Je! Wewe Una Akili ya Kuulizia-ulizia Mambo?
UDADISI ni “tamaa ya kutaka kujua.” Udadisi mwingi unafanya mtu awe na shauku ya kujifunza mambo, kugundua habari zinazoyahusu. Yehova alipanda sana shauku hiyo ndani yetu, hivi kwamba karibu na pale mwanzo katika dakika ya kuzaliwa sisi tumekuwa na kichocheo cha kupeleleza ulimwengu unaotuzunguka. Kuwako kwetu kwenyewe ni utaratibu wa kujifunza mambo ambako hakufikii mwisho kamwe. Ili tuweze kuwa watu wazima waliokomaa, waliorekebika vizuri, tunahitaji kutosheleza udadisi wetu, tamaa yetu ya kutaka kugundua jinsi mambo yalivyo.
Ndivyo ilivyo hasa katika mambo ya kiroho. Matazamio yetu ya uzima wa milele yanategemea kujifunza kwetu juu ya Yehova Mungu. (Yohana 17:3) Biblia inatuambia kwamba yeye anataka tuulizie-ulizie habari zinazomhusu yeye, ‘tupapase-papase na kwa kweli tumpate.’ (Matendo 17:23, 24, 27, NW) Tukigandamiza udadisi wetu au tukishindwa kuuruhusu upate ukuzi, maendeleo yetu yatakuwa ya polepole sana. Kwa kweli, ukosefu wa kupendezwa na mambo ya kiroho unaweza kuleta kifo.—Zaburi 119:33, 34; Hosea 4:6.
Kulingana na hilo, watu wa Yehova kuanzia nyakati za kale wamekaziwa sikuzote uhitaji wa kupata maagizo na kujifunza mambo ili watosheleze tamaa inayofaa ya kujifunza habari. (Kumbukumbu 6:6, 7; 31:12; 2 Nyakati 17:9) Yesu Masihi alikuwa ndiye mwalimu mkubwa zaidi aliyekuwa duniani. (Mathayo 9:35) Wanafunzi wake walifuata mfano wake. Hata walipokuwa wakielekeana na upinzani, wao “waliendelea bila kuacha wakifundisha na kuzitangaza habari njema.” (Matendo 5:42, NW) Kufundisha kwao kuliamsha kupendezwa katika akili zenye kuulizia-ulizia mambo. Wengi walikuwa kama Waberoya, walioitikia kwa “shauku iliyo kubwa zaidi ya akili, wakiyachunguza Maandiko kwa uangalifu kila siku juu ya kama mambo hayo yalikuwa hivyo.”—Matendo 17:11, NW.
Vivyo hivyo, mwingi wa utendaji mbali-mbali wa kundi la kisasa la Kikristo unategemea kufundisha. Hivyo, kundi linatimiza kusudi la msingi la kuwako kwalo, yaani, kuendeleza na kutosheleza tamaa ya kujifunza habari zinazohusu Yehova na makusudi yake. Aina hiyo ya udadisi ni yenye mafaa na yenye faida.
Mipaka Inayofaa Kuwekewa Udadisi
Ijapokuwa hivyo, nyakati nyingine inakuwa lazima watoto walindwe na udadisi wao wenyewe. Wakati mtoto mchanga anapojitahidi kufikilia kitu fulani chenye moto akiguse au anapoingiza mdomoni mwake kioo fulani akitaka kujulia habari za kitu hicho ili aonje ladha yacho, huenda akapata dhara. Sisi hatuwi tunazuia ukuzi wake tunapomvunja moyo aache udadisi wake katika pande hizo.
Wakati watoto wanapokuwa wakubwa zaidi, huenda udadisi wao ukawaongoza tena waingie matatani. Hivyo, huenda mvulana tineja akawa mdadisi sana akitaka kujua habari zilizo katika gazeti lenye picha za umalaya. Au huenda msichana tineja akafanya majaribio ya kutumia tumbaku au dawa nyingine za kulevya kwa sababu ya udadisi. Huenda kikundi cha vijana kikakutana pamoja na kunywa pombe nyingi kwa kujaribu kulewa—ili waone tu inakuwaje mtu akilewa! Hapo tena, sisi hatuwi tukizuia ukuzi wa kiasili wa tineja na maendeleo yake tukimvunja moyo aache aina hiyo ya udadisi.
Je! kuna maeneo ambayo katika hayo udadisi wa Mkristo aliyekomaa huenda ukamwingiza matatani? Ndiyo, kweli kweli. Paulo alimwonya Timotheo dhidi ya wale ambao huenda wakavutia udadisi wa Mkristo wakijitahidi kupindua imani yake. “0 Timotheo,” akasema Paulo, “linda kilichowekwa katika amana pamoja nawe, ukigeukia kando kutoka kwenye semi zilizo tupu zinazochafua kilicho kitakatifu na kutoka kwenye mapingano ya kile kinachoitwa kwa uwongo ‘maarifa.’ Kwa sababu ya kujionyesha juu ya maarifa kama hayo wengine wameiacha njia wakatoka kwenye ile imani.”—1 Timotheo 6:20, 21, NW.
Katika barua yake ya pili kwa Timotheo, Paulo alitoa onyo zaidi: “Watu hao hao wameiacha njia wakatoka kwenye ukweli, wakisema kwamba ufufuo umekwisha kutukia tayari; nao wanaipindua imani ya wengine.” (2 Timotheo 2:18, NW) Je! wewe unaweza kuwazia usemi kama huo uliamsha udadisi kama nini? Huenda watu wasio na habari wakawa walijiuliza hivi: ‘Watu hawa wanamaanisha nini? Wao wanaweza kusemaje kwamba ufufuo umekwisha kutukia tayari?’ Kwa kutaka sana kujua, huenda wao wakawa walisikiliza. Matokeo yakawa nini? Imani ya wengine wao ilipinduliwa. Kusikiliza usemi kama huo kwa sababu ya udadisi kulikuwa hatari kwa njia ile ile ambayo ni hatari kujaribia dawa za kulevya au vitabu vyenye picha za umalaya kwa sababu ya udadisi.
Je! hiyo inamaanisha kwamba Wakristo wana akili nyembamba, wasio na nia ya kusikiliza maoni ya watu wengine? Hapana, hiyo siyo maana. Bali, wao wanashauriwa waepuke kufungulia akili zao mambo yanayoweza kuwaletea kihoro baadaye. Ebu wazia tu historia ingaliweza kuwa tofauti kama nini ikiwa Hawa angalikataa kutosheleza udadisi wake kwa kusikiliza maneno ya udanganyifu ya Shetani Ibilisi! (Mwanzo 3:1-6) Mtume Paulo alionya wazee Waefeso juu ya “mbwa-mwitu” ambao, wakidhihirisha roho moja na ile ambayo Shetani alikuwa amedhihirisha kuelekea Hawa, ‘wanasema mapotovu, wawavute hao wanafunzi wawaandamie wao.’ (Matendo 20:29, 30) Wao wanatumia “maneno ya bandia” yaliyotungwa kwa ajili ya ‘kututumia sisi kwa faida yao.’ Maneno hayo yanatokeza fikira zilizo na sumu kwa hali ya kiroho ya Mkristo.—2 Petro 2:3, NW.
Kama wewe ungejua kwamba kinywaji fulani kina sumu, je! ungekinywa kwa sababu ya udadisi uone ladha yacho ikoje? Au ili uone kama mwili wako una nguvu za kutosha kupambana na sumu hiyo? Bila shaka sivyo. Vivyo hivyo, je! ni jambo la hekima kufungulia akili yako maneno ambayo yametungwa kwa makusudi ili yakudanganye wewe na kukuvuta utoke kwenye ukweli? Ni vigumu!
Jihadhari na Falsafa za Kilimwengu
Udadisi unaweza kutudhuru sisi, pia, ikiwa unatuongoza tuchunguze falsafa za kilimwengu. Falsafa inafasiliwa kuwa “jitihada za kibinadamu za kufahamu na kufasili kupitia sababu za kufikiri na kuwazia-wazia mambo yanayohusu matukio yote yanayopata mwanadamu, visababishi na kanuni zilizo chini ya jambo lo lote linalotokea.” Ijapokuwa hivyo, hatimaye wale wenye kutokeza falsafa za kibinadamu zifuatwe wanakuja kuwa kama wale ambao ‘wanajifunza sikuzote, ila wasiweze kabisa kuufikia ujuzi wa kweli.’ (2 Timotheo 3:7) Kushindwa kwao kunaletwa na kosa moja la msingi: Wao wanategemea hekima ya kibinadamu badala ya hekima inayotoka kwa Mungu.
Kosa hilo lilifunuliwa waziwazi na mtume Paulo. Yeye alisema na Wakorintho juu ya “hekima ya ulimwengu huu,” ambayo ni “upumbavu kwa Mungu.” (1 Wakorintho 3:19, NW) Naye alionya Warumi dhidi ya wale waliokuwa “na vichwa vitupu katika sababu zao za kufikiri.” (Warumi 1:21, 22, NW) Yehova ndiye chanzo cha vitu vyote tulivyo navyo. Kwa kufaa, sisi tunamtegemea yeye atuandalie “maarifa sahihi na utambuzi kamili” na kutufunulia “mambo yenye kina kirefu ya Mungu.” (Wafilipi 1:9; 1 Wakorintho 2:10, NW) Chanzo cha kwanza cha hekima ya Mungu ni Neno lake, Biblia.
Kwa sababu falsafa za kibinadamu zinatupilia mbali Neno la Mungu, haitupasi kamwe sisi tuipuuze hatari inayotokezwa na falsafa hizo. Fikira za kisasa za kifalsafa zimetongoza walimu wengi wa Jumuiya ya Wakristo walikubali fundisho la mageuzi na hata waache imani yao juu ya kwamba Biblia ina roho ya Mungu kwa kupendelea uchambuzi wa juu zaidi katika jitihada ya kupata heshima ya kwamba wao ni watu wenye akili sana. Falsafa za kisiasa na kijamii zenye kukazia uhuru wa mtu binafsi zimeongoza kwenye kituko cha utoaji mimba, ukosefu wa adili ulioenea sana katika mambo ya ngono, matumizi mabaya ya dawa za kulevya na mazoea mengine yenye uharibifu. Fikira za kufuatia vitu vya kimwili zinaongoza watu walio wengi leo wapime furaha na mafanikio ya mtu kulingana na mali za kimwili alizo nazo.
Falsafa zote hizo zinaonyesha jitihada za kutatua matatizo au kutafuta furaha zinafanywa kwa kutegemea sababu za kufikiri kwa njia ya kibinadamu na bila msaada wa Mungu. Zote zinatupilia mbali ukweli wa msingi ambao Yeremia aliutambua: “Ee [Yehova], najua ya kuwa njia ya mwanadamu haimo katika nafsi yake; kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.” (Yeremia 10:23) Furaha na wokovu wetu vinategemea utii wetu na tegemeo letu juu ya Yehova. Hivyo mwendo ulio wa hekima ni kupinga kishawishi cha kuachilia udadisi wetu uwe na uhuru wa kututawala vyo vyote tu, huku tukifungua akili zetu ziingiwe na mawazo ya kibinadamu yanayoweza kuchafua fikira zetu na hatimaye yatuache tukiwa tumepotea miongoni mwa wale wasio na tumaini lo lote.
Udadisi Juu ya Mwisho Unaokaribia
Tangu Yehova alipotoa ufunuo wake katika Edeni kwamba alikuwa na kusudi la kuondoa matokeo maovu ya uasi wa Shetani, watumishi Wake waaminifu wamekuwa sikuzote na udadisi wenye uchangamfu juu ya kutimia kwa kusudi la kimungu hatua kwa hatua. Ndiyo, hata malaika wameonyesha udadisi juu ya jambo hilo! (1 Petro 1:12) Katika siku za Yesu, wengi walipendezwa sana sana na kujua wakati barabara ambapo Ufalme ungekuja. Ijapokuwa hivyo, Yesu aliwaambia kwa kurudia-rudia kwamba hayakuwa mapenzi ya Yehova wajue jambo hilo. (Mathayo 25:13; Marko 13:32; Matendo 1:6, 7) Kama wangalifanya jaribio lo lote la kuthibitisha tarehe fulani ya wazi ingalikuwa kazi ya bure tu. Badala ya hilo, yeye aliwahimiza kwa hekima waelekeze fikira kwenye madaraka yao ya Kikristo, huku wakidumisha maoni ya kuona uharaka kila siku.—Luka 21:34-36.
Leo, matukio ya ulimwengu yanaandaa ushuhuda mwingi sana kwamba mwisho uko karibu, na udadisi ni mwingi sana juu ya tarehe ambayo mwisho huo utatukia. Huenda matukio fulani yakawa yalisadikisha watu fulani kwamba walikuwa wameigundua siku ile na saa ile. Wao walipatwa na masumbufu makali ya akilini, labda hata wakafikia hatua ya kuanguka waache kutumikia Mungu, wakati mataraja yao hayakutimia. Ni vizuri zaidi kuacha jambo hilo mikononi mwa Yehova, tukiwa na tumaini kwamba yeye ataleta mwisho katika wakati unaofaa barabara. Kila kitu tunachohitaji ili tuwe katika tayari kimekwisha kuandaliwa.
Uhitaji wa Usawaziko
Kwa hiyo, kama ilivyo kuhusu mambo mengi maishani, udadisi wetu unaweza kuwa baraka au laana. Ukielekezwa kwa njia inayofaa, unaweza kufunua maarifa yenye vito vya thamani kubwa sana yanayoleta furaha na burudisho. Udadisi wenye afya juu ya Muumba wetu, mapenzi yake, na makusudi yake unaweza kuridhisha na kufaidi kweli kweli. Udadisi usiozuiwa kwa hatamu, ulio mgonjwa-mgonjwa, unaweza kutuvuta tutopee katika kukisia-kisia nadharia za kibinadamu. Nasi tukiwa humo imani ya kweli na kujitolea Mungu haviwezi kuendelea kuwa hai. Kwa sababu hiyo, wakati udadisi wetu unapotisha kutuongoza ndani ya jambo fulani lenye mashaka, “jihadharini msije mkapotezwa . . . na kuanguka mtoke katika imara yenu wenyewe.”—2 Petro 3:17, NW.