Je! Wewe Unaheshimu Zawadi ya Mungu ya Kuzaa?
“NILIPOKUWA nimelala juu ya meza ngumu, nyembamba ya chumba cha kufungulia watoto,” anakumbuka Joanne, “yale maumivu makali sana yalifikia kilele. Daktari alikuwa akinawa mikono lakini si kwa haraka ya kutosha. ‘Daktari,’ mwuguzi wa kike akapiga ukelele, ‘mtoto anatoka.’ Akikimbia pale mezani, daktari akahimiza hivi: ‘Fanya tena.’ Yale maumivu yalikuwa ni kama hayavumiliki! Halafu ikawaje?
“‘Pole sana,’ akasema yule daktari, ‘umepata kisichana kizuri.’ Maumivu niliyokuwa nayo muda mfupi tu uliopita yalipotea yakasahaulika wakati ule mwili mdogo wenye joto ulio mwororo ulipowekwa karibu na titi langu. Mkono wa mume wangu ukiwa umeshika wangu, tukautazama muujiza huo mdogo ulio mzuri ambao ulitokezwa na upendano wetu.”
Zawadi ya Mungu ya kuzaa ni jambo la kustaajabia. Baada ya miongo ya miaka ya kufanya mambo ya tiba, Dakt. Joseph Krimsky aliandika hivi: “Kuchukua mimba na kuzaa ni miujiza isiyoweza kueleweka na ufahamu wetu . . . Lile oni lenyewe la moyoni linalohusu upendo na hali yenye kurusha fahamu inayofanya kuwa na muungano wa chembe za kiume na kike ni fumbo . . . ambalo sayansi haiwezi kueleza.”—The Doctor’s Soliloquy.
Elezo la Biblia
‘Oni la moyoni la upendo na lenye kurusha fahamu’ linalofurahiwa na wenzi wa ndoa ni zawadi kutoka kwa Mungu. Ikiambia wanaume waliooa, Biblia inasema: “Furahi sana pamoja na mke wa ujana wako . . . Kwa upendo wake upate kuwa katika hali ya kurusha fahamu daima.” (Mithali 5:18, 19, NW ) Kwa wazi, Mungu aliikusudia ngono kati ya mwanamume na mke wake isaidie kuleta kifungo chenye uchangamshi cha kudumu. Watoto wenye kutokana na muungano huo wangekuwa na mwanzo mzuri maishani. Hivyo kusudi la Mungu kwa wanadamu kuijaza dunia lingetimizwa kwa njia nzuri sana.—Mwanzo 1:27, 28.
Lakini wengi hawakufurahia mwanzo mzuri maishani. Wengine wamekuwa katika mazingira mabaya ya kiadili na wengine wamekuwa katika jamaa zilizogawanyika. Kasoro ilitokea wapi? Biblia inaeleza jinsi watu wawili wa kwanza walivyomwasi Mungu na kuvunja amri yake. Watoto wao walichukua mimba muda fulani baada ya wao kutenda dhambi. (Mwanzo 3:1–4:1) Hivyo wazao wao walirithi hali ya kutokukamilika na elekeo la kutenda dhambi. (Warumi 5:12) Kwa sababu ya hilo, zawadi ya Mungu ya kuzaa imetumiwa vibaya.
Je! Viongozi wa Kidini Wameendeleza Maoni ya Biblia?
Leo, matumizi mabaya ya ngono yamefikia kiwango kilichoruka mipaka mno. Kwa sababu gani iko hivyo? Katika muda wote wa karne iliyopita, mamilioni ya watu wametegemea makanisa ya Jumuiya ya Wakristo kwa uongozi wa kiadili. Je! viongozi wa dini wametumia maongozi yao kuendeleza heshima kwa nguvu za kuzaa?
“Makanisa ya Kiprotestanti ambayo yamekuwako kwa muda mrefu—ya Kilutheri, ya Kirifomu, Kianglikana, Kikongrigeshenali, Kimethodisti, na ya mitaa mingi ya Kibaptisti —yalijirekebisha kwa urahisi . . . kufuata lile wazo la mageuzi,” kinaeleza kichapo The Enclyopcedia Britannica. Lakini fikiria hivi: Je! mageuzi ni jambo ambalo wale wanaodai kuwa wanaiwakilisha Biblia wanapaswa ‘kujirekebisha’ ili walifuate? Hapana, kwa sababu mageuzi ni nadharia isiyojali hata kidogo mambo ya adili. Yanakataa uumba wa Mungu na uhitaji wa wanadamu kuokolewa katika dhambi na kifo.—Mwanzo 2:7, 18, 19; 1 Wakorintho 15: 21, 22.
Kanisa Katoliki pia limekubali kujiacha liongozwe na nadharia ya mageuzi. Mwaka 1950, Papa Pius wa 12 alitoa kitia-moyo kuwe na uchunguzi wa mageuzi katika barua yake iliyoitwa Humani generis. Wakati wa mwaka 1982, wanasayansi 11 walialikwa Mji wa Vatican kwenye mazungumzo yaliyohusu mageuzi yakiongozwa na msimamizi wa Chuo Maalum cha Sayansi ya Upapa. Baadaye, baraza kuu zaidi la kisayansi la Kanisa Katoliki lilichapisha kitabu chenye dai la kwamba “ukoo unaoongoza kwa wanadamu, sokwe na sokwe-mtu unaonekana ni kama uligawanyikana kutokana na babu yao wote mmoja . . . kuanzia miaka milioni 5 mpaka 7 iliyopita.”
Nadharia ya mageuzi inaikataa Biblia, inayosema ya kwamba wanadamu na wanyama waliumbwa mbali mbali ‘kwa jinsi zao.’ (Mwanzo 1:20-27) Tena ni vizuri kuangalia kwamba Biblia ilitabiri hivi: “Kwa sababu ya kuongezeka maasi, upendo wa wengi utapoa.” (Mathayo 24:3, 11, 12, 33) Je! mageuzi yameshiriki kuleta ‘ongezeko la maasi’?
Je! Mageuzi Yameendeleza Maasi Yanayohusu Adili?
Kwa kujipatanisha na nadharia ya mageuzi, viongozi wa kidini wengi wamebomoa imani ya watu katika Biblia. ‘Ikiwa masimulizi ya Mwanzo juu ya uumbaji si kweli, basi namna gani sehemu ile nyingine yote ya Biblia? ’ watu wanauliza. Kwa hiyo hata viongozi wa kidini wanadokeza mashaka juu ya mambo ambayo Biblia inasema kuhusu ngono kabla ya ndoa na kulalana kwa watu wa jinsia moja, na pia maoni ya Biblia juu ya uhai wa vitoto ambavyo havijazaliwa.—Kutoka 20:13,14; 21:22,23; Mambo ya Walawi 18:22; 1 Wakorintho 6:9, 10.
Kuna njia nyingine ambayo nadharia ya mageuzi imeshiriki kuleta maasi. Hivi majuzi, wakati wa kipindi cha televisheni kinachoonyesha vituko vyenye kuongozwa na tamaa kali, mamilioni ya watu katika nchi fulani “ya Kikristo” walitazama hadithi ya baba mmoja aliyemshika binti yake wakafanya ngono. Kulingana na jarida Science 85, ilisemekana kwamba “hakuna mwanamume au mwanamke anayeweza kuhesabiwa kuwa mwenye lawama kabisa kwa sababu ya mwenendo wake ikiwa nyege zake zimekuwa kali.” Mamilioni ya watu, gazeti hilo linasema, wana nia ya kukubali maoni hayo. Kwa sababu gani? Kwa sababu wao wanaamini kwamba “wanadamu wana uhusiano wa karibu sana na wanyama.” Jarida hilo la kisayansi linakiri kwamba, watu, “wamekuwa wenye kukubali mno maoni ya Darwin hivi kwamba ‘Bado umbo la kimwili la mwanadamu lina dalili zizizofutika za kwamba ana asili ya mnyama.’ “
Mawazo ya mageuzi yamekuwa na matokeo mabaya juu ya maoni ya watu kuhusu Biblia. Je! jambo hilo limeleta baraka? Hapana. Kukataa viwango bora vya Biblia juu ya maadili kumeleta ongezeko kubwa la ajabu la utoaji mimba na magonjwa yenye kuambukiza kupitia ngono. Pia, watoto wengi zaidi na zaidi wanazaliwa nje ya ndoa, wasijue kamwe ile baraka inayotokana na maisha ya kijamaa yenye uchangamfu.
Biblia Inaweza Kukusaidiaje Wewe?
Biblia inamfunua Muumba wa wanadamu Yehova, kuwa Mungu wa rehema. (Zaburi 103:10-13) Yeye anataka kusaidia wanadamu watenda dhambi wafikie viwango vyake vya adili. (Isaya 1:18; 55:6-9) Kwa mfano, ufikirie mji wa kale wa Kolosai, ambako ngono kabla ya ndoa na uzinzi ni mambo yaliyofanywa sana “Katika hayo ninyi nanyi mlitembea zamani, mlipoishi katika hayo,” inasema barua ya Kibiblia walioandikiwa Wakristo katika Kolosai. (Wakolosai 3:5-7) Hata hivyo, kwa kutiwa moyo na Neno la Mungu na kwa uwezo wa roho takatifu yake, Wakolosai wengi walifanya mabadiliko mazuri katika mtindo wao wa maisha Wakawa Wakristo wa kweli.
Fikiria, pia, wakaaji wa Korintho wa kale. Mji wao ulikosa adili kwa kujawa na watu wenye kulalana na wengine wa jinsia yao na makahaba. “Na baadhi yenu mlikuwa watu wa namna hii,” inatangaza barua ya Kibiblia walioandikiwa. “Lakini mlioshwa, lakini mlitakaswa, lakini mlihesabiwa haki katika jina la Bwana Yesu Kristo, na katika [roho ya] Mungu wetu.”—1 Wakorintho 6:9-11; Ona pia Luka 11:13.
Je! jambo lile lile linatukia leo? Ndiyo, kwa maana baada ya kusoma matoleo ya wakati uliopita ya gazeti hili, maelfu ya watu wamesaidiwa wakapatanisha maisha zao na Biblia. Fikiria mfano wa kijana-tineja katika Afrika aliyetendwa ubaya wa ngono akiwa mtoto. Baada ya muda, msichana huyo alijihusisha katika namna zote za mwenendo wa ukosefu wa adili, kutia na kulalana na wasichana wenzake. Yeye alisema, “Huenda ulimwengu ukampa mtu raha kwa muda mfupi lakini inakuwa ni kama kutumia dawa ya kulevya inayomfanya ajisikie hafai kitu.” Kwa kukata tamaa, msichana huyo alijaribu kujiua, lakini katika muda huo wenye magumu sana jambo fulani likatukia lililobadili maisha yake. Alianza kuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova na akakubali shauri alilopewa kwamba asome Biblia kila siku. Jambo hilo lilimtia nguvu ashinde mazoea ya ukosefu wa adili. “Sasa ninajisikia nikiwa afadhali zaidi,” anasema. “Inastaajabisha kuona jinsi Yehova anavyoweza kusaidia mtu.”
Vijana wanaokua wakiwa katika jamaa ya Kikristo yenye uchangamfu wamo katika hali bora kuliko wengine. Wazazi Wakristo wanapaswa kufanya yote wawezayo waeleze watoto wao ajabu za nguvu za kuzaa. (Waefeso 6:4) Watoto hao watasaidiwa hivyo waheshimu viungo vyao vya uzazi na wasivitumie kama vitu vya kuchezea. Mara nyingi kupiga punyeto ndiyo hatua ya kwanza kuelekea namna zilizo mbaya zaidi za ukosefu wa adili.a
Leo, kuna uhitaji wa haraka wa kushinda mazoea ya ukosefu wa adili. “Kwa ajili ya mambo hayo,” Biblia inaonya, “ghadhabu ya Mungu” inakuja. (Wakolosai 3:5, 6) Ndiyo, rehema ya Yehova ina mipaka. Yeye ni Mungu wa haki. (Kumbukumbu la Torati 32:4) Baada ya kutabiri ‘ongezeko la maasi’ lililopo siku hizi, Yesu alisema: “Wakati huo kutakuwapo dhiki kubwa, ambayo haijatokea namna yake tangu mwanzo wa ulimwengu hata sasa, wala haitakuwapo kamwe.” (Mathayo 24:11, 12, 21) Kitendo hicho kitakachofanywa na Mungu kitakomesha ukosefu wa kutii sheria kisha kilete mfumo mpya wenye uadilifu.—Zaburi 37:9-11, 29.
[Maelezo ya Chini]
a Ona makala “Baba Aongea na Watoto Wake wa Kiume” katika gazeti Amkeni! la Machi 1977, na “Mama Aongea na Binti Zake” katika Amkeni! la Aprili 1977, na pia kitabu Kupata Faida Zote za Ujana Wako, sura ya 5, inayosema “Punyeto na Ngono za Wanaume kwa Wanaume na Wanawake kwa Wanawake.”
[Picha katika ukurasa wa 5]
Watoto wanahitaji mazingira ya jamaa yenye uchangamfu ili waweze kuanza maisha vizuri
[Picha katika ukurasa wa 7]
Wazazi wanaoogopa Mungu wanapaswa wasaidia watoto kuwa na maoni yanayofaa juu ya nguvu za kuzaa