Je! Desturi Zinatawala Maisha Yako?
MWANAMUME Mjapani mwenye kutembelea nchi nyingine ya Esia aliendelea kutazama akiwa ameduwaa asiamini. Mkaribishaji wake, akitumia vijiti vyake mwenyewe vya kulia chakula, alipekua-pekua nyama iliyokuwa katika sahani ya kupakulia, akachagua kipande kimoja kizuri sana, ndipo akakiweka juu ya bakuli la wali la mgeni huyo! Kule nyumbani katika Japani, jambo hilo lingechukuliwa kuwa ni tabia mbaya. Hakuna mtu angetumia vijiti vyake mwenyewe vya kulia chakula atoe mlo katika sahani inayotumiwa na watu wote mpaka kwanza vijiti hivyo vigeuzwe ili ncha zilizotiwa mdomoni zisikiguse chakula. Hata hivyo mkaribishaji wake alikuwa tu akitafuta kumwonyesha heshima, wala si kumwudhi. Jambo lililokuwa halifikiriki kutendwa katika Japani lilikuwa ishara ya heshima katika nchi hiyo!
Lo, desturi zinatofautiana kama nini! Lo, desturi nyingi zinahitilafiana kama nini! Tena ni nani awezaye kusema ni zipi zilizo bora kuliko nyingine? Ijapokuwa hivyo, desturi fulani zinategemea mambo ya kishirikina au mafundisho ya uwongo. Kwa wale ambao dhamiri zao zimezoezwa na Biblia, kwa wazi wanapaswa kuepuka desturi hizo. Ni jambo gani linaloweza kusaidia mtu anayetamani kufurahisha Mungu aamue ni desturi zipi zinazoweza kushikwa na kwa kadiri gani? Kufuata kanuni za Biblia kunaweza kumsaidia. Kwa maana Mkristo anakubali Biblia kuwa kiwango chake hata kama anaishi wapi ulimwenguni.
Kutumia Kanuni za Biblia
Imekwisha kuonyeshwa vya kutosha kwamba Neno la Mungu lina nguvu kubwa za kufanya kazi katika moyo mnyenyekevu wa mtu na kuzidi-zidi kupatanisha maisha yake na njia ya Mungu. Mtume Paulo alisema kwamba Wakristo Wathesalonike walipokea Neno la Mungu “sawa na vile lilivyo kikweli, kama neno la Mungu, ambalo linafanya kazi pia ndani yenu waamini.” (1 Wathesalonike 2:13, NW) Neno hilo ni lenye nguvu nyingi hivi kwamba, kama vile 1 Wakorintho 6:9-11 linavyoonyesha, lilikuwa limefanya watu wengi katika Korintho wa kale, mji uliojulikana sana kwa uzembe wa kiuasherati, waache mwendo wao wa kwanza wa uibaji, uasherati, ulevi, na ngono na mtu wa jinsia moja. Je! Neno la Mungu linafanya kazi ndani yako pia? Je! kanuni zalo zinaongoza maisha yako kwa kadiri yenye ukamili mkubwa zaidi, zikikuwezesha utambue la kufanya unapokabiliwa na desturi za kikwenu?
Nyakati nyingine ni wazi kwamba desturi fulani inahitilafiana moja kwa moja na kanuni za Biblia. Katika visa kama hivyo mtu anayejua viwango vya Yehova na kutamani kumpendeza yeye anaepuka desturi hizo. Kwa mfano, huenda desturi yenyewe ikawa ni ile ya kuchoma uvumba kwenye maziko ili kutuliza aliyekufa au “nafsi iliyotoka” yake au kumsindikiza vizuri na kufurahisha “nafsi.” Au huenda ikawa kwamba violezo fulani vya nyumba, televisheni, magari, na vitu kama hivyo, vinachomwa kwa moto kwa kusudi la kumwandalia mtu huyo furaha katika makao ya kiroho. Ijapokuwa hivyo, Mkristo anayeamini taarifa ya Biblia kwamba wafu “hawajui neno lo lote” anajua kwamba mazoea hayo yanategemea imani za uwongo na hivyo anayaepuka.—Mhubiri 9:5, 10; Zaburi 146:4.
Ijapokuwa hivyo, inapokuwa kwamba desturi haivunji kanuni za Biblia moja kwa moja, bali inafanya iwe vigumu zaidi kutumikia Yehova Mungu kwa ukamili, ni vigumu zaidi kuweka mpaka na kuonyesha kwamba kanuni za Biblia zinaongoza maisha yako. Kuheshimu sana elimu na mafanikio ya vitu vya kimwili, kujitiisha chini ya wazazi muda wa maisha yote ya mtu, na wazazi kuchagulia watoto wao wenzi wa ndoa ni miongoni mwa desturi hizo zilizoenea sana zinazoweza kuharibu uhusiano wa mtu na Yehova. Kanuni za Biblia zinaweza kutumiwaje katika hali kama hizo?
[Picha katika ukurasa wa 3]
Kuchoma violezo vya vitu kwenye maziko