Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w86 6/15 kur. 15-20
  • ‘Panda kwa Ukarimu, Vuna kwa Ukarimu’

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • ‘Panda kwa Ukarimu, Vuna kwa Ukarimu’
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kupanda kwa Ukarimu Kuhusu Funzo la Biblia
  • Kupanda kwa Ukarimu Kuhusu Hudhurio la Mikutano
  • Kupanda kwa Ukarimu Kuhusu Sala Zetu
  • Kupanda kwa Ukarimu Kuhusu Huduma Yetu
  • Kupanda kwa Ukarimu Kuhusu Uhusiano wa Kijamaa
  • Uwe Mvunaji!
  • Je! Wewe Unapanda kwa Wingi?
    Huduma Yetu ya Ufalme—1994
  • Kupanda kwa Wingi Huleta Baraka Tele
    Huduma Yetu ya Ufalme—2002
  • Panda kwa Uadilifu, Vuna Fadhili-Upendo za Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2002
  • Panda kwa Wingi Lakini kwa Busara
    Huduma Yetu ya Ufalme—2004
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
w86 6/15 kur. 15-20

‘Panda kwa Ukarimu, Vuna kwa Ukarimu’

“Apandaye haba atavuna haba; apandaye kwa ukarimu atavuna kwa ukarimu.”​—2 WAKORINTHO 9:6.

1. Kwa sababu gani Yehova Mungu ndiye mtu mwenye furaha zaidi katika ulimwengu mzima?

MUNGU Yehova ndiye ‘Mungu mwenye furaha.’ Bila shaka sababu moja ni kwamba yeye ni Mpaji mkarimu (wa utele). Mwanaye, Yesu Kristo, alieleza hivi: “Kuna furaha nyingi katika kutoa kuliko zilivyo katika kupokea.” (1 Timotheo 1:11; Matendo 20:35, NW) Hakuna mtu ametoa vingi zaidi ya Yehova​—tangu alipomtokeza Mwanaye mzaliwa pekee yule Logos, mpaka wakati huu wa sasa. Kwa hiyo bila kivuli cha shaka lo lote yeye ndiye mtu mwenye furaha zaidi katika ulimwengu mzima.

2, 3. (a) Ni kwa njia gani Mungu amepanda kwa ukarimu? (b) Kwa sababu gani inaweza kusemwa kwamba Yehova amevuna na bado atavuna kwa ukarimu?

2 Kanuni ambayo kidogo inafanana ha hiyo imetajwa kwenye 2 Wakorintho 9:6: “Apandaye haba atavuna haba; apandaye kwa ukarimu [utele] atavuna kwa ukarimu [utele].” Yehova Mungu amepanda kwa ukarimu kweli kweli kuhusiana na kazi zake za uumbaji! Neno Lake linaeleza juu ya mamia ya mamilioni ya viumbe wa kiroho. (Ufunuo 5:11) Angalia pia magalaksi yasiyohesabika katika mbingu zenye nyota, kila moja likiwa na maelfu ya mamilioni ya nyota. Tukishuka kuja kwenye dunia hii, ni nyingi kama nini namna za vitu vinavyokaribia kutohesabika, vyenye uhai na visivyo na uhai, ambavyo Yehova Mungu aliumba. Kwa uhakika ‘dunia imejaa mali zake.’ (Zaburi 104:24) Zaidi ya hilo, yeye ametujalia katika akili zetu, katika hisia zetu, na katika mwili wetu kwa ukarimu jinsi gani! Kwa kweli sisi ‘tumeumbwa kwa jinsi ya ajabu.’​—Zaburi 139:14.

3 Hakuna shaka kwamba Yehova Mungu amepanda kwa ukarimu (utele). Ndivyo ilivyo si katika kazi zake za uumbaji tu bali pia katika shughuli zake pamoja na viumbe wake wa kidunia. Je, yeye pia amevuna kwa ukarimu? Kweli kweli! Jinsi gani? Ni kwa sababu yeye amekuwa, na anaendelea kuwa, na bado atakuwa na viumbe wengi sana wenye akili wanaomtumikia kwa kuongozwa na upendo. Wanapofanya hivyo wanaufurahisha moyo wa Yehova, hasa kwa sababu jambo hilo linathibitisha Ibilisi mwenye kutoa malawama ni mwongo.​—Mithali 27:11.

4. Kanuni ya 2 Wakorintho 9:6 inatumikaje katika maisha zetu?

4 Biblia ina ushuhuda tele kwamba, kuanzia na Logos, watumishi wengi waaminifu wa Yehova Mungu wamepanda kwa ukarimu na vivyo hivyo wakavuna kwa ukarimu. Hivyo ndivyo inavyopasa kuwa, kwa maana kanuni za Yehova zinatumika nyakati zote na kuhusu watu wote. Kwa hiyo, ile kanuni ya kupanda inaweza kuwa kweli katika maisha yako.

5, 6. (a) Ni maadui gani wanaofanya iwe vigumu kwetu kupanda kwa ukarimu? (b) Ni lazima tuwe na nia ya kufanya nini, na katika pande gani za utumishi mtakatifu wetu?

5 Ingawa Maandiko yana sababu na mifano tele juu ya jinsi sisi tunavyoweza kupanda kwa ukarimu, si jambo rahisi kufanya hivyo. Kwa sababu gani? Kwa sababu tuna maadui watatu wanaotupinga vikali tusifanye hivyo. Kwanza, kuna maelekeo yetu wenyewe tuliyorithi ya kuwa na uchoyo. Tunasoma hivi kwenye Mwanzo 8:21: “Mawazo ya moyo wa mwanadamu ni mabaya tangu ujana wake.” Neno la Mungu linatuarifu pia kwamba moyo wa kibinadamu ni wenye hila na wenye ugonjwa wa kufisha (Yeremia 17:9) Pili, inatupasa tushindane na mikazo kutoka ulimwengu mwovu, ulio katika uwezo wa yule mwovu. (1 Yohana 5:19) Tatu Ibilisi mwenyewe yuko tayari kutumeza tusipojihadhari.​—1 Petro 5:8.

6 Je, wewe unakaa chonjo daima kuwaona maadui hao watatu? Kwa sababu ya wapinzani hao, ni lazima tuwe na hamu nyingi ya ‘kusikiliza mashauri na kukubali nidhamu ili tupate kuwa wenye hekima katika wakati ujao wetu.’ (Mithali 19:20, NW) Kwa kweli, ni lazima tufanye kama alivyofanya mtume Paulo, ‘kupiga-piga ngumi miili yetu na kuifanya kama watumwa,’ tusije tukashindwa kufanikiwa mwishowe. (1 Wakorintho 9:27) Kanuni ya kwamba tukipanda kwa ukarimu tutavuna kwa ukarimu inatumika kuhusu pande zote mbalimbali za utumishi mtakatifu unaofanywa na mashahidi wote Wakristo wa Yehova. Ndiyo, ko kote tunakotazama, tutakuta kwamba kanuni hiyo inatumika: katika funzo letu la kibinafsi, katika hudhurio letu la mikutano, katika sala zetu, katika kutoa ushuhuda uliopangwa rasmi na wa vivi hivi, na katika uhusiano wetu wa kijamaa.

Kupanda kwa Ukarimu Kuhusu Funzo la Biblia

7, 8. (a) Ili tupande kwa ukarimu kuhusu funzo letu la kibinafsi la Biblia, ni lazima tuwe na nini? (b) Ni miradi gani tunayopaswa kuweka, na tunaweza kuifikiaje?

7 Ili tuwe wahudumu wa Yehova Mungu wenye kuzaa matunda, ni lazima kwanza tupande kwa ukarimu kuhusu funzo letu la kibinafsi la Biblia. Inatupasa tutake kuwa na hamu nyingi sana ya kula chakula cha kiroho, kwa kuthamini kwamba hatuishi kwa kutegemea vitu vya kimwili tu. Kwa sababu ya kusongwa na mahangaikio na utendaji mbali-mbali wa maisha ya kila siku, jitihada ya kujikaza sana inahitajiwa ili tuujue vizuri uhitaji wetu wa kiroho. (Mathayo 13:19) Ingekuwa vizuri kweli kweli sisi binafsi tulithamini Neno la Mungu kama mtunga zaburi alipoandika hivi: “Naifurahia ahadi yako, kama apataye mateka mengi.”​—Zaburi 119:162.

8 Tunapata msaada halisi katika kufanya hivyo tunapotii shauri la ‘tuangalie sana jinsi tunavyoenenda; si kama watu wasio na hekima, bali kama watu wenye hekima.’ (Waefeso 5:15, 16) Unaweza hata kujichunguza katika sehemu mbalimbali zinazohusiana na jambo hilo. Jiulize: Je, mimi ninapanga mambo yangu ili nitafute wakati wa kusoma kila gazeti la Mnara wa Mlinzi na Amkeni! linapotokea? Namna gani Kitabu cha Mwaka, na pia vitabu na vichapo vingine tunavyopata kwenye mikusanyiko? Huenda tusiweze siku zote kupata saa moja au mbili za kuvisoma, lakini kwa kuwa chonjo tunaweza kupata dakika chache hapa na pale tusome sura moja ya Biblia au makala ya gazeti. Wakristo kadha wanapanga kuamka dakika 10 au 15 mapema zaidi kila siku ili wasome wanapokuwa chonjo zaidi. Wengine wanaona kwamba wanaweza kusoma sana wanaposafiri katika magari ya abiria. Namna gani wewe?

9. Tunaweza kuvunaje kwa ukarimu kuhusu funzo letu la kibinafsi la Biblia?

9 Kwa kupanda kwa ukarimu kwa njia hizi, sisi pia tunaweza kutumainia kuvuna kwa ukarimu. Jinsi gani? Kwa sababu tutakuwa na imani yenye nguvu zaidi, tumaini lenye matazamio mazuri zaidi, na hali ya akilini yenye furaha na mwelekeo mzuri. Zaidi ya hilo, tutakuwa tumetayarika vizuri zaidi kutolea wengine ushuhuda. Tutaweza kuchanga katika maongezi mambo yenye mafaa na kusaidia ndugu zetu tupatapo nafasi. Angalia kutokana na 1 Timotheo 4:15, 16 matokeo yanaweza kuwa nini.

Kupanda kwa Ukarimu Kuhusu Hudhurio la Mikutano

10. Mwelekeo wetu unapasa kuwa nini kuhusu mikutano yetu?

10 Wewe unaweza kuuliza: Je, kanuni hii ya kuvuna kwa ukarimu tukipanda kwa ukarimu inatumika pia kuhusu kuhudhuria kwetu mikutano ya kundi? Hakika ndivyo ilivyo! Inatupasa tujisikie kama mtunga zaburi Daudi aliposema hivi: “Nalifurahi waliponiambia, Na twende nyumbani kwa [Yehova].” Ndiyo, inatupasa tujisikie tukivutwa na moyo kutaka kukutana na ndugu zetu.​—Zaburi 122:1.

11, 12. Tunaweza kupanda na kuvunaje kwa ukarimu kuhusu kuhudhuria mikutano yetu?

11 Hiyo inatutaka tufanye nini? Inamaanisha tuhudhurie kwa ukawaida na kwa uaminifu mikutano yetu mitano ya kila juma, kutokuacha hali ya hewa iliyo mbaya kidogo au kasoro ndogo sana ya afya ya kimwili iwe udhuru wa kubaki nyumbani. Ni mara ngapi tunapoiona hali ya hewa​—yenye joto au baridi, yenye mvua au ukavu​—ikivuruga kuhudhuria mikutano? Hata hivyo, kadiri ambavyo vipingamizi tunavyolazimika kushinda ili tuhudhurie vinavyozidi kuwa vingi, ndivyo baraka ambayo Yehova anaelekea kutuletea inavyokuwa kubwa zaidi. Tunaweza kupanda kwa ukarimu kwa kuja mapema pia ili tuwe na maongezi ya kutiana moyo kabla ya mikutano, kisha kukaa-kaa kidogo baadaye kwa kusudi ilo hilo. Ni kwa kadiri gani wewe binafsi unatimiza jambo hilo? Je, inakupasa ujaribu kupanda kwa ukarimu zaidi? Kujitayarisha vizuri kwa ajili ya Funzo la Mnara wa Mlinzi na mikutano ile mingine kunahusika pia. Sababu ya hilo ni kupanda kwa ukarimu kwa kutoa maelezo kadiri ambavyo nafasi inatokea.

12 Ni kwa njia gani tunaweza kutumainia kuvuna kwa ukarimu kwa sababu ya kufanya hivyo? Hatuwezi kusema maneno ya kutia moyo bila ya sisi wenyewe kutiwa moyo; hatuwezi kuchangamsha nafsi iliyoshuka moyo bila ya mioyo yetu wenyewe kuinuliwa. Ndiyo, hatuwezi kujieleza wenyewe mikutanoni bila ya imani yetu wenyewe kutiwa nguvu na kweli tunazotamka. Ni jambo la wazi tu: “Nafsi ya mtu mkarimu itawandishwa; anyweshaye atanyweshwa mwenyewe.”​—Mithali 11:25.

Kupanda kwa Ukarimu Kuhusu Sala Zetu

13, 14. Ni kwa njia gani tunaweza (a) kupanda kwa ukarimu, (b) kuvuna kwa ukarimu kuhusu sala zetu?

13 Kanuni ya Kimaandiko ya kupanda kwa ukarimu inahusu pia sala zetu za kibinafsi. Je, sala zetu zinasemwa kwa kurudia-rudia maneno na mawazo yale yale tu bila kubadilishwa, au kwa kweli zinatoka moyoni? Je, zinatia ndani si maombi tu bali pia sifa na shukrani zenye kutoka moyoni, na pindi kwa pindi, maneno ya kusihi sana? Je, kwa kweli sisi tunalichukua kwa uzito pendeleo lenye thamani kubwa la sala? Je, tunammwagia Baba yetu wa kimbingu mioyo yetu? Au tunafanya haraka haraka kumaliza sala zetu, nyakati nyingine hata tukiwa wenye shughuli mno tusiweze kusali? Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yanaonyesha kwamba sala ilikuwa jambo kubwa sana katika maisha za Yesu Kristo na mtume Paulo.​—Luka 6:12, 13; Yohana 17:1-26; Mathayo 26:36-44; Wafilipi 1:9-11; Wakolosai 1:9-12.

14 Kwa kadiri ambayo sisi tunapanda kwa ukarimu kuhusu sala zetu, kwa kadiri iyo hiyo tunaweza kutumainia kuvuna kwa ukarimu kwa kujibiwa sala hizo na Yehova na kwa kuwa na uhusiano mwema pamoja naye. Sala za kijamaa zinasaidia kufanya washiriki wawe na uhusiano wa karibu zaidi na mwenye kuitoa sala. Acheni tuzingatie pia maneno ya Yesu kwenye Mathayo 7:7: “Ombeni, nanyi mtapewa; tafuteni nanyi mtaona; bisheni nanyi mtafunguliwa.”

Kupanda kwa Ukarimu Kuhusu Huduma Yetu

15. Ni wapi hasa kupanda na kuvuna kwa ukarimu kunaweza kufurahiwa?

15 Labda hakuna mahali ambako kichwa chetu cha habari hii kinaonekana wazi zaidi kama kilivyo kuhusiana na kazi yetu ya kutoa ushuhuda. Kwa wazi, kadiri ambavyo tunaweza kutumia wakati mwingi zaidi kwenye kazi hiyo, ndivyo tutakavyoelekea kuvuna zaidi kwa kupata maono yenye kupendeza, ziara za kurudia zenye matunda, na mafunzo ya nyumbani ya Biblia yenye mazao, matokeo yawe ni kupata barua zilizo hai za kutupendekeza.​—2 Wakorintho 3:2.

16, 17. (a) Kupanda kwa ukarimu kuhusu utumishi wa shambani kunatutaka tufanye nini? (b) Tukifanya hivyo, tunaweza kutazamia matokeo gani?

16 Lakini, kupanda kwa ukarimu kuhusu huduma ya shambani hakuhusu wingi tu bali ubora pia. Tunataka ‘kupashwa moto kwa roho’ tunaposhiriki katika huduma. (Warumi 12:11) Tunapaswa kufikia watu tukiwa na uhuru wa kusema, tukiwa na tabasamu changamfu la kirafiki. Jambo hilo linahusika kama tunaenda nyumba kwa nyumba au tunashiriki katika ushuhuda wa barabarani. Msaada wetu mpya wa kutolea ushuhuda Reasoning from the Scriptures utapasa kutusaidia sisi sote tuwe wenye matokeo mazuri zaidi, na hivyo tuwe wenye mazao zaidi, tuvune mengi zaidi kutokana na wakati na nishati tunazotumia katika huduma.

17 Na je, kupanda kwa ukarimu kuhusu huduma yetu ya shambani hakumaanishi pia kudhamiria kuandika mahali ambapo tumepata watu wanaopendezwa? Jambo linalohusiana na kufanya hivyo ni kukubali wajibu wa kurudi tukasitawishe hali hiyo ya kupendezwa kufikia hatua ya kuanza funzo la nyumbani la Biblia ikiwezekana. Zaidi ya hilo, ni lazima tuwe waangalifu tujenge kwa vifaa visivyoweza kuteketezwa na moto. Hiyo inamaanisha tufundishe kwa usadiki, lakini kwa kujitia katika shida za watu na kuwa wenye ufahamu, kutumia ustadi kuwafanya wanafunzi wa Biblia waeleze maoni yao ya moyoni juu ya kanuni za Biblia. Ni kwa kupanda kwa ukarimu tu katika njia hizo tunaweza kutumainia kufanya watu wawe Wakristo watakaoweza kuyapinga mashambulizi ya Shetani na mfumo wake wa mambo.​—1 Wakorintho 3:12-15.

Kupanda kwa Ukarimu Kuhusu Uhusiano wa Kijamaa

18. Ni shauri gani tunalopaswa kuzingatia kuhusu uhusiano wetu wa kijamaa?

18 Ile kanuni ya kitheokrasi kwamba tunavuna kulingana na njia ambayo tunapanda inatumika pia ndani ya jamaa. Hapa tunaweza kuzingatia maneno ya Yesu kwenye Luka 6:38: “Wapeni watu vitu nanyi mtapewa; kipimo cha kujaa na kushindiliwa na kusukwa-sukwa hata kumwagika, ndicho watu watakachowapa vifuani mwenu. Kwa kuwa kipimo kile kile mpimacho ndicho mtakachopimiwa.”

19. Waume na wake wanaweza kupandaje kwa ukarimu na kujifaidi kwa kufanya hivyo?

19 Kuna nafasi nyingi sana ambazo waume na wake wanapaswa kupanda kwa ukarimu kwa kufanya vitendo vyenye shauku ya upendo vya kufikiriana na kutokuwa wachoyo! Mtume Paulo anatoa shauri bora, kwenye Waefeso 5:22-33. Tafadhali soma mistari hiyo unapofikiria jinsi wewe unaweza kupanda kwa ukarimu zaidi. Kwa kadiri ambayo mke Mkristo anajitiisha kweli kweli, kufanya ushirikiano, na kuunga mumeye mkono, kwa kadiri hiyo yeye ataelekea kuvuna kwa ukarimu. Kwa njia gani? Kwa kuonyeshwa na mumeye shauku yenye joto na upendo wa kumthamini, huku mumeye akisukumwa na moyo ampende kama mwili wake mwenyewe. Vivyo hivyo, kwa kadiri ambayo mume Mkristo anajitahidi kumjali mkeye kama inavyohimizwa kwenye 1 Petro 3:7 na kumpenda bila choyo kama inavyokaziwa kwenye Waefeso 5:28, 29, kwa kadiri hiyo yeye anaweza kutumainia kuvuna utiifu wa mkeye na kuungwa mkono naye kwa ushikamanifu.

20. Kupanda kwa ukarimu kunaweza kutumiwaje kuhusu kulea watoto, na kwa matokeo gani?

20 Wala haitupasi kusahau daraka letu kulea watoto wetu katika nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova. (Waefeso 6:4, NW) Kwa kweli, kufanya hivyo kunapasa kutangulizwe mbele ya wajibu mbalimbali wa kitheokrasi na mapendeleo mengine. Jambo la kusikitisha ni kwamba, hii ni kanuni ambayo imeachiliwa na wazazi wengine Wakristo. Kwa upande mwingine, ni lazima wazazi wawe na nia ya kujinyima raha na starehe mbalimbali kwa faida ya masilahi ya kimoyo na kiroho ya watoto wao, wakitumia wakati wa kutosha pamoja nao na kuwaonyesha upendo mwingi. Kwa upande mwingine, ni lazima wazazi waonyeshe uthabiti. Wao wanashauriwa hivi: “Mrudi mwanao naye atakustarehesha; naam, atakufurahisha nafsi yako.” Panda kwa njia hizo, na inaelekea sana kwamba utavuna kwa ukarimu kwa kuwa na watoto washika ukamilifu wenye kukuheshimu na kujisikia wakiwa na uhusiano wa karibu nawe.​—Mithali 29:17.

Uwe Mvunaji!

21, 22. Ni kwa njia gani mbalimbali tunaweza kupanda na kuvuna kwa ukarimu kuhusu utumishi mtakatifu wetu na uhusiano wetu wa kijamaa?

21 Basi, tunaona kwamba ile kanuni ya kuwa tunavuna kulingana na njia ambayo tunapanda inatumika katika pande zote za Ukristo. Tukipanda kwa ukarimu kuhusu funzo letu la kibinafsi la Biblia, tutavuna imani yenye nguvu, tumaini lenye matazamio mazuri, na ustadi katika huduma yetu. Tukipanda kwa ukarimu kuhusu mikutano yetu, imani yetu wenyewe itatiwa nguvu, nasi tutatia nguvu imani ya wengine. Tukipanda kwa ukarimu kuhusu sala zetu, tutavuna uhusiano mwema pamoja na Baba yetu wa kimbingu na sala zetu zitajibiwa. Nasi tukipanda kwa ukarimu kuhusu kazi yetu ya kutoa ushuhuda, tutapata faida kibinafsi, na tunaweza kutumainia kuwa na barua za pendekezo kuonyesha jitihada zetu.

22 Vivyo hivyo, na tusisahau kamwe kwamba kanuni hii inatumika katika uhusiano wetu wa kijamaa. Tukipanda kwa ukarimu kwa kufikiriana kwa upendo na kufanya vitendo visivyo na choyo, sisi waume, wake, wazazi au watoto tunaweza kutumainia kuvuna maisha ya jamaa yenye ukarimu (utele) kwa kupata ushirika na maono yenye kuthawabisha. Jambo hilo pia litawapa ushuhuda mzuri wale walio nje, lipendekeze njia yetu ya maisha.

23. Ingetufaa tutii shauri gani?

23 Kwa hiyo kila shahidi Mkristo wa Yehova na ajiulize mwenyewe hivi: Je, mimi ningeweza kupanda kwa ukarimu zaidi? Maneno ya Paulo kwenye 1 Wathesalonike 4:1 yanafaa sana: “Iliyobaki, ndugu, tunakusihini na kuwaonya kwamba mwenende katika Bwana Yesu; kama mlivyopokea kwetu jinsi iwapasavyo kuenenda na kumpendeza Mungu, kama nanyi mnavyoenenda, vivyo hivyo mpate kuzidi sana.” Ndiyo, acheni sisi sote tujaribu kupanda kwa ukarimu zaidi ili tuvune kwa ukarimu zaidi, kwa heshima ya Yehova na baraka yetu wenyewe na ndugu zetu.

Mambo ya Kurudia Kujikumbusha

◻ Yehova Mungu anaonyeshaje mfano wa ukweli unaopatikana kwenye 2 Wakorintho 9:6?

◻ Wewe unaweza kufanya nini uvune kwa ukarimu zaidi kuhusu funzo la Biblia na mikutano ya Kikristo?

◻ Unaweza kupanda na kuvunaje kwa ukamili zaidi kuhusu utumishi wa shambani?

◻ Ni hatua gani zenye mafaa zinazoweza kusaidia jamaa yako ipande na kuvuna kwa ukarimu zaidi?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki