Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w86 9/15 kur. 27-29
  • Yule Mungu wa “Agano la Kale”—Je! Yeye Ni Mungu wa Upendo?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Yule Mungu wa “Agano la Kale”—Je! Yeye Ni Mungu wa Upendo?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Yehova—Sikuzote ni Mungu wa Upendo
  • Upendo wa Mungu Kuelekea Israeli
  • Upendo Unaonyeshwa Kupitia Mwanaye
  • Kusudi Lenye Upendo la Mungu Kwako Wewe
  • Mpende Mungu Anayekupenda
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
  • Mtukuze Yehova—Mungu wa Pekee wa Kweli
    Mwabudu Mungu wa Pekee wa Kweli
  • Upendo wa Kikristo Wenye Msingi wa Upendo wa Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • “Katika Hayo Lililo Kuu ni Upendo”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
w86 9/15 kur. 27-29

Yule Mungu wa “Agano la Kale”​—Je! Yeye Ni Mungu wa Upendo?

“YULE Mungu wa Agano la Kale yaani Yahweh wa dini ya Wayahudi, ni mungu wa kulaani, mungu wa hasira, mungu wa wivu, nami siwezi kujisikia nikiwa na uhusiano wa karibu naye.” Hivyo ndivyo anavyosema Youji Inoue, padre Mkatoliki aliye Mjapani, katika makala yenye kichwa “Wajapani na Ukristo” katika moja la magazeti makuu ya Japani, linaloitwa Asahi Shimbun. Lakini, yeye anaendelea kusema, Mungu huyo mwishowe “alikua akageuka akawa jinsi yeye alivyo akiwa ndiye Mungu wa Agano Jipya, yaani, Mungu ambaye Yesu alifundisha habari zake.”

Kwa uhakika, si padre Inoue peke yake anayeshikilia maoni kama hayo. Lakini Je! wewe unakubaliana naye? Je! wewe pia unajisikia kwamba yule Mungu wa “Agano la Kale” au Maandiko ya Kiebrania, ni Mungu mkatili na mwenye kulipa kisasi anapolinganishwa na Mungu wa “Agano Jipya” au Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo?

Kuhusu wanadamu, utu unaweza kubadilika. Kwa mfano, Biblia inahimiza wale wanaopenda Mungu ‘wavae utu mpya ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu katika uadilifu wa kweli na ushikamanifu.’ (Waefeso 4:24, NW) Kwa kujifunza Biblia na kutumia mambo ambayo wamejifunza, wengi ambao hapo kwanza walikuwa wameweka wivu moyoni, hasira, na mambo kama hayo, wamefanya mabadiliko makubwa, hivi kwamba sasa wanaonyesha wazi katika maisha zao za kila siku lile tunda la roho ya Mungu​—“upendo, furaha, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujiweza.”​—Wagalatia 5:22, 23, NW.

Lakini Je! inaweza kusemwa ivyo hivyo juu ya Muumba, Yehova Mungu? Je! yeye ‘amekua akageuka’ akaacha kuwa “mungu wa hasira” akawa Mungu wa Kikristo mwenye upendo, kama vile wengine wanavyotaka kumwita?

Yehova—Sikuzote ni Mungu wa Upendo

“Mungu ni upendo,” akaandika mtume Yohana. (1 Yohana 4:8) Humo yeye alitaja ukweli wa milele: Muumba, Yehova, amekuwa Mungu wa upendo usiobadilika, ndivyo alivyo hata sasa, naye ataendelea sikuzote kuwa hivyo. Na tangu mwanzo mpaka mwisho, kumbukumbu la Biblia launga mkono maneno hayo.

Wakati Yehova alipoiumba dunia, aliifanya kwa upendo ikawa makao mazuri kabisa kwa ajili ya wanadamu. (Isaya 45:18) Baadaye, alipoumba mwanamume na mwanamke wa kwanza, Adamu na Hawa, yeye aliwafanya “kwa mfano wake,” yaani, aliwapa sifa za kimungu kama upendo, haki, hekima, na uwezo. Aliweka mbele yao pia taraja la kuwa na watoto, kuigeuza dunia mzima iwe paradiso, na kuishi ndani milele. (Mwanzo 1:27, 28) Je! Haya yote hayakuwa ushuhuda wa kwamba Mungu ni upendo?

Wakati watu wawili wa kwanza waliposhindwa na kishawishi kilichowekwa na Shetani kupitia nyoka, walipoteza baraka za milele si zao wenyewe tu bali pia za watoto wao wasiokuwa wamezaliwa. Katika wakati huo wenye umaana mkubwa, Yehova alitamka unabii wa kwanza ulioandikwa katika Biblia, yaani, kwamba ‘uzao fulani wa mwanamke’ ulioahidiwa ungeponda kichwa cha nyoka. (Mwanzo 3:15) Je! ahadi hiyo ya tumaini na ukombozi haikuwa wonyesho mwingine wa kutokeza wa upendo wa Mungu?

Karibu miaka 2,000 baadaye, Yehova alimwahidi hivi Abrahamu mtumishi mwaminifu: “Katika uzao wako mataifa yote ya dunia watajibarikia,” hivyo akifunua kwamba ‘uzao wa mwanamke’ ungekuja kupitia ukoo wa jamaa ya Abrahamu. (Mwanzo 22:18) Ahadi hiyo iliimarisha tumaini la ukombozi ikaonyesha kwamba upendo wa Yehova kwa wanadamu haukuwa umefifia baada ya muda kupita. Kwa kutoa ahadi hiyo, yeye alikusudia wanadamu wapate baraka wakati ujao. Yeye ni Mungu wa upendo!

Upendo wa Mungu Kuelekea Israeli

Zaidi ya hilo, Yehova Mungu aliwakomboa Waisraeli kutoka utumwani Misri mwaka 1513 K. W. K. na akafanya Agano la torati pamoja nao kupitia Musa. Katika ya pili ya zile Amri Kumi, Yehova alisema: “Kwa maana mimi, Yahweh Mungu wako, ni Mungu mwenye wivu [Mungu mwenye kudai ibada ya pekee, New World Translation] nami naadhibu kosa la baba katika wana, wajukuu na vijukuu vya wale wanaonichukia mimi lakini mimi naonyesha fadhili kwa maelfu ya watu wanaonipenda mimi na kushika amri zangu.”​—Kutoka 20:5, 6, The Jerusalem Bible.

Akiwa ndiye Mwenye Enzi Kuu na mwenyeji-mume, Yehova alikuwa na haki ya kudai ibada ya pekee kutoka kwa watu wake wa agano, Israeli. (Isaya 54:5; Yeremia 3:14) Wakati watu wake walipoacha uaminifu wakageukia miungu ya uwongo tena na tena, je! halikuwa ni jambo linalopatana na akili nzuri kwamba Yehova awatie nidhamu kwa sababu ya kuwapenda, akionyesha kwamba alikataa na alilaani mwendo wao wa upotovu?

Katika pindi nyingi, Yehova alionyesha hangaikio kubwa kwa ajili ya watu wake na akawasihi wamrudie. (Isaya 55:7) Ingawa yeye aliwaadhibu kwa dhambi zao, mwishowe akiuacha utaifa wao uharibiwe na wao wachukuliwe mateka kuingia nchi ya kigeni, baada ya muda aliwarudisha kwenye nchi ya kwao. Yote hayo yanaonyesha nini juu ya Yehova? Je! yeye ni Mungu mwenye wivu, mwenye chuki, na mwenye kulipa kisasi? Hapana! Bali, yanaonyesha kwamba yeye ni “Mungu mwingi wa huruma, mwenye fadhili, si mwepesi wa hasira, mwingi wa rehema na kweli.”​—Kutoka 34:6; Nehemia 9:17; Yoeli 2:13; Nahumu 1:2, 3.

Upendo Unaonyeshwa Kupitia Mwanaye

Katika muda wa karne zilizoendelea kupita, Yehova Mungu aliandaa maelezo zaidi kuhusu ule ‘uzao wa mwanamke’ na ‘uzao wa Abrahamu,’ na kupita manabii Wake Yeye akatabiri juu ya kuja kwa Masihi. Wakati uliowekwa ulipofika, Mungu alionyesha upendo wake kwa njia isiyo ya kifani​—kwa kutuma Mwanaye mzaliwa pekee aje duniani kutoa ile dhabihu ya ukombozi.

Juu ya uandalizi huo mzuri sana, mtume Yohana aliandika hivi: “Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.” (Yohana 3:16) Kwa sababu upendo wa Mungu kupitia Mwanaye, Yesu Kristo, ni wenye ukarimu mwingi, wengine wamekosea kwa kukata shauri kwamba Yeye hangaliweza kuwa ndiye Mungu yule yule anayetajwa katika Maandiko ya Kiebrania kuwa akileta adhabu na hukumu.

Lakini Je! yule Mungu ambaye habari zake zilifundishwa na Yesu ni tofauti sana na yule Mungu anayeonyeshwa katika Maandiko ya Kiebrania? Au, ni kwamba watu wamechagua kuona kile tu wanachotaka kuona? Je! lile andiko linalojulikana sana, Yohana 3:16, halionyeshi waziwazi kwamba mtu ‘asipomwamini’ Mwana, huyo ‘atapotea’ (‘ataharibiwa,’ NW)? Tena, Yohana aliendelea kusema: “Yeye asiyemtii Mwana hataona uzima, bali ghadhabu ya Mungu inabaki juu yake.” (Yohana 3:36, NW) Ikiwa maneno hayo hayapunguzi kwa vyo vyote ukubwa wa upendo wa Mungu, mbona basi wonyesho wa hasira yake juu ya Israeli waaminifu na watu wengine katika Maandiko ya Kiebrania umfanye asiwe Mungu wa upendo?

Kusudi Lenye Upendo la Mungu Kwako Wewe

Kupitia Malaki nabii wake, Mungu alisema: “Mimi, [Yehova], sina kigeugeu.” (Malaki 3:6) Si kwamba amebaki tu bila ugeugeu akiwa Mungu wa upendo bali pia kusudi lake lenye upendo kuhusu wanadamu wa dunia limebaki bila ugeugeu. Kama vile Yehova alivyoweka mbele ya Adamu na Hawa taraja la uzima wa milele katika paradiso ya kidunia, ndivyo huyo Mungu wa upendo anavyokutaka wewe uwe kati ya wale watakaoishi milele kwa furaha katika Paradiso hiyo. (Luka 23:43; 2 Petro 3:13; Ufunuo 21:4) Lakini ni jambo gani linalotakwa? Yesu alisema: “Hii ndiyo maana ya uzima wa milele, wapate maarifa ya kukujua wewe, Mungu wa kweli mmoja tu, na ya yeye uliyemtuma, Yesu Kristo.” (Yohana 17:3, NW) Mashahidi wa Yehova watafurahi kukusaidia ujifunze juu ya Yehova, yule Mungu wa upendo usio na ugeugeu.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki