtoza ushuru. Mimi nafunga mara mbili kwa juma; hutoa zaka katika mapato yangu yote.” Lakini mkusanya kodi huyo (mtoza ushuru) aliendelea kujipiga-piga kifua, akisema: “Ee Mungu, uniwie radhi mimi mwenye dhambi.” Yesu alimaliziaje? “Huyu [mkusanya kodi] alishuka kwenda nyumbani kwake amehesabiwa haki kuliko yule [Mfarisayo].”—Luka 18:9-14.
Watumishi wa Yehova walio wanyenyekevu kweli kweli wanatambua pia cheo walicho nacho mbele zake. Wao wako chini kidogo kuliko malaika, hali Yehova ndiye Mwenye Enzi mkuu zaidi wa ulimwengu wote, wa milele. (Zaburi 8:3-5, 9; 90:1-4) Wakati watu mmoja mmoja wanapopata nafasi ya kusema na wafalme au watawala wa ulimwengu huu, kwa kawaida wanafanya hivyo kwa heshima na fahari, wakilithamini sana pendeleo hilo. Je, tupunguze heshima na uthamini wetu tunaposema na “Mungu aliye hai, Mfalme wa milele”? (Yeremia 10:10) Hapana. Hivyo, kusema maneno kama, “Habari ya alasiri, Yehova” au, “Tunataka kusema nawe, Yehova” hayafai katika sala, hali moja na maneno ya kimaongezi kama, “U hali gani leo? ” “Mpe Yesu salamu zetu,” au, “Uwe na siku nzuri.”—Linganisha Mhubiri 5:1, 2.
Ingawa hivyo, je, mtume Paulo hakusema kwamba tunapaswa kumfikia Yehova “kwa uhuru wa kusema”? (Waebrania 4:16, NW; linganisha 1 Yohana 3:21, 22, NW.) Je, hiyo haitupi sisi uhuru wa kusema kama tuonavyo inafaa? Sivyo hasa. Maneno ya Paulo yalimaanisha kwamba kwa sababu ya dhabihu ya Yesu tunaweza kumfikia Yehova ijapokuwa tuna hali yenye dhambi. Tunaweza kumfikia katika sala wakati wo wote na kuhusu habari yo yote. Lakini hata tunaposali tukiwa na uhuru wa kusema, ni lazima tutambue kwa unyenyekevu kwamba sisi ni watu wadogo sana. Hivyo, Yehova alisema: “Mtu huyu ndiye nitakayemwangalia, mtu aliye mnyonge, mwenye roho iliyopondeka, atetemekaye asikiapo neno langu.”—Isaya 66:2.
Mashauri Yenye Maonyo
Yesu Kristo alitoa mashauri zaidi juu ya sala katika Mahubiri ya Mlimani yake. Katika mahubiri hayo alionya kwamba wakati tunaposali haitupasi ‘kurudia-rudia kusema mambo yale yale, kama mataifa wafanyavyo.’ (Mathayo 6:7, NW ) Hiyo haimaanishi kwamba haitupasi kurudia kusali juu ya habari ile ile moja (mradi tuna uhakika ndilo jambo linalofaa kusali). Tunaambiwa hivi: “Endeleeni kuomba, nanyi mtapewa; endeleeni kutafuta, nanyi mtapata; endeleeni kubisha, nanyi mtafunguliwa.” (Mathayo 7:7, NW ) Bali, onyo la Yesu lilimaanisha kwamba haitupasi kurudia-rudia mambo mpaka yawe hayana maana. Ndiyo kusema, “Usitamke marudio-rudio matupu.”—Mathayo 6:7, maelezo ya chini, Biblia ya Marejezo ya New World.
Watu fulani wana desturi ya kurudia-rudia misemo ile ile katika sala bila kuyafikiria maneno yenyewe. Nyakati nyingine misemo hiyo inakuwa na maneno ambayo mwenye kusali hayafahamu. Hiyo ni namna moja ya ‘rudio-rudio tupu.’ Nyingine ni hii: Wazia Mkristo anayeingia kwa uzembe katika tabia ya kutumia-tumia maneno yale yale kila siku anapomtolea Yehova sala. Mwishowe, vifungu hivyo vya maneno vinakosa maana. Hata jina la kimungu, Yehova, linaweza kutumiwa kwa njia hii. Ni kweli kwamba tunahimizwa tuliite jina la Yehova. (Zaburi 105:1) Lakini tukitumia jina hilo mwishoni mwa karibu kila sentensi katika sala yetu, unakuwa kama kitabia kisichofaa au ‘rudio-rudio tupu.’
Paulo aligusia kanuni nyingine ya maana alipoandika hivi: “Nikiomba kwa lugha, roho yangu huomba, lakini akili zangu hazina matunda. . . . Wewe ukibariki [ukisifu, NW ] kwa roho, yeye aketiye katika mahali pa mjinga ataitikiaje, Amina, baada ya kushukuru kwako, akiwa hayajui usemayo? ” (1 Wakorintho 14:14-16) Katika siku za Paulo Wakristo fulani walipokea kipawa cha kimuujiza cha kusema lugha mbalimbali, na kwa wazi wengine kati yao walisali kwa kutumia lugha hizo mbele ya kundi. Lakini kama vile Paulo alivyoonyesha, wale wengine kundini hawakuwaelewa.
Leo, sisi hatuna kipawa hicho cha kimuujiza. Lakini Wakristo wanaosali kwa ajili ya wengine wanapaswa kusali kwa njia itakayoeleweka. Kwa mfano, mwanzoni mwa hotuba ya watu wote, tunakaribisha watu wa kutoka nje wajiunge nasi katika sala. Katika sala ya namna hiyo, hakika lingekuwa jambo la akili kuepuka maneno au habari ambayo ingekuwa ngumu kueleweka na wageni.
Sala Ziwe na Urefu Gani?
Sala za faragha zinaweza kuwa na urefu tunaotaka. Kabla Yesu hajawachagua mitume wake 12, yeye alisali usiku kucha. (Luka 6:12) Ingawa hivyo, sala inayotolewa mbele ya watu iwe na urefu gani? Kabla ya kupitishiana mifano wakati alipokuwa akianzisha Ukumbusho wa kifo chake, Yesu ‘alibariki’ na ‘kushukuru,’ kwa wazi akifanya hivyo katika sala zilizo fupi. (Mathayo 26:26-28) Kwa upande mwingine, sala ya Sulemani kwenye wakfu wa hekalu ilikuwa ndefu sana. Ndivyo na sala ya Yesu usiku uliotangulia kufa kwake.—2 Mambo ya Nyakati 6:14-42; Yohana 17:1-26.
Kwa hiyo, hakuna sheria juu ya urefu wa sala. Lakini hakuna wema wa pekee unaopatikana kwa kutoa sala ndefu-ndefu. Kwa kweli, Yesu aliwalaumu waandishi ‘waliokula nyumba za wajane, na kwa unafiki wakasali sala ndefu.’ (Luka 20:46, 47) Sala zinazosemwa kwa ajili ya wengine zinapasa kutaja wazi hali au mahitaji yao na zinapasa kuwa na urefu unaoifaa pindi yenyewe. Hatuhitaji kutoa sala ndefu zinazozunguka-zunguka kwa kutaja-taja mambo mengi yasiyohusiana. Tunapotoa sala kwa ajili ya chakula, sala ingeweza kuwa fupi sana. Wala hakuna uhitaji wa kwamba sala ya kufungua mkutano wa Kikristo iwe ndefu. Mwenye kuwakilisha jamaa mwanzoni au mwishoni mwa siku, au mwenye kumalizia kusanyiko katika sala, huenda akataka kuzungumza mambo zaidi yanayoifaa pindi hiyo.
Sala inayotolewa kwa ajili ya wengine itakuwa na matokeo mazuri ikitokana na moyo mnyenyekevu na ikisemwa kwa usawaziko unaofaa na kujali hali zinazopasa kufikiriwa. Itajenga hali ya kiroho ya wale wanaosikiliza na itajenga uhusiano wao pamoja na Yehova. Matokeo ni kwamba, kama ilivyokuwa kwa watu wale walioishiriki sala ile ya kutoka moyoni iliyotolewa na Daudi sanduku la agano lilipoletwa Yerusalemu, wote wenye kusikiliza watasukumwa na moyo ‘kusema “Amin” na kumpa Yehova sifa.’—1 Mambo ya Nyakati 16:36.
[Sanduku katika ukurasa wa 22]
Je, inafaa wasikilizaji waseme “Amin” kwa sauti yenye kusikika mwishoni mwa sala inayotolewa mbele ya watu?
Ndiyo, ikiwa wanataka au wanajisikia wakisukumwa na moyo kufanya hivyo. Paulo aliitaja “Amina” inayosemwa na wale wanosikiliza sala, ingawa hakusema wazi kama waliitoa kwa sauti yenye kusikika, au kwa unyamavu katika mioyo yao. (1 Wakorintho 14:16) Lakini, chini ya Torati ya Musa, kulikuwa na pindi moja ambapo Waisraeli waliagizwa waziwazi waseme “Amina” kwa sauti kubwa. (Kumbukumbu la Torati 27:14-26) Kwa hiyo, wakati mtu mwenye kusali anapoonyesha sala yake imefikia mwisho kwa kusema “Amina,” inafaa wasikilizaji waseme “Amina” katika mioyo yao au kwa sauti ya chini yenye kusikika. Inawapasa wazazi wazoeze watoto wao kuonyesha uthamini unaofaa katika njia ambayo wanaitamka “Amina” yo yote ya sauti ya chini.
[Sanduku katika ukurasa wa 23]
Mtoto mchanga akianza kulia, simu ikilia, au jambo jingine lenye kusumbua litokee wakati wa sala ya kundi, je, ni dharau msikilizaji mmoja akishughulikia hali hiyo ya dharura?
Hapana. Kwa kweli, ungekuwa wonyesho wa upendo mtumishi wa huduma mmoja akiliacha kundi lenye kusali kwa utulivu na kushughulikia hali hiyo ya dharura kwa utaratibu. (1 Wakorintho 14:40) Hivyo, wale wengine kundini wanaweza kuendelea kusali bila kusumbuliwa. Yeyote anayeshughulikia hali hiyo ya dharura anaweza kujiunga tena na sala hali hiyo ikiisha.