Yehova Alibariki Maamuzi Yangu
Kama ilivyosimuliwa na Samuel B. Friend
KULE nyuma katika Julai 1952 nilikuwa nikiimba kila usiku wa Jumamosi katika wonyesho wenye kupendwa na watu wengi la mashambani katika sehemu ya Little Rock, Arkansas. Wonyesho huo wa muda wa saa tatu ulipendwa sana si na watazamaji wenye kuhudhuria tu bali na maelfu waliosikiliza kupitia kituo cha redio chenye wati 50,000 cha KLRA. Jambo hilo lilitukia kule nyuma kabla televisheni hazijaletwa kwenye sehemu hiyo ya kusini ya United States.
Usiku mmoja, nilipokuwa nikimalizia wonyesho, mpelelezi shirika MGM (Metro-Goldwyn-Mayer) stadi wa kurekodi alinijia. “Ningependa wewe uwe ukituimbia,” akasema. Na papo hapo yeye akanitolea mkataba wa kurekodi wenye mshahara mnono. Alisema kwamba kwa majuma kadha alikuwa akitazama wonyesho ule, na akaona kwamba mimi ningeweza kufanya vizuri wakati ujao katika shughuli ya kurekodi.
Nilipomwambia sikupendezwa, aligutuka. Nikamweleza kwamba mimi nilikuwa nikifanya wonyesho ule nisaidie kuruzuku mke wangu na mimi mwenyewe katika huduma ya wakati wote na kwamba sikutaka kuhusika zaidi katika shughuli ya muziki.
Baadaye mwaka huo, televisheni zililetwa Arkansas—kule katika Little Rock. Mkurugenzi wa programu aliniomba niwe msimamizi wa sherehe kwa ajili ya programu ile ya kwanza, huo ukiwa ni wonyesho wa kimuziki wenye mambo mbalimbali. Nilipendezwa na nikalikubali toleo hilo kwa furaha, nikieleza kwamba ningethamini kuwa na kazi ya nusu-siku katika kituo kile. Yeye akasema angenijulisha baada ya ile programu ya kwanza.
Programu hiyo ya kwanza ilifanikiwa kweli kweli. Mimi nilikaribisha jukwaani waimbaji wastadi na nikaimba mwenyewe nyimbo kadha. Baadaye nikauliza kama ningeweza kupewa ile kazi ya nusu-siku. “Hapana, mimi sikutaki uwe wa nusu-siku,” akasema. “Nakutaka wakati wote.” Kwa kuwa hakutaka kuliacha lile jambo la kufanya kazi wakati wote. nililazimika kufanya uamuzi. Kuwa ndani katika ghorofa ya chini ya kituo cha kwanza cha televisheni katika Arkansas kulikuwa taraja lenye kushawishi. Lakini, kwa kweli halingeweza kulingana na kutumikia Baba yetu wa kimbingu Yehova Mungu, katika huduma ya painia wa wakati wote! Kwa hiyo nikalikataa toleo hilo.
Niliposema na Jean mke wangu baada ya ule wonyesho, yeye alikubaliana nami kabisa. Usiku huo tuliporudi nyumbani, unajua ni kitu gani kilichokuwa katika sanduku la barua? Ulikuwa ni mwaliko wa kutumikia nikiwa mwangalizi wa mzunguko, nikitembelea makundi ya watu wa Yehova kuwatia nguvu kiroho. Nilijisikia kwamba Yehova alikuwa amebariki kweli kweli uamuzi wangu.
Wakati Mwingine wa Uamuzi
Huo haukuwa ndio uamuzi wa kwanza wa aina hiyo. Nilipomaliza masomo ya shule ya sekondari katika Mlima Ida, Arkansas, Fred ndugu yangu na mimi tulijiunga na kikundi cha kimuziki cha magharibi chenye kuitwa Texas Rangers. Kwa karibu miaka mitatu wakati wa ile ya kukaribia 1940, mimi nilisafiri na kikundi hicho katika mikoa mingi ya kusini. Kikundi chetu cha waimbaji kilipokea matoleo ya kupewa pesa nyingi na wadhamini wa sehemu za mbali kama Chicago. Sisi ndio tulioshinda zawadi ya kwanza kwenye mashindano ya mikoa katika Mississippi na Arkansas, na katika shindano moja la mkoa wa Arkansas mimi nilishinda zawadi ya kwanza nikiwa mwimbaji bora zaidi wa kiume. Kwa hiyo nilikuwa na shughuli ya maisha yenye matazamio mazuri.
Lakini nilikuwa nimegawanyika mawazo. Nilipokuwa kijana katika miaka ya kuanza 1920, jamaa yetu ilikuwa imetembelewa na wawakilishi wa Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi. Kwa kweli, walipokuwa wakitembelea eneo letu maili kadha magharibi ya Hot Springs, Arkansas, wahudumu wenye kusafiri (walioitwa wasafiri) walikuwa wakikaa nyumbani kwetu. Jamaa yetu ilifurahia kuwasikiliza na kwa ujumla ikakubali mambo waliyofundisha.
Kwa hiyo katika ukuzi wangu nilikuwa na maarifa ya msingi ya ukweli wa Biblia. Na hata nilisema na rafiki zangu juu ya mambo ambayo wahudumu hao wenye kusafiri walisema na yale tuliyosoma nyumbani katika Mnara wa Mlinzi. Floyd Garrett alikuwa mmoja wa marafiki hao wa siku za uvulana. Tulienda shule pamoja katika miaka ya katikati kuanzia 1930. Floyd aliyaitikia mambo niliyomsimulia, na, baada ya muda akafanya wakfu kwa Mungu na kuanza huduma ya wakati wote mwaka 1940. Leo hii yeye anatumikia akiwa mwangalizi anayesafiri.
Basi, wakati ambao mimi nilikuwa nikisafiri na kile kikundi cha waimbaji, baba alikuwa akiniandikia juu ya hotuba ambazo ndugu wenye kusafiri walikuwa wakitoa katika nyumba yetu ya mashambani. Halafu mwishoni-mwishoni mwa mwaka 1938, tulipokuwa katika Jackson, Mississippi, nilialikwa nisikilize hotuba iliyorekodiwa yenye kusema “Jazeni Dunia” aliyokuwa ameitoa msimamizi wa Sosaiti J. F. Rutherford kwenye mkusanyiko mmoja katika London, Uingereza. Jambo hilo liliamsha tena hali yangu ya kupendezwa iliyokuwa imekaa miaka mingi bila kuguswa. Nilijua kwamba ilinipasa kufanya uamuzi fulani. Mwaka uliofuata nikakiacha kile kikundi cha waimbaji na kurudi nyumbani Arkansas.
Maendeleo ya Kiroho
Muziki, na pia kuvua samaki na kuwinda, sasa yakawa ni mambo yenye kuchukua mahali pa pili katika maisha yangu. Mambo ya kiroho yakawa yenye maana zaidi nilipoanza kutafuta kwanza Ufalme. (Mathayo 6:33) Yehova akawa halisi kwangu, nami nilikuwa na tamaa yenye kuwaka ya kumtumikia. Nilifanya wakfu kwa Yehova na kubatizwa Novemba 27, 1939, katika kijito chenye baridi cha Arkansas. Mama alibatizwa muda mfupi baada ya hapo.
Nilinunua gari lenye umri wa miaka 11 kwa dola 50 na katika Novemba 1940, nikaingia utumishi wa painia wa wakati wote katika sehemu za mashambani za Arkansas, nikiwa na umri wa miaka 23. Hiyo ilikuwa siku yenye furaha kama nini! Ikawa wazi ni mwendo gani ningefuata maishani, nami nikajisikia Yehova akiniunga mkono na hilo ndilo lililokuwa jambo la maana zaidi ya mengineyo.
Siku hizo, halikuwa jambo rahisi kutafuta watu wenye mfano wa kondoo katika sehemu za mashambani kando kando ya Hot Springs. Hiyo ilihitaji niendeshe gari miendo mirefu katika barabara za mavumbi, vijito vidogo-vidogo, na kutembea nikiteremka katika njia za magari ya kukokotwa na farasi ili nifikie nyumba zilizokuwa peke yazo. Nilibadilishana na watu vitabu vya Biblia kwa matunda, mboga, kuku, mayai, vyakula vilivyotiwa mikebeni na vitu kama hivyo. Mpaka sasa ningali nikiyathamini sana mambo hayo niliyoona.
Magumu Wakati wa Miaka ya Vita
Wakati United States ilipoingia katika Vita ya Ulimwengu ya Pili mwaka 1941, ulikuwako upinzani wenye kuenea sana kwa Mashahidi wa Yehova kwa sababu ya kutokuwamo kwao. (Isaya 2:4) Vikundi vya watu wenye ghasia vilikusanywa katika sehemu zote za nchi ili kuwapinga, na maelfu ya Mashahidi vijana wakafungwa gerezani. Ingawa nilipokea kitambulisho cha kuonyesha mimi ni mhudumu, nilikabili upinzani mkali kutia na vitisho vya kuuawa.
Akinielekezea bunduki yake ya kuwindia, mwanamume aliniagiza hivi:
“Ondoka katika uwanja wangu kabla sijakupiga risasi.” Yeye alikuwa amenitambua kuwa ni Shahidi nilipokuwa nikikaribia nyumba yake. Ni wazi kwamba niliondoka bila kusita-sita. Halafu pia nilionywa na mwanamume mmoja niliyekuwa nikijifunza naye Biblia kwamba alikuwa amepata habari juu ya mtu fulani wa upande mwingine mashariki ya mji aliyekuwa akipanga kuniua nikifika nyumbani kwake.
Miezi michache baadaye nilipokuwa katika eneo hilo, nilikaribishwa ndani ya nyumba na mke mwenye kazi za nyumbani nami nikaanza kufungulia sahani ya santuri yenye hotuba moja ya Biblia iliyotolewa na Ndugu Rutherford. Sahani ile ilipokuwa ikiendelea kusema, mume wake aliingia akasimama kati yangu na mlango, akatoa kisu chake. Akaniuliza shughuli yangu ni nini, lakini hata bila kunipa nafasi ya kueleza. “Wewe utakubali kusalimu bendera au upigane jeshini? ” Yeye akadai huku akinipungia-pungia kisu chake Mara nikakumbuka onyo nililopewa na rafiki yangu hata sikujua nijibu vipi.
“Wewe ungeonaje,” nikamwuliza mtu huyu mwenye kunipungia kisu “kama mtu angekushtaki wewe kwamba unaunga mkono Chama cha Nazi? ” Kwa kuchukizwa na hali hiyo, nikaendelea kusema: “Mimi simwungi mkono Hitler sawasawa na vile wewe usivyomwunga mkono. Jambo moja tu ninalopendezwa nalo ni kusaidia watu waifahamu Biblia.” Kwa njia fulani jibu hilo lilimtuliza mtu huyo, nami nikaweza kwenda zangu kwa usalama. Nilipokuwa nikiondoka, nilimshukuru Yehova kwa ulinzi wake na kwa kutia maneno yaliyofaa katika kinywa changu.
Katika pindi nyingine, nilikuwa nimefungulia sahani iliyorekodiwa hotuba ya Biblia ili mwanamume mmoja aisikilize wakati nilipoona kwamba kulikuwa na kasoro fulani. Uso wake ulikunjamana na kwa kweli ukabadilika rangi na kuwa mweupe. Lakini aliendelea kusikiliza. Sahani ile ilipomalizika, nilimwuliza kwa ubaridi aliionaje. Yeye alitua kidogo akajibu: “Mara ya kwanza nilifikiri ni Mashahidi wa Yehova, nami ningekuua,” Nikamsifu kwa kusikiliza jambo kabla ya kuhukumu nami nikampa mahubiri yaliyoandikwa na kwenda zangu. Nilitaka ajue mimi ni nani lakini kufikia wakati ambao angejua hivyo nilikuwa nimekwenda zangu.
Kundi jipya lilianzishwa katika Bonnerdale nilikokulia. Baada ya kutumikia nikiwa mtumishi wa kampuni, au kundi, kwa miaka miwili na kukiona kile kikundi kikiongezeka kufikia wahubiri 17, niliombwa na mwangalizi mwenye kusafiri nihamie Hot Springs nikatumikie nikiwa mwangalizi wa kundi. Nilifanya hivyo mwaka 1942. Kushirikiana na ndugu waliokomaa wenye umri mkubwa kuliko mimi kule, kuliyafaidi sana maendeleo yangu ya kiroho.
Siku hizo, Yehova aliniandalia mahitaji yangu kwa njia nyingi sana. Wakati mmoja sikuwa na pesa za kulipa dola 5 ili kuandikisha upya leseni ya gari langu. Nilipelekea Yehova sala kuhusu jambo hilo nami nikaenda katika huduma. Asubuhi hiyo nilipokea msaada wa dola 5 barabara bila kuuomba!
Utumishi wa Betheli
Mwaka 1944 nilipewa mgawo kuwa painia wa pekee katika Joliet, Illinois. Nilipokuwa kule makala ilitokea katika Informant (ambayo sasa ni Huduma ya Ufalme Yetu) juu ya utumishi wa Betheli katika Brooklyn, New York. Nikaamua kujaza ombi nami nikakubaliwa.
Nilipofika Betheli Machi 1945, walikuwako washiriki karibu 230 wa jamaa ya makao makuu ya ulimwengu katika Brooklyn wakilinganishwa na zaidi ya 2,500 walioko leo! Kwa miaka mitano nilifurahia kufanya kazi katika sehemu mbalimbali, kutia na Idara ya Utumishi. Halafu siku moja Ndugu Knorr, msimamizi wa Sosaiti, akaniita kwenye afisi yake.
“Wewe umechaguliwa usimamie kituo cha redio cha Sosaiti cha WBBR,” akasema. Ilikuwa vigumu kwangu kuamini.
“Mimi sijui lo lote juu ya kusimamia kituo cha redio,” nikasema.
“Wewe ulikuwa ukiimba katika kimoja, sivyo? ” akauliza.
“Lakini hiyo ni tofauti na kusimamia kimoja,” mimi nikabisha.
Ndugu Knorr alinitia moyo niukubali mgawo huo, nami nikakubali kuufanya kwa nguvu zangu zote. Lilikuwa jambo gumu kweli kweli lakini pia furaha na pendeleo. Zaidi ya washiriki 90 wa jamaa ya Betheli wangekuwa katika zile programu mbalimbali kila juma. Mpango huo mpya ungekuwa ni wa karibu asilimia 65 muziki uliorekodiwa, kutia na programu ya dakika 15 ya kuimba kwangu kila juma. Muda ule mwingine wote ulitumiwa kwa hotuba za Biblia, mafunzo ya Biblia, kujibu maulizo ya Kibiblia, na njia nyingine za kutangaza habari za Biblia, na pia matangazo ya matukio na habari kuhusu kuwa na usalama kati ya watu.
Kubatiza Baba Yangu
Wakati nilipokuwa likizoni kutoka Betheli katika kiangazi cha mwaka 1950, nilipata furaha isiyo na kifani ya kubatiza baba yangu mwenyewe! Kwa miaka 27 yeye alikuwa amesoma vichapo vya Sosaiti, lakini ilimchukua miaka mingi kukubali kwa ukamili kwamba Yehova anatumia tengenezo ambalo kupitia hilo Yeye anatolea watu kweli Zake. (Mathayo 24:45-47) Wakati mmoja baba kwa kweli alikuwa amekuwa ni mtu asiyeamini kuna Mungu. Sababu ilikuwa nini?
Basi, wakati Jim ndugu yangu wa miaka 13 alipokufa, kiongozi wa dini alihubiri akisema kwamba yeye alienda moja kwa moja ndani ya moto mkali wa mateso kwa sababu mvulana huyo hakuwa wa kanisa lo lote. Jambo hilo lilimshangaza sana baba. Yeye aliwaza hivi: ‘Sababu gani niabudu mungu mkatili sana, mtesi-tesi? ’ Yeye alifikiri kwamba yaliyosemwa na mhubiri huyo yalikuwa katika Biblia. Kwa hiyo akawa haamini kuna Mungu. Lakini imani yake katika Mungu ilirudishwa wakati, katika mazungumzo yake ya kwanza pamoja na Mwanafunzi wa Biblia mmoja (Shahidi wa Yehova), mwanamke huyo alipomsadikisha kutokana na Biblia kwamba heli si mahali pa mateso bali ni kaburi la ujumla la wanadamu.
Ndoa
Mwaka 1952 nilikabili uamuzi mwingine. Jean Mylton, painia mwenye bidii pamoja nami, tuliamua kufunga ndoa. Mtu fulani alimwuliza Jean alikuwa na mipango gani ya wakati ujao, naye akaeleza kwamba kwa kuwa wakati huo hakukuwa na mpango wa wake walioolewa kupelekwa Betheli, sisi tungepainia katika Little Rock, Arkansas. “Mnawezaje kwenda kule na hali hamna cho chote upande wa kimwili? ” mtu yule akauliza. Ni kweli sisi hatukuwa na pesa nyingi, kwa maana mimi nilikuwa nimekuwa katika utumishi wa wakati wote kwa miaka 12 na Jean kwa miaka 7. Mtu huyo alidokeza kwamba sisi wote wawili tufanye kazi ya wakati wote kwa muda wa miezi sita ili ‘tununue gari na kuokoa pesa zipatazo dola 600.’ Jean aliponiuliza habari hizo, mimi nilisema: “Tunajuaje hatuwezi kufaulu —hata hatujajaribu. Kama kutakuwa na uhitaji, tunaweza kuacha baadaye kisha tufanye kazi wakati wote, lakini kwanza na tujaribu.”
Tulistaajabu kupewa zawadi za arusi ambazo zilikuwa gari na dola 600 barabara. Yehova alijua tulizihitaji, naye akatuandalia kwa sababu tulifanya uamuzi wa kubaki katika kazi ya wakati wote. (Malaki 3:10) Tulipainia miezi michache, halafu nikaalikwa kuingia katika kazi ya mzunguko baadaye mwaka wa 1953, na mwaka uliofuata tukaalikwa kwenye Shule ya Gileadi ya Biblia ya Sosaiti yetu. Baada ya kuhitimu Jean aliandamana nami katika kazi ya wilaya kwa miaka miwili.
Kutumikia Katika Nchi za Kigeni na Kurudi Betheli
Mwaka 1957 tulikuwa tukitumikia katika Pasco, Washington, wakati mleta barua alipotuletea barua ya usafirishaji wa pekee kutoka Afisi ya Msimamizi wa Sosaiti. Nilijiuzulu kutoka ule mkutano wa utumishi niliokuwa nimefanya na akina ndugu, halafu Jean na mimi tukaingia jumba jingine na kuifungua barua. Tulialikwa kwenda Meksiko, nami nikaombwa nitumikie nikiwa mwangalizi wa tawi. Niligutuka! Sisi hatukuijua lugha ya Hispania, nami sikujua mengi juu ya kazi ya tawi. Lakini tumaini letu lilikuwa katika Yehova, na hakika tulilihitaji. Shamba lilikuwa kubwa na utengenezaji mwingi wa kazi ulitakwa, lakini ndugu wa kule walikuwa wana nia na Yehova aliibariki kazi.
Baada ya kutumikia kwa miaka fulani katika Meksiko, nilipewa tena pendeleo la kuhudhuria Shule ya Gileadi katika New York. Nilipohitimu, Jean na mimi tulipewa mgawo mpya wa kazi ya mzunguko katika Guatemala. Jean alikuwa na matatizo fulani ya kiafya, kwa hiyo tukarudi United States ambako niliendelea kutumikia katika kazi ya kusafiri. Kwa miaka fulani nikafundisha pia madarasa ya majuma mawili ya Shule ya Huduma ya Ufalme ya wazee. Mwishowe, tukarudi ili tuchukue utumishi wa Betheli katika Brooklyn, na tumekuwa katika nafasi hiyo iliyobarikiwa sana tangu wakati huo.
Kwa hiyo mimi hapa nikiwa na umri wa miaka 69, nikiwa nimekwisha kufurahia mapendeleo mengi yasiyostahilika katika utumishi wa wakati wote kwa muda wa miaka 45 iliyopita. Naweza kusema kwamba Yehova ni mwema na baraka zake ni nyingi. Jean, mke wangu mwaminifu wakati wa miaka 34 iliyopita, amekuwa baraka kubwa kwangu kweli kweli. Mimi najua kwamba Yehova anaweza kubariki wadogo kwa wakubwa. Nami nimezithamini baraka zangu nikiwa mdogo. (Zaburi 115:13) Uamuzi na tamaa yangu ni kuendelea kutumikia Mungu wetu mkuu mwenye upendo Yehova kwa njia yo yote anayoelekeza, kwa heshima na sifa yake.
[Blabu katika ukurasa wa 25]
“Wewe ungeonaje,”nikamwuliza mwenye kunipungia kisu, “kama mtu fulani angekushtaki wewe ya kwamba unaunga mkono chama cha Nazi? ”
[Picha katika ukurasa wa 23]
Sam Friend kulia, mapema katika shughuli yake ya maisha ya kimuziki
[Picha katika ukurasa wa 24]
Kutoa Mnara wa Mlinzi barabarani katika Hoi Springs, Arkansas, mwaka 1942
[Picha katika ukurasa wa 26]
Sam Friend na Mkeye Jean leo