Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w87 7/1 kur. 26-31
  • Kukaa Karibu Sana na Tengenezo la Yehova

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kukaa Karibu Sana na Tengenezo la Yehova
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Ubora wa Mazoezi ya Mapema
  • Kuwezana na Tatizo la Kibinafsi
  • Msiba Katika Jamaa Waniathiri Mimi
  • Kuingia Utumishi wa Wakati Wote
  • Mapendeleo ya Utumishi
  • Kurudia Utumishi wa Betheli
  • Mahusiano Yenye Thamani Kubwa
  • Kutumikia Kwenye Makao Makuu ya Ulimwengu
  • Miaka Sabini ya Kushikilia Upindo wa Nguo ya Mtu Aliye Myahudi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2012
  • “Kutafuta Kwanza Ufalme”
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Usitawi wa Muundo wa Tengenezo
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Yehova Amenifundisha Tangu Ujana Wangu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2003
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
w87 7/1 kur. 26-31

Kukaa Karibu Sana na Tengenezo la Yehova

Kama ilivyosimuliwa na John Barr

NILIKUWA kwenye sehemu ya mwisho ya ziara yangu nyumbani mwaka uliopita mwezi Juni uliopita, nikisafiri kwa ndege kutoka Glasgow kwenda Aberdeen. Ndege yetu ilikuwa ikipanda kwa kuinuka sana juu ya nchi yenye mashamba ya rangi ya chanikiwiti ya Kiskochi na juu ya Mto Clyde wenye kutiririka kizembe-zembe, mawazo yangu yalirudi nyuma haraka sana kwenye mwaka 1906 na kwenye kijiji hicho cha Bishopton, kilichoegemea mahali fulani chini kule kusini mwa mto huo.

Waona, huo ndio mwaka na mahali ambapo nyanya yangu Emily Jewell, alianza kusoma kitabu cha Charles T. Russell, The Divine Plan of the Ages. Mara moja macho yake yalifunguliwa akaona ukweli kwamba Biblia haikufundisha lile fundisho la kidini la moto wa mateso. Upesi binti zake wawili waliokuwa watu wazima Bessie na Emily (wa pili akawa mama yangu) pia wakaanza kuona nuru ya ukweli ikiangaza kwa kupenya ukungu wa mafundisho ya kidini ya uwongo yaliyofundishwa na United Free Church ya Scotland. Katika 1908 Nyanya alibatizwa katika wonyesho wa wakfu wake ili kufanya mapenzi ya Mungu, na binti zake walibatizwa muda mfupi baada ya hapo.

Baba yangu ndiye aliyekuwa karani wa kipindi katika kanisa ilo hilo la United Free Church katika Bishopton. Sikuzote yeye alikuwa ameliona kuwa jambo gumu kukubali fundisho la Utatu, kwa hiyo mhudumu wa kanisa hilo akajitolea kuhubiri mahubiri ya pekee kwa manufaa yake Jumapili moja. Hilo ndilo lililomweza! Aliposikia jaribio hilo la kulieleza, baba yangu sasa akasadikishwa kwamba hilo fundisho la Utatu lilikuwa si la kweli. Alijiuzulu kutoka kanisa hilo na akabatizwa katika 1912 katika wonyesho wa wakfu wake kwa Yehova. Muda mfupi baada ya hapo wazazi wangu walihamia kaskazini mwa Aberdeen pamoja na watoto wao wawili, Louie na James, nami nikazaliwa huko katika 1913.

Mawazo yangu juu ya miaka hiyo ya mapema na juu ya jitihada za wazazi wangu za kutulea sisi watoto watatu “katika nidhamu na rekebisho la moyoni la Yehova” yalikaa pamoja nami ndege yetu ilipoanza kushuka juu ya vilima, mito, na mabonde ambayo nilikuwa nimejua tangu utotoni. (Waefeso 6:4, NW) Katika asubuhi hii nzuri yenye jua, nilihisi kumshukuru Yehova kama nini kwa mazoezi hayo ya wazazi! Nilijua kwamba yalikuwa yamenisaidia nibaki sikuzote karibu sana na tengenezo la Yehova.

Ubora wa Mazoezi ya Mapema

Sikuzote jamaa yetu ilikuwa na furaha ya kuwa yenye umoja. Ikiwa wakati wo wote Baba na Mama walipata kuwa na tofauti za maoni, walijaribu kutoonyesha kamwe mbele yetu sisi watoto. Hilo lilijenga ndani yetu sisi si heshima tu kwa wazazi wetu bali pia mazingira ya imani na usalama halisi ndani ya nyumba yetu.

Baadhi ya kumbukumbu ninazopenda sana zinahusu vikusanyiko vya tafrija vya jamaa yetu katika jioni nyingi. Tulitoa tafrija zetu wenyewe, tukifanya mambo kama vile kuimba kufuatana na chombo cha muziki tulichopiga sisi wenyewe na kucheza pamoja michezo ya mbao kama vile Monopoli. Pia, hata Baba awe alikuwa na shughuli nyingi namna gani, yeye hakushindwa kamwe kutumia wakati pamoja nasi karibu kila siku, akisoma kwa sauti kutoka Biblia na vichapo vya Sosaiti, pamoja na vichapo vingine vya mambo mepesi na pia vya mambo mazito zaidi. Mambo haya yote yalitumika kuifanya jamaa yetu ifungamane pamoja kadiri tulivyoendelea kukua.

Tulikuwa sisi ndio jamaa ya “ukweli” pekee katika sehemu hiyo ya kaskazini ya Scotland katika miaka hiyo ya mapema. Kama matokeo, makao yetu yakaja kujulikana na wengi wa wawakilishi wenye kusafiri (wahaji, kama walivyojulikana wakati huo) wa Sosaiti, kama vile Albert Lloyd, Herbert Senior, na Fred Scott. Wengine hata walikuja kutoka makao makuu ya Sosaiti katika Brooklyn, New York, kutia na W. E. Van Amburgh na A. H. Macmillan. Ziara hizo zilikuwa vipimo vya maendeleo katika miaka yangu ya mapema.

Kufikia siku hii mimi huhisi kuwa mwenye shukrani sana kwa roho halisi ya ukaribishaji-wageni iliyoonyeshwa na wazazi wangu. Jambo hilo lilitajirisha sana maisha ya jamaa yetu, na ingawa nilikuwa mchanga, nilianza kupanuka katika uthamini wangu wa ushirika mzima wa ndugu. Lo! jinsi wazazi wanavyoweza kufanya mengi katika kusitawisha kifungo cha upendo chenye uchangamshi baina ya watoto wao na ushirika wa ulimwenguni pote wa ndugu zao!

Kuwezana na Tatizo la Kibinafsi

Nilipokuwa nikiingia katika miaka yangu ya mapema ya utineja, nikawa mvulana mwenye kuzidi kuwa na haya na kujitenga na watu wengine. Kadiri nilivyoendelea kukua ndivyo nilivyozidi kuona ugumu wa kukutana na watu wengine na kuzungumza pamoja nao. Hali hii ya kuona haya ilitokeza kizuizi kikubwa katika njia nyingi lakini hasa ikawa hivyo kuhusu kuthibitisha wonyesho wa imani yangu wa kuhubiri habari njema za UfaIme.

Muda mfupi baada ya Vita ya Ulimwengu ya Kwanza nyanya na mama yangu wakawa Mashahidi wa kwanza katika Aberdeen kushiriki katika huduma ya nyumba kwa nyumba. Sisi watoto tulishiriki katika kugawa trakti, lakini sasa, kwangu mimi kuzungumza hasa na watu kwenye nyumba zao—lo, hilo likawa jambo tofauti kabisa! Huo ulikuwa mwito wa ushindani kweli kweli! Lakini mwishowe niliukubali. Sitasahau kamwe alasiri ya Jumapili hiyo katika Novemba 1927 nilipomwambia baba yangu kwamba ningeambatana naye katika huduma ya nyumba kwa nyumba. Ulikuwa ndio wakati wa kwanza kwangu kupata kuona machozi katika mashavu ya babangu—katika kisa hiki ni machozi ya furaha!

Msiba Katika Jamaa Waniathiri Mimi

Hali tulivu yenye amani ya maisha ya jamaa yangu ilivunjwa-vunjwa jioni ya Juni 25, 1929, nilipokuwa wa miaka 16. Baada ya siku nzima katika huduma, mama yangu na dada yangu walikuwa wakiharakisha kurudi nyumbani wakamtayarishie Baba chakula cha jioni. Ghafula, pikipiki yenye mwendo wa kasi sana ilimgonga mama, na kumburuta barabarani kwa mwendo wa karibu meta 37. Majeraha ya kichwa yalikuwa mabaya sana hivi kwamba hakutazamiwa kuendelea kuishi. Lakini shukrani kwa miezi mingi ya uangalizi wa upendo ya dada yangu Louie, mama alipona. Baadaye, Mama aliweza kuwa na maisha ya kawaida kwa kulinganisha mpaka kifo chake katika 1952.

Ono hilo lenye kuumiza sana lilifanya jambo la maana sana kwangu—lilinifanya nifikirie kwa uzito sana maisha yangu na kile nilichokuwa nikifanya nayo. Kiangazi hicho nilianza kujifunza Biblia kwa kina kirefu zaidi ya nilivyokuwa nikifanya hapo kwanza —nilifanya ukweli kuwa wangu mwenyewe. Hiyo ndiyo iliyokuwa pindi kubwa ya badiliko katika maisha yangu, nami niliweka maisha yangu wakfu kwa utumishi wa Yehova. Hata hivyo, haikuwa mpaka baada ya miaka kadha kwamba nilipata nafasi ya kuonyesha wakfu wangu kwa ubatizo wa maji.

Kuingia Utumishi wa Wakati Wote

Nilipomaliza shule katika 1932, nilianza mtaala wa mazoezi katika uhandisi wa mashine na umeme. Katika Uingereza siku hizo hakukuwa na kile kitia-moyo kilicho leo kwa vijana waingie kwenye kazi ya wakati wote ya kuhubiri wakiwa mapainia. Lakini, kadiri miaka ilivyopita, nilijua ni mahali gani nilipopaswa kuwa nikitumia nishati zangu—katika huduma ya wakati wote.

Nakumbuka kwa wazi sana jambo fulani tulilojifunza mapema katika 1938 ambalo lilikaza ndani yangu manufaa ya kukaa karibu sana na tengenezo la Yehova na kutumia kibinafsi maagizo yalo. Lilikuwa toleo la gazeti la Mnara wa Mlinzi kuhusu Yona lililoeleza maono aliyoyapata katika kutoroka kutoka mgawo wake wa utumishi. Nilizingatia moyoni sana somo hilo, nikafanya uamuzi kwamba sitakataa kamwe mgawo wo wote unaonijia kupitia tengenezo la Yehova. Wakati huo sikujua sana juu ya migawo mingi ya kitheokrasi iliyokuwa mbele yangu ya kujaribu azimio langu.

Nilisali nipate mwongozo, nalo jibu likaja kwa njia ya barua yenye kushangaza kutoka makao makuu ya Sosaiti katika London, ikiniomba nifikirie uwezekano wa kuwa mshiriki wa jamaa ya Betheli. Nilishika kwa shauku nafasi hiyo ya kuingia kupitia mlango mkubwa uongozao kwenye mapendeleo makubwa zaidi ya utumishi. Hivyo, katika Aprili 1939 nilijikuta mwenyewe nikifanya kazi pamoja na Harold King, ambaye baadaye alitumikia akiwa mmisionari katika China na, kwa sababu ya utendaji wake wa kuhubiri, akatumika miaka mingi katika gereza la kikomunisti. Tulifanya kazi ya kuunganisha vinanda vilivyotumiwa kupigia sahani za santuri zenye mahubiri yaliyorekodiwa kwenye milango ya nyumba za watu.

Harold na mimi tuliwazia aina zote mbali-mbali za watu ambao mwishowe wangesikiliza ujumbe wa Ufalme kupitia vifaa tulivyokuwa tukifanyiza. Katika njia hii hatukukosa kamwe kuona tokeo la mwisho la kazi yetu. Tangu hapo, katika migawo yote mbalimbali ambayo nimepewa katika Betheli, nimejitahidi kudumisha maoni hayo. Jambo hilo limefanya kazi yangu iwe yenye furaha halisi na sikuzote kuwa yenye maana kuhusiana na kazi ya kuhubiri Ufalme.

Mapendeleo ya Utumishi

Muda mfupi baada ya kufika Betheli ya London, niliwekwa kuwa mtumishi wa kampani (anayeitwa sasa mwangalizi msimamizi) wa kundi lililokuwa na wahubiri zaidi ya 200. Kabla ya hapo nilikuwa nimekuwa mwangalizi wa kundi la wahubiri kumi tu! Kisha nikawekwa nisimamie Idara ya Vikuza-Sauti kwa mkusanyiko mzuri ajabu wa nchini pote uliofanyiwa Leicester katika 1941. Kufikia wakati huo nilikuwa nimekuwa na ujuzi mchache tu kuhusiana na vikuza-sauti.

Baadaye nilipewa mgawo wa kazi ya kusafiri nikiwa mtumishi wa akina ndugu, anayeitwa sasa mwangalizi wa mzunguko. Kulikuwako watumishi kama hao sita tu katika Uingereza kazi hiyo ilipoanzishwa katika Januari 1943. Mgawo wangu ulikuwa ule wa mwezi mmoja tu, lakini hatimaye ukawa kwamba nilitembelea makundi kwa zaidi ya miaka mitatu. Katika pindi iyo hiyo ya miaka migumu ya Vita ya Ulimwengu ya Pili, nilisimamia mikusanyiko mitatu mikubwa—jambo ambalo nilikuwa sijapata kufanya kabla ya hapo.

Kazi ya kusafiri katika siku hizo ilikuwa tofauti kabisa na ilivyo leo. Sikuzote tulikuwa katika mwendo, na kusafiri katika nchi yote ya Uingereza katika pindi hiyo ya miaka ya vita nyakati nyingine lilikuwa jambo gumu sana. Zaidi ya pindi moja nililazimika kutumia baiskeli kwa sehemu ya safari kati ya makundi. Badala ya kutembelea kundi moja kwa juma moja kama wanavyofanya leo waangalizi wasafario, ikiwa makundi yalikuwa madogo, tungetembelea mengi kufika sita katika juma moja!

Hapa pana mfano wa iliyokuwa ratiba ya siku moja: Unaamka saa 11:30 karibu na alfajiri, na baada ya kiamshakinywa, usafiri kwenye kundi linalofuata ili uanze kukagua maandishi ya kundi kuanzia saa 2 asubuhi. Kwa kawaida alasiri ilitumiwa katika huduma ya shambani, hii ikifuatwa jioni na mkutano wa saa moja pamoja na watumishi wa kundi na kisha hotuba kwa kundi. Ni mara chache nilipoweza kwenda kulala kabla ya saa 5 usiku au hata baadaye ikiwa niliandika ripoti ya siku hiyo juu ya kundi jioni iyo hiyo. Kila Jumatatu iliwekwa kando kwa ajili ya kumaliza ripoti za juma hilo, kwa funzo la kibinafsi, na kwa kazi yo yote ya matayarisho kwa juma linalofuata.

‘Ni ratiba ya juma lenye shughuli nyingi sana,’ wewe wasema? Ndiyo, ilikuwa hivyo, lakini, lo! lilikuwa jambo lenye kuthawabisha kama nini kuhisi kwamba tulikuwa tukitia nguvu ndugu katika pindi hiyo ya miaka ya vita wakati ambapo sikuzote hakukuwa na mawasiliano ya karibu-karibu kama ilivyo sasa pamoja na tengenezo! Katika maana halisi sana, tulikuwa na uradhi wa kuhisi kwamba tulikuwa tukisaidia makundi ‘yatiwe nguvu katika ile imani.’—Matendo 16:5.

Kurudia Utumishi wa Betheli

Niliombwa nirudie utumishi wa Betheli katika Aprili 1946. Nilifurahia kufanya hivyo, lakini nilihisi kwamba maisha yangu yalikuwa yametajirishwa kiroho kama matokeo ya miaka hiyo mitatu na nusu katika kazi ya kusafiri. Tengenezo lilimaanisha mengi zaidi kwangu sasa, na nilihisi kana kwamba nilikuwa nikifanya yale yaliyoelezwa kwenye Zaburi 48:12, 13: “Tembeeni katika Sayuni, uzungukeni mji, ihesabuni minara yake. . . . Yafikirini [kagueni, NW] majumba yake.” Kuwa kuwa nilikuwa nimetembea miongoni mwa watu wa Mungu na kukuza upendo wangu kwa “ushirika mzima wa ndugu.”—1 Petro 2:17, NW.

Kufuata kurudia kwangu Betheli, nilipendelewa niangalie nyingi ya kazi ya kupiga chapa iliyofanywa kwenye mashine zetu za kupiga chapa katika London na baadaye nikashughulika na kazi ya kufanya mabamba pia. Ndipo, katika Septemba 1977 nikatolewa lile pendeleo la pekee sana la kuwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova, lililoko Brooklyn, New York, U.S.A.

Ni lazima nikiri kwamba nyakati nyingine nilihisi kama ‘nikitoroka’ baadhi ya migawo niliyopewa iliyokuwa migumu zaidi. Lakini ndipo ningemkumbuka Yona na lile kosa alilofanya, na ningejirudia mwenyewe ile ahadi nzuri ajabu inayopatikana kwenye Zaburi 55:22: “Umtwike [Yehova, NW] mzigo wako naye atakutegemeza, hatamwacha mwenye haki aondoshwe milele.” Nimeona maneno hayo yakiwa kweli kama nini!

Yehova hamuulizi ye yote wetu kamwe kufanya jambo fulani ambalo yeye anajua hatutaliweza. Hata hivyo, ni katika nguvu zake tu kwamba tunawezeshwa kufanya yale anayotuomba tufanye. Na jambo jingine—ikiwa unapenda kikweli ndugu zako wanaofanya kazi pamoja nawe, watakuunga mkono na kukutegemeza, wakifanya kazi pamoja nawe “bega kwa bega” ili wakusaidie utimize furushi la mgawo wako.—Sefania 3:9.

Mahusiano Yenye Thamani Kubwa

Bila shaka, sikuzote kuna ndugu Wakristo ambao unahisi kuwa na ufungamano wa pekee pamoja nao. Mmoja wa hawa alikuwa Alfred Pryce Hughes, ambaye alikufa katika 1978. Simulizi la maisha yake lilitokea katika toleo la Aprili 1, 1963, la Mnara wa Mlinzi (Kiingereza). Kwa miaka mingi alitumika akiwa mshiriki wa Halmashauri ya Tawi. Yeye alipendwa sana sana na ndugu katika shamba la Uingereza kwa sababu ya heshima yake kubwa na ushikamanifu kwa tengenezo la Yehova na upendo wake kwa ndugu wote. Jambo jingine lilikuwa upendo wake kwa huduma ya shambani. Huo haukupungua kamwe muda wote wa maisha yake, hata awe alilazimika kuchukua daraka gani. Kufanya kazi pamoja na ndugu waaminifu kama Pryce kumemaanisha mengi sana kwangu, kukitia nguvu azimio langu la kukaa karibu sana na tengenezo la Yehova na kubaki nikiwa mtendaji katika huduma.

Kwenye Oktoba 29, 1960, niliingia katika uhusiano wenye thamani kubwa sana pamoja na painia mwenye bidii na mmisionari wa muda mrefu wa darasa la 11 la Gileadi, ambaye wakati huo alikuwa akitumikia katika Ailandi. Kwenye tarehe hiyo Mildred Willett na mimi tulioana, na tangu hapo yeye amekuwa msaidizi mwaminifu kwangu katika utumishi wa Betheli.

Kabla ya mama ya Mildred kufa katika 1965, yeye alimshauri binti yake ‘asimwonee wivu Yehova.’ Sikuzote Mildred amekumbuka maneno ya mama yake, na hilo limesaidia kumzuia asikose kuridhika wakati ninapolazimika mara nyingi kufanya kazi ya ziada. Hilo limesaidia sana kuangalia kwa furaha migawo yangu ya kazi iliyoongezeka ambayo imenijia. Sote wawili tumefurahia hasa kushiriki mambo mengi yenye kuthawabisha tuliyoona katika huduma.

Mume na mke vijana tuliojifunza Biblia pamoja nao, kwa mfano, walifanya maendeleo ya haraka kufikia hatua ya wakfu na ubatizo na wakashiriki kwa ukawaida huduma. Tulipendezwa kama nini! Kisha, ghafula, bila sababu yo yote iliyo wazi, wakaacha kuwa washiriki. Mildred na mimi tulishiriki kukatishwa tamaa huko, nasi tuliendelea kujiuliza ni wapi tulipokuwa tumekosea katika kuwazoeza. Tuliendelea kusali kwa Yehova kwamba bado angefungua mioyo yao wathibitishe upendo wao kwa ajili ya ukweli. Je! waweza kuwazia furaha yetu tulipopokea barua kutoka watu hao wawili kama miaka kumi baadaye wakituambia kwamba walikuwa washiriki tena wenye kutenda na kwamba nyumba yao ilikuwa sasa kituo cha funzo la kitabu?

Mumeye Will aliandika hivi: “Nataka kuwashukuru ninyi kwa msaada wote na fikira zenye upendo mlizotuandalia sisi. . . kuanguka kwangu kulikuwa makosa yangu, uthamini wa moyo wangu haukuwa sawa . . . tumepata furaha nyingi kwa kurudi katika tengenezo la Yehova . . . Ninawaandikia usiku huu nikiwa na kumbukumbu za mambo yenye kupendeza sana, Yehova na aendelee kuwabariki ninyi wawili katika utumishi wenu kwake.”

Katika barua nyingine, mama mmoja alituandikia kuhusu mvulana wake Mike: “Mimi nina furaha sana kwamba malaika walimkalisha kando yenu.” Alikuwa akimaanisha nini? Basi, Mike alikuwa amekuja kwenye mkusanyiko pamoja na mama yake na ndugu mchanga, lakini yeye hakuwa amependezwa sana na ukweli. Mildred alimwona mvulana huyo akiwa anakaa peke yake na akaongea naye. Kisha tukamwalika yeye na ndugu yake mchanga waje Betheli ya London na kuona kazi tuliyofanya.

Baadaye, Mike alikuja, na yale aliyoona yakawasha kupendezwa kwake vya kutosha kuendelea kuwa na funzo la Biblia. Matokeo yakawaje? Sasa yeye ni mzee katika kundi, na mke wake na wavulana wawili wote ni watendaji katika huduma. Wakati fulani uliopita, mke wa Mike aliandika, “[Mike] amekuwa akitaja mara nyingi kuwa akikutana na ninyi wawili . . . Namna alivyovutiwa na fadhili na kupendezwa kwenu katika yeye.”

Wakati mke wangu na mimi tunapopokea maneno ya kuthamini kutoka mtu fulani kama Will au Mike ambao tumependelewa kusaidia, mioyo yetu inafurika ushukurifu kwa Yehova! “Barua zenye sifa” zilizo hai ni thawabu zenye bei kubwa kama nini—zote zikiwa sehemu ya furaha iliyopokewa kwa kukaa karibu sana na tengenezo la Yehova.—2 Wakorintho 3:1-3.

Kutumikia Kwenye Makao Makuu ya Ulimwengu

“Taifa kwa lenyewe.” Ndivyo mhariri mmoja wa gazeti la Brooklyn Heights alivyoeleza jamaa kubwa ya zaidi ya Mashahidi 3,500 wanaoishi kwenye makao makuu ya ulimwengu ya Mashahidi wa Yehova katika Brooklyn, New York, na kwenye Mashamba ya Sosaiti yalioko umbali wa karibu kilometa 160 kaskazini mwa jimbo la New York. Kwa kweli, wapakwa-mafuta wa Yehova ni taifa la kiroho machoni pa Yehova! Leo, umati mkubwa kutoka mataifa mengi ya ulimwengu wanajitokeza na kusema kwa wale wa taifa hili hivi: “Tutakwenda pamoja nanyi, kwa maana tumesikia kwamba Mungu yu pamoja nanyi.”—Zekaria 8:23; 1 Petro 2:9.

Basi, je! unaweza kuthamini jinsi lilivyokuwa jambo lenye kusisimua kwa mke wangu na mimi kuwa sehemu ya kudumu ya jamaa hii kubwa ya Betheli? Ningeweza kusema bila kusita ko kote kwamba ile miaka minane ya mwisho ya maisha yangu imekuwa ndiyo yenye kutokeza zaidi sana katika maono yangu yote ya kitheokrasi. Hapa unahisi mpigo-pigo wa tengenezo lionekanalo la Yehova; hapa chakula cha kiroho kinatayarishwa na kisha kupelekwa nje kwenye zile pembe nne za dunia; hapa unaona roho ya Yehova ikitenda kazi ikielekeza na kuongoza maamuzi yenye maana kubwa ambayo lazima yafanywe; na hapa unaona zaidi ya mahali penginepo pote ushuhuda wenye kuongezeka wa baraka ya Yehova juu ya kazi ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi. Mambo yote hayo niliyoona na kutia moyoni hivi karibuni yamenipa kichocheo zaidi cha kukaa karibu hata zaidi na watu wa Yehova.

Nimesimulia mambo machache tu niliyoona katika maisha yangu. Hata hivyo, huenda yakakusaidia ufahamu kwa sababu gani, ndege yangu ilipotua mwishowe kwenye Uwanja wa Ndege wa Aberdeen asubuhi hiyo ya Juni yenye jua, nilihisi kuwa na shukrani sana kwa Yehova kwamba nilikuwa ningali sehemu ya ushirika wetu wa ndugu ulimwenguni pote wenye upendo. Nilikuwa nimetumia wakati wa kuruka kwa ndege nikijikumbusha juu ya miaka yangu katika ukweli, na hilo lilinikumbusha kwa mara nyingine tena jinsi lilivyo jambo lenye manufaa kwetu kusimulia pindi kwa pindi baraka zetu nyingi tunazopokea kutoka mkono wa Yehova.—Zaburi 40:5.

Dada yangu, Louie alikuwa hapo kunisalimu—akiwa angali mwaminifu, mwenye bidii, na mshikamanifu baada ya zaidi ya miaka 60 ya utumishi wa wakfu kwa Yehova. Nilimshukuru Yehova kwa baraka hiyo ya ziada, kwa kuwa je! mtume Paulo hakusema kwamba uaminifu ndio Yehova anatazamia katika “mawakili” wake wote? (1 Wakorintho 4:2) Ni kitia-moyo kikubwa kama nini ambacho mshiriki mmoja wa jamaa anaweza kumpa mwingine kwa kubaki akiwa mwaminifu!

Musa wakati mmoja alisali hivi: “Utujulishe kuzihesabu siku zetu, tujipatie moyo wa hekima.” (Zaburi 90:12) Kadiri Mildred nami tunavyozidi kuzeeka, tunathamini uhitaji wa sikuzote kutegemea hekima ya Yehova ili tutumie maisha zetu katika njia inayoonyesha upendo wetu kwake na ndugu zetu. Kwa upendo Yehova anatuonyesha sisi njia hiyo ikiwa tunakaa karibu sana na tengenezo lake.

[Picha katika ukurasa wa 28]

John Barr (mbele kushoto) karibu mwaka 1930, akiwa pamoja na dada yake, ndugu, na wazazi

[Picha katika ukurasa wa 31]

John Barr leo, akiwa pamoja na mke wake Mildred

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki