Kutoka kwa Wasomaji Wetu
Hisiamoyo Zisizofaa Asanteni kwa mfululizo wa makala nzuri ajabu zenye kichwa “Wewe Unaweza Kushinda Hisiamoyo Zisizofaa.” (Oktoba 8, 1992) Nimekuwa na tatizo hilo kwa muda mrefu. Lakini sasa kwa vile Yehova amenipatia zawadi za makala hizo, hatimaye nimepata nguvu ya kukinza hisia hizo. Kuona akilini wakati ujao ambao ametuwekea mbele yetu na baraka ambazo tutafurahia wakati huo ni msaada mkubwa.
C. I., Italia
Nilishuka moyo baada ya kujihusisha kimahaba na mtu mmoja aliyethibitika kuwa mwongo kabisa. Kwa miezi mingi nilijitesa kwa mawazo yasiyofaa kama vile, ‘Ni lazima niwe mjinga kwa kukubali uwongo wake.’ Au, ‘Mimi siwezi kutambua vizuri utu wa mtu.’ Hilo liliongoza kwenye mkataa wa kushuku watu: ‘Sitamtumaini mtu tena kamwe.’ Mfikio wenye kutumika wa makala hiyo wa kuwa na fikira zifaazo unanisaidia nikuze tena kujiheshimu na kujikumbusha kwamba kisa hicho kilikuwa ono jingine tu la kujifunza.
R. M., United States
Ninasifu jinsi mlivyoshughulikia tatizo la hisiamoyo zisizofaa. Hata hivyo, si hisiamoyo zote zisizofaa zinazoletwa na fikira za mtu kujua. Fikira hali mtu akiwa hajui—kama vile kumbukumbu zenye kuzuiliwa za kudhulumiwa wakati wa utoto—zaweza kuchochea hisia mbaya pia. Huenda wengine wakajaribu kutumia habari hiyo ila tu kupata kwamba kufanya hivyo hakuwafanyi wahisi vizuri zaidi. Tatizo lao laweza kuwa la ndani zaidi. Hivyo, watu wanaohisi uhitaji wa kufanya kazi kwa undani zaidi katika afya yao ya kiakili na kihisiamoyo—iwe hiyo inahusu msaada wa wastadi au la—hawapaswi kuonwa kuwa wanapita mipaka.
M. W., United States
Asante kwa maelezo hayo. Wasomaji wanapaswa wakumbuke kwamba makala hiyo haikuelekezwa kwa watu wanaougua kwa matatizo makubwa kama mshuko mkuu wa moyo au madhara ya kudhulumiwa utotoni. Watu kama hao wanaweza kunufaika kwa kiasi fulani kwa kutumia madokezo yaliyoonyeshwa; hata hivyo, kama ilivyosemwa mwanzoni, makala hizo zilikazia “hisiamoyo zisizofaa za kawaida ambazo kila mtu hupata.” Kuhusu kushuka moyo vibaya, makala hiyo ilikiri kwamba magonjwa kama hayo “huenda yakahitaji tiba ya wastadi.”—MHARIRI.
Machozi Hivi karibuni nilihudhuria maziko ya Mkristo mwaminifu aliyekuwa ametumikia akiwa mzee katika kundi letu kwa miaka mingi. Walipoondoa jeneza nje ya jumba kwa kigari cha kusukuma, nililia kwa uchungu. Hata hivyo, wengi waliohudhuria walidhibiti hisia zao. Siku moja tu baadaye, nilipokea toleo la Amkeni! la Septemba 22, 1992 Kiingereza chenye makala “Mbona Machozi Hayo Yote?” Ilinisaidia nielewe kwamba machozi si ishara ya udhaifu bali ni wonyesho wa hisiamoyo nyingi. Asanteni sana kwa makala hiyo yenye kuelimisha.
S. Z., Ujerumani
Mikono Makala “Mikono Yetu ya Kustaajabisha” (Agosti 8, 1992 Kiingereza) ilikuwa ya kupendeza kwelikweli. Nilikuwa ninajua tayari kwamba mikono yetu imefanywa kwa njia ya ajabu. Lakini makala hiyo ilinisaidia nihisi ukuu wa Muumba wetu.
K. Y., Japan
Sala Asanteni kwa makala “Vijana Wanauliza . . . Je! Mungu Hujibu Sala Zangu?” (Septemba 22, 1992) Niliona makala hiyo ikiwa yenye kusaidia sana. Ilinifundisha kwamba sala zangu hazipaswi kuwa na maombi ya kipuuzi ya vitu vya kimwili. Pia nilijifunza kwamba ninahitaji kudumu katika sala kwa sababu Yehova sikuzote hajibu mara hiyo. Na huenda asitupatie jibu tunalopendelea.
B. G., United States