Kumfikia Mungu Katika Sala
YEHOVA MUNGU anasema hivi: “Aliyelitia sikio mahali pake asisikie?” (Zab. 94:9) Mtu ye yote, mdogo au mkubwa, anayesali kwake kwa unyofu wa moyo, anaweza kuwa na hakika kabisa kwamba ombi lake litasikiwa na Mungu. Biblia yatuambia hivi: “Hakuna tofauti ya Myahudi na Myunani; maana yeye yule ni Bwana wa wote, mwenye utajiri kwa wote wamwitao.”—Rum. 10:12.
Walakini, inatupasa tumfikie Mungu kwa nia nzuri, ile yenye heshima kuu, pamoja na ufahamu wa uhusiano wetu kwake. Yeye ni Mfalme wa ulimwengu wote, Muumba wetu mwenye nguvu zote.
Kwa hiyo, kama vile mtu asivyokwenda haraka-haraka mbele ya mfalme wa kidunia kwa ghafula, bila adabu nzuri, vivyo yeye anayetaka kusikiwa na Mungu katika sala atamfikia kwa roho na adabu inayofaa. Lakini jambo hili halimfanyi awe Mungu aliye mbali sana na asiyependezwa, kwa maana mtume Paulo alikiambia kikundi cha wanaume na wanawake katika Athene kwamba Mungu amewapangia wanadamu wote wamtafute na kwamba “hawi mbali na kila mmoja wetu. Kwa maana ndani yake yeye tunaishi, tunakwenda, na kuwa na uhai. . . Maana sisi sote tu wazao wake.”—Matendo 17:26-28.
Kwa fadhili Mungu ametupasha habari juu ya njia ambayo katika hiyo tunaweza kuwa na hakika tutasikiwa. Ameonyesha wazi sana kwamba yampasa afikiwe “katika jina lake Bwana wetu Yesu Kristo.” (Efe. 5:20) Mara nyingi Yesu aliwaeleza mitume wake kwamba akiisha kufufuliwa imewapasa waombe katika jina lake, na kwamba jambo lo lote ambalo wangeomba kupatana na mpango wa Mungu lingepewa. (Yohana 14:13, 14; 15:16) Kwa wale ambao ni watumishi wa Mungu waliojiweka wakf, alionyesha kwamba lisingekuwa shauri la kuomba tu katika jina la Kristo kwa sababu Mungu hangejibu. Sivyo, Yesu alisema hivi: “Na siku ile mtaomba kwa jina langu; wala siwaambii ya kwamba mimi nitawaombea kwa Baba; kwa maana Baba mwenyewe awapenda kwa kuwa ninyi mmenipenda mimi, na kusadiki ya kwamba mimi nalitoka kwa Baba.” (Yohana 16:26, 27) Yehova yuko tayari kutoa baraka wakati wo wote tunapozipokea.
Basi, ni kwa sababu gani inatakiwa kumfikia kupitia kwa Yesu Kristo? Kwa sababu sisi wenyewe hatuna njia ya kumfikia Mungu, kwa vile sisi ni wenye dhambi sisi si wa jamaa yake safi. (Rum. 3:21-23) Dhabihu ya Yesu ilitoa funiko ya kupatanisha dhambi za wanadamu na msingi wa kwamba awe Kuhani Mkuu wa Mungu kwa ajili ya wanadamu. Kwa habari ya cheo hiki chenye maana cha Yesu Kristo, mwandikaji aliyeongozwa na Mungu alisema hivi: “Hatuna kuhani mkuu asiyeweza kuchukuana nasi katika mambo yetu ya udhaifu; bali yeye alijaribiwa sawasawa na sisi katika mambo yote, bila kufanya dhambi. Basi na tukikaribie kiti cha neema [cha Mungu] kwa ujasiri, ili tupewe rehema, na kupata neema ya kutusaidia wakati wa mahitaji.”—Ebr. 4:15, 16.
Wakati wa kumaliza sala zetu imetupasa kwa vyo vyote tumkiri Yesu kama ndiye njia ya kumfikia Mungu. Mtume Paulo aliandika hivi: “Ahadi zote za Mungu zilizopo katika yeye ni Ndiyo [maana yake, hakika]; tena kwa hiyo katika yeye ni Amin; Mungu apate kutukuzwa kwa sisi.” (2 Kor. 1:20) “Amin” au “Amina,” baada ya kumalizia sala katika jina la Kristo, inamaanisha “iwe hivyo,” usemi wa kuthibitisha, yaani, kwamba ahadi zote za Mungu zinatimizwa tena zitatimizwa kupitia kwa Kristo. Katika kusema kwao “Amina” Wakristo wanamtukuza Mungu. Ikiwa mmoja anasali, wengine wakisikia na kukubaliana na sala wanaweza pia kusema kimya “Amina,” katika mioyo yao, au kwa sauti yenye kusikika, kama wanapenda kufanya hivyo.
Mtume Paulo anawatia moyo Wakristo waendeleze vita vyao vya imani huku ‘kwa sala zote wakisali kila wakati katika Roho.’ (Efe. 6:18) Kila sala, kama ni ile inayotolewa kwa sauti yenye kusikika ama kwa kimya, ina kusudi. Kuna namna nyingi za sala, kwa mfano, “maombezi,” ambazo katika hizo Mkristo anaombea wengine, kutolewa kwa “shukrani,” sala za kuomba baraka, sala za “dua” juu ya mahitaji au matatizo fulani. (1 Tim. 2:1; Flp. 4:6) Vilevile kuna pindi nyingi za kusali. Huenda zikatokea hali fulani tunapohitaji kumwomba Mungu, au huenda zikawako nyakati za kawaida au pindi, kama vile wakati wa mikutano ya Kikristo. (Yak. 5:13-16; Matendo 6:5, 6) Sala zimepaswa zilingane na pindi.
Kwa sababu hiyo, inafaa wakati wa kusali kusema waziwazi jambo lenyewe kadiri iwezekanavyo. Kuwe kusudi linalotakiwa kutimizwa wakati huo; haipaswi sala iwe yenye maneno matupu yasiyo na maana ndani yake na yasiyo na shabaha. Kwa mfano, katika kutoa shukrani wakati wa chakula isingefaa kwa kawaida kutoa sala ndefu, inayoshughulika na mambo mengine yasiyohusu pindi hiyo. Hapa sala fupi ingefaa kusudi. Lakini wakati wa kuamka au wakati wa kulala labda tutataka tutaje mambo yanayotokea kila siku katika maisha zetu na maisha za wale walio katika ushirika wa ndugu katika ulimwengu wote. Kwa njia hiyo labda sala hiyo itakuwa na mambo mengi zaidi. Bila shaka, kuna nyakati ambapo “hatujui kuomba jinsi itupasavyo; lakini Roho mwenyewe hutuombea kwa kuugua kusikoweza kutamkwa.” (Rum. 8:26) Mungu anakubali sala yetu yenye shauku katika hali hizi, akijibu kwa kadiri ya mahitaji yetu, kana kwamba tulikuwa tumeomba tupate jibu hilo.
Alipokuwa akifundisha wanafunzi wake namna ya kusali, Yesu aliwapangia kifupi mambo kulingana na taratibu ya maana (ukubwa) yao. (Mt. 6:9-13) Vilevile alishauri juu ya kutorudia maneno yale yale yasiyo na maana katika sala. Wakati wa kuzungumza na mtu katika mazungumzo ya kawaida tungeona ni upumbavu kusema jambo lile lile mara nyingi. Ndivyo ilivyo hata tunaposema na Mungu, ambaye “anajua mnayohitaji kabla ninyi hamjamwomba.” (Mt. 6:8) Tena, kama vile katika kusema na rafiki tusingetaja jina lake mara nyingi katika kila usemi, vivyo hivyo tusingetaja jina la Yehova mara nyingi katika sala.
Mifano ya Biblia juu ya sala yatufunulia kwamba hakuna kikao maalum au namna yo yote inayotakiwa kuweka mikono. Yesu “akaanguka kifulifuli, akaomba” katika bustani ya Gethsemane. (Mt. 26:39) Pindi nyingine, “Yesu akainua macho yake juu.” (Yohana 11:41; Luka 18:13) Alisema juu ya kusimama wakati wa kusali. (Marko 11:25) Mtume Paulo “akapiga magoti, akaomba pamoja” na wazee wa Efeso.—Matendo 20:36.
Kwa hiyo, penye mkutano wakati mtu mmoja anapoongoza kikundi katika sala imepasa kila mtu ajitalie kikao au hali yenye heshima, lakini hakuna kikao maalum kinachoifanya sala iwe takatifu zaidi. Imetupasa pia tukumbuke kwamba, penye mkutano wa watu wote, wajapokuwa ni wenye urafiki huenda wasioamini wakakataa kuinamisha vichwa vyao pamoja na kundi. Ingetosha kutangaza tu kwamba ‘sasa tutamfikia Yehova katika sala,’ au kutumia usemi mwingine unaofanana.
Sala inayotolewa kwa Yehova Mungu katika jina la Yesu Kristo ina nguvu nyingi. Katika nyakati za chakula, sala za shukrani zinampendeza Mungu kumwongoza awabariki walaji katika kutumia kwao chakula kinachopatikana. Mtume aliandika hivi: “Kila kiumbe cha Mungu ni kizuri, wala hakuna cha kukataliwa, kama kikipokewa kwa shukrani; kwa kuwa kimetakaswa kwa neno la Mungu [likikubali mambo yote ambayo Mungu ameumba vipate kuliwa] na kwa kuomba.” (1 Tim. 4:4, 5) Mtu asiyetoa shukrani kwa Mungu kwa ajili ya chakula chake si mwenye kuthamini, na hawezi kutazamia kupata baraka zote za Mungu. Hatutaki tuwe kama wanyama, wasiojua Chanzo cha kweli na Mpaji wa vitu vyote vyema.
Yakobo, ndugu mzazi mmoja na Yesu, anasema juu ya kufaa kwa sala hivi: “Kuomba kwake mwenye haki kwafaa sana, akiomba kwa bidii. Eliya alikuwa mwanadamu mwenye tabia moja na sisi, akaomba kwa bidii mvua isinye; na mvua haikunya juu ya nchi muda wa miaka mitatu na miezi sita. Akaomba tena, mbingu zikatoa mvua, nayo nchi ikazaa matunda yake.”—Yak. 5:16-18.
Hivyo kuna thawabu kubwa katika kusali kwa Mungu. Fikiria ile baraka isiyolinganika ambayo Kornelio afisa wa Kirumi alipokea kutokana na sala. (Matendo sura ya 10) Kwa hiyo, imetupasa tuombe kwa imani nyingi na kwa uhakika sana. Kwa maana Yehova, anayeipa jina kila mojawapo ya mamilioni na mamilioni ya nyota, anaweza kuzisikia sala za mamia ya maelfu ya waabudu wake wote na kuwafikiria mmoja mmoja.—Zab. 147:4.