Waepaji Ni Akina Nani Hasa?
“KUEPA uhakika.” Hivyo ndivyo mtu wa ukoo alivyosema juu ya kijana mmoja mhudumu alipohamia Pasifiki ya Kusini ili kufanya utendaji wa umisionari. Na watu wengi wangetoa maoni ayo hayo. Kwa mfano, mahoji yaliyofanywa katika redio katika New Zealand, yalisikiwa hivi majuzi yakidokeza kwamba wakati hali za kiuchumi zinapozorota, idadi kubwa za watu wanaanza kuamini Mungu, hiyo ikiwa namna ya uepaji.a
Lakini je, wale wanaotumia maisha zao kwenye shughuli ya faida za kiroho ni waepaji kweli kweli? Sivyo kulingana na Yesu Kristo. Yeye hakuwa na maoni kwamba kuamini Mungu ni jambo la kudanganya macho tu, uvumbuzi wa mtu, au fikira ya kuwaziwa tu. Kwenye Yohana 7:28 yeye alisema: “Sikuja kwa nafsi yangu; ila yeye aliyenipeleka ni wa kweli.”
Lakini Yesu hakuamini Mungu na kujikalia kitako tu. Alisukumwa na moyo kumtolea Mungu maisha yake, akisema, “Tazama, nimekuja . . . niyafanye mapenzi yako, Mungu.” (Waebrania 10:7) Wakristo wa kweli leo wanajisikia wakilazimika kufanya vivyo hivyo. Kwa mfano, angalia shauri ambalo Paulo aliandikia Timotheo, mzee mashuhuri katika kundi la karne ya kwanza. Paulo alijua kwamba wengine kundini walikuwa na mali nyingi za kimwili. Lakini kwa sababu imani yao ilitegemea mambo ya kweli, wao wangesukumwa na moyo kuzitumia mali hizo. Paulo alisema: “Waambie wale walio matajiri katika ulimwengu huu uliopo wasiwe wakidharau wengine, wala wasiweke uzito wa uhakika wao juu ya uwezo wa muda tu wa utajiri bali juu ya Mungu aliye hai, atupaye sisi kila kitu kwa ukarimu ili tukifurahie. Waambie watende mema, wawe matajiri katika vitendo vya fadhili, wawe tayari kuwapa wengine na kusikitikia wale walio katika taabu nyingi. Usalama wao unapasa uwekwe akiba katika maisha yatakayokuja, ili kwamba wapate kuwa na uhakika wa kushika hisa fulani katika uzima ulio wa kweli na wenye kudumu.”—1 Timotheo 6:17-19, Phillips.
Basi Ukristo si kutoroka tukio halisi. Unatia ndani kuelekeana kiume na madaraka. Mungu tunayeabudu si wa kuwaziwa tu; bali ni wa kweli. Maisha ya utumishi tunayoishi ni yenye maana na yanatimiza makusudi fulani. Tumaini letu katika thawabu ya wakati ujao, badala ya kuwa ni dhana isiyo na msingi, ahadi za Mungu asiyeweza kusema uwongo ni msingi walo hakika.—Waebrania 6:18.
Ingawa hivyo, namna gani wale wanaoukana uhitaji wa kutumikia Mungu na ambao wanajenga maisha zao kutegemea vitu vya kimwili au kazi fulani ya maisha ya kujifaidi wenyewe? Je! ingeweza kuwa kwamba kwa kweli hao ndio waepaji?
Sulemani yule mtu mwenye hekima alitumia maneno kama vile “ubatili” na “kujilisha upepo” kueleza maisha ambamo vitu vya kimwili na anasa za kimwili zilitangulizwa kwanza. Yeye alieleza matokeo, akisema: “Wala sikuyanyima macho yangu cho chote yalichokitamani; wala sikuuzuia moyo wangu katika furaha yo yote; maana moyo wangu ulifurahi kwa sababu ya kazi yangu yote, na hii ilikuwa sehemu yangu katika kazi yangu yote. Kisha nikaziangalia kazi zote zilizofanywa kwa mikono yangu, na taabu yote niliyotaabika katika kuzitenda; na tazama, yote ni ubatili na kujilisha upepo, wala faida hakuna chini ya jua.”—Mhubiri 2:10, 11.
Ndiyo, hata maisha ya kufuatia vitu vya kimwili yalileta furaha ya aina fulani. Lakini kulikuwa na ukosefu wa kutimiza mambo yenye kuridhisha na wa kupata furaha inayodumu. Maisha kama hayo ni “ubatili” mtupu. Kwa kweli, neno la Kiebrania la kusema “ubatili” lina maana halisi ya “pumzi” na basi linamaanisha kitu kisicho na uthabiti na udumifu. Hivyo The New English Bible inatumia neno “utupu”.
Kwa sababu hii, je, mtu anayeishi aina ya maisha ambayo Sulemani aliyabandika jina “ubatili” amo katika hali ya kuweza kushtaki Mkristo kwamba anaepa na kuingia ndani ya uradhi wa kuwaziwa tu? Ni vigumu. Kwa kweli, mtume Paulo anaendelea kuonyesha kwamba “tamasha ya ulimwengu huu inabadilika.” (1 Wakorintho 7:31, NW) Hapa yeye anafananisha ulimwengu huu usiomwogopa Mungu na jukwaa la mawonyesho yenye tamasha zinazobadilika-badilika daima. Leo kitu kinachoonekana kuwa kizuri sana, chenye kupendeza, hata cha kutazamisha, huenda kisiwepo kesho. Nafasi ya “waigizaji” waliopo leo inakuja kuchukuliwa baadaye na wengine. Hata hivyo, kwa kulinganishwa na jitihada zote walizofanya, maisha zao hazitokezi ubora wenye kudumu. Wanakuwa hawana tumaini la kweli kwa wakati ujao.
Ni kama vile Philip Chesterfield Mwingereza wa karne ya 18 aliyekuwa mtumishi wa sebule la mfalme na mhutubu pia, alisema hivyo kwa kufaa: “Mimi nimefurahia anasa vya kutosha kwa njia ya kipumbavu, tena nimeziachilia mbali zote. Nimefurahia anasa zote za ulimwengu, nami nazikadiria kama zinavyostahili kuwa, na kwa kweli ni za hali ya chini sana . . . Ninapofikiria mambo ambayo nimeona, . . . na mambo ambayo nimefanya, ni vigumu kwangu kujisadikisha kwamba pirika-pirika zote zisizo na maana za kufuatia anasa ulimwenguni zilikuwa na ubora wo wote.”
Lakini, Wakristo ni kama Abrahamu ambaye “alikuwa akiutazamia mji wenye misingi, ambao mwenye kuubuni na kuujenga ni Mungu.” (Waebrania 11:10) Kwa sababu imani yao ni hakika, wao hawana uhitaji wa kuepa bali kujaza maisha zao utendaji wenye kuridhisha. Namna gani maisha yako? Je! ni ya ‘kuepa’ tu, au yamejengwa imara juu ya mambo yaliyo hakika?
[Maelezo ya Chini]
a “Uepaji” unafafanuliwa kuwa ni “kuendelea kugeuza akili kando kwenye mambo ya Kuwaziwa tu, kama njia ya kuepuka ugumu wa maisha,” au “kuepuka ugumu wa maisha kwa kushughulisha sana akili katika . . . hali, utendaji, na mambo mengine ya kuwaziwa tu.”