Je! Wewe Unapanda kwa Wingi?
1 Kuna msemo usemao: “Kadiri unavyojitahidi kwa kitu fulani, ndivyo kadiri utapata mafanikio.” Hilo ni kweli hasa kuhusu ibada yetu. Kadiri tutumiavyo wakati na jitihada nyingi kujitayarisha kwa ajili ya mikutano, kuhubiri ujumbe wa Ufalme, na kuonyesha upendo kwa ndugu zetu, ndivyo tutakavyonufaika na ukuzi wa kiroho. Ndivyo ilivyo pia na kufanya kinyume cha hivyo. Ikiwa hatujitahidi wenyewe au twafanya mambo kwa moyo nusu-nusu, je, kwa kweli twaweza kutazamia matokeo yenye kutosheleza?
2 Mtume Paulo aliandika vizuri kanuni iliyo kwenye 2 Wakorintho 9:6, NW: “Yeye apandaye kwa uhaba atavuna pia kwa uhaba; na yeye apandaye kwa wingi atavuna pia kwa wingi.” Je! wewe unapanda kwa wingi?
3 Funzo la Biblia la Kibinafsi: Ili tuwe wahudumu wenye matokeo, ni lazima kwanza tupande kwa wingi katika funzo letu la kibinafsi. Twapaswa kuwa na hamu nyingi ya kiroho. (Zab. 119:97, 105; Mt. 5:3) Kukiwa na shughuli nyingi za kila siku zenye kutusonga, yahitaji jitihada nyingi kusitawisha utambuzi halisi wa mahitaji yetu ya kiroho. Kwa wengi wetu, twahitaji ‘kuukomboa wakati.’ (Efe. 5:16) Watu fulani hupanga kuamka asubuhi na mapema siku maalum ili wafanye funzo la kibinafsi. Wengine wametenga jioni fulani kwa kusudi hilo. Ni katika njia gani tunayovuna kwa wingi? Twapata imani yenye nguvu, tumaini jangavu, na hali ya akili yenye furaha na chanya.—Rum. 10:17; 15:4; 1 Pet. 1:13.
4 Mikutano ya Kutaniko: Kwenye Zaburi 122:1, Daudi alisema: “Nalifurahi waliponiambia, na twende nyumbani kwa BWANA.” Wewe wahisi vivyo hivyo? Kupanda kwa wingi kwamaanisha hudhurio la kawaida katika mikutano yetu mitano ya kila juma. Azimia kwamba hautaruhusu hali mbaya ya hewa ikuzuie. Kwa kawaida, kadiri tunavyoshinda vipingamizi vingi, ndivyo tunavyopata baraka nyingi.
5 Fika mapema na ukawie baadaye ili ushiriki mazungumzo yenye kujenga pamoja na ndugu zako. Ongeza ushirika wako utie ndani wengi tofauti kadiri uwezavyo. Jitayarishe vizuri kwa ajili ya Funzo la Mnara wa Mlinzi na mikutano mingine ili uweze kupanda kwa wingi kwa kutoa maelezo unapopata fursa. Kwa ‘kunywesha kwa utele’ wengine katika mikutano, wewe pia ‘utanyweshwa kwa utele.’—Mit. 11:25.
6 Huduma ya Shambani: Labda kanuni hii ya kupanda kwa wingi haitimizwi mahali popote zaidi ya jinsi ilivyo kwenye huduma ya shambani. Kadiri tutumiavyo wakati mwingi kwayo, ndivyo twaelekea kuvuna maono yenye kupendeza, ziara za kurudia zenye matokeo, na mafunzo ya Biblia yenye matokeo.
7 Kupanda kwa wingi katika huduma ya shambani kwatia ndani ubora na wingi. Msaada mzuri zaidi wa kutusaidia tuboreshe ubora wa huduma yetu ni kitabu Kutoa Sababu. Kurasa 9-15 zaorodhesha matangulizi zaidi ya 40 yanayoshughulikia mambo 18 ya kusaidia kuamsha kupendezwa milangoni. Ukipata upendezi, hakikisha umeandika ili uweze kurudi na kuvuna matunda ya kupanda kwako. Huenda jitihada zako zikaongoza kwenye funzo la Biblia, na uweze kumfundisha mtu fulani jinsi ya kupanda kwa wingi.
8 Tukipanda kwa wingi, twaweza kutazamia baraka nyingi kutoka kwa Yehova.—Mal. 3:10.