Je, Mabaraza ya Kidini Yanakubaliwa na Mungu?
NENO “baraza” linakumbusha mtu sehemu inayojulikana sana ya serikali ya mitaa. Maneno kama “baraza la jiji” na “baraza la mji” yanafahamiwa upesi. Lakini, yasiyojulikana sana huenda yakawa ni maneno “baraza la kidini” au “baraza la kanisa.” Baraza kama hilo la wanadini limeelezwa kuwa “mkutano wenye kuwakilisha kanisa ulio na mamlaka ya kuzungumza mambo makubwa na mara nyingi kutoa sheria katika masuala yanayohusu imani, maadili, na nidhamu ya kanisa.”
Juu ya mabaraza mengi ya kidini yaliyofanywa muda wa karne zilizopita, Kanisa Katoliki la Roma linayafikiria 21 kati ya hayo kuwa yenye kuwakilisha jamii yote ya Wakatoliki, nayo ni kuanzia Baraza la Nisia katika mwaka 325 W.K. mpaka Baraza la Pili la Vatikani la 1962-65. Kulingana na kitabu The Encyclopedia Americana, “mabaraza ya kanisa yanaitwa na papa, anayeyasimamia, anaamua orodha ya mambo yatakayozungumzwa, anamalizia baraza, na kutangaza rasmi amri zinazotolewa na baraza. . . . Likiwa pamoja na papa baraza la kanisa ndilo kiungo chenye mamlaka cha kanisa, na katika muungano pamoja naye kinawakilisha mamlaka ya kanisa ya kufundisha isiyoweza kuwa na kosa katika mambo ya imani na maadili.”—Buku la 8, ukurasa 85.
Kutafuta Chanzo Chao
Viongozi wengi wa kidini wanaamini kwamba mabaraza ya kidini ya Jumuiya ya Wakristo zinalinganika na ule mkutano wa karne ya kwanza wa mitume na wanaume wazee katika Yerusalemu. Hivyo, mabaraza ya baadaye ya kanisa yanasemwa kuwa yana mamlaka kama hiyo ya kuamua mambo ya imani ya maadili, (Matendo 15:2, 6, 22) Lakini je, mabaraza hayo ya kidini yamepewa mamlaka na Mungu? Je, yeye ameyakubali?
Jambo la kupendeza ni kwamba, katika Marko 3:6 maneno ‘kufanya shauri’ yametokana na neno la Kigiriki linalomaanisha ‘mkutano wa watu wanaotoa maoni na mashauri yao.’ Katika mstari huo, tunasoma kwamba Wafarisayo ‘walifanya shauri’ na wafuasi wa chama cha Herode ili wamwangamize Yesu. Hakika Mungu hakukubali baraza hilo! Na Yesu aliwaonya wanafunzi wake wasiwatumaini watu kama hao. (Marko 8:15) Je, kuna ruhusa ya kutotumaini mabaraza ya kidini ya Jumuiya ya Wakristo jinsi iyo hiyo?
Yesu alisema pia: “Kwa matunda yao mtawatambua.” (Mathayo 7:20) Basi, acheni tuchunguze matunda ya mabaraza mbalimbali ya kanisa.
Yanatawalwa na Nini?
Kulingana na kitabu The Encyclopedia Americana, mabaraza ya kijimbo yaliyotumika kuratibisha kitengenezo makanisa ya Katoliki katika Spania, Uingereza, na kwingineko “yaliitwa mara nyingi na kutawalwa na mamlaka ya kilimwengu.” Mabaraza ya ujumla ya viongozi wa kidini yaliyotokana na milki nzima ya Kiroma “hayakujulikana kabla ya Baraza la Nisia (325 A.D.),” lililoitwa na Mfalme Konstantino. Mwanahistoria Mwingereza H. G. Wells alidokeza kwamba Konstantino ndiye aliyeingiza siasa na utawala wa kimabavu katika Jumuiya ya Wakristo iliyokuwa imekwisha kugawanyika sana. Wells aliandika hivi: “Si kwamba baraza la Nisia lilikusanywa tu na Konstantino Mkuu, bali mabaraza yote makuu, mawili katika Konstantinopo (381 na 553), Efeso (431), na Kalkedoni (451) yaliitwa yaje pamoja na mamlaka hiyo ya kikoloni.” Lakini je, Mungu angewezaje kukubaliana na jambo hilo, kwa kuwa Wakristo wa kweli hawajaribu kuchanganya dini yao na siasa, bali wanadumisha kutokuwamo kamili?—Yohana 17:16; Yakobo 1:27.
“Mabaraza makuu ya baadaye yalifunikwa mara kwa mara na siasa za kanisa za kikoloni na ushindani uliohusu maeneo yale makubwa-makubwa [yenye kusimamiwa na askofu au askofu mkuu],” kinaongezea kitabu The Encyclopedia Americana. Kwa kuwa mabaraza kama hayo ya kanisa yalikuwa na siasa na ushindani wa wanadini, hayakuzaa matunda ya roho ya Mungu kama upendo na amani. Bali, yalitiwa madoa na kazi za kimwili ambazo zilikuwa ni pamoja na “matendo ya ukatili, kuzozana, wivu, . . . ushindani wa kichoyo, migawanyiko, fitina-fitina.” Kwa habari ya kazi za mwili, mtume Paulo alionya hivi: “Wale wanaofanya mambo kama hayo hawataurithi ufalme wa Mungu! ” (Wagalatia 5:19-23, New American Bible ya Katoliki) Basi, inaweza kusemwaje kwamba mabaraza ya kanisa ya Jumuiya ya Wakristo yamekubaliwa na Mungu?
Matendo ya Kinyama ya Kugutusha!
H. G. Wells alishikilia kwamba roho ya Konstantino ndiyo iliyotawala mambo ya kanisa, na akasema: “Wazo la kuondolea mbali kabisa mabishano na migawanyiko yote, kuondolea mbali kabisa mawazo yote, kwa kulazimisha waamini wafuate imani moja yenye kuongozwa na maoni ya kibinafsi, . . . ndilo wazo la mwanadamu mwenye kujitegemea anayeona kwamba ili aweze kuendelea na kazi yake ni lazima kusiwe na mtu wa kumpinga wala kuonyesha makosa yake. Sasa basi historia ya Kanisa chini ya maongozi [ya Konstantino] inakuwa historia ya mapambano yenye jeuri ambayo ilikuwa lazima yatokee alipotoa amri za ghafula na kali-kali kwamba wote wafuate maoni mamoja. Kutokana naye Kanisa likajipatia nia ya kuamuru-amuru watu bila kuulizwa sababu ya kutenda mambo linayotenda, kusitawisha tengenezo lenye kutegemea mahali pamoja pakuu na kuwa sambamba na ile milki.”
Kushtaki watu kuwa ni uzushi kukawa ni njia ya ukatili ya kuondolea mbali wapinzani waliothubutu kuasi mabaraza ya kanisa ya Jumuiya ya Wakristo. Watu wo wote waliotoa maoni tofauti au hata wakajaribu kutoa uthibitisho wa Kimaandiko wenye kukanusha maoni ya kibinafsi na sheria za mabaraza ya kanisa walibandikwa jina la kuwa ni wazushi.
Jitihada ya kupiga moyo konde ili kuondolea mbali kabisa upinzani ulitokeza matendo ya unyama yenye kuogopesha sana. Wengi wa wale waliotangazwa kuwa na hatia ya uzushi kinyume cha yale maoni ya kibinafsi ya baraza yenye kufuatwa sana walichomwa kwa moto wakiwa juu ya mti, wakapata maumivu machungu sana ya kifo cha polepole wakiwa tamasha mbele ya watu—hayo yakafanywa kwa jina la Kristo ati!
Kwa mfano, Baraza la Constance (1414-18) liliitwa ili likomeshe mzozano juu ya ni nani aliyekuwa papa wa halali na kushughulika na uzushi wa Wycliffe na Hus. Inasemekana kwamba farasi elfu thelathini walipeleka watu kwa Constance kwa ajili ya tukio hilo kuu. Wakati wa baraza, John Hus alijaribiwa na kulaaniwa, kisha akapokezwa kwa wakuu wa kilimwengu na kuchomwa kwa moto akiwa juu ya mti.
Namna Gani Mafundisho?
Ni kweli kwamba Wakristo wote wa kweli “wananena mamoja.” Lakini hiyo si kwa sababu ya kuwekwa chini ya mkazo wa wanadini. Bali, ni kwa sababu imani na mazoea yao zinategemea kwa njia yenye akili Neno la Mungu aliloliongoza kwa roho yake. (1 Wakorintho 1:10; Matendo 17:10, 11; 2 Timotheo 3:16, 17) Hata hivyo, mabaraza ya kanisa yanaonekana kuwaje tunapofikiria maamuzi yao yanayohusu mafundisho?
Ingawa mabaraza ya kanisa yanaweza kufanana na mawe yaliyopakwa chokaa barabarani kuonyesha umbali ambao uanadini umefikia mpaka sasa, katika akili za watu wengi yamekuwa kama mawe ya makaburi ambayo ni alama za kuonyesha jinsi yameharibu sana mafundisho safi ya Kikristo. Mfano: Katika mwaka 325 W.K. Baraza la Nisia lilianzisha fundisho la Kristo Asiyekufa, au Mungu-mtu. Katao hilo la kwamba Yesu hakuwa mwanadamu kikweli likawa moja la mafundisho yenye kupoteza zaidi ya Jumuiya ya Wakristo. (Linganisha 2 Yohana 7.) Limegeuza mamilioni ya watu wamwache Yehova na kufuata Utatu wenye kuvuruga akili! Hakuna lo lote la mabaraza yaliyofanywa baada ya hapo lililojaribu hata kidogo kurekebisha kosa hilo. Hata hivyo ni wazi fundisho la Utatu halipatani na Maandiko, kwa maana Yesu alisema: “Baba ni mkuu kuliko mimi.” (Yohana 14:28) Je, Mungu angeweza kweli kukubali baraza lo lote linaloficha ukweli juu ya jinsi yeye na Mwanaye walivyo?
Maoni ya kibinafsi yenye kuanzishwa na baraza moja yanaweza kupinduliwa na baraza jingine. Kwa mfano, kama inavyoonyeshwa katika orodha inayoambatana na makala hii, matumizi ya sanamu katika ibada yalikataliwa wakati wa baraza lililofanywa katika Konstantinopo mwaka 730 W.K. Lakini hatua ilichukuliwa na baraza la baadaye kuzirudisha. Bila shaka, Biblia inaonyesha kwamba kufanya na kutumia sanamu za kidini ni ibada ya sanamu wala si ya Kikristo.—Kutoka 20:4-6; 1 Yohana 5:21.
Kama ilivyoonyeshwa pia katika orodha, kati ya mafundisho yenye kukubaliwa katika mabaraza ya kanisa ya Jumuiya ya Wakristo yalikuwa ubatizo wa vitoto vichanga, kuamuru na kutaka mapdri na watawa wa kike wasioe au wasiolewe, kutokeza fundisho la purgatori, na moto wa mateso. Lakini, Maandiko hayaungi mkono ubatizo wa vitoto vichanga, wala kutokuoa au kutokuolewa kwa watawa, wala moto wa mateso, wala hayaitaji hata kidogo purgatori. (Mathayo 28:19, 20; 1 Timotheo 4:1-3; Ayubu 14:13) Kwa kuwa ni lazima wale wanaotaka upendeleo wa Yehova wamwabudu yeye “katika roho na kweli,” angewezaje kukubali mabaraza yanayositawisha mafundisho ya uwongo?—Yohana 4:23, 24.
Mkusanyiko wa Yerusalemu
Kwa habari ya mabaraza ya kidini Otto Karrer aliandika hivi: “Isipokuwa kwa habari ya lile linaloitwa Baraza la Mitume [la karibu mwaka 49 W.K.] ambalo uamuzi walo ni sehemu ya mapokeo ya tangazo la kimungu lililo la kimungu, mabaraza yote ni mazao ya kanisa lililotokea baada ya siku za mitume. Hayakuwako katika kile kipindi cha kuanzishwa kwa kanisa.”—The Councils of the Church.
Bila shaka, mabaraza yote ya kanisa ya Jumuiya ya Wakristo yametofautiana sana na mkusanyiko ule wa karne ya kwanza wa mitume na wazee katika Yerusalemu. Wakati huo hakukuwa na mapadri wenye kuweka kongwa zito juu ya shingo za wengine wala wa kupepea mioto kwenye miti ya kuulia watu wakiwa na njaa ya kutaka mamlaka. Bali, matunda ya roho ya Mungu yalidhihirishwa. Mazungumzo wakati huo yalielekezwa na roho nayo yalipatana na Neno la Mungu. Na kielelezo hicho cha kutatulia masuala ya Kimaandiko kinafuatwa na Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova leo.
Barua ambayo mitume na wazee wa Yerusalemu walipelekea waamini wenzao ilisema hivi kwa ufupi: “Roho takatifu na sisi wenyewe tumependelea tusiongeze mzigo zaidi kwenu ninyi, isipokuwa mambo haya ya lazima, kuendelea kushika mwiko wa vitu vinavyotolewa dhabihu kwa sanamu na wa damu na wa vitu vinavyonyongwa na wa uasherati.” (Matendo 15:22-29, NW ) Hizo hazikuwa sheria zenye kuanzishwa na wanadamu bali yalikuwa matakwa kwa yenye kutegemea amri zilizotolewa mapema na Mpaji-Sheria aliye mkuu.—Mwanzo 9:3, 4; Kumbukumbu la Torati 5:8-10, 18; Isaya 33:22.
Mkutano huo wa karne ya kwanza wa mitume na wazee katika Yerusalemu ulikuwa na kibali cha Yehova, kwa maana maamuzi yao yalipata baraka yake, nayo yaliiendeleza kazi ya kuuhubiri Ufalme iliyoingiza watu wengi wa Mataifa katika kundi la Kikristo. Lakini, mambo ya hakika ya historia yanatoa ushahidi ulio wazi kwamba mabaraza ya kanisa ya Jumuiya ya Wakristo hayajapata kamwe kukubaliwa na Mungu.
[Chati katika ukurasa wa 26]
FUNDISHO LILILOKUBALIWA BARAZA TAREHE
Ubatizo wa vitoto vichanga Carthage 253 W.K.
Mapadri na watawa kutofunga ndoa Trent 1545 W.K.
Talaka Inayotokana na Uzinzia Aries 314 W.K.
Talaka Yakatazwa Trent 1545 W.K.
Moto wa Mateso Lyons 1274 W.K.
Florence 1573 W.K.
Sanamu Zakataliwab Konstantinopo 730 W.K.
Sanamu Zarudishwa Konstantinopo 842 W.K.
Nisia 787 W.K.
Kuzaliwa na Bikira Avignon 1457 W.K.
Kristo Awa Mungu-Mtu Nisia 325 W.K.
Kalkedoni 451 W.K.
Akina Yahe Wasihubiri
Kwenye Jukwaa la Kanisa Konstantinopo 681 W.K.
Purgatori Florence 1573 W.K.
Trent 1545 W.K.
Utatu Nisia 325 W.K.
[Maelezo ya Chini]
a Mafundisho haya tu ndiyo yanayopatana na Biblia
b Mafundisho haya tu ndiyo yanayopatana na Biblia