“Kutano Lenye Kutajirisha Kweli Kweli”
KATIKA pindi ya kiangazi cha 1984, Gerard, mwanamume kijana kutoka Ufaransa, alianza safari ya kujasiria ya miezi sita—safari ya kuendesha baiskeli kupitia United States na Kanada. Milima ya Rocky yenye fahari ilimsisimua, bustani zenye amani zilimtuliza, lakini tamasha aliyoiona katika Montmagny, Quebec, Kanada, ilimvuta zaidi; ilibadili mwendo wa maisha yake.
Jumapili, Septemba 16, Gerard alikuwa akiendesha baiskeli kupitia Montmagny alipoona mstari mrefu wa magari yaliyoegeshwa kando ya barabara. Kisha, aliona mamia ya watu waliosongamana wakitembea huku na huku katika sehemu ya ujenzi. “Ni nini linalotukia hapa?” akamwuliza mmoja wa wafanya kazi aliyekuwa akielekeza magari. Ijapokuwa mwanamume huyo alikuwa na shughuli nyingi, yeye alichukua wakati kumweleza Gerard kwamba wafanya kazi hao wote walikuwa Mashahidi wa Yehova wakitumia mwisho-juma wao kujenga jumba la mikutano yao ya kidini. Gerard bila kujua, alikuwa amefika mahali hapo katika pindi ya saa za mwisho zenye shughuli nyingi za mpango wa ujenzi wa Jumba la Ufalme wa siku mbili. Yeye alivutiwa sana na yote aliyoona na kusikia. Jioni hiyo aliandika katika kitabu chake cha matokeo ya kila siku hivi: “Jioni nilikutana na Mashahidi wa Yehova. Wamejenga nyumba katika siku mbili. Walikuwako zaidi ya 1,000. Kutano lenye kutajirisha kweli kweli.”
Muda mfupi baada ya hapo Gerard alirudi Ufaransa. Miaka miwili baadaye, Julai 26, 1986, alipeleka barua kwa posta kwa Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova katika Montmagny. Yeye aliandika hivi:
‘Je! mngali mnakumbuka mkizungumza na mwendeshaji baiskeli kutoka Ufaransa katika pindi ya siku ya pili ya mpango wenu wa ujenzi wa Jumba la Ufalme? Siku hiyo msawazishaji wa magari alipanda mbegu. Miezi fulani baadaye Mashahidi walinitembelea katika Ufaransa, nami nikakubali toleo la kujifunza Biblia pamoja nao. Kwa kuwa mimi natoka katika jamaa yenye kufuata Ukatoliki kwa nguvu sana, funzo hilo halikuwa rahisi. Lakini Yehova alifanya mbegu ikue. Majuma mawili yaliyopita nilibatizwa kwenye mkusanyiko katika Nantes. Namshukuru Yehova kwa kuniruhusu niupate ukweli, na ninashukuru kwa ajili ya yote ambayo ndugu huyo alinifundisha Jumapili hiyo, Septemba 16, 1984. Salamu za kidugu kutoka mjasiri aliyeongolewa kufuata ukweli.’
Kundi hilo katika Montmagny lilihisi furaha iliyoje kusikia barua ya Gerard ikisomwa katika Jumba la Ufalme lao! Wale wote waliosaidia katika kujenga jumba hilo waliona ukweli wa maneno ya Sulemani: “Tupa chakula chako usoni pa maji; maana utakiona baada ya siku nyingi.” (Mhubiri 11:1) Ndiyo, matokeo mazuri ya mijengo ya Majumba ya Ufalme yanadumu kwa muda mrefu na yanafika mbali katika njia nyingi.