Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w87 2/1 uku. 10
  • Dhihirisha Shauku ya Kuzitangaza Habari Njema

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Dhihirisha Shauku ya Kuzitangaza Habari Njema
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Wakati wa Uharaka
  • Shauku—Inadhihirishwaje?
  • “Mdeni” kwa Wote
  • “Sizionei Aibu Habari Njema”
  • Nguvu za Kunufaisha Zinaongeza Matokeo
  • Hubiri Habari Njema kwa Hamu
    Huduma Yetu ya Ufalme—1999
  • Tangaza Habari Njema kwa Hamu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2000
  • Kuna Habari Njema Ambayo Watu Wote Wanahitaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2011
  • ‘Hatuoni Aibu Kuhusu Habari Njema’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
w87 2/1 uku. 10

Dhihirisha Shauku ya Kuzitangaza Habari Njema

“Kuna shauku kwa upande wangu kuzitangaza habari njema kwenu nini pia.”​—WARUMI 1:15, NW.

1, 2. Watu mara nyingi wanatendaje katika tukio la dharura?

WAO walikuja kutoka kila mahali . . . mamia ya wenye kujitolea wakimiminika kuingia eneo la manispaa mbili, wakafika wakiwa wamejaza chakula na mavazi katika magari makubwa ya mizigo, wakaanzisha vibanda vya kuhamishia watu kwa uharaka, wengine wao wakifanya kazi muda wa saa 18 mpaka 20 kwa siku, wengine wakawa hawana nafasi ya kulala katika siku za kwanza baada ya mvunjiko huo wa kutisha wa ukuta wenye kuyazuia mafuriko ya maji.”

2 Hivyo ndivyo watu walivyotenda wakati gharika ya ghafula ilipokumba mtaa fulani wa kati ya Kalifornia masika yaliyopita, ikafanya watu wapatao 24,000 wakimbie kupata usalama. Ndiyo, wakati maafa—kuanzia gharika za mahali mahali mpaka matetemeko ya ardhi mpaka mikasa ya kinyukilia—yanapotokea bila kutazamiwa, mara nyingi watu wanaitikia kwa kujitolea na kujitupa ndani wasaidie. Wanajikakamua, wanajasiria kupitia katika hatari nyingi na hali zenye kuwatia katika shida, na kwa shauku wanakuja kusaidia wengine—hata watu wasiowajua kabisa.

Wakati wa Uharaka

3. Ni tukio gani la dharura linaloelekea wanadamu leo?

3 Leo, wanadamu wanaelekeana uso kwa uso na afa lililo kubwa zaidi katika historia. Hiyo si kwa sababu ya madhara ambayo mwanadamu anafanya kwenye mazingira, wala si kwa sababu ya tisho la vita ya kinyukilia, wala si kwa sababu ya ongezeko la uhalifu na jeuri, ingawa mambo hayo ni mazito sana. Bali, wanadamu wanaelekeana na kile ambacho Yesu Kristo alikiita “dhiki kubwa ya namna ambayo haijatukia tangu mwanzo wa ulimwengu mpaka sasa, la, wala haitatukia tena.” Kuonyesha jinsi “dhiki kubwa” hiyo itakavyopiga mkumbo mkubwa, Yesu aliendelea kusema: “Kwa kweli, kama siku hizo zisingekatwa ziwe fupi, hakuna mwili ambao ungeokoka.”​—Mathayo 24:21, 22, NW.

4. Kwa kuelekewa na tukio hilo la dharura, inatupasa sisi tutendeje?

4 Wewe ungetendaje kama ungejua kwamba watu wengi, kutia na wengine walio na uhusiano wa karibu nawe, wangeangamia karibuni katika dhiki hiyo? Je! ungekuwa na shauku ya kusaidia? Kumbuka njozi ya kiunabii ya Ezekieli juu ya yule mtu mwenye kidau cha wino cha mwandishi. Yeye aliambiwa kwamba wale tu waliokuwa wameipokea alama ya mfano juu ya vipaji vya nyuso zao ndio wangeuokoka uharibifu wa Yerusalemu, na ni yeye aliyepaswa kuwatia alama hiyo yenye kuokoa uhai. Yeye aliitikiaje? “Nimefanya kama ulivyoniamuru,” akaripoti.​—Ezekieli 9:1-11.

5. Sisi tuko chini ya amri ya kufanya kazi gani, nayo ni yenye uharaka jinsi gani?

5 Je! wewe unadhihirisha nia na shauku ile ile kama mtu huyo aliyevikwa kitani, ukifanya sawasawa na yale ambayo Yehova ameamuru? Yehova ameamuru nini? Kupitia Mwanaye Yesu Kristo, yeye ametoa agizo hili: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, . . . kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi.” (Mathayo 28:19, 20, NW) Hiyo ni kazi yenye kuokoa uhai sawasawa na utiaji alama ya mfano katika vipaji vya nyuso za watu katika siku za Ezekieli. Mtu ye yote asiyeitikia na kuwa mwanafunzi wa Yesu Kristo atapatwa na uharibifu mikononi mwa Mfishaji Mkuu wa Mungu. (2 Wathesalonike 1:6-8) Je! wewe unauhisi uharaka uliopo? Je! unaonyesha hivyo kwa kudhihirisha shauku ya kuzitangaza habari njema?

Shauku—Inadhihirishwaje?

6. Ni nini maana ya “shauku”?

6 Kwa ujumla, watu wa Yehova wanahisi uharaka uliopo wa wakati huu. Sisi sote tuna shauku nyingi ya kuona watu wengi iwezekanavyo wakiokolewa kutoka katika “dhiki kubwa” inayokaribia. Kulingana na kamusi moja, shauku ni “hamu nyingi au yenye bidii katika kufuatia au kujipatia jambo.” Mtu aliye na shauku juu ya jambo fulani anaelekeza wazo hata tendo juu ya kulipata jambo hilo. Yeye atafanya kila awezalo ashinde kipingamizi na kizuizi cho chote, naye atadumu katika kufanya hivyo mpaka afikie mradi wake. Hivyo ndivyo mtume Paulo alivyohisi juu ya huduma yake, nasi ingetufaa tumwige yeye.​—1 Wakorintho 4:16.

7. Kwa sababu gani Paulo alitaka kwenda Rumi?

7 Kwa mfano, fikiria maneno ambayo Paulo aliwaambia Wakristo katika Rumi, kwenye Warumi 1:13-16 (NW). “Mara nyingi mimi nilikusudia kuja kwenu,” akawaambia. Kwa sababu gani? “Ili kwamba niweze kujipatia tunda fulani miongoni mwenu pia,” yeye akaeleza. Je! kwa kusema hivyo Paulo alikuwa akifikiria kutembelea akina ndugu katika Rumi na labda kuwatia moyo wasitawishe kwa ukamili zaidi “tunda la roho,” kama vile waelezaji wengine wanadai? (Wagalatia 5:22, 23, NW) Hapana, kwa maana maneno yake aliyoongeza “hata kama ilivyo miongoni mwa mataifa yale mengine.yote” yanaonyesha wazi kwamba yeye alikuwa amekusudia sana kupata tunda la Ufalme miongoni mwa mtaa wa watu wasio Wakristo kule Rumi. Yeye alitaka kuleta habari njema Rumi na labda kuanzia kule azifikishe kwenye sehemu za mbali.​—Warumi 15:23, 24, NW.

8. Ni jinsi gani Paulo alikuwa ‘amezuiliwa’ kwenda Rumi?

8 “Lakini mimi nimezuiwa mpaka sasa,” Paulo akasema. Akazuiwa na nini? Je! yeye alikuwa na shughuli nyingi mno za mambo ya kibinafsi asiweze kujitahidi kufikilia sehemu hizo? Ni kweli kwamba Paulo alikuwa mtu mwenye shughuli nyingi lakini si kuhusiana na mapendezi ya kibinafsi. Kufikia wakati alipoandikia Warumi (karibu na 56 W.K.), yeye alikuwa amekwisha kumaliza safari mbili ndefu za umisionari na alikuwa akihusika katika shughuli nyingi za safari yake ya tatu. Mara nyingi katika safari hizo yeye alielekezwa na roho takatifu kwenye migawo fulani iliyotajwa waziwazi. (Ona Matendo 16:6-9.) Hata alipokuwa akiandika barua yake, mipango ilikuwa imefanywa tayari aende Yerusalemu “kuwahudumia watakatifu” kule. (Warumi 15:25, 26, NW) Na pia yeye alikuwa amepatwa na ‘vizuizi’ vingine vingi sana vya namna hiyo. —Ona 2 Wakorintho 11:23-28.

9. Paulo alidhihirishaje shauku ya kuzitangaza habari njema?

9 Hata hivyo, Paulo hakuhisi kwamba alikuwa na mambo ya kutosha ya kufanya, wala yeye hakusababu (hakutoa sababu) ya kwamba alikuwa na mgawo wa kufanya hayo na yalikuwa mambo tele. Yeye alitaka kufanya zaidi. Kwa kweli, yeye alisema: “Kunabaki kwa upande wangu kuzitangaza habari njema kwenu pia huko katika Rumi.” Hivyo ndivyo hasa mtu mwenye shauku anavyokuwa! Kwa kufaa, Profesa F. F. Bruce katika kitabu chake The Epistle of Paul to the Romans alisema hivi juu ya mtume huyo: “Kuhubiri injili kumo katika damu yake, naye hawezi kujiepusha nako; kwake yeye hakuna siku inaposemwa kwamba ‘leo ilikuwa siku yake ya kutokuja kazini,’ bali analazimika kuifanya daima akizidisha kidogo-kidogo kulipa deni alilo nalo kwa wanadamu wote—deni ambalo hakuna siku atakapoweza kulilipa kwa ukamili maadamu yuko hai.” Je! hivyo ndivyo wewe unavyoiona huduma?

10. Ni ‘vizuizi’ gani vinavyoweza kuwa mbele yetu, lakini inatupasa tushughulike navyo jinsi gani?

10 Leo, watu wote wa Yehova wanajishughulisha na madaraka mengi. Wengine wana jamaa za kutunza. Wengine wana wajibu mbalimbali katika maeneo mengine. Wengine wana mipaka katika mambo wanayoweza kufanya kwa sababu ya umri au afya. Na bado wengine wana migawo mizito katika kundi la Kikristo. Hata hivyo, sisi tunatambua pia kwamba wakati unaendelea kuishia mfumo wa mambo uliopo, na ushahidi wa Ufalme ni lazima utolewe. (Marko 13:10) Hivyo, kama Paulo, inatupasa sisi tudhihirishe shauku ya kujitahidi kufikilia mambo zaidi katika kazi ya kuhubiri kujapokuwa na ‘vizuizi’ mbele yetu. Haitupasi tuhisi tukiwa na kinaya, tukifikiri kwamba mambo tuliyo nayo ya kufanya yanatosha bila uhitaji wa kuongezewa mengine.​—1 Wakorintho 15:58.

“Mdeni” kwa Wote

11. Ni nini maana ya “Mimi ni mdeni”?

11 Kulikuwa na kani nyingine yenye kusukuma jitihada za Paulo za kutokuchoka katika kuzitangaza habari njema. “Kwa wote Wagiriki na kwa Washenzi, kwa wote wenye hekima na kwa wasiotumia akili mimi ni mdeni,” akasema Paulo. (Warumi 1:14, NW) Ni kwa njia gani Paulo alikuwa “mdeni”? Tafsiri nyingine zinatafsiri neno hilo kuwa “Mimi niko chini ya wajibu” (New English Bible). “Mimi nina wajibu fulani” (Today’s English Version), au “Mimi ninawia wajibu fulani” (Jerusalem Bible). Basi je! yeye alikuwa akisema kwamba kazi ya kuhubiri ilikuwa wajibu au sharti lenye kulemea kama mzigo ambalo alipaswa kutimiza mbele za Mungu? Ni rahisi kukuza mwelekeo kama huo tukiacha kuona uharaka uliopo au tukipotoshwa fikira na vivutia-macho vya kilimwengu. Lakini hilo silo jambo ambalo Paulo alikuwa nalo akilini.

12. Paulo alikuwa “mdeni” kwa nani, na kwa sababu gani?

12 Akiwa “chombo kichaguliwa” cha Mungu na “mtume kwa mataifa,” Paulo alikuwa na daraka zito sana mbele za Mungu. (Matendo 9:15; Warumi 11:13, NW) Hata hivyo yeye hakuhisi wajibu wake kwa Mungu tu. Yeye alisema alikuwa “mdeni” kwa ‘Wagiriki, Washenzi, wenye hekima na wasiotumia akili yao.’ Kwa ajili ya rehema na pendeleo alilopewa, yeye alihisi ulikuwa wajibu wake kuhubiri ili kwamba watu wote wapate kuzisikia habari njema. Alitambua, pia, kwamba ni mapenzi ya Mungu “namna zote za watu waokolewe na kuja kwenye maarifa yaliyo sahihi ya ukweli.” (1 Timotheo 1:12-16; 2:3, 4, NW) Hiyo ndiyo sababu yeye alifanya kazi ya jasho kwa kurudia-rudia, si ili aishi kwa kusudi la kutimiza tu daraka lake kuelekea Mungu na basi, bali pia ili atimize deni lake kwa wanadamu wenzake. Je! wewe unahisi ukiwa na deni kama hilo la kibinafsi kuelekea watu katika eneo lenu? Je! wewe unahisi kuwa unawawia watu hao deni la kujitahidi sana uwaletee habari njema.

“Sizionei Aibu Habari Njema”

13. Paulo alizikadiria habari njema kuwa zenye ubora gani?

13 Kwa uhakika Paulo alikuwa mfano wa kutokeza katika kudhihirisha shauku juu ya kuzitangaza habari njema. Yeye alithamini kwa kina kirefu fadhili zisizostahilika alizoonyeshwa na Mungu. naye hakutaka ziwe za bure tu. (1 Wakorintho 15:9, 10) Hiyo ndiyo sababu yeye aliendelea kusema: “Kwa maana mimi sizionei aibu habari njema.” (Warumi 1:16, NW) Kutokana na maoni ya kibinadamu, zaidi ya Wakristo kuwa wasiopendwa na watu wengi walikuwa pia wakidharauliwa. “Tumefanywa kama takataka za dunia, na tama ya vitu vyote.” Paulo akasema. (1 Wakorintho 4:13) Hata hivyo yeye hakuaibika kupeleka habari njema Rumi, mji uliokuwa ndio kitovu cha ulimwengu wenye masomo ya juu na makao ya Milki ya Rumi yenye makoloni. Tunapokabiliwa na ubaridi, matukano, au hata upinzani katika kazi yetu ya kuhubiri, tunaweza kukumbuka mfano wa Paulo unaotia moyo.

14. Kwa sababu gani Paulo ‘hakuziaibikia habari njema’?

14 ‘Kutoaibikia habari njema’ kwa kweli ni njia nyingine ya kusema ‘tunajivunia zile habari njema,’ na hivyo ndivyo tunavyopaswa kuwa. Kwa sababu gani? Kwa sababu “hizo, kwa kweli, ndizo nguvu za Mungu za kutolea wokovu kila mmoja aliye na imani,” Paulo akaeleza. Yeye alikuwa amejionea kibinafsi mambo ya kutosha maishani ya kuweza kuunga mkono maneno yake. Tukiwa na habari njema, Paulo akasema, “sisi tunapindua njia za kufikiria sababu za mambo na kila kitu kilichoinuliwa juu sana dhidi ya maarifa ya kumjua Mungu; nasi tunaleta kila wazo ndani ya uteka ili tukifanye kumtii Kristo.” (2 Wakorintho 10:5, NW) Ziwe zilikuwa dhidi ya mapokeo ya Wayahudi, falsafa ya Wagiriki, au uwezo mkuu wa Waroma, habari njema zilithibitika kuwa zenye shangwe ya ushindi.

15. Ni jinsi gani shauku ilikuwa kani yenye kusukuma Paulo katika maisha yake?

15 Ni jambo zuri kama nini kwamba badala ya Paulo kuhisi daraka lake alilopewa na Mungu lilikuwa mzigo, yeye alikuwa ‘na shauku’ ya kulitimiza! Ni kama vile yeye mwenyewe alivyoeleza jambo hilo: “Maana nimewekewa sharti; tena ole wangu nisipoihubiri Injili!” (1 Wakorintho 9:16) Shauku hiyo ilimsaidia aendelee kwa miaka mingi ya kutumikia bila kuchoka, hivi kwamba mwishowe yeye angeweza kusema: “Nimevipiga vita hivyo vizuri, mwendo nimeumaliza, Imani nimeilinda.”​—2 Timotheo 4:7.

Nguvu za Kunufaisha Zinaongeza Matokeo

16. Ni mambo gani yenye ushindani yangeweza kumwelekea yule mtu mwenye kidau cha wino cha mwandishi katika njozi ya Ezekieli?

16 Kama Paulo, yule mtu mwenye kidau cha wino cha mwandishi katika njozi ya Ezekieli bila shaka alikuwa pia na shauku juu ya mgawo wake. Yeye alirudisha ripoti njema: Utume katekelezwa! Usimulizi hautuambii jinsi yeye aliwatafuta wote ‘wenye kuugua na kulia kwa sababu ya machukizo yote yenye kufanywa.’ (Ezekieli 9:4) Ingawa hakuna lo lote lililosemwa juu ya jinsi kazi yote hiyo ya kutia alama ingefanywa, kwa wazi haikuwa kazi nyepesi.

17. (a) Ni mambo gani yenye ushindani unayoelekeana nayo katika kazi ya kufanya wanafunzi, nawe unashughulikaje nayo? (b) Je! jitihada zinazohitajiwa zinastahili kufanywa?

17 Vivyo hivyo leo, utume wetu si mwepesi. Basi, ulizo ni hili: Ni kwa kadiri gani sisi tuna nguvu za kunufaisha watu katika kazi hii ya kuokoa uhai? Ili kufanya watu wengi iwezekanavyo wawe wanafunzi, ni lazima sisi tujitie katika kazi hiyo kwa ukawaida na kwa mpangilio mzuri, bila kuipita nafasi yo yote ya kuzishiriki habari njema. Watu katika mtaa wetu wana shughuli nyingi pia kama sisi; huenda wakawa nyumbani mara chache sana tunapowatembelea, na hata ikiwa wamo nyumbani, mara nyingi wao wanakuwa tayari na shughuli zao. Tunaweza kufanya nini? Basi, tunahitaji kuweka kumbukumbu za maandishi sahihi na kurudi nyakati tofauti-tofauti, tena na tena, tukitumaini kwamba tutakuta mtu wa kusema naye. Je! jitihada hizo zinastahili kufanywa? Acha vibarua vifupi vinavyofuata kutoka kwa wenye nyumba wawili vitoe jibu:

“Mimi ningependa kuonyesha shukrani zangu kwa Mashahidi wa Yehova kwa ajili ya ziara zao nyingi ambazo wamefanya nyumbani kwangu. Najua nyakati nyingine utume wenu hauonwi kwa shauku inayoustahili sana na watu walio nje ya kanisa lenu. Kwa hiyo mimi nimefikiri ingefaa nishiriki nanyi mambo niliyoona na kusema asanteni!”

“Kuna watu wengi sana kati yetu wanaohisi njaa ya ukweli, kwa kuwa wengi sana kati yetu tunaamini kwamba njia zote zinaongoza kwenye wokovu. Ninyi mnaothubutu kuendelea kutafuta mtu wa kuhudumia, msichoshwe nasi kisha mtuache! Sisi si watu wabaya sana, ingawa tunawatolea maneno mabaya, tunawaaibisha, na kuwakataa. Msichoke na kuacha, kwa sababu sisi tumefundishwa mengi ya uwongo, tukasimuliwa hadithi nyingi za kuchukiza sana, na tukaelimishwa kuwachukia ninyi, ili ujumbe wa Ufalme wa Yehova uzuiwe usitufikie sisi.”

18. (a) Wewe unaweza kusaidiaje wengine waipate maana ya habari njema? (b) Mhubiri mmoja alishindaje ubaridi aliouona akionyeshwa?

18 Ili kufikia moyo wa watu na kuwasaidia waipate maana ya habari njema, mengi yanahitajiwa zaidi ya kukutana nao kijuu-juu. kutoa ujumbe fulani uliotayarishwa, au kuwaachia vitabu fulani vya Kibiblia. Ni lazima tujitahidi kutambua mahitaji na mahangaikio yao, mapendezi na machukio yao, hofu zao na maoni mabaya wanayofuata bila msingi mzuri., Kufanya yote hayo kunahitaji fikira na jitihada nyingi sana​—na shauku kwa upande wetu. Fikiria jambo lililoonwa linalofuata:

Mhubiri mmoja alisema na mwanamke kwenye mlango wa nyumba moja ya ghorofani lakini hakuitikiwa sana. Alipoona kwamba hapo palikuwa na watoto kadha, mhubiri huyo wa kike aliuliza mwanamke huyo ana watoto wangapi. Yeye akajibu kwamba hao si watoto wake bali ni wa mlamu wake, ambaye hivi karibuni tu alikuwa amehamia nchi hiyo kutoka nchi nyingine. Upesi maongezi yakafikia habari ya kwamba nyumba za kuishi haziwafai sana watu. Mhubiri akakubali kwamba katika majiji makubwa ni vigumu kupata nyumba nzuri kwa bei nafuu, kwa kuwa yeye pia ana watu wa ukoo ambao wangekuja karibuni. Basi akajitolea kusaidia mwanamke huyo. Bibi huyo alifurahi sana akaita mlamu wake aje pale mlangoni. Mazungumzo yakaendelea, nao wakabadilishana namba za simu. Bila kusahau kusudi la ziara, mhubiri akatumia busara kufungua ukurasa 157 katika kitabu Kuishi Milele na kueleza kwamba katika mfumo mpya ulioahidiwa, matatizo ya kupata nyumba zinazofaa na kazi ya kuajiriwa yatakuwa yamepita. Mwanamume yule alivutwa sana na akakikubali kitabu hicho kwa utayari. Baadaye, mhubiri yule alirudi kusema amepata nyumba ya kukodi katika ghorofa; pia akaanzisha tena mazungumzo yao ya Kibiblia.

19. Sasa ni wakati wetu wa kufanya nini? Na tunahitaji kuzungumza nini zaidi?

19 Wakati wa kuzihubiri habari njema unamalizika mbio-mbio. Sisi hatujui ni kwa muda gani zaidi wale “malaika wanne” wataendelea ‘kuzifumbata zile pepo nne za dunia.’ (Ufunuo 7:1, NW) Vyo vyote iwavyo, ile “dhiki kubwa” ingali mbele, na watu wenye mioyo minyofu wanakusanywa. Kweli kweli, “mashamba” ni “meupe, tayari kwa mavuno.” (Mathayo.24:21, 22: Yohana 4:35) Sasa ndio wakati wetu wa kujitahidi kweli kweli katika kazi hii ambayo haitarudiwa kamwe. Tunaweza kuutumiaje wakati uliobaki kwa njia iliyo bora zaidi? Tunaweza kufanya nini tuwe na ushiriki kamili zaidi katika kazi hii yenye kuokoa uhai? Na ni jambo gani linaloweza kutusaidia tuendelee kudhihirisha shauku ya kuzitangaza habari njema? Maulizo hayo yatazungumzwa katika makala inayofuata.

Fikiria mfano wa Paulo Kulingana na Warumi 1:13-16—

◻ Kwa sababu gani yeye alikuwa na shauku ya kwenda Rumi?

◻ Ni nini kilichomzuia asiende? Lakini yeye alitendaje?

◻ Yeye alikuwa “mdeni” kwa nani na kwa sababu gani?

◻ Yeye alihisije juu ya habari njema? Kwa sababu gani?

◻ Kama Paulo, sisi tunaweza kufanya nini tuwe na nguvu za kunufaisha watu katika kuzitangaza habari njema?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki