Maswali Kutoka kwa Wasomaji
■ Je! mtu anayeweka maisha yake wakfu kwa Yehova Mungu anaweza kwa kufaa kusema juu ya jambo hilo kuwa nadhiri?
Wanadamu wanaokuja kumpenda Mungu wa kweli na ambao wanaazimia kumtumikia kabisa kabisa wanapaswa waweke maisha zao wakfu kwa Yehova kisha wabatizwe. Ingawa Biblia haitumii neno “nadhiri” kuhusiana na wakfu wa Kikristo, kufanya hivyo hakuonekani kuwa kunaweza kukatazwa.
Kitabu Aid to Bible Understanding kinaeleza kwamba Kimaandiko nadhiri ni “ahadi nzito inayotolewa kufanya tendo fulani, kutoa toleo fulani au zawadi, au kuingia katika utumishi fulani au sharti; kujifunga kwa ahadi, ama inayofaa au isiyofaa.” Nadhiri fulani za maandishi ya Kibiblia zilihusu kujifunga kwa ahadi kufuata mwendo ulioelezwa ikiwa kwanza Mungu atafanya jambo fulani. Kwa mfano, Hesabu 21:2 inasimulia hivi: “Basi Israeli akaweka nadhiri kwa [Yehova] akasema, Kama wewe utawatia watu hawa mikononi mwangu kweli ndipo mimi nitaiharibu miji yao kabisa.” (Mwanzo 28:20-22; Waamuzi 11:30-39) Bila shaka wakfu wa Mkristo wa maisha yake kwa Yehova si nadhiri kama hiyo ya masharti. Si kana kwamba yeye anasema hivi: ‘Ikiwa wewe, Yehova, utanifanya niwe mwenye furaha na ufanisi sasa na kunihakikishia mimi uzima wa milele katika mfumo mpya wa mambo, mimi naahidi kukutumikia wewe maisha yangu yote.’
Biblia inatoa nadhiri fulani kuwa hazikutafutwa na hazikuombwa. Kamusi Wilson’s Old Testament Word Studies husema juu ya neno la Kiebrania linalohusika hivi: “[na·daŕ] kutoa nadhiri, yaani, kuahidi kwa kupenda kutoa au kufanya kitu; lile wazo la msingi ni lile la kuweka kando.” Kwa hiyo mtu huweka nadhiri kwa Mungu kwa kujitolea. Hivyo inaweza kusababiwa kwamba mtu kuwa mwanafunzi wa Yesu aliye wakfu na kubatizwa hakungeweza kuwa ni nadhiri kwa sababu Mungu sasa anataka wote wanaotaka kibali chake wajiweke wakfu?a
Hata hivyo, uhakika wa kwamba Yehova ana matakwa fulani ili mtu awe rafiki yake haumaanishi kwamba hakuna uchaguzi wa kibinafsi unaohusika. Musa aliwaambia Waisraeli hivi: “Nimekuwekea mbele yako uzima na mauti, baraka na laana; basi chagua uzima, ili uwe hai, wewe na uzao wako.” (Kumbukumbu 30:19, 20; Zaburi 15:1-5; linganisha Yoshua 24:15; 1 Wafalme 18:21.) Kumbuka maneno ya Yesu: “Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha. Jitieni nira yangu, mjifunze kwangu; kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo; nanyi mtapata raha nafsini mwenu.” (Mathayo 11:28, 29) Je! Hilo ni takwa lisilo la hiari, dai? Au je! ni mwaliko unaoruhusu itikio la hiari?
Yesu alizaliwa katika taifa lililokuwa wakfu kwa Mungu; nyingi za sehemu za maisha na kifo chake zilikuwa zimetangulia kuamuliwa katika unabii; na Mungu alimtayarishia Yesu mwili autoe dhabihu. Ingawa hivyo, uamuzi wa kupenda kwa Kristo katika kujitoa mwenyewe kwa ajili ya utumishi wa pekee unaonyeshwa katika maneno yake haya: “Ndipo niliposema, Tazama, nimekuja (katika gombo la chuo nimeandikiwa) niyafanye mapenzi yako, Mungu.” (Waebrania 10:5-10) Katika njia inayofanana na hiyo, kila mtu mmoja mmoja lazima aamue kibinafsi kuwa Mkristo aliye wakfu na kubatizwa.
Kwa kuongezea, Wakristo leo wanatambua kwamba matumizi ya neno kama vile “nadhiri” hayawekewi mipaka kwa jinsi ile tu lilivyotumiwa katika Biblia. Mashahidi wa Yehova kwa muda mrefu wametumia “nadhiri za ndoa” katika arusi zinazofanywa kwa ajili ya heshima katika Majumba ya Ufalme yao.b Hiyo inalingana na maana ya ujumla ya “nadhiri,” kama vile katika fasili ifuatayo: “ahadi nzito au shughuli, hasa katika namna ya kiapo kwa Mungu.”—Oxford American Dictionary, 1980, ukurasa 778.
Kwa hiyo, haionekani kuwa lazima kuwekea mipaka matumizi ya neno “nadhiri.” Mtu anayeamua kumtumikia Mungu huenda akahisi kwamba, kwake yeye, wakfu wake usio na masharti unakuwa nadhiri ya kibinafsi —nadhiri ya wakfu. Yeye ‘anaahidi kwa uzito au anakuwa na shughuli ya kufanya jambo fulani,’ na hivyo ndivyo nadhiri ilivyo. Katika habari hii, ni kutumia maisha yake akimtumikia Yehova, akifanya mapenzi Yake kwa uaminifu. Mtu kama huyo apaswa ahisi kwa uzito jambo hilo. Inapaswa kuwa kama vile ilivyokuwa kwa mtunga zaburi, ambaye, akitaja mambo aliyokuwa ametolea nadhiri, alisema: “Nimrudishie [Yehova] nini kwa ukarimu wake wote alionitendea? Nitakipokea kikombe cha wokovu; na kulitanganza jina la [Yehova]; nitaziondoa nadhiri zangu kwa [Yehova].”—Zaburi 116:12-14; ona pia Zaburi 50:14.
[Maelezo ya Chini]
a Huo ndio msimamo uliochukuliwa katika Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) wa Oktoba 1, 1973, ukurasa 607.
b Wakati wa arusi, bibi-arusi na bwana-arusi wanawekeana nadhiri, lakini pia wanafanya hivyo mbele ya mashahidi na machoni pa Mungu.