Wanawake Kazini—Majaribu na Magumu
“WANAWAKE wameingia jeshi rasmi la wafanya kazi kwa idadi zisizotangulia kuwa na mfano katika miongo mitatu iliyopita.” Hivyo ndivyo linavyoripoti tengenezo la uchunguzi linaloitwa Worldwatch Institute. “Katika nchi zilizo tajiri na maskini pia,” ripoti hiyo ikaendelea, “infuleshoni inatia moyo wanawake wafanye kazi ya malipo.” Au kama alivyoeleza mwanamke mmoja Mnaijeria: “Mkazo wa kiuchumi ni mwingi sana hivi kwamba ninalazimika kabisa kwenda nikafanye kazi.”
Kama “mke mwema” wa nyakati za Biblia, wanawake wengi wanafurahi kutoa mchango wa kiuchumi unaohitajiwa sana kwenye masilahi ya jamaa zao. (Mithali 31:10, 16, 24) Na wengine wanaona kuwa na kazi ni jambo lenye kuvutia na lenye kuridhisha. Lakini ingawa kazi ya kimwili ina manufaa fulani fulani, inaweza pia kuwa na vipingamizi.
Kwa mfano, mwanamke mmoja aliye meneja wa duka anasema: “Mimi napenda kazi yangu. Bwana mkubwa wangu ni mzuri sana, afisi yangu inapendeza. Lakini ninachukia wakati kazi hiyo inapochukua wakati mwingi kuliko ule ninaoweza kuitolea, kwa sababu baada ya hapo ninakuwa na kazi nyingine yenye kuningoja nyumbani—nikiwa mke na mama watoto.” Na bado, wanawake wengi wanatunza kazi ya kuajiriwa, nyumba, na jamaa zao kwa uhodari sana, na wanaweza kusifiwa kwa uchangamfu kwa sababu ya jambo hilo.
Ingawa hivyo, kazi za kimwili zinafungulia wanawake pia magumu kadha yanayopatikana mahali pa kazi. Kwa wengi, gumu ni kuendeleza mwelekeo uliosawazika wakati wanapolazimika kufanya kazi katika mazingira yenye mashindano makali, au yenye kujawa na ubaridi. Tamaa ya kusonga mbele, kupanda ngazi, imesukuma sana wanawake fulani wafanye kazi zao za kuajiriwa ziwe ndilo jambo kuu la kukazia maisha zao.
Nyakati nyingine mahali pa kazi ni chanzo pia cha mikazo ya kiadili. Kufunguliwa hali za kila siku zenye maongezi ya kushusha heshima ni lalamiko moja la kawaida linalotolewa na wanawake wanaofanya kazi. Na vibaya zaidi ya hivyo, wengine wanajikuta wakisumbuliwa daima kuhusiana na mambo ya ngono. “Mimi nilipoanza mara ya kwanza kufanya kazi,” anakumbuka mwanamke mmoja Mkristo, “ni mimi tu niliyekuwa msichana katika afisi. Wanaume walikuwa wakiniambia maneno ya kudokeza kwamba walinitaka, na mambo yalikuwa magumu kweli kweli kwangu.”
Magumu kama hayo ni hangaisho kweli kweli kwa wanawake wanaolazimika kuelekeana nayo kila siku, hasa wale wanaotamani kudumisha viwango vya Kikristo. Jambo la kufurahisha ni kwamba kuna chanzo cha msaada wa kweli kwao.