Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w87 3/15 kur. 4-7
  • Wanawake Wakristo—Kudumisha Ukamilifu Mahali pa Kazi

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Wanawake Wakristo—Kudumisha Ukamilifu Mahali pa Kazi
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Waajiri-kazi Ambao “Ni Wagumu Kupendeza”
  • Kubaki Ukiwa Safi Kiadili
  • Hatua za Kuzuia
  • Kukomesha Hali ya Kusumbuliwa sumbuliwa
  • Kazi Yako na Ukamilifu Wako!
  • Kusumbuliwa Kingono—Jinsi Unavyoweza Kujikinga
    Amkeni!—1996
  • Wanawake Kazini—Majaribu na Magumu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
  • Naweza Kupambanaje na Kusumbuliwa Kingono?
    Amkeni!—2000
  • Dumisha Utimilifu Wako!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2019
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
w87 3/15 kur. 4-7

Wanawake Wakristo—Kudumisha Ukamilifu Mahali pa Kazi

“NYAKATI nyingine mkazo ulio [kazini] ni mnene sana hivi kwamba ungeweza kuukata kwa kisu.” Hivyo ndivyo alivyosema mwanamke mmoja anayefanya kazi.a Mkazo wa kutaka kufanya mengi zaidi, mashindano makali sana, wasimamizi wa kazi wenye kudai, kuchoshwa na kazi kwa kufanya mambo yale yale tu—hayo ni machache tu kati ya mambo yanayofanya nyingi za kazi za kuajiriwa zisipendeze sana. Ni kazi chache zinazokuwa na upendezi mwingi sana na msisimuko unaoahidiwa na porojo za vyombo vya habari. Lakini ikiwa wewe ni mwanamke anayefanya kazi, inakupasa ujitahidi kufanikisha kazi yako.

Ijapokuwa hivyo, kwa kusema hivyo, hatumaanishi pato la kifedha. Mahali pa kazi ni uwanja ambamo ukamilifu wa Kikristo wako unajaribiwa! Njia yako ya kufanya mambo kazini, kuondolea mbali roho ya mashindano ya kupindukia, na kupinga sana vishawishi vya ukosefu wa adili, yote hayo yanafunua ni kwa kadiri gani wewe umejitoa kwa kanuni za kutii Mungu. Ili kupata upendeleo wa Yehova Mungu, ni lazima mwanamke anayefanya kazi aweze kusema kama mtunga zaburi: “Nimekwenda kwa ukamilifu wangu.”—Zaburi 26:1.

Biblia inakusaidia ufanye hivyo hasa. Kwa mfano, unapoulizwa ushushe hali yako iwe ya kutumia mbinu za kujifaidi kwa kuumiza wengine au unaposhawishwa uache kazi ifunike madaraka ya kijamaa, funzo la Biblia, mikutano ya Kikristo, na huduma, unaweza kuyakumbuka vizuri maneno ya Mfalme Sulemani: “Tena nikafikiri amali zote, na kila kazi ya ustadi, ya kwamba inatoka katika mtu kupingana na mwenzake. Hayo nayo ni ubatili na kujilisha upepo.” (Mhubiri 4:4) Kuiona kazi ya kimwili kwa njia hiyo kunazuia au kupoleza tamaa kali sana ya kujitakia makuu. Kunakusaidia uwe na maoni yanayofaa juu ya kazi ya kuajiriwa, ukiiona kuwa ya pili kwa mambo ya kiroho. —Mathayo 6:33.

Lakini je! hiyo inamaanisha kuwa usiyependezwa na kazi ya kimwili? La, kwa sababu Biblia inakataza uvivu. (Mithali 19:15) Inasema juu ya ‘kuona mema kwa sababu ya kazi ngumu yako.’ (Mhubiri 2:24, NW) Zaidi ya hilo, kuruzuku jamaa ni daraka ambalo mtu amepewa na Mungu. (1 Timotheo 5:8) Kwa hiyo ikiwa kutimiza wajibu huo kunamaanisha kufanya kazi ya kimwili isiyopendeza, fikiria maneno ya Biblia kwenye Wakolosai 3:23, NW: “Lo lote mnalofanya, lifanyeni kwa nafsi yote, kama kwa Yehova, wala si kwa wanadamu.” Kujiona mwenyewe kuwa ukifanya “kama kwa Yehova” ni kichocheo chenye nguvu cha kufanya mengi kazini, chenye kukusukuma zaidi ya kutaka tu uongezewe mshahara au kuvutwa upandishwe cheo.

Waajiri-kazi Ambao “Ni Wagumu Kupendeza”

Mwanamke mmoja jina lake Sally anasema: “Mimi nahisi kama kwamba [msimamizi wangu wa kazi] ananichunga-chunga nyakati zote. Yeye hawi kamwe na jambo jema la kuambia mtu ye yote.” Kufanya kazi chini ya bwana mkubwa ambaye ‘ni mgumu kupendeza’ au mwenye hasira ya haraka haraka kunaweza kutatiza ivyo hivyo, hasa wakati mtu anapokuwa mpya mahali pa kazi.—1 Petro 2:18, NW.

Ingawa hivyo, kuiacha kazi huenda kusiwe kunafaa kiuchumi. Hivyo huenda likawa jambo bora zaidi kufuata shauri la Biblia kwamba wafanya kazi—wa kiume na wa kike—‘watii.’ (1 Petro 2:18) Badala ya kuzidisha pambano la maneno kwa misemo mikali ya kupuuza au ukosefu wa heshima, jaribu “kuwapendeza vizuri [waajiri-kazi], si kurudisha maneno.” (Tito 2:9, NW) Kujiweza kwa namna hiyo huenda hata kukakuzuia usipoteze kazi yako. Sulemani alisema: “Roho ya mtawala [mtu fulani aliye katika mamlaka] ikipanda dhidi yako, usiondoke mahali pako mwenyewe, kwa maana utulivu wenyewe hupunguza madhambi makubwa.” —Mhubiri 10:4, NW.

Myapara mkali-mkali huenda hata akaaibika ukosefu wake wa subira ukikabiliwa kwa upole, madai yake yasiyo ya kiasi yakikabiliwa kwa neema. (Mithali 15:1; Wakolosai 4:6) Na wakati wewe unapothibitisha uhodari wako wa kazi na kutegemeka, huenda pole kwa pole mwelekeo wake juu yako ukawa mzuri zaidi. Ikiwa sivyo, huenda usiwe na la kufanya sana isipokuwa ‘kujizoeza subira,’ ukijua kwamba Mungu anafurahishwa na mwenendo wako wa Kikristo. —Yakobo 5:7, 8, NW.

Kubaki Ukiwa Safi Kiadili

Ukamilifu unatia ndani pia maadili ya Kikristo. Makala moja katika kichapo Ladies’ Home Journal ilionya hivi: “Kule afisini—ambako kila mtu anatazamiwa avalie vizuri, ajiendeshe vizuri, atumie wakati pamoja na kufuatia miradi ya ujumla—kuna mazingira yanayoweza kwa urahisi kutokeza mambo ya ngono.” Mapenzi yenye kufanywa afisini ni jambo la kawaida sana. Kwa hiyo ni jambo la hekima kutahadhari. Fanya uhusiano wako na wanaume kazini uwe wa kikazi tu. Epuka maongezi ambayo yangeweza kuamsha hisia za kimahaba. “Maana hayo ndiyo mapenzi ya Mungu, . . . mwepukane na uasherati.”—1 Wathesalonike 4:3, 4.

Ingawa hivyo, nyakati nyingine wanawake wanakuwa wenye kupatwa na tatizo la tangu kale: kusumbuliwa sumbuliwa kwa sababu ya ngono. Biblia Inatuambia kwamba mwanamume mmoja jina lake Boazi aliagiza wanaume vijana aliokuwa amewaajiri kazi ‘wasimguze’ Ruthu, mwanamke mwenye kufanya kazi katika shamba lake. Mwanachuo wa Biblia John P. Lange anasema juu ya “mizaha ya kukosa adabu ambayo labda vibarua hao shambani walikuwa wamezoea kutumia katika kushambulia wanawake.” (Ruthu 2:9) Na ingawa waajiri-kazi fulani wa kisasa wanajaribu kukinga waajiriwa kazi wao wa kike, wengine wanakadiria kwamba asilimia 40 mpaka asilimia 85 ya wanawake wanaofanya kazi (katika United States) wamewahi kuwa katika hali ya namna fulani ya kusumbuliwa sumbuliwa kuhusiana na ngono.

Mwanamke mmoja kijana jina lake Valerie, kwa mfano, alifanya kazi akiwa mhazili (sekretari). Mara kwa mara, bwana-mkubwa wake —ambaye umri wake ni mkubwa kuliko wake kwa zaidi ya mara tatu—alikuwa akisema-sema juu ya mavazi yake kwa njia ya kuonyesha alimtaka. Wakati mmoja mkubwa huyo alijaribu kutumia ujanja ili kumfanya atazame picha za uasherati. Hatimaye, akamwita afisini mwake na kumwambia, “Ili udumishe kazi yako, utalazimika kufanya ngono nami.” Bila shaka, mwanamke huyo kijana alikataa kufanya hivyo.

Kutendwa kwa njia hiyo yenye kutwezwa ni kwa namna nyingi. Linasema hivi gazeti la Uingereza New Statesman: “Jambo hilo linaanza na kutazamwa kwa njia ya tamaa, kuchunwa kidogo, mgusano wa mwili bila saBabu na kutukanwa.” Mara nyingi mkazo wa kujihusisha katika ngono isiyo ya kiadili unakuwa wa werevu sana kama vile kuitwa majina ya mapenzi, (Mpenzi n.k.) au unakuwa wa wazi sana kama vile dokezo lisilofichwa. Wanawake wengine wanavumilia kusumbuliwa sumbuliwa hivyo kwa kuogopa kupoteza kazi zao. Na uchunguzi unaonyesha kwamba wanawake wachache sana hata wanaonekana kubembelezwa na uangalifu huo!

Lakini ingawa huenda uangalifu kutoka jinsia tofauti ukawa wa kubembeleza, mara nyingi kuzoeana kupita kiasi ndiko hatua inayoufungulia mchezo wa utongozi. Hivyo hilo ni ushambulizi juu ya ukamilifu wako na twezo kwa heshima yako ya Kikristo!—1 Wakorintho 6:18.

Hatua za Kuzuia

“Wakati hekima inaingia ndani ya moyo wako . . . , uwezo wa kufikiri wenyewe utaendeleza lindo juu yako, utambuzi wenyewe utalinda wewe salama.” (Mithali 2:10, 11, NW) Basi wewe unaweza kutumiaje hekima yenye mafaa na utambuzi ili kujilinda mwenyewe? Mwanamke mmoja anayefanya kazi jina lake Diane anasema: “Mimi naacha ijulikane kazini kwamba mimi ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova.” (Linganisha Mathayo 5:16.) Wakati wanaume wanapojua wewe una viwango bora vya kiadili, mara nyingi hawaelekei sana kufanya matongozi.

Mwanamke mmoja mwenye utambuzi jina lake Betty anachukua hatua nyingine ya tahadhari. Yeye anasema: “Mimi ninakuwa mwangalifu sana juu ya kushirikiana na wafanya kazi wenzangu kwa sababu adili zao haziko sawa na zangu.” (1 Wakorintho 15:33) Hiyo haimaanishi mtu ajitenge mbali au kuwa mwenye uhasama kwa wafanya kazi wenzake. Lakini wakati wao wanaposisitizia kuzungumzia mambo yenye kuudhi Mkristo, usisitesite kujiondoa kati yao. (Waefeso 5:3, 4) Kule kusikiliza tu maongezi kama hayo ya ukosefu wa adili kungeweza kuwapa wanaume kazini wazo la kwamba wewe ungeitikia matongozi yao.

Kudumisha hali ya kujiendesha kikazi kunaweza pia kuvunja moyo uangalifu usiotakwa. Pia, Biblia inashauri wanawake “wajipambe kwa mavazi ya kujisitiri, pamoja na adabu nzuri, pamoja na moyo wa kiasi.” (1 Timotheo 2:9; tofautisha Mithali 7:10.) Kinasema hivi kitabu Sexual Harassment On the Job: “Mavazi yenye kuamsha nyege za wengine—yaani, mavazi yenye mikato ya shingoni inayoteremka sana kukaribia kufichua matiti; mavazi mepesi sana yanayovaliwa wakati wa joto jingi; kaptura, marinda mafupi sana; na marembo marembo mengi mno—hayo si ya mahali pa kazi hata. . . . Nafasi zako za kufanya uwe na sura ya kikazi zinafanywa kuwa bora ukichagua kuvaa kwa njia isiyotazamisha watu.”

Hatimaye, mwanamke mwenye utambuzi anaepuka hali za kuachisha msimamo. Mwaliko wa kunywa kileo au kubaki kazini baada ya saa za kazi kwa sababu isiyo wazi huenda hata ukawa ni mtego! (Linganisha 2 Samweli 13:1-14.) “Mwenye busara huyaona mabaya na kujificha,” inasema mithali yenye hekima.—Mithali 22:3.

Kukomesha Hali ya Kusumbuliwa sumbuliwa

Bila shaka, si jambo liwezekanalo kuwazia kwamba unaweza kupangua kufikiri kwa wanaume wote kazini au kubadili violezo vya tabia vilivyoimarika kwa muda mrefu sana. (Linganisha Yeremia 13:23.) Wala si haki kukata shauri kwamba wanaume wote ambao kidogo wanaonekana wenye urafiki kupita kiasi wana “macho yenye kujaa uzinzi.” (2 Petro 2:14, NW) Kwa hiyo nyakati nyingine inafaa kutotilia watu mashaka ikiwa huna uhakika.

Lakini wakati unapokuwapo uzoelevu wa kupita kiasi ulio wazi, chukua msimamo imara. Wakati Sulemani alipoanzisha matongozi yasiyotakwa kwa mwanamwali mmoja, yeye hakujilegeza-legeza kwa haya. Yeye alijibu maneno yake ya ubembe kwa misemo ya upendo usioyumbayumba kwa mvulana mchungaji wa kiwango cha maisha ya kiasi. Kwa kuwa msichana huyo alikuwa amekataa kukubali matongozi ya Sulemani, yeye angeweza kusema, “Mimi nalikuwa ukuta.”—Wimbo Ulio Bora 8:9.

Onyesha imara ile ile. Mara nyingi matongozi yanaweza kukatiliwa mbali yakiwa yangali machanga, kwa kusema: “Usiniguse, tafadhali,” “Niite kwa jina langu,” au “Mimi sithamini ucheshi wa namna hiyo.” Mwanamke mmoja Mkristo amesema zaidi ya mara moja hivi tu, “Koma!” Kwa vyo vyote, onyesha wazi kwamba la yako inamaanisha La! (Linganisha Mathayo 5:37.) Jibu dhaifu au lisilo wazi huenda likamtia moyo msumbuaji ajaribu hata zaidi.

Ikiwa wewe umeolewa, ingekuwa vizuri kushiriki hisia zako pamoja na mume wako. Huenda yeye akawa na mawazo fulani yenye mafaa juu ya jinsi ya kushughulika na hali hiyo. Ikionekana kama inafaa zaidi ubadili kazi utafute nyingine, kumbuka ahadi ya Mungu: “Sitakupungukia kabisa, wala sitakuacha kabisa.” —Waebrania 13:5.

Kazi Yako na Ukamilifu Wako!

Kwa hiyo ingawa mara nyingi kazi ya kimwili inahitajiwa kabisa, katika visa fulani inaweza kutokeza hatari kwa ukamilifu wako wa Kikristo. Hivyo maneno ya Yesu kwenye Mathayo 10:16, NW yanafaa sana hapa: “Jithibitisheni wenyewe kuwa wenye tahadhari kama nyoka na bado kama njiwa wasio na hatia.”

Kuendeleza ukamilifu wa Kikristo mahali pa kazi si jambo rahisi, lakini kunawezekana. Maelfu ya wanawake miongoni mwa Mashahidi wa Yehova wanafanya hivyo kwa kufuata mashauri ya Biblia. Wao wanajiendeleza wakiwa na nguvu za kiroho kupitia funzo la Biblia, sala, mikutano ya Kikristo, kazi ya kuhubiri Ufalme, na utendaji mwingine wa kimungu. Matokeo ni kwamba wao wanafurahia jambo fulani wasiloweza kupewa na mshahara wo wote. Jambo hilo ni maarifa ya kujua kwamba wao wana upendeleo wa Yehova, Yeye ambaye Neno lake linaahidi hivi: “Yeye anayetembea katika ukamilifu atatembea katika usalama.”—Mithali 10:9, NW.

[Maelezo ya Chini]

a Hapa neno hili linamaanisha mwanamke aliyeajiriwa kazi ya kimwili. Bila shaka, wanawake wanaotunza mambo ya kinyumbani, akina mama, na wanawake wengine pia wanafanya kazi.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Ili Kudumisha Ukamilifu Mahali pa Kazi:

Acha ijulikane kwamba wewe una viwango bora vya kiadili

Uwe mwangalifu juu ya kushirikiana kirafiki pamoja na wafanya kazi wenzako

Jipambe kwa mavazi ya kiasi

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki