Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w98 10/1 kur. 19-23
  • Utamaduni wa Wenyeji na Kanuni za Kikristo—Je, Zapatana?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Utamaduni wa Wenyeji na Kanuni za Kikristo—Je, Zapatana?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Maeneo Yasiyo na Utata
  • Vipi Desturi Zisizo na Madhara?
  • Desturi Zinapozuia Maendeleo ya Kiroho
  • Kufikiria Mapendezi ya Wenyeji
  • Jihadhari Kuvuka Mpaka!
  • Utamaduni Una Sehemu Yake
  • Maoni Yaliyosawazika juu ya Desturi Zinazopendwa
    Amkeni!—2000
  • Je! Desturi Zinatawala Maisha Yako?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
  • Jihadhari na Desturi Zisizompendeza Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
  • Vizuizi Vinavyozuia Mawasiliano
    Amkeni!—1996
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
w98 10/1 kur. 19-23

Utamaduni wa Wenyeji na Kanuni za Kikristo—Je, Zapatana?

STEPHEN, Shahidi kutoka Ulaya Kaskazini, alipewa mgawo wa kuwa mishonari katika nchi moja ya Kiafrika. Walipokuwa wakitembea mjini pamoja na ndugu mwenyeji, alishtuka wakati ndugu huyo alipoushika mkono wake.

Kule kuwazia kutembea katika barabara iliyojaa watu wakishikana mkono na mwanamume mwingine kulimshangaza Stephen. Katika utamaduni wake desturi kama hiyo hudokeza ugoni-jinsia-moja. (Waroma 1:27) Hata hivyo, kwa ndugu Mwafrika, kushikana mikono kulikuwa wonyesho tu wa urafiki. Kukataa kuushika mkono kungeonyesha kukataa urafiki.

Kwa nini mgongano wa utamaduni utuhangaishe? Kwanza ni kwa sababu watu wa Yehova wana bidii ya kutimiza utume wao wa kimungu wa ‘kufanya wanafunzi kwa watu wa mataifa yote.’ (Mathayo 28:19) Ili kutimiza kazi hii, wengine wamehama wakatumikie kulipo na uhitaji mkubwa zaidi wa wahudumu. Ili wafanikiwe katika mazingira yao mapya, lazima waelewe na kubadilikana ili wafaane na tamaduni mbalimbali wanazokuta huko. Ndipo watakapoweza kufanya kazi kwa upatano na ndugu na dada zao, na vilevile kuwa wenye matokeo zaidi katika huduma yao ya hadharani.

Zaidi ya hilo, katika ulimwengu huu wenye ghasia, watu wengi wametoroka nchi zao za nyumbani kwa sababu za kisiasa au kiuchumi nao wamehamia katika nchi nyingine. Kwa hiyo, yaelekea twaweza kuona kwamba tunapohubiria majirani hawa wapya, twakabiliwa na desturi mpya. (Mathayo 22:39) Kujua kwetu kwa mara ya kwanza mambo tofauti-tofauti kwaweza kutokeza vurugu kuhusu desturi mpya.

Maeneo Yasiyo na Utata

Utamaduni umefumwa katika mfumo wa jamii ya kibinadamu. Kwa hiyo, lingekuwa jambo lisilonufaisha kuwa “na haki [“mwadilifu,” NW] kupita kiasi” na kuchunguza kila desturi ndogo-ndogo kuamua kama inapatana na kanuni za Biblia!—Mhubiri 7:16.

Kwa upande ule mwingine, kuna uhitaji wa kutambua desturi za kienyeji zinazopinga waziwazi kanuni za kimungu. Ingawa hivyo, kwa ujumla, kufanya hivyo si vigumu kwa kuwa Neno la Mungu lapatikana ili “kunyoosha mambo.” (2 Timotheo 3:16) Kwa mfano, kuwa na wanawake wengi ni desturi ya nchi kadhaa, lakini kwa Wakristo wa kweli kiwango cha Kimaandiko ni kwamba mwanamume awe na mke mmoja tu.—Mwanzo 2:24; 1 Timotheo 3:2.

Vivyo hivyo, desturi nyingine za maziko zinazokusudiwa kufukuza roho waovu, au zinazotegemea kuitikadi katika nafsi isiyoweza kufa, hazingekubaliwa na Mkristo wa kweli. Watu fulani hufukiza uvumba au hutoa sala kwa aliyekufa ili kufukuza roho waovu. Wengine huwa na makesha au hata maziko ya pili wakiwa na lengo la kusaidia aliyekufa kujitayarisha kwa ajili ya uhai ‘katika ulimwengu unaofuata.’ Hata hivyo, Biblia hufundisha kwamba mtu afapo, ‘hajui neno lolote,’ na hivyo, hawezi kufanya wema au kudhuru mtu yeyote.—Mhubiri 9:5; Zaburi 146:4.

Bila shaka, kuna desturi nyingi ambazo zapatana na Neno la Mungu. Inaburudisha kama nini kupata desturi ambazo roho ya ukaribishaji-wageni bado husitawi, ambamo desturi yasisitiza kwamba kila mgeni apewe salamu changamfu na kwamba, inapowezekana, akaribishwe nyumbani! Unapoona jambo hilo mara ya kwanza, je, huchochewi kufuata kielelezo hiki? Ukifanya hivyo, kielelezo hicho kitaboresha utu wako wa Kikristo.—Waebrania 13:1, 2.

Ni nani kati yetu ambaye angependa kucheleweshwa? Katika nchi kadhaa mara nyingi haiwi hivyo kwa sababu kuwahi huonwa kuwa muhimu. Biblia hutuambia kwamba Yehova ni Mungu wa utaratibu. (1 Wakorintho 14:33) Kwa sababu hiyo, ameweka ‘siku na saa’ ya kumaliza uovu, naye atuhakikishia kwamba tukio hili ‘halitakawia.’ (Mathayo 24:36; Habakuki 2:3) Tamaduni zinazoendeleza kuwahi hutusaidia kuwa wenye utaratibu na kuonyesha staha inayofaa kwa watu wengine na wakati wao, jambo ambalo kwa hakika lapatana na kanuni za Kimaandiko.—1 Wakorintho 14:40; Wafilipi 2:4.

Vipi Desturi Zisizo na Madhara?

Ijapokuwa desturi nyinginezo kwa wazi zapatana na njia ya Kikristo ya maisha, nyingine hazipatani. Lakini vipi zile desturi ambazo haziwezi kuamuliwa kuwa nzuri au mbaya? Desturi nyingi hazina madhara, na mtazamo wetu kuzielekea waweza kuonyesha usawaziko wetu wa kiroho.

Kwa mfano, kuna aina nyingi za salamu, yaani, kupeana mkono, kuinama, busu, au hata kumbatio. Vivyo hivyo, kuna desturi nyingi mbalimbali zinazoongoza adabu za mezani. Katika nchi fulani watu hula katika sahani moja. Kucheua ni wonyesho unaokubalika—hata kutamanika—wa kuonyesha uthamini katika nchi fulani, ilhali katika nchi nyingine haukubaliki na ungeweza kuonwa kuwa ukosefu mkubwa wa adabu.

Badala ya kuamua ni zipi kati ya hizi desturi zisizo na madhara unazopenda au usizopenda, kazia kuwa na mtazamo ufaao kuzielekea. Shauri lenye kudumu kutoka katika Biblia hupendekeza kwamba tusifanye ‘jambo lolote kwa ugomvi au kwa majisifu ya bure, bali kwa hali ya akili ya kujishusha chini, tunafikiria kwamba wengine ni wakubwa kuliko sisi.’ (Wafilipi 2:3) Vivyo hivyo, Eleanor Boykin, katika kitabu chake This Way, Please—A Book of Manners, asema hivi: “Moyo wenye fadhili ndicho kitu unachohitaji kwanza.”

Mfikio huu wenye unyenyekevu utatuzuia kudharau desturi za wengine. Tutahisi tumechochewa kuchukua hatua ya kwanza na kujifunza jinsi watu wengine wanavyoishi, kushiriki desturi zao na kuonja vyakula vyao badala ya kusita au kushuku kila kitu kinachoonekana kuwa tofauti. Kwa kuwa na akili iliyofunguka na kuwa tayari kujaribu njia mpya, twaheshimu mkaribishaji wetu au jirani zetu wasio wenyeji. Pia twajinufaisha ‘tunapopanua’ mioyo yetu na upeo wetu wa ufahamu.—2 Wakorintho 6:13.

Desturi Zinapozuia Maendeleo ya Kiroho

Vipi tukikabili desturi zisizo na kosa Kimaandiko, lakini hazichochei maendeleo ya kiroho? Kwa mfano, katika nchi fulani, huenda watu wakapenda sana kuahirisha mambo. Mfikio huu ulio rahisi maishani waweza kupunguza mkazo, lakini utafanya iwe vigumu zaidi kwetu kutimiza huduma yetu ‘kikamili.’—2 Timotheo 4:5.

Twaweza kutiaje wengine moyo waepuke kuahirisha mambo ya maana hadi “kesho”? Kumbuka kwamba “moyo wenye fadhili ndicho kitu unachohitaji kwanza.” Tukichochewa na upendo, twaweza kuweka kielelezo kisha kwa fadhili tueleze manufaa za kutoahirisha hadi kesho mambo yapaswayo kufanywa leo. (Mhubiri 11:4) Kwa wakati uleule, lazima tuwe waangalifu tusikose kutumainiana na kuaminiana kwa sababu tu twataka ufanisi. Madokezo yetu yakikosa kukubaliwa na wengine mara moja, hatupaswi kupiga ubwana juu yao au kuwalaumu-laumu kwa sababu tumevunjika moyo. Sikuzote upendo wapaswa kuwa wa maana kuliko ufanisi.—1 Petro 4:8; 5:3.

Kufikiria Mapendezi ya Wenyeji

Twahitaji kuhakikisha kwamba dokezo lolote tunalofanya ni halali na si jitihada tu ya kulazimisha mapendezi yetu ya kibinafsi. Kwa mfano, mitindo ya mavazi, hutofautiana sana. Katika maeneo mengi inafaa mwanamume anayehubiri habari njema kuvaa tai, lakini katika nchi kadhaa za joto, kwaweza kuonekana kuwa vazi la kirasmi. Kufikiria mapendezi ya wenyeji kuhusu mavazi yafaayo kwa mtu wa kibiashara anayeshughulika na umma mara nyingi kwaweza kuwa mwongozo usaidiao. “Utimamu wa akili” ni muhimu tunaposhughulikia suala nyetivu la mavazi.—1 Timotheo 2:9, 10.

Vipi ikiwa desturi fulani haitupendezi? Je, yapaswa kukataliwa mara moja? Si lazima. Desturi ya wanaume kushikana mikono, iliyotajwa awali, ilikubalika kabisa hasa katika jumuiya hiyo ya Kiafrika. Mmishonari huyo alipoona kwamba wanaume wengine walikuwa wakitembea wakishikana mikono, alistarehe zaidi.

Wakati wa safari zake ndefu za umishonari, mtume Paulo alitembelea makutaniko ambayo washiriki wake walitoka katika malezi mbalimbali. Bila shaka, mara nyingi kulikuwako na migongano ya desturi. Hivyo, Paulo alibadilikana afaane na desturi zozote zile kwa kadiri alivyoweza huku akishikilia imara kanuni za Biblia. “Nimekuwa mambo yote kwa watu wa namna zote,” akasema, “ili nipate kwa vyovyote kuokoa wengine.”—1 Wakorintho 9:22, 23; Matendo 16:3.

Maswali machache yafaayo huenda yakatusaidia tuamue jinsi tunavyopaswa kutenda tunapokabili desturi mpya. Kwa kukubali tamaduni fulani—au kukataa kufanya hivyo—twaonekanaje kwa watu wanaotutazama? Je, watavutiwa na ujumbe wa Ufalme kwa sababu wanaweza kuona kwamba twajaribu kukubali utamaduni wao? Kwa upande mwingine, tukikubali utamaduni fulani wa wenyeji, je, huduma yetu ‘ingetafutiwa kosa?’—2 Wakorintho 6:3.

Tukitamani kuwa “mambo yote kwa watu wa namna zote,” huenda tukahitaji kurekebisha baadhi ya maoni fulani ya ndani sana kuhusiana na linalofaa na lisilofaa. Mara nyingi njia iliyo “sawa” na yenye “kosa” ya kufanya jambo fulani hutegemea tu mahali tunapoishi. Hivyo, katika nchi moja kushikana mikono miongoni mwa wanaume ni wonyesho wa urafiki, ilhali katika nchi nyingi nyinginezo, kwa kweli kufanya hivyo kungefanya watu wasisikilize ujumbe wa Ufalme.

Hata hivyo, kuna tamaduni nyinginezo ambazo zakubalika katika maeneo mbalimbali na ambazo huenda hata zikafaa kwa Wakristo, lakini ni lazima tuwe waangalifu.

Jihadhari Kuvuka Mpaka!

Yesu Kristo alisema kwamba ingawa wanafunzi wake hawangeweza kuondoshwa ulimwenguni, iliwabidi ‘kutokuwa sehemu ya ulimwengu.’ (Yohana 17:15, 16) Ingawa hivyo, nyakati nyingine si rahisi kutambua mpaka kuhusu ni ipi iliyo sehemu ya ulimwengu wa Shetani na ni nini kilicho utamaduni tu. Kwa mfano, muziki na kucheza dansi kumeenea karibu katika kila tamaduni, ijapokuwa katika nchi kadhaa huwa na umaana mkubwa zaidi.

Huenda tukaamua haraka, tukitegemea malezi yetu badala ya sababu nzuri za Kimaandiko. Alex, ndugu Mjerumani, alipokea mgawo kwenda Hispania. Katika mazingira yake ya awali, kucheza dansi hakukupendwa sana, lakini katika Hispania hiyo ni sehemu ya utamaduni. Alipoona ndugu na dada wakicheza dansi ya kienyeji, alivurugika. Je, dansi hiyo ilikuwa mbaya au labda ya kilimwengu? Je, angekuwa akishusha viwango vyake ikiwa angekubali desturi hii? Alex alipata kujua kwamba ijapokuwa muziki na kucheza dansi kulitofautiana, hakukuwa na sababu ya kuwazia kwamba ndugu na dada zake Wahispania walikuwa wakishusha viwango vya Kikristo. Kuvurugika kwake kulitokana na tofauti katika tamaduni.

Hata hivyo, Emilio, ndugu ambaye hufurahia dansi ya kitamaduni ya Kihispania, hutambua kwamba kuna hatari. “Natambua kwamba aina nyingi za dansi hutaka watu wawili wakaribiane sana,” aeleza. “Nikiwa mseja, natambua kwamba hilo laweza kuathiri hisia za angalau mmoja wa wenzi hao. Nyakati nyingine, kucheza dansi kwaweza kutumiwa kuwa udhuru wa kumwonyesha shauku mtu fulani unayevutiwa naye. Kuhakikisha kwamba muziki unafaa na kwamba kukaribiana kwa kimwili kuna mipaka kwaweza kuwa ulinzi. Hata hivyo, lazima nikubali kwamba akina ndugu na dada wachanga walio waseja waendapo kucheza dansi pamoja, ni vigumu sana kudumisha hali ya kitheokrasi.”

Kwa hakika, hatungependa kutumia utamaduni wetu kuwa udhuru wa kujiingiza katika mwenendo wa kilimwengu. Kuimba na kucheza dansi kulikuwa na sehemu katika utamaduni wa Israeli, na Waisraeli walipokombolewa kutoka Misri kwenye Bahari Nyekundu, msherehekeo wao ulitia ndani kuimba na kucheza dansi. (Kutoka 15:1, 20) Hata hivyo, aina yao hasa ya muziki na dansi ilitofautiana na ile ya wapagani waliowazunguka.

Kwa kusikitisha, walipokuwa wakimngoja Musa kutoka Mlima Sinai, Waisraeli walikosa subira, wakafanya sanamu ya ndama na baada ya kula na kunywa “wakaondoka wacheze.” (Kutoka 32:1-6) Musa na Yoshua waliposikia sauti ya kuimba kwao, iliwashtua mara moja. (Kutoka 32:17, 18) Waisraeli walikuwa wamevuka “mpaka” huo, na aina yao ya kuimba na kucheza dansi sasa ilionekana kuwa ile ya wapagani waliowazunguka.

Vivyo hivyo, leo, muziki na kucheza dansi kwaweza kukubalika katika eneo letu na huenda kusiudhi dhamiri za wengine. Lakini taa zikipunguzwa mwangaza, nuru zenye kuwaka na kuzimika ghafula zikiongezwa, au muziki wenye mdundo tofauti ukipigwa, ule ambao ulikuwa unakubalika hapo awali sasa waweza kudhihirisha roho ya ulimwengu. “Ni utamaduni wetu tu,” labda twaweza kutoa hoja. Aroni alitumia udhuru huohuo alipokubali kimya-kimya aina za tafrija na ibada za kipagani, akizifafanua kimakosa kuwa “sikukuu kwa BWANA.” Udhuru huu usiofaa haukuwa halali. Kwani, mwenendo wao hata ulionekana kuwa “dhihaka kati ya adui zao.”—Kutoka 32:5, 25.

Utamaduni Una Sehemu Yake

Desturi za kiajabu huenda zikatushtua mara ya kwanza, lakini si lazima zote ziwe hazikubaliki. ‘Nguvu zetu za ufahamu zikizoezwa,’ twaweza kuamua ni desturi zipi zinazopatana na kanuni za Kikristo na ni zipi zisizopatana na hizo. (Waebrania 5:14) Tunapoonyesha moyo wenye fadhili uliojaa upendo kwa mwanadamu mwenzetu, tutaitikia ifaavyo tunapokabiliwa na desturi zisizodhuru.

Tunapohubiri habari njema ya Ufalme kwa watu katika eneo la kwetu au eneo la mbali, mfikio uliosawazika kuelekea mchanganyiko mbalimbali wa tamaduni utatuwezesha kuwa ‘mambo yote kwa watu wote.’ Na bila shaka tutaona kwamba tunapokaribisha tamaduni mbalimbali, itachangia kuwa na maisha yenye maana, yenye kupendeza, na yenye kuvutia sana.

[Picha katika ukurasa wa 20]

Salamu za Kikristo zaweza kuonyeshwa ifaavyo katika njia nyingi

[Picha katika ukurasa wa 23]

Maoni yaliyosawazika ya tamaduni mbalimbali yaweza kuleta maisha yenye maana, yenye kupendeza

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki