Je! Wewe Umeupata Ule Ufunguo?
KWA sababu gani upendo ni wa maana sana kwa Wakristo? Kwa sababu ya aina ya Mungu wanayeabudu. Mtume Yohana alieleza habari zake kwa maneno haya: “Mungu ni upendo.” (1 Yohana 4:8) Sawa na vile wazazi wengi wanavyotumainia kwamba watoto wao watafuata hatua zao, ndivyo Yehova Mungu anavyotaka Wakristo wajaribu kufanana naye. Hivyo, mtume Paulo alihimiza hivi: “Mfuateni Mungu, kama watoto wanaopendwa; mkaenende katika upendo.”—Waefeso 5:1, 2.
Upendo pia unasawazisha zile sifa nyingine za Kikristo. Katika siku za Yesu, Wayahudi—hasa viongozi wao—walikuwa wanafunzi wenye bidii wa Biblia. Lakini fikiria yale ambayo Yesu aliwaambia: “Mwayachunguza maandiko, kwa sababu mnadhani kwamba ninyi mna uzima wa milele ndani yake; . . . Walakini nimewajua ninyi ya kuwa hamna upendo wa Mungu ndani yenu.” (Yohana 5:39, 42; Luka 11:42) Kama wao wangalikuwa wana upendo na pia maarifa, wangalimtambua Yesu kuwa ndiye masihi. Kama ilivyokuwa, walio wengi kati yao waliipoteza nafasi ya kuwa washiriki wa kwanza wa kundi la Kikristo.
Wakumbuke, pia, wale viongozi wa Roma Katoliki waliopeleka dini yao kwenye Ulimwengu Mpya (Amerika) baada ya kuiteka sehemu hiyo. Bila shaka walikuwa na imani yenye nguvu na bidii kali sana ndipo wakaweza kutimiza mambo waliyofanya. Lakini ni hakika kwamba sifa hizo hazikuongozwa na upendo. Ama sivyo, wasingalinyang’anya, kutesa, kuingilia wanawake kinguvu, wala kuua wakaaji wa mabara ya Amerika.
Hivyo, upendo ndio sifa ya Kikristo iliyo kuu. Ni nani anayepaswa kuonyeshwa upendo huo? Yesu anatuambia hivi: “ ‘Ni lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili zako zote.’ Hiyo ndiyo amri kubwa zaidi ya yote na ndiyo ya kwanza. Ya pili, kama hiyo, ni hii, ‘Ni lazima umpende jirani yako kama wewe mwenyewe.’ ”—Mathayo 22:37-39, NW.
Kwa kweli, upendo wa Mkristo unasonga mbele zaidi ya hapo. Yesu alisema pia: “Wapendeni adui zenu, waombeeni wanaowaudhi; ili mpate kuwa wana wa baba yenu aliye mbinguni; maana yeye huwaangazia jua lake waovu na wema, hunyeshea mvua wenye haki na wasiohaki.” (Mathayo 5:44, 45) Ndiyo kusema, upendo wa Mkristo unatia ndani karibu kila mtu! Lakini hiyo ina maana gani kwa matendo?
Ikiwa Tunampenda Mungu Kweli Kweli
Kwanza, ikiwa sisi tunataka kumpenda Mungu kweli kweli, tutahitaji kupata kumjua vizuri zaidi. Mungu mwenyewe amefanya jambo hilo liwezekana kwa kutuandalia Biblia, ambayo kwa kweli ni barua aliyotuandikia sisi. Tunapopokea barua kutoka kwa mpendwa, walio wengi kati yetu tunaisoma bila kukawia hata kama tunashuguli nyingi namna gani. Je! tufanye tofauti na hivyo kuhusiana na Biblia? Bila shaka sivyo? Ni kweli kwamba kwa wengi maisha leo yamejawa na mambo ya kuelekeza fikira kando, na walio wengi wanaelekea kupendelea zaidi kutazama televisheni badala ya kusoma mambo kwa uzito. Lakini Wakristo wa kweli hawaachi jambo hilo liwazuie kusoma Neno la Mungu. Hivyo, wao wako kama mtunga zaburi aliyeandika hivi: “Nafsi yangu imezishika shuhuda zako [ambazo leo zinapatikana katika Biblia], nami nazipenda mno.”—Zaburi 119:167.
Katika Biblia, Mungu anatuambia jinsi anavyotutaka tutende. Sawa na vile wazazi wanavyoweka viwango vya mwenendo vifuatwe na watoto wao, Yehova ameweka viwango anavyotutazamia tudumishe—viwango ambavyo si vya kufanyiwa majadiliano pamoja naye vionekane kama vinafaa au havifai. Kwa mfano, Biblia inatuambia: “Waasherati hawataurithi ufalme wa Mungu wala waabudu sanamu, wala wazinzi, wala wafiraji, wala walawiti, wala wevi, wala watamanio, wala walevi, wala watukanaji, wala wanyang’anyi.” (1 Wakorintho 6:9, 10) Lo, ni orodha ndefu hiyo! Lakini mtu ye yote anayependa Mungu kweli kweli atafurahi kuikubali. Kwa sababu gani? Kwa sababu kama vile mtume Yohana alivyoonyesha wazi, “Huku ndiko kumpenda Mungu, kwamba tuzishike amri zake.”—1 Yohana 5:3.
Jambo la kusikitisha ni kwamba, mengi ya mazoea yaliyokatazwa katika Biblia yanakuwa yenye kukubalika leo, hata kati ya watu walio “Wakristo.” Ripoti moja iliyotolewa katika Kanada na dhehebu moja la Kiprotestanti ilipendekeza kwamba watu wa jinsia moja wanaolalana wafikiriwe kukubaliwa wawe wahudumu, ikashikilia kwamba kufanya ngono bila kuoana kunaweza kukubaliwa chini ya hali fulani-fulani, na ikadokeza kwamba hakuna uhitaji wa kuepuka uzinzi ili kuwe na uaminifu katika ndoa. Bila shaka watungaji wa ripoti hiyo walitaka kuonekana kwamba ni watu wenye akili pana na wenye kujali. Lakini je, kwa kufanya hivyo walikuwa wakionyesha upendo, ama kuelekea Mungu ama kuelekea wale waliokuwa wakiwatia moyo wafuate njia hizo za ukosefu wa adili? Ni vigumu, kwa kuwa Paulo alisema kwamba wazoeaji wa mambo kama hayo hawangeurithi Ufalme wa Mungu. Ni jambo la upendo zaidi kushika bila woga viwango vya Mungu, kuwasaidia wanyonge wafanye vivyo hivyo, badala ya kupatwa na msisimuko usioongozwa na fikira thabiti ili kuwatia moyo wafuate mwendo rahisi zaidi ambao mwishowe utaongoza kwenye msiba.
Moyo Wafutwa Ili Wagawane na Wengine
Wakati tunaposoma Biblia, tunajifunza pia juu ya mambo mazuri ajabu ambayo Mungu amekusudia kwa ajili ya wanadamu. Tunajifunza kwamba “Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.” (Yohana 3:16) Tunajifunza pia juu ya kusudi la Mungu kuondolea dunia uovu na kuleta mfumo wa mambo wenye amani, wa kiparadiso, kupitia Ufalme wake ulio chini ya Yesu uyo huyo. (Mathayo 6:9, 10; Ufunuo 21:3, 4) Ni kama vile Biblia inavyoahidi: “Bado kitambo kidogo asiye haki hatakuwako . . . Bali wenye upole watairithi nchi, watajifurahisha kwa wingi wa amani.”—Zaburi 37:10, 11.
Kwa kweli, ujumbe wa Biblia ni ya aina ile ile ambayo jamii ya kibinadamu inahitaji. Na ndiyo sababu ni jambo la kusikitisha kusoma kwamba wamisionari wa Jumuiya ya Kikristo wanavuta fikira kando na umaskini na udhalimu wanaouona katika nchi zilizo maskini zaidi hivi kwamba wanajihusisha katika siasa na hata katika mapinduzi. Mapinduzi hayatatatua matatizo ya nchi hizo. Je! wamisionari hao wanampenda Mungu kweli kweli? Ikiwa ndivyo, hawangeonyesha imani katika ahadi zake na kuelekeza makundi yao kwenye Ufalme wake? Hakika wachungaji wanaopenda makundi yao kweli kweli wangeyaonyesha jinsi kutii sheria ya Mungu kunavyoweza kusaidia hata sasa, badala ya kuwahusisha katika mipango ya kisiasa inayoweza kuwaletea mvurugo wa akili tu.
Ukweli ni kwamba, ujumbe wa Biblia ni mzuri sana hivi kwamba hakuna mtu mwenye upendo angeweza kujikalia nao bila kueleza wengine. Ndiyo sababu upendo unasukuma Wakristo wa kweli wagawie wengine mambo ambayo wao wanajua. Katika Jumuiya ya Wakristo kazi ya kusema na wengine juu ya Biblia kwa kawaida inaachiwa jamii ndogo inayolipwa mshahara—mapadri. Jambo hilo linaleta matokeo mabaya. Ni kama vile mchungaji mmoja Mlutheri alivyokiri katika gazeti Christianity Today, “Kanisa ni dhaifu leo kwa sababu viongozi wa kiroho wameshindwa kuzoeza jamii ya waamini wafanye aina ile ile ya kazi wanayofanya. Au kwa sababu waamini wameshindwa kutambua na kukubali huduma ya namna hiyo.”
Wakristo wa kweli “wanatambua na kukubali huduma ya namna hiyo.” Wao wanayachukua kwa uzito maneno haya ya mtume Paulo: “Na tulishike sana ungamo la tumaini letu, lisigeuke; maana yeye aliyeahidi ni mwaminifu.” (Waebrania 10:23) Kusudio lao ni nini? Ni sawa na lile lililosukuma kikundi cha Wakristo katika karne ya kwanza waliosifiwa kwa uchangamfu na mtume Paulo; “Hawa wanamhubiri [Kristo] kwa pendo “—Wafilipi 1:16.
Upendo kwa Wakristo Wenzi
Ndiyo, upendo ndio ufunguo wa kupata Ukristo wa kweli kwa sababu unahusu kila upande wa maisha za Wakristo wa kweli. Hivyo wao wanakuwa tofauti sana na watu wanaowazunguka. Kwa sababu gani? Mtume Yohana alisema hivi juu ya ulimwengu huu: “Ulimwengu mzima umo katika uwezo wa yule mwovu.” (1 Yohana 5:19, NW ) Yule mwovu ni Shetani Ibilisi, na ulimwengu unaonyesha kuwa unafuata viwango vyake katika mwingi wa utendaji wao. Maongozi ya Shetani yanaonekana katika udanganyifu ulioenea sana, ukosefu wa adili, udhalimu, msukosuko wa kikabila, na uonevu wa mambo ya kiuchumi uliopo leo. Ni lazima Mkristo anayeabudu Mungu mwenye upendo na kumwiga yeye kwa kusitawisha ile sifa ya upendo awe tofauti!
Hilo si jambo jepesi kufanya. Kwa hiyo, Biblia inatutia moyo pia tuwatafute wale walio na uthamini kama huo kwa ile sifa ya upendo. Hivyo, Wakristo wanaweza kusaidiana. Hiyo ndiyo sababu mtume Paulo aliandika maneno haya yenye kutia moyo: “Tukaangaliane sisi kwa sisi na kuhimizana katika upendo na kazi nzuri; wala tusiache kukusanyika pamoja, . . . bali tuonyane.”—Waebrania 10:23-25.
Ikiwa wewe ungependa kuitikia himizo hilo, Mashahidi wa Yehova wangependezwa sana kukuonyesha kikundi cha watu wanao jaribu sana kuonyesha wazi upendo wa Kimungu katika maisha zao. Bila shaka kuna kikundi cha watu kama hao katika mtaa wako, na roho ya Mungu iko juu yao kwa sababu, katika uchanganuzi wa mwisho, hicho ndicho chanzo cha upendo wa kweli wa Kikristo. “Tunda la roho ni upendo.” (Wagalatia 5:22, NW ) Kushirikiana nao kutakusaidia utii kitia moyo hiki cha mtume Petro: “Muupende ushirika mzima wa ndugu.”—1 Petro 2:17, NW.
Sitawisha Upendo
Lingekuwa jambo lenye msiba kama nini kujikuta kati ya wale ambao, baada ya kujaribu sana kumtumikia Mungu, ungeyasikia yale maneno ya Yesu yenye kukata maneno: “Sikuwajua ninyi kamwe; ondokeni kwangu, ninyi mtendao maovu.” (Mathayo 7:23) Tukisitawisha upendo, ule ufunguo unaoonyesha Ukristo wa kweli, jambo hilo halitatupata sisi. Upendo utatusukuma tuisome Biblia, tuishi kulingana na viwango vyayo, tutafute Wakristo wengine tushirikiane nao, na kueleza wengine juu ya mambo mazuri yaliyo katika Biblia. Ndiyo, upendo utatusukuma tufanye yale ambayo Mungu anatutaka tufanye. Na, kama vile Yesu alivyosema, “yeye afanyaye mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni” ndiye atakayerithi ahadi za Mungu. Mtume Yohana aliongeza hivi: “Yeye afanyaye mapenzi ya Mungu adumu hata milele.”—Mathayo 7:21; 1 Yohana 2:17.
Ndiyo, sitawisha upendo. Uache ukusukume ufanye mapenzi ya Mungu. Hivyo, utajithibitisha kuwa u Mkristo wa kweli, kwa kuwa Yesu alisema: “Hivyo watu wote watatambua ya kuwa ninyi mmekuwa wanafunzi wangu, mkiwa na upendo ninyi kwa ninyi.” (Yohana 13:35) Nawe utazifurahia thawabu za milele ambazo Mungu amewaahidi wale wanaompenda.
[Picha katika ukurasa wa 7]
Sitawisha Upendo