Ufunguo wa Kupata Dini ya Kweli
KATIKA karne hii ya 20, watu zaidi wanadai kuwa ni wa dini ya Kikristo kuliko dini nyingine yo yote. Hata hivyo karne hii imekuwa ndiyo yenye msukosuko mwingi zaidi katika historia ya kibinadamu. Mbona iwe hivyo hali wenye dini ni wengi zaidi?
Kwanza, wengi hawaichukui dini yao kwa uzito. Kwao, Ukristo ni jambo la kuchukuliwa kivivi-hivi tu, wala si kani yenye kuongoza maisha zao. Zaidi ya hilo, wanaoichukua dini yao kwa uzito sana wanafuata imani nyingi zenye kupingana na hata viwango vinavyotofautiana katika maadili. Nao wamegawanywa na tofauti za kitaifa, kikabila, na kiuchumi. Tena, wao wamedhulumiana, hata wakatesana, wakapigana katika vita, na kuuana. Hivyo, vile vita viwili vilivyo vikubwa zaidi katika historia vilipiganwa sana-sana kati ya mataifa “ya Kikristo.”
Tunaweza kukata shauri gani kutokana na jambo hilo? Kwamba ama Ukristo si dini ya kweli ama pana tofauti kubwa kati ya kudai tu kuwa Mkristo na kuwa mmoja kweli kweli. Kulingana na Yesu mwenyewe, mwanzilishi wa ukristo, kukata shauri kwa njia ile ya pili ndilo jambo sahihi. Katika pindi moja, yeye alinena habari za wengine ambao wangemwita “Bwana, Bwana.” Ndiyo kusema, wangedai kuwa ni Wakristo, wakimkubali Yesu kuwa Bwana wao. Na wangekuwa wenye shughuli nyingi sana wakifanya zenye kuonekana kuwa kazi za maana kwa jina lake. Hata hivyo Yesu angewaambia: “Sikuwajua ninyi kamwe; ondokeni kwangu, ninyi mtendao maovu.”—Mathayo 7:22, 23.
Hakika, hakuna wo wote kati yetu wangetaka kuwa katika hali hiyo! Kwa hiyo, tunaweza kujuaje kama sisi ni Wakristo wa kweli au sivyo? Je! pana ufunguo wa kupata Ukristo wa kweli?
Ule Ufunguo
Ndiyo, upo. Bila shaka uko, Ukristo unatia ndani mambo mengi. Kwa mfano, Mkristo wa kweli anapaswa kuwa na imani yenye nguvu katika Mungu, kwa sababu “pasipo imani haiwezekani kumpendeza [Mungu].” (Waebrania 11:6) Pia anapaswa kuwa akifanya kazi zinazofaa. Mwanafunzi Yakobo alionya kwamba: “Imani pasipo matendo imekufa.” (Yakobo 2:26) Zaidi ya hilo, mtume Paulo aliukazia umaana wa kuwa na “maarifa sahihi ya mapenzi yake [Mungu] katika hekima yote na ufahamu wa kiroho.” (Wakolosai 1:9, NW ) Lakini hakuna lo lote la mambo hayo linalotoa ufunguo wa kupata Ukristo.
Uhakika ni kwamba, tunaweza kuwa na maarifa ya kutosha ya Biblia na imani yenye nguvu na tuwe wenye shughuli nyingi katika kazi njema, lakini bado tuwe tu Wakristo wa kusingizia. Hilo linawezekanaje? Mtume Paulo alieleza hivi: “Nijaposema kwa lugha za wanadamu na malaika, kama sina upendo, nimekuwa shaba iliayo na upatu uvumao. Tena nijapokuwa na unabii, na kujua siri zote na maarifa yote, nijapokuwa na imani timilifu kiasi cha kuweza kuhamisha milima, kama sina upendo, sina kitu mimi. Tena nikitoa mali zangu zote kuwalisha maskini, tena nikijitoa mwili wangu niungue moto, kama sina upendo, hainifaidii kitu.”—1 Wakoritho 13:1-3.
Ndiyo, ufunguo wa kutambua dini ya kweli ni kuthamini kwamba hiyo inategemea upendo wa kweli. Imani yetu, kazi njema, na maarifa sahihi ni mambo yanayohitajiwa kabisa. Lakini tusipoyatendesha kazi kwa upendo, hayatuletei faida kubwa. Kwa sababu gani? Ni nini kinachoifanya sifa ya upendo iwe ndiyo ya maana zaidi?