Jinsi Wengine Wamejifunza Kushinda Hisiamoyo Zisizofaa
NYAKATI nyingine kila mtu huwa na hisiamoyo zisizofaa. Kwa sababu ya matatizo makubwa kama vile ugonjwa mbaya, uzee, au kifo cha wapendwa, wengine huenda wakawa na hisiamoyo zisizofaa za ndani sana ambazo zinaweza kuathiri sana maisha zao.
Hata hivyo, hata miongoni mwa hao wa mwisho, kuna wale ambao wamejifunza kudhibiti hisiamoyo hizo ili kwamba waweze kuendelea na shughuli zao za kila siku kwa mafanikio. Ifuatayo ni mifano ya watu kama hao, kama walivyohojiwa na gazeti Amkeni!
Janis hupata matibabu kwa ajili ya ugonjwa unaoathiri hisiamoyo zake. Hata hivyo, yeye asema: “Nilipata kwamba njia yenye matokeo zaidi ya kukabiliana na tatizo hilo ni kudhibiti mawazo yangu. Mimi hufanya hivyo kwa kuwafanyia watu wengine vitu, kama vile kuoka na kushona. Mimi pia hufanya jitihada ya pekee kukazia fikiri kumbukumbu ya mambo yenye kupendeza na matukio ya wakati ujao ninayotazamia. Kwa sababu ya ugonjwa wangu, yote hayo si rahisi. Wakati mwingine ingekuwa rahisi zaidi kushindwa na kuhisi vibaya. Lakini matokeo mazuri yanastahili jitihada hiyo.”
Baada ya miaka 45 ya ndoa, mume wa Ethel alikufa. Ingawa alipata kihoro, Ethel hudhibiti hisiamoyo zake. Yeye aeleza: “Mimi hujishughulisha kwa kuwafanyia wengine vitu. Kwa mfano, mimi hufurahia kufundisha wengine kuhusu makusudi ya Mungu kama yanavyopatikana katika Biblia. Mwanamke mmoja mchanga alifurahia sana mambo mazuri aliyokuwa akijifunza hivi kwamba uthamini wake ulinisaidia kuwa mwenye shangwe zaidi. Ninapokazia fikira mambo chanya katika Biblia ili niwafundishe wengine, inasaidia kuondoa mawazo yasiyofaa akilini mwangu. Pia, wanawake wachanga huja kwangu kutafuta msaada wakiwa na matatizo mbalimbali, na kuzungumzia mambo chanya wanayoweza kufanya maishani mwao hunisaidia pia kushinda hisiamoyo zisizofaa.”
Kwa miaka mingi, Arthur alikuwa na maisha yenye shughuli na utendaji. Halafu, kwa sababu ya ugonjwa mbaya, alilazimika kuacha kazi ya kimwili na kufanya utendaji wake wote nyumbani. Kwa miezi mingi Arthur alihisi hafai kitu na akashuka moyo. Yeye alishughulikiaje hisi hizo? “Niliacha kufikiria yale nisingeweza kufanya tena. Badala yake, nilikazia fikira yale niliyoweza kufanya kusaidia watu wengine wafanye maendeleo na kuwatia moyo waliposhuka moyo. Kwa vile siwezi kuondoka nyumbani, mimi hutumia simu sana. Kwa vile nilijishughulisha kusaidia wengine na kuwatia moyo, sikuwa na wakati wa kujisikitikia.”
Baada ya mifululizo ya misiba, kutia na kifo cha mume wake, Nita kwa kueleweka alipata huzuni nyingi na mshuko wa moyo. Kwa wakati alijifunza kudhibiti hisia hizo: “Ninapopata hisia ya huzuni, mimi hutafuta utatuzi wenye kujenga. Mimi hujilazimisha kwenda kutembea, kupigia simu rafiki mfadhili, kusikiliza muziki, au kufanya chochote ambacho ninajua kutokana na wakati uliopita kitatuliza mshuko wa moyo. Mimi hujaribu kujitendea kwa huruma kama vile ambavyo ningemtendea rafiki mwema.”
Mary amekuwa na matatizo ya kiafya kwa muda wa miaka 32. Akitumia kigari–kisukumwa, yeye huondoka nyumbani tu ili kwenda kumwona daktari. Mary huwezaje kushinda kutamauka kupita kiasi? Yeye aeleza: “Mume wangu amekuwa akinitegemeza sana. Pia, mimi mara nyingi husoma mambo yanayojenga. Mimi hupigia rafiki zangu simu kwa kawaida, na mara nyingi huchukua hatua ya kwanza kuwaalika nyumbani kwangu. Mimi hufurahia ziara zao na situmii pindi hizo kulalamika au kujisikitikia. Mimi situmii wakati nikifikiria mambo yasiyofaa maishani mwangu kwa sababu nina mambo mengi chanya ya kufanya.”
Kwa asili, Margaret hufikiria mambo kihalisi. “Wakati hisi zisizofaa zinapotokea,” yeye asema, “mimi hutafuta ushirika wa mtu anayefikiri kwa njia chanya—sio mwenye kuwazia tu—bali mtu ambaye ananifahamu vema na atakayenikumbusha mafanikio yangu na kunitia moyo.”
Rose Marie amepata upasuaji mkubwa mara tano kwa muda wa miaka kadhaa, naye na mumewe wamepata vifo saba katika familia zao katika kipindi cha hivi karibuni cha muda wa mwaka mmoja unusu. Kwa kweli, ugumu wa mambo hayo ulisababisha hisiamoyo zisizofaa. Hata hivyo, wao hawafikirii mambo hayo. Wakiwa Mashahidi wa Yehova, wao hutegemezwa na tumaini chanya lenye kufariji ambalo Biblia hutoa la ulimwengu mpya mwadilifu ulio karibu ambapo Mungu “atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena, wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena.” Hata wafu watafufuliwa, kwa maana kama vile Yesu alivyosema, “saa yaja, ambayo watu wote waliomo makaburini [maziara ya ukumbusho, NW] wataisikia [sauti ya Mwana wa Mungu]. Nao watatoka.”—Ufunuo 21:4; Yohana 5:28, 29.
[Picha katika ukurasa wa 9]
Janis hudhibiti hisiamoyo zake kwa kuwafanyia watu wengine vitu, kufikiria kumbukumbu ya mambo yenye kupendeza, na kutazamia matukio ya wakati ujao