Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w87 11/1 kur. 10-12
  • “Ni Lazima Ninyi Mwe Watakatifu . . . ”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Ni Lazima Ninyi Mwe Watakatifu . . . ”
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Mungu Mtakatifu, Waabudu Watakatifu
  • ‘Ile Sheria Ni Takatifu, Adilifu, na Njema’
  • “Amri ya Yehova Ni Safi”
  • Wasafi Katika Ulimwengu Usio Safi
  • Kukamilisha utakatifu Katika Kumhofu Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
  • Watu Waliosafishwa kwa Ajili ya Kazi Zilizo Bora
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2002
  • Lazima Mwe Watakatifu Kwa Sababu Yehova Ni Mtakatifu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • “Mtakatifu, Mtakatifu, Mtakatifu, Ni Bwana”
    Mkaribie Yehova
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
w87 11/1 kur. 10-12

“Ni Lazima Ninyi Mwe Watakatifu . . . ”

“Kupatana na Mtakatifu aliyewaita, ninyi pia iweni watakatifu wenyewe katika mwenendo wenu wote, kwa sababu imeandikwa: ‘Ni lazima ninyi mwe watakatifu, kwa sababu mimi ni mtakatifu.’”​—1 PETRO 1:15, 16, NW.

1, 2. (a) Ni kikumbusha gani kilichowekwa kuwa wonyesho juu ya kilemba cha kuhani mkuu, nacho kilitumikia kusudi gani? (b) Ni kwa sababu gani kikumbusha cha utakatifu wa Yehova kinafaa leo? (c) Ni onyo gani la upole ambalo Petro anatoa kuhusu utakatifu?

“UTAKATIFU ni wa Yehova.” Maneno haya yenye kuchochea yaliwekwa wazi yaonekane kwa wote, yakiwa yamenakishiwa juu ya kipande cha dhahabu safi kilichofungiwa kwenye kilemba ambacho kilivaliwa na kuhani mkuu wa Israeli. (Kutoka 28:36-38, NW) Hayo yalitumika kuwa kikumbusha chenye kumetameta kwamba tofauti na mataifa ya kipagani ambayo yaliabudu miungu michafu, Israeli waliabudu Mungu safi, mtakatifu.

2 Ikiwa tayari wewe ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova, je! wewe unathamini jinsi hasa yule Mungu ambaye wewe unaabudu alivyo safi, bila uchafu, mtakatifu, na mwadilifu? Kikumbusha cha ukweli huo wa msingi huenda kikaonekana kuwa hakihitajiwi kabisa hata kidogo. Ingawaje, tukiwa watu wa Yehova, sisi tumebarikiwa kuwa na mwono wa ndani wa “yale mambo yenye kina kirefu ya Mungu”—maunabii ya Biblia yaliyo magumu kufahamika, utumizi wa kanuni za Biblia, fundisho la Biblia. (1 Wakorintho 2:10, NW; linganisha Danieli 12:4.) Hata hivyo, inaonekana wazi kwamba uthamini wa kutoka moyoni wa utakatifu wa Yehova unakosekana upande wa wengine. Kwa sababu gani? Kwa sababu kila mwaka maelfu wanarudia namna namna za ukosefu wa adili. Maelfu mengine mengi wanakaribisha balaa kwa kujitia katika vitendo ambavyo vinakaribia sana kuwa uhalifu wa sheria ya Biblia. Kwa wazi, wengine hawafahamu kabisa uzito wa yale maneno kwenye 1 Petro 1:15, 16, NW: “Kupatana na Mtakatifu aliyewaita, ninyi pia iweni watakatifu wenyewe katika mwenendo wenu wote, kwa sababu imeandikwa: ‘Ni lazima ninyi mwe watakatifu, kwa sababu mimi ni mtakatifu.’”

Mungu Mtakatifu, Waabudu Watakatifu

3. Ni chini ya hali gani Musa alimweleza Yehova kuwa mtakatifu?

3 ‘Mtu asiyekamilika—awe mtakatifu? Haiwezekani!’ huenda wewe ukasema. Hata hivyo, fikiria hali ambayo katika hiyo onyo la upole la Petro lilitolewa. Hapa mtume huyo alinakili maneno ambayo kwanza yalielekezwa kwa Israeli muda mfupi baada ya kule Kutoka Misri. Kupitia huu ukombozi wa kimuujiza, Yehova alikuwa amefunuliwa kuwa Mkombozi, Mtimiza-ahadi, “mtu wa kiume wa vita.” (Kutoka 3:14-17; 15:3, NW) Katika wimbo wa kuadhimisha anguko la ghafula la Wamisri kwenye ile Bahari Nyekundu, Musa sasa akafunua bado upande mwingine wa Yehova: “Ni nani miongoni mwa miungu aliye kama wewe, O Yehova? Ni nani aliye kama wewe, mwenye kujihakikisha kuwa hodari katika utakatifu?” (Kutoka 15:11, NW) Hii ndiyo pindi ya kwanza iliyorekodiwa ambayo katika hiyo utakatifu unahesabiwa kwa Yehova.

4. (a) Ni katika njia gani Yehova ni ‘hodari katika utakatifu’? (b) Hivyo Yehova alitofautianaje na miungu ya Kanaani?

4 Maneno ya Kiebrania na Kigiriki yanayotafsiriwa “-takatifu” katika Biblia hufunua wazo la kuwa ‘-angavu, -pya, -bichi, bila doa, na safi.’ Hivyo Musa alimweleza Yehova kuwa safi katika kiwango cha juu zaidi sana, asiye na hali yo yote isiyo safi, asiyeweza kufisidiwa, asiyeacha kutovumilia uchafu. (Linganisha Habakuki 1:13.) Hivyo Yehova alisimama katika utofautiano wenye kung’aa na ile miungu ya nchi ambayo wao karibuni wangekaa—Kanaani. Hati zilizofukuliwa katika Ras Shamra, mji ulioko kaskazini mwa pwani ya Shamu, hutoa mtazamo wa kiasi tu, lakini hata hivyo wenye kuelimisha, ndani ya jamii yote ya miungu ya Wakanaani. Maandishi haya yanaeleza miungu ambayo ilikuwa “yenye ubishi, wivu, kulipa kisasi, ashiki,” kulingana na kitabu The Canaanites cha John Gray.

5, 6. (a) Kuabudu miungu mifasiki kulikuwa na matokeo gani juu ya Wakanaani? (b) Kuabudu Mungu mtakatifu kulikuwa na matokeo gani juu ya Waisraeli?

5 Kwa kutabirika, utamaduni wa Kikanaani ulionyesha sifa za miungu mifasiki ambayo wao waliabudu. Chaeleza kichapo The Religion of the People of Israel: “Matendo katika kuiga miungu yalionwa kuwa utumishi kwa hiyo miungu. . . . [Yule mungu-mke wa ngono] Astarti alikuwa na hesabu fulani ya watumishi wanaume na wanawake ambao walielezwa kuwa watu waliowekwa wakfu . . . Wao walijiweka wakfu wenyewe katika utumishi wake kwa umalaya.” Anaongeza mwanachuo William F. Albright: “Wakati wa kiwango chao kilicho kibaya zaidi sana, hata hivyo, ule upande wa kushushwa kwa maadili ya dhehebu lao lazima uwe ulishuka kwenye vina vibaya sana kupita kiasi vya ufasiki wa kijamii.” Ile ibada ya kiungo cha uzazi cha kiume ya “maashera,” kudhabihu watoto, uganga, kupiga mafundo, ngono za kiukoo, usodoma, na ugoni-mnyama—yote hayo yakaja kuwa ‘ile njia ya nchi’ katika Kanaani.—Kutoka 34:13; Walawi 18:2-25, NW; Kumbukumbu 18:9-12.

6 Yehova, kwa upande mwingine, ni ‘hodari katika utakatifu.’ Yeye hangeweza kuvumilia kushushwa huku kwa maadili katika waabudu wake. (Zaburi 15) Kwa hiyo, tofauti na miungu hiyo ya Wakanaani yenye kushusha maadili, Yehova alikweza watu wake. Akinena maneno ambayo Petro angenakili baadaye, Yehova kwa kurudia-rudia alisihi hivi: “Inawapasa ninyi kujithibitisha wenyewe kuwa watakatifu, kwa sababu mimi Yehova Mungu wenu ni mtakatifu.”—Walawi 19:2; 11:44; 20:26, NW.

‘Ile Sheria Ni Takatifu, Adilifu, na Njema’

7, 8. (a) Waisraeli ‘wangejithibitishaje wenyewe kuwa watakatifu’? (b) Tofautisha Sheria ya Yehova na Fungu la Sheria la Hammurabi la Kibabuloni.

7 ‘Kujithibitisha wenyewe kuwa watakatifu’ hakukumaanisha wala ukamilifu wala kujifanya kwa njia isiyo ya kweli kuwa mtu wa dini; kulimaanisha utii kwa fungu la sheria lenye sheria nyingi walilopewa Israeli kupitia Musa. (Kutoka 19:5, 6) Tofauti na sheria nyingineyo yote ya kitaifa, Sheria ya Mungu ingeweza kuelezwa kuwa “takatifu na ya uadilifu na njema.”—Warumi 7:12, NW.

8 Ni kweli, Fungu la Sheria la Kibabuloni la Hammurabi, ambalo lasemekana kuwa lilitangulia kwa wakati Sheria ya Musa, lilizungumzia habari nyingi kadiri iyo hiyo. Baadhi ya amri hizo, kama vile ile sheria ya ‘jicho kwa jicho’ au talioni, zinafanana na kanuni za Musa. Hivyo wachambuzi hudai kwamba Musa aliazima tu sheria zake kutoka kwa fungu la sheria la Hammurabi. Fungu la sheria la Hammurabi, hata hivyo, halikufanya jambo lililo zaidi ya kumtukuza Hammurabi na kutumikia masilahi yake ya kisiasa. Sheria ya Mungu walipewa Waisraeli ‘kwa ajili ya mema yao sikuzote, kwamba wao waweze kuendelea kuishi.’ (Kutoka 6:24, NW) Pia hakuna ushuhuda mwingi kwamba sheria ya Hammurabi ilipata kuwa sheria mbayo lazima ifuatwe kisheria katika Babuloni, ikatumika tu kama “msaada wa kisheria kwa watu waliotafuta shauri.” (The New Encyclopcedia Britannica, chapa ya 1985, Buku 21, uku. 921) Ile Sheria ya Musa, hata hivyo, ilikuwa sharti ifuatwe na kutotii kulileta adhabu ya haki. Kwa kumalizia, fungu la sheria la Hammurabi linakazia jinsi ya kushugulika na watenda makosa; 5 tu kati ya sheria zalo 280 zikiwa makatazo ya moja kwa moja. Hata hivyo, mkazo wa Sheria ya Mungu, uliwekwa juu ya kuzuia, si kuadhibu, watenda makosa.

9. Ni uvutano gani Sheria ya Musa ilikuwa nao juu ya maisha za Wayahudi?

9 Kwa sababu ilikuwa ‘takatifu, adilifu, na njema,’ ile Sheria ya Musa ilikuwa na uvutano wenye nguvu nyingi juu ya maisha ya binafsi ya Wayahudi. Hiyo ilirekebisha ibada yao, iliandalia Sabato za kuacha kufanya kazi, iliongoza muundo wa kiuchumi wa taifa hilo, ilitoa mambo kwa muhtasari juu ya matakwa fulani kuhusu mavazi, na ikatoa mwongozo wenye kunufaisha katika mambo ya chakula, utendaji wa kingono, na mazoea ya usafi wa afya. Hata utendaji mbalimbali wa kawaida wa mwili ulikuja chini ya uchunguzi wa Sheria ya Musa.

“Amri ya Yehova Ni Safi”

10. (a) Ni kwa sababu gani ile Sheria ilijishughulisha yenyewe na maeneo mengi sana ya maisha? (b) Ile Sheria iliendelezaje usafi wa kimwili na afya njema? (Tia ndani maelezo ya chini.)

10 Marekebisho kama hayo yenye mambo mengi madogo-madogo kutia ndani maisha ya siku baada ya siku yalikuwa na kusudi tukufu: Kufanya Waisraeli kuwa safi—kimwili, kiroho, kiakili, na kiadili. Mathalani, sheria zilizowataka wao waoge, wafunike kinyesi chao, wawatenge mbali wenye ugonjwa wa kuambukia, na waepuke chakula fulani-fulani yote hayo yaliendeleza afya na usafi wa kimwili.a—Kutoka 30:18-20; Walawi, sura ya 11; 13:4, 5, 21, 26; 15:16-18, 21-23; Kumbukumbu 23:12-14.

11. Ilimaanisha nini kuwa mchafu kisherehe?

11 Hata hivyo, kwa kweli usafi wa kiroho ulitangulizwa mbele ya afya njema na usafi. Ndiyo sababu mmoja ambaye pengine alikula mojapo vyakula vilivyokatazwa, akajitia katika mahusiano ya kingono, au akagusa maiti alitangazwa pia kuwa mchafu katika njia ya kisherehe. (Walawi sura za 11, 15; Hesabu sura ya 19) Hivyo mmoja kama huyo aliyekuwa mchafu alikatazwa asishiriki katika ibada—katika visa fulani kwa adhabu ya kifo! (Walawi 22:3-8; 15:31) Lakini makatazo kama hayo yalihusianaje na usafi wa kiroho?

12. Zile sheria za usafi wa kisherehe ziliendelezaje usafi wa kiroho?

12 Ibada ya kipagani ilikuwa na tabia ya kufanya umalaya, ibada ya wafu, na karamu zenye kupita kiasi. Lakini The International Standard Bible Encyclopedia inaeleza hivi: “Hakuna kitendo cha kingono kilichoruhusiwa kama njia ya kuabudu Yahweh. Utendaji wote huo katika habari hii, kwa hiyo, ulimfanya mmoja kuwa mchafu. . . . Katika Israeli wafu walipokea heshima yao inayowastahili, lakini kwa vyo vyote wao hawakupewa heshima isiyofaa wala hawakuwa vitu vya ibada . . . Zaidi ya hilo ushirika kwenye sherehe za majirani wapagani, ambazo zingetia ndani kuwa na karamu, haungewezekana kwa Mwisraeli, kwa sababu chakula chao kilikuwa kichafu.” Kwa hiyo, yale marekebisho ya sheria yalifanyiza “ukuta” wa mtenganisho na vianzo vichafu vya kidini.—Waefeso 2:14.

13. Ile Sheria iliendelezaje usafi wa kiakili?

13 Pia ile Sheria ilitokeza usafi wa kiadili wa Waisraeli. Amri zayo kuhusu mahusiano ya kingono, mathalani, yalitumikia kuinua kufikiri kwa mtu. (Walawi 15:16-33) Waisraeli walijifunza kujiweza katika mambo ya kingono, wasijiache washindwe na harara isiyozuiliwa kama Wakanaani. Ile Sheria hata ilifundisha wafuasi wayo kuzuia hisia na tamaa zao, ikishutumu kufikiri kwenye kutamani vya wengine.—Kutoka 20:17.

14. Sheria ya Mungu ilikuwaje ya pekee kwa habari ya kuendeleza usafi wa kiadili?

14 Jambo la kutazamisha zaidi ya yote, hata hivyo, lilikuwa mkazo wa Sheria juu ya usafi wa kiadili. Ni kweli, fungu la sheria la Hammurabi pia lilishutumu makosa kama vile uzinzi. Hata hivyo, nakala moja katika The Biblical Archaeologist ilieleza hivi: “Tofauti na Wababuloni na Waashuri ambao waliona uzinzi kuwa tu uhalifu dhidi ya haki za umaliki za mume, ule mfanyizo wa sheria wa Agano la Kale huona uzinzi pia kuwa kosa zito dhidi ya adili.”

15. (a) Toa kielezi jinsi Mwisraeli angekuwa na sharti la kufanya jitihada nyingi kubaki akiwa safi. (b) Waisraeli walinufaikaje kutokana na jitihada hizo?

15 Jinsi yalivyo ya kweli, basi, maneno ya mtunga Zaburi: “Amri ya Yehova ni safi, ikifanya macho yang’ae.” (Zaburi 19:8, NW) Inakubalika, nyakati fulani kubaki mtu akiwa safi kulitaka jitihada kubwa. Akina mama wapya, majuma machache tu baada ya kuzaa watoto wao, walikuwa sharti waende Yerusalemu ili wakafuate taratibu za kutakaswa. (Walawi 12:1-8; Luka 2:22-24) Wanaume na wanawake pia walitakwa wajitakase wenyewe kisherehe kufuatia uhusiano wa kingono, na pia katika hali nyingine zilizohusiana na hizo. (Walawi 15:16, 18; Kumbukumbu 23:9-14; 2 Samweli 11:11-13) Ikiwa wangefuata kwa kudhamiria sheria hiyo na kubaki wakiwa safi, wao ‘wangejinufaisha wenyewe’—kimwili, kiakili, kiadili, na kiroho. (Isaya 48:17, NW) Zaidi ya hilo, umaana na uzito wa kubaki wakiwa safi ungekazwa kikiki bila kufutika ndani yao. Jambo bora zaidi ya yote, jitihada za unyofu kama hizo za kudumisha utakatifu zingewapatia kibali cha Mungu.

Wasafi Katika Ulimwengu Usio Safi

16, 17. (a) Ni kwa kadiri gani Wakristo leo wanatakwa wabaki wakiwa safi? (b) Ni kwa sababu gani mtu kubaki akiwa safi ni jambo gumu sana leo? (c) Watu mmoja mmoja mashuhuri wameshindwaje wakiwa violezo vya kuigwa?

16 Sasa tunaweza kuthamini vizuri zaidi maneno ya Petro kwa Wakristo: “Ninyi mkiwa watoto wenye kutii, acheni kufanyizwa kwa mtindo unaolingana na tamaa mlizokuwa nazo zamani katika ujinga wenu, bali, kupatana na Mtakatifu aliyewaita, ninyi pia iweni watakatifu wenyewe katika mwenendo wenu wote, kwa sababu imeandikwa: ‘Ni lazima ninyi mwe watakatifu, kwa sababu mimi ni mtakatifu.’”​—1 Petro 1:14-16, NW.

17 Inakubaliwa, hili si jambo jepesi. Kila mahali tunapotazama, sisi tunaona watu wakizoea udanganyifu, ukosefu wa unyofu, ngono zisizo za adili. The New York Times linaripoti: “Waamerika wanazidi kuchagua kuishi pamoja kabla ya kufunga ndoa.” Hata watu mashuhuri wanaweka mifano mibaya. Baadhi ya watu wanaojulikana sana ulimwenguni leo katika maeneo ya michezo, siasa, na vitumbuizo wanazoea peupe namna fulani za uchafu. “Inatamausha sana,” akaomboleza mshabiki mmoja wa michezo, “kuwa na imani katika mtu fulani akiwa kiolezo chako cha kuigwa na kuwapata wakiwa wenye mawaa.” Tatizo ni nini? Wanariadha kadha wenye kujulikana sana walikuwa wameugama kuwa watumiaji wa dawa za kulevya. Ni mara nyingi kama nini watu mmoja mmoja wanaoheshimiwa sana wanaishi maisha machafu, ndiyo, hata maisha yenye ufisadi, wakiwa wazinzi, waasherati, wagoni-jinsia-moja wa kiume, wagoni-jinsia-moja wa kike, wevi, wanyang’anyi, and wazoevu wa dawa za kulevya! Huenda wakaonekana kuwa safi kimwili, lakini vinywa vyao vimejawa na maneno machafu-machafu ya kishenzi. Wao huenda hata wakafurahia kudharau mwenendo mzuri unaowafaa watu wote, wakijisifu juu ya matendo yao ya kujasiria mwenendo usio wa adili.

18. Ni jinsi gani wengi ambao wanaishi maisha machafu ‘wanavuna kile walichopanda’?

18 Hata hivyo, maneno haya ya Biblia hayawekwi kando kwa urahisi: “Mungu hadhihakiwi; kwa kuwa cho chote apandacho mtu, ndicho atakachovuna. Maana yeye apandaye kwa mwili wake, katika mwili wake atavuna uharibifu.” (Wagalatia 6:7, 8) Tabia yenye ufisadi mara nyingi inatokeza ugonjwa, huzuni, na kifo cha mapema kutokana na magonjwa kama vile kaswende, kisonono, na UKIMWI, kutaja yale yenye kutokeza. Ukosefu wa usawaziko wa kiakili na kimoyoni, mshuko wa moyo, na hata kujiua pia ni mambo ambayo mara nyingi yanatokezwa na mitindo ya maisha ya ngono za ovyoovyo. Kwa hiyo, ingawa wale wanaoshiriki katika mazoea yasiyo ya adili huenda wakacheka kwa kudharau wale wanaojaribu kujiweka wenyewe wakiwa safi, kicheko hicho kinakwisha wadhihaki hao waanzapo ‘kuvuna kile walichopanda.’—Linganisha Warumi 1:24-27.

19, 20. Viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo wamejithihitishaje kuwa wamechafuliwa kidini na kiadili?

19 Sisi tunaishi pia katika ulimwengu uliochafuliwa kidini. Viongozi wa kidini huenda wakavalia mavazi mazuri, safi, lakini wao wanafundisha mafundisho yasiyo safi ya Kibabuloni, kama vile ibada ya sanamu, Utatu, moto wa mateso, kutokufa kwa nafsi ya kibinadamu, na purgatori. Hao ni kama wale viongozi wa kidini ambao kwa habari yao Yesu alisema: “Ole wenu, waandishi na Mafarisayo, wanafiki! kwa kuwa mmefanana na makaburi yaliyopakwa chokaa, nayo kwa nje yaonekana kuwa mazuri, bali ndani yamejaa mifupa ya wafu, na uchafu wote. Vivyo hivyo ninyi nanyi, kwa nje mwaonekana na watu kuwa wenye haki, bali ndani mmejaa unafiki na maasi.”—Mathayo 23:27, 28.

20 Viongozi wa kidini hata wanaachilia uchafu katika kundi lao. Watu mmoja mmoja ambao wanajulikana kuwa wakosefu wa adili na wasio safi—wazoevu wa uasherati, uzinzi, ugoni-jinsia-moja—wanaruhusiwa kubaki katika msimamo mzuri. Juu ya jambo hili Newsweek linaripoti hivi: “Msaikolojia Richard Sipe wa Maryland, ambaye hapo kwanza alikuwa kasisi, anakata maneno kwamba asilimia yapata 20 ya makasisi Wakatoliki wa U.S. 57,000 ni wagoni-jinsia-moja . . . matabibu wengine hufikiri hesabu ya kweli leo huenda ikakaribia zaidi asilimia 40.” Mwanatheolojia John J. McNeill (anayekubali kuwa mgoni-jinsia-moja) anatetea waziwazi ugoni-jinsia-moja: “Upendo baina ya wagoni-jinsia-moja wawili wa kike au wa kiume, kwa kudhani kwamba ni upendo wa kibinadamu wenye kujenga, si wenye dhambi wala hautengi mbali wapenzi hao na mpango wa Mungu, bali unaweza kuwa upendo mtakatifu.”—The Christian Century.

21. Ni kwa jinsi gani kile kikumbusha “Utakatifu ni wa Yehova” kinafaa kwetu sisi leo?

21 Hivyo kile kikumbusha kilichowekwa wazi kionekane juu ya kilemba cha kuhani mkuu kinafaa zaidi kuliko wakati mwingine wo wote uliotangulia: “Utakatifu ni wa Yehova.” (Kutoka 28:36, NW) Yehova hutaka, ndiyo, huamuru, kwamba sisi tubaki tukiwa safi katika mambo yote! Lakini ni jinsi gani mmoja anaweza kufanya hivyo? Ni maeneo gani ambayo huenda yakahitaji kukaziwa fikira za pekee? Makala ifuatayo itazungumzia maswali haya.

[Maelezo ya Chini]

a Sheria ya Hammurabi haikuwa na maandalizi kama hayo; wala fungu la sheria za usafi wa kiafya linalolingana na hilo halijavumbuliwa miongoni mwa Wamisri wa kale, ingawa wao walitumia namna ya hali ya juu ya dawa kwa kulinganisha. Kinasema kitabu Ancient Egypt: “Maneno na maelezo ya michanganyiko ya kiuganga yanachanganywa pamoja bila kizuizi [katika vitabu vya dawa vya Wamisri] na hati zilizoandikwa zinazopatana na akili.” Sheria ya Mungu, hata hivyo, haikuwa na madokezo yo yote ya kishetani lakini ilikuwa sahihi kisayansi. Ni katika nyakati za ki-siku-hizi, kwa mfano, kwamba madaktari wameona uhitaji wa kujiosha baada ya kugusa maiti, jambo ambalo Sheria ya Musa ilitaka mileani nyingi zilizopita!—Hesabu sura 19.

Maswali kwa Ajili ya Kurudia

◻ Ni jinsi gani Yehova ni ‘hodari katika utakatifu,’ na hili linamaanisha nini kwa waabudu wake?

◻ Ile Sheria ya Musa ilitofautianaje na zile sheria za mataifa mengine yote?

◻ Ile Sheria ya Musa iliendelezaje usafi wa kimwili, kiroho, kiakili, na kiadili?

◻ Ni jinsi gani wengi ambao wanaishi maisha machafu ‘wanavuna kile walichopanda’?

[Picha katika ukurasa wa 11]

Ile ibada ya miungu mifasiki iliongoza kwenye kushushwa kwa maadili ya Wakanaani wenyewe

[Credit Line]

Courtesy of the British Museum, London

[Picha katika ukurasa wa 12]

Sheria ya Hammurabi ilileta utengemano kwa ile milki na ikamtukuza mfalme, lakini haikuleta utakatifu kwa Wababuloni

[Credit Line]

Louvre Museum, Paris

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki