Wewe Unaweza Kuongozaje Maoni Yako ya Moyoni?
WATU wengi leo wanatamani kuchochewa maoni yao ya moyoni. Wanatafuta msisimuko kwa kuendesha magari haraka sana, kufanya michezo hatari, ngono za haramu, na kutumia dawa zenye kuamsha mwili. Kwa kweli, ulimwengu wa biashara na vitumbuizo unakazia uhitaji wa kuchochea maoni ya moyoni. Hivyo, watu wengi hawapendi sana amani na utulivu, kwa kujisikia kwamba wanastahili kupata msisimuko mwingi zaidi wa maoni ya moyoni kutokana na maisha.
Bila shaka, sisi sote tuna maoni ya moyoni. Kwa mfano, wakati tunapotabasamu, kucheka, au kulia, tunaonyesha hali ya maoni ya moyoni tuliyo nayo wakati huo. Lakini je, wewe ulijua kwamba maoni ya moyoni yanaweza kuleta matokeo fulani katika mwili wako, kama vile kusababisha mabadiliko katika mkazo wa damu, kiasi cha mpigo wa moyo, na utoaji jasho? Yanaweza pia kuleta masumbuko ya mwili, kama vile maumivu ya kichwa, tumbo lililovurugika, na matatizo ya mgongo. Kwa hiyo, kwa ujumla watu wanatafuta kuwa na maoni ya moyoni yanayopendeza na kuepuka yale yasiyopendeza. Watu fulani wanajaribu kuyaepuka yale yasiyopendeza kwa kuwazia-wazia raha zisizo za kweli, kula kupita kiasi, na kunywa kupita kiasi. Kwa upande mwingine, hali inayofaa ya maoni ya moyoni inaendeleza masilahi ya mtu. Mithali 14:30 inasema: “Moyo uliotulia ndio uzima wa nyama ya mwili.” (NW)
Jambo la kupendeza ni kwamba Neno la Mungu linataja namna zote za maoni ya ndani ya kibinadamu, kama vile upendo, chuki, furaha, huzuni, ushujaa, na woga. Huenda ikawa unakumbuka kwamba wakati mmoja ‘Yesu alilia machozi,’ akionyesha maoni yake ya moyoni kuhusu kifo cha rafiki. (Yohana 11:35) Yusufu alijikaza akijaribu kuzuia machozi “kwa sababu moyo wake ulimwonea shauku nduguye,” ambaye hakuwa amemwona kwa miaka mingi.—Mwanzo 43:3.
Kwa Sababu Gani Uongoze Maoni Yako ya Moyoni?
Kwa kuwa tunaishi katika “nyakati za mkazo” na sisi ni watu wasio wakamilifu, maoni mengi ya ndani yasiyo ya kupendeza ndiyo yanayopenya maisha zetu kuliko yale yanayopendeza. (2 Timotheo 3:1-5, Revised Standard) Kama vile Biblia inavyosema, “uonevu tu unaweza kufanya mwenye hekima atende kwa upumbavu mwingi.” (Mhubiri 7:7 NW) Kwa hiyo tusipojaribu kuzuia maoni ya moyoni yasiyofaa, tunaweza kuharibu uhusiano wetu na jamaa yetu, wanashule wenzetu, wafanya kazi wenzetu, na washirika wa Kikristo.
Kwa asili, sisi sote tunabadilishwa maoni ya moyoni na kile ambacho Biblia inakiita “wakati na tukio lisilotazamiwa.” (Mhubiri 9:11, NW) Kwa mfano, mume na mkeye, waliokuwa katika huduma ya wakati wote, walirudi kwenye kijumba chao wakakuta kwamba wameibiwa nyingi za mali zao. Jambo hilo liliwaudhi, hata kufikia hatua ya kujisikia ni wagonjwa. Iliwachukua siku kadha ndipo wakaweza kuongoza tena maoni yao ya moyoni. Walipopata nafuu, waliendelea katika kazi yao ya “kuwafariji wote waliao.”—Isaya 61:2.
Au huenda wewe ukawa unawajua watu wanaojiacha wachochewe tamaa zao za moyoni kwa kutazama sinema fulani. Wanajihusisha sana na watu wanaoonyeshwa katika sinema hizo mpaka mara nyingi wanalia kwa sababu ya hadithi hizo za kutungwa tu. Fikiria, pia, kisa cha mwanamke mseja mwenye kuishi peke yake. Usiku mmoja alianza kutazama sinema yenye mambo ya kuogopesha sana. Ingawa ‘aliogopeshwa kweli kweli,’ hakuweza kuacha kutazama. Baadaye akatatizika kulala. Mwishowe alipopata usingizi wenye mishtuko-mishtuko, unaweza kuwazia aliota juu ya nini: mizuka yenye kufyonza damu ya waliolala, na juu ya madubwana. Wazo hapa ni hili: sisi tunapatwa na mabadiliko fulani katika maoni ya moyoni kutokana na mambo yanayotendeka karibu na sisi. Basi, kwa uhakika inatupasa tuwe wachaguzi, tuepuke yaliyo na madhara au yanayovuruga usawaziko wa maoni yetu ya moyoni bila sababu.
Kukazia Maoni ya Moyoni Yanayofaa
Kwa upande mwingine, neno la Mungu linapendekeza kwamba tuwe “wenye kiasi katika mazoea,” tukitumia “uwezo wetu wa kuona sababu za mambo.” (Tito 2:2; Warumi 12:1, NW) Hiyo haimaanishi kwamba tujizuie kufikia hatua ya kwamba tunakuwa baridi kuhusu maisha. Maoni ya moyoni yenye kuzuiwa kwa njia inayofaa yanaongeza utamu maishani. Kwa mfano, Biblia inasema: “Hakuna jema kupita mwanadamu kuzifurahia kazi zake.”—Mhubiri 3:22.
Basi, ili kufanya maisha yafurahike kweli kweli, tunaweza kujifunza jinsi ya kusitawisha maoni ya moyoni yenye mwelekeo wa kutazamia mazuri. Mweleko huo, badala ya mawazo ya kutazamia mabaya, unaweza kutusaidia tuwe “wenye hamu ya kutenda yaliyo mema.” (Tito 2:14, New International Version) Misisimuko yenye uthabiti na iliyo mizuri inatia nguvu uamuzi imara na ustahimilivu wetu ili tuweze kufanya mambo yanayofaa. Bila shaka, Wakristo wanajua kwamba hawatimizi mambo katika utumishi wa Mungu kwa sababu ya mawazo yenye mwelekeo mzuri tu. Bali wanautambua uhitaji wa kutegemea kabisa roho ya Yehova ili wakabiliane na wakati ujao. (Luka 11:13; Mithali 19:21) Basi, je, tunaweza kuzuiaje maoni yetu ya moyoni, huku tukiyakuza yale yaliyo na faida?
“Wala Msifanye Wasiwasi”
Maoni ya moyoni kama vile hasira, wivu, uadui, na woga yanahitaji kuzuiwa kwa sababu yanaleta madhara. Kuonyesha mfano wa jinsi tunavyoweza kufanya hivyo, fikiria mfano wa oni moja tu la moyoni: wasiwasi.
Kani ya utendaji ya Mungu iliwatia nguvu watumishi wake wenye nia na uaminifu siku zilizopita, kama inavyofanya leo. Kwa kuongozwa na roho takatifu, Yesu alihifadhi maoni ya kutazamia mazuri kwa kupendezwa sana na mambo ya kiroho. Yeye aliwatia moyo wafuasi wake ‘wasifanye wasiwasi.’ (Luka 12:29) Yeye hakukosa kamwe uhakika wa kwamba baba yake angemtunza kwa upendo. (Yohana 15:9, 10) Bidii na shauku yake haikuzuiwa na ukosefu wa kazi ya kupendeza wala na kuvurugika mawazo. Vivyo hivyo, ikiwa wewe unataka kuzuia wasiwasi wa kupita kiasi, shughulisha akili yako na “mambo yanayostahili sifa.” (Wafilipi 4:8, NW) Ndiyo, kumtumaini Yehova kwa uhakika kunaweza kutupa nje mawazo ya kutazamia mabaya.
Kwa mfano, msichana mwenye kizuizi cha mwili katika São Paulo, Brazili, aliona wasiwasi kuhusu ukosefu wake wa kutokujua mambo ya ufundi na juu ya wakati ujao wake. Yeye alitunza watoto wadogo nyumbani huku wazazi wake wote wawili wakienda kazini. Kwa sababu ya kujisikia si mtu wa maana sana, yeye aliandika, “Mimi naogopa kwamba mwishowe nitarukwa na akili, nifanye jambo fulani la kipumbavu. Hata nilifikiria kujiua. Najisikia kwamba sitaweza kamwe kuolewa.” Baada ya kupokea barua iliyomhimiza aongeze kujifunza kwake Biblia, yeye aliandika: “Nilianza kujisikia kwamba mwishowe mtu fulani alikuwa akipendezwa na kuchanganua matatizo yangu, Wewe ulinionyesha jinsi lilivyo jambo la maana sana kuishi katika mfumo mpya wa Yehova.” Hivyo, badala ya kukaa ukiona wasiwasi tu mbona usijiwekee miradi fulani ya wazi, hasa ya kiroho, kama vile kufanya mengi zaidi katika kueneza habari njema za Ufalme au kutumia wakati mwingi zaidi ukijifunza Neno la Mungu?
Ni kweli kwamba kitulizo cha muda kidogo kinaweza kutokana na kujistarehesha, kutembea kidogo, kubadili kawaida yako ya maisha au mazingira, au kusikiliza muziki unaotuliza mawazo. Hata hivyo, huenda tukawa na maelekeo ya kutazamia mabaya na kufanya wasiwasi, ikitegemea mambo ambayo tumefundishwa au yale ambayo yametupata maishani. Kwa sababu hiyo, uwezo wa akili na uthabiti wa nia hautoshi kumpa mtu amani ya akili wala kumwingiza katika upendeleo wa Mungu. Ni lazima tujifunze ‘kumtwika Yehova fadhaa zetu zote.’ Unaweza kufanya hivyo ‘kwa maana yeye hujishughulisha sana kwa mambo yako.’—1 Petro 5:7.
Mungu Anapendezwa Kibinafsi na Wewe
Muumba hakukusudia kwamba watu wote wafanane na kuitikia mambo kwa njia ile ile moja. Katika Biblia, yeye alitoa kanuni za uongozi zinazofaa na zenye kutosha kwa watu wote. Alitutolea pia mifano yenye kufahamiwa waziwazi kuonyesha kwamba yeye anapendezwa kibinafsi na masilahi ya watumishi wake. “[Yehova] yu karibu nao waliovunjika moyo . . . Mateso ya mwenye haki ni mengi, lakini [Yehova] humponya nayo yote.” (Zaburi 34:18, 19) Kwa kweli, Yehova anayajua maoni tuliyo nayo kwa ndani kabisa, hata taabu na machozi yetu. Zaburi 56:8 inaeleza jambo hilo kwa njia hii: “Uyatie machozi yangu katika chupa yako; je! hayamo katika kitabu chako?” Kwa hiyo, wakati tunapokuwa na uhitaji wa kweli, hata ‘maskini na wahitaji,’ Yehova anaweza kuwa ‘msaada na mwokozi wetu.’ (Zaburi 40:17) Lakini ni mambo gani unayotakwa ufanye ili upokee msaada huo?
Kuthamini sifa bora kabisa za Mungu, “rehema zilizo nyororo” zake, kunatusaidia tuepuke kukaza fikira zote juu yetu wenyewe kwa njia isiyofaa. (2 Wakorintho 1:3, 4, NW) Hatuwezi kufuata maoni yetu ya moyoni kwa upofu huku tukijifikiria sisi wenyewe tu kwa sababu moyo wa kibinadamu unaweza kuwa “mdanganyifu,” ukiongoza kwenye vitendo visivyo vya akili, hata ngono za ukosefu wa adili. (Yeremia 17:9) Kwa mfano, mwanamke mmoja aliyeolewa katika Latini Amerika alivutiwa na mwanamume mmoja jirani. Kwa kusukumwa na maoni yake ya moyoni, mwanamke huyo aliitafutia sababu tamaa yake ya kutaka “kumsaidia” mwanamume huyo. Jambo zuri ni kwamba yeye alitafuta shauri la kiroho kwa Wakristo waliokomaa. Kwa kupata uthamini mwingi zaidi wa sifa za Mungu, alikomesha uhusiano huo. Sasa yeye anasema kwa furaha hivi: “Ndoa yangu iliokolewa.” Kwa uhakika, ingefaa sisi sote tusitawishe nia ya kutaka kufundishwa na Yehova na kumkaribia yeye.—Zaburi 19:7-11.
Imani yenye nguvu, yaani, tazamio lenye uhakikisho na tumaini thabiti, inasaidia kuleta mwelekeo wa kutazamia mambo mazuri, hali mambo yasiyojulikana yanaamsha wasiwasi na woga. (Waebrania 11:6) Kwa kweli, fikira za kutazamia mabaya au kuwa na mashaka zinaweza kutufanya tushindwe, hali tungaliweza kufanikiwa. Ukosefu wa imani unaonyesha kuna uhitaji wa kusitawisha tumaini hakika zaidi kwamba Mungu ana uwezo wa kuchukua hatua. (1 Yohana 5:10) Basi, ni jambo la maana sana kutegemea Mungu, kutoa sala za mara kwa mara ili tupate msaada wa kuongoza maoni yetu ya moyoni!—Yakobo 1:5.
Kujiweza na kuwa na kiasi, pia, ni sifa tunazohitaji kusitawisha ili tuendeleze uhusiano unaopendeza pamoja na wengine. “Mwenye roho ya utulivu ana busara,” akiongoza maoni yake ya moyoni. (Mithali 17:27) Zaidi ya hilo, mtume Paulo aliandika: “Acheni kiasi chenu kijulikane na watu wote,” kwa njia hiyo tusaidie kuleta maisha yenye utaratibu na amani.—Wafilipi 4:5, NW.
Kupenda wengine kunaendeleza maoni ya ndani yaliyo ya kupendeza zaidi, kuwa na nia ya kutaka kuwatia moyo wengine na kuwafanya wajisikie wamestarehe. “Katika upendo wa kidugu iweni na upendo mwororo wenye shauku kwa mmoja na mwenzake. Katika kuonyeshana heshima iweni wa kwanza.” “Upendo ni wenye subira na fadhili: hauna wivu wala majivuno wala kiburi; upendo hauna tabia mbaya wala si mchoyo wala hauudhiki; upendo hauweki kumbukumbu la makosa.”—Warumi 12:10, NW; 1 Wakorintho 13:4, 5, Today’s English Version.
Ukiendelea kusitawisha sifa hizi, unaweza kuwa na uhakika kwamba utapata msaada wa Yehova. Ni kama vile Paulo alivyoandika: “Amani ya Mungu, ipitayo akili zote, itawahifadhi mioyo yenu na nia zenu katika Kristo Yesu.”—Wafilipi 4:7.
Wewe Unataka Kufanya Nini?
Ingawa kila mmoja wetu huenda akawa anatambua vizuri zaidi uhitaji wake mwenyewe wa kuongoza maoni fulani ya moyoni, tunaweza kuwa na uhakika kwamba kuna uwezekano wa kufanya maendeleo na kupata furaha kubwa zaidi. Kwa kusudi hilo, inatupasa tujiangalie sana tusije tukawa tukikaa kitako tu bila kufanya lo lote huku tukifikiria-fikiria mambo yasiyo na msingi wala tusijiachilie tuongozwe na maoni ya moyoni yasiyozuiliwa kama vile kufanya wasiwasi bila sababu. Bali, acheni tujitahidi sana kusitawisha maoni ya moyoni yenye kutazamia mazuri na yenye afya ile tuwe na amani pamoja na sisi wenyewe, washirika wetu, na Mungu.
Ndiyo, inastahili kupiga moyo konde tufanye hivyo, tukiitazamia siku ambayo Yehova “atashibisha kila kilicho hai matakwa yake.” (Zaburi 145:16) Kwa hiyo, jitahidi hatua kwa hatua ukielekea kufurahia maisha katika mfumo mpya wa mambo ya Mungu ulio na amani. Kufanya hivyo kutasaidia kukuleta furaha hata sasa, na hakika hilo ni oni la moyoni linalofaa sana.