Kupanda kwa Wingi Huleta Baraka Tele
1 Sisi sote twatazamia sana utimizo wa ahadi bora zilizo katika Neno la Mungu. Hata sasa, Yehova hutubariki sana na kufanya maisha yafurahishe zaidi. Hata hivyo, kufaidika kwetu kunategemea sana jitihada zetu wenyewe. Kama vile mtume Paulo alivyosema, “yeye apandaye kwa wingi atavuna pia kwa wingi.” (2 Kor. 9:6) Fikiria sehemu mbili ambazo tunaweza kutumia kanuni hiyo.
2 Huduma Yetu: Kuwahubiria watu habari njema tunapopata fursa ya kutoa ushahidi hutuletea thawabu nyingi. (Mit. 3:27, 28) Wengi wanastahili kupongezwa kwa kupanda kwa wingi wanapopanua huduma yao, ambayo inatia ndani kufanya upainia-msaidizi au upainia wa kawaida. Sisi sote twaweza kupanda kwa wingi kwa kuwa macho tunapowarudia wale waliopendezwa ili kuchochea upendezi wowote walioonyesha na kuwatolea funzo la Biblia hali inaporuhusu. (Rom. 12:11) Tunapojitahidi katika njia hizi sisi hupata mambo yaliyoonwa yenye kutia moyo na shangwe yetu katika huduma huongezeka.
3 Kutegemeza Masilahi ya Ufalme: Paulo alisema juu ya ‘kupanda kwa wingi’ kuhusiana na kutoa vitu vya kimwili. (2 Kor. 9:6, 7, 11, 13) Leo, kuna mengi tunayoweza kufanya kwa njia ya kimwili ili kutegemeza masilahi ya Ufalme. Twaweza kusaidia katika ujenzi wa Majumba ya Ufalme na Majumba ya Kusanyiko. Pia twaweza kujitolea kusafisha na kudumisha mahali hapo pa ibada ya kweli. Kwa kuongezea, twaweza kutoa michango ya kifedha ya kushughulikia gharama za kutaniko letu na vilevile michango ya kazi ya ulimwenguni pote ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi. Sisi sote tufanyapo sehemu yetu, tunakuwa na shangwe kama nini kuona baraka tele za Yehova katika kazi hii tuliyopewa Naye!—Mal. 3:10; Luka 6:38.
4 Neno la Mungu hutusihi “kufanya mema, kuwa matajiri katika kazi zilizo bora, kuwa wakarimu, tayari kushiriki.” Tunapotii shauri hilo, tunafurahia baraka tele sasa. Vilevile, tutakuwa ‘tunajiwekea wenyewe kuwa hazina salama msingi bora kwa ajili ya wakati ujao na uhai ulio halisi’ utakaokuja.—1 Tim. 6:18, 19.