Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w87 11/15 kur. 21-23
  • Waanabaptisti na “Kile Kiolezo cha Maneno Yenye Afya”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Waanabaptisti na “Kile Kiolezo cha Maneno Yenye Afya”
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “Kile Kiolezo” Chasimamishwa
  • Mafundisho ya Msingi
  • Maoni Yao Kuhusu Ulimwengu
  • Mateso—Na Baadaye
  • “Kile Kiolezo” cha Leo
  • Wanabaptisti Walikuwa Akina Nani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2004
  • Yale Mapinduzi Makubwa ya Kidini
    Jitihada ya Ainabinadamu ya Kutafuta Mungu
  • Zoeeni Kufanya Mambo Ambayo Mmejifunza
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2002
  • Fanya Fundisho Lenye Afya Liwe Njia Yako ya Maisha
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
w87 11/15 kur. 21-23

Waanabaptisti na “Kile Kiolezo cha Maneno Yenye Afya”

MTUME Paulo alionya kwamba baada ya kifo chake, Wakristo waasi-imani, kama “mbwa-mwitu wakali” wangeingia miongoni mwa kundi la Mungu na wangetafuta ‘kuwavuta hao wanafunzi wawaandamie wao.’ Wao wangefanyaje hivyo? Kwa kuingiza mapokeo na mafundisho ya uwongo kuupotoa ule ukweli wa Maandiko.—Matendo 20:29, 30; 1 Timotheo 4:1.

Kwa sababu hii, Paulo alisihi mwanamume kijana Timotheo hivi: “Endelea kushika kile kiolezo cha maneno yenye afya ambayo wewe umesikia kutoka kwangu mimi kwa imani na upendo ambavyo ni kuhusiana na Kristo Yesu. Amana hii bora itunze kupitia kwa roho takatifu inayokaa ndani yetu.” Hiki “kiolezo cha maneno yenye afya” kilikuwa nini?—2 Timotheo 1:13, 14, NW.

“Kile Kiolezo” Chasimamishwa

Vitabu vyote vya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo vilimalizwa katika karne ya kwanza ya Wakati Wetu wa Kawaida. Ijapokuwa viliandikwa na waandikaji tofauti-tofauti, roho takatifu ya Mungu, au kani ya utendaji, ilihakikisha kwamba vinalingana si vyenyewe kwa vyenyewe tu bali pia na Maandiko ya Kiebrania yaliyotangulia. Katika njia hii, “kiolezo” cha fundisho la Kimaandiko lililo timamu kilifanyizwa nacho kilifuatwa na Wakristo, kama vile Yesu alivyokuwa amekuwa “kiolezo” kwao ili wakifuate.—1 Petro 2:21, NW; Yohana 16:12, 13.

Wakati wa zile karne za giza la kiroho zilizofuata kifo cha mitume, ni nini kilichotendeka kwa “kile kiolezo cha maneno yenye afya”? Watu wengi wanyofu walijaribu kukigundua tena, ijapokuwa wakati wa kurudishwa kikamili kungengoja mpaka “wakati wa mwisho.” (Danieli 12:4) Nyakati nyingine ilikuwa sauti moja pekee, na nyakati nyingine kikundi kidogo cha watu ndicho kilichokuwa kikitafuta “kile kiolezo.”

Wawaldense wanaonekana kuwa walikuwa kikundi hicho cha wachachea hicho. Wao waliishi Ufaransa, Italia, na sehemu nyingine za Ulaya wakati wa karne ya 12 hadi 14. Kutokana na kikundi hiki Waanabaptisti wakatokea baadaye. Wao walikuwa akina nani, nao waliitikadi nini?

Mafundisho ya Msingi

Mara ya kwanza Waanabaptisti walipopata kujulikana ilikuwa kama mwaka 1525, katika Zurich, Uswisi. Kutoka mji huo itikadi zao zilienea kwa haraka sana kwenye sehemu nyingi za Ulaya. Ule Mgeuzo Mkuu wa mapema karne ya 16 ulifanya mabadiliko fulani, lakini machoni mwa Waanabaptisti, yalikuwa hayajafika mbali vya kutosha.

Wakiwa na tamaa ya kurudia mafundisho ya Kikristo ya karne ya kwanza, wao walikataa mengi ya mafundisho ya Katoliki ya Roma kuliko walivyofanya Martin Luther na wanamgeuzo wengine. Kwa mfano, Waanabaptisti walishikilia kwamba kungekuwa tu na kujitoa wakfu kwa Kristo kwa watu wazima peke yao. Kwa sababu ya zoea lao la kubatiza watu wazima, hata wale ambao walikuwa wamebatizwa wakiwa watoto wachanga, wao walipewa jina “Waanabaptisti,” linalomaanisha “wanaobatiza tena.”—Mathayo 28:19; Matendo 2:41; 8:12; 10:44-48.

“Kwa Waanabaptisti kanisa la kweli lilikuwa ushirika wa watu wenye kuitikadi,” akaandika Dakt. R. J. Smithson katika kitabu chake The Anabaptists—Their Contribution to Our Protestant Heritage. Kwa hiyo, wao waliojiona wenyewe kuwa jamii ya wenye itikadi ndani ya mtaa na mwanzoni-mwanzoni wao hawakuwa na wahudumu waliozoezwa kwa njia ya pekee, au wenye kulipwa. Kama wanafunzi wa Yesu, wao walikuwa wahubiri wa kwenda huku na huku wakitembelea miji na vijiji, wakizungumza na watu katika sehemu za soko, viwanda vya kufanyia kazi na nyumbani.—Mathayo 9:35; 10:5-7, 11-13; Luka 10:1-3.

Kila Mwanaanabaptisti mmoja mmoja alionwa kuwa ana wajibu wa kibinafsi kwa Mungu, akifurahia uhuru wa hiari na kuonyesha imani yake kwa kazi zake, lakini akitambua kwamba wokovu haupatikani kwa kazi pekee. Kama mtu angeikosea imani, yeye angeweza kufukuzwa kutoka katika kundi. Angerudishwa tena ikiwa tu kulikuwa na ithibati ya toba inayofaa.—1 Wakorintho 5:11-13; Linganisha 2 Wakorintho 12:21.

Maoni Yao Kuhusu Ulimwengu

Waanabaptisti walitambua kwamba wao hawangeweza kuugeuza ulimwengu. Ingawa Kanisa lilikuwa limefanya urafiki na Serikali tangu wakati wa mmaliki Mroma Konstantino katika karne ya nne W.K., kwa wao hilo halikumaanisha kwamba serikali ilikuwa imekuwa ya Kikristo. Kutokana na yale ambayo Yesu alikuwa amesema, wao walijua kwamba Mkristo hapasi kuwa “sehemu ya ulimwengu,” hata kama jambo hilo lingetokeza mateso.—Yohana 17:15, 16, NW; 18:36.

Mahali ambapo hapakuwa na hitilafu kati ya dhamiri ya Mkristo na masilahi ya kilimwengu, Waanabaptisti walikubali kwamba Serikali zapasa kuonyeshwa heshima na utii katika njia inayofaa. Lakini Mwanaanabaptisti hangejiingiza katika siasa, hangeshikilia cheo cha kiserikali, hangekuwa hakimu, au hangeapisha viapo. Akiepuka aina zote za jeuri na utumiaji nguvu yeye pia hangejihusisha katika vita au utumishi wa kijeshi.​—Marko 12:17; Matendo 5:29; Warumi 13:1-7; 2 Wakorintho 10:3, 4.

Waanabaptisti walidumisha kiwango cha juu cha adili katika maisha ya kujiweza yaliyo rahisi, yaliyo huru kutokana na vitu vya kimwili na tamaa. Kwa sababu ya upendo wao kwa mmoja na mwenzake, mara nyingi wao walianzisha mitaa, ijapokuwa walio wengi wao walikataa maisha ya ujamaa. Hata hivyo, kwa msingi wa kwamba kila kitu ni cha Mungu, wao sikuzote walikuwa tayari kutumia mali zao za kimwili kuwasaidia maskini.—Matendo 2:42-45.

Kupitia funzo la uangalifu la Biblia, hasa la Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, Waanabaptisti wengine walikataa fundisho la Utatu wa watu watatu katika Mungu mmoja, kama vile mengine ya maandishi yao yanavyoshuhudia. Kwa kawaida njia yao ya kuabudu ilikuwa rahisi sana, Chakula cha Jioni cha Bwana kikiwa na mahali pa pekee. Wakikataa maoni ya kimapokeo ya Katoliki ya Roma, ya Kilutheri, na ya Kikalvinisti, waliliona tendo hili la kuadhimisha kuwa ukumbusho wa kifo cha Yesu. “Kwa wao,” aandika R. J. Smithson, “hicho kilikuwa kitendo chenye uzito ambacho katika hicho Mkristo anaweza kushiriki, kikihusu kufanywa upya kwa agano la mwenye itikadi kuyatoa maisha yake kwa utumishi wa Kristo bila masharti.”

Mateso—Na Baadaye

Waanabaptisti walifahamiwa kimakosa, sawa na vile Wakristo wa mapema walivyofahamiwa. Wao walionwa kuwa wenye kuvuruga utaratibu uliosimamishwa wa jamii, ‘wakipindua dunia inayokaliwa.’ (Matendo 17:6. NW) Katika Zurich, Uswisi, wenye mamlaka, wakiungana na mwanamageuzo Huldrych Zwingli, waliwachukulia hatua Waanabaptisti kwa sababu ya kukataa kwao kubatiza vitoto vichanga. Katika 1527 wao walimfisha maji kwa ukatili Felix Manz, aliyekuwa mmoja wa viongozi wa Waanabaptisti, nao waliwatesa vikali sana Waanabaptisti Waswisi hivi kwamba karibu wote wamalizike.

Katika Ujeremani Waanabaptisti waliteswa vikali sana na Wakatoliki na Waprotestanti. Amri ya kifalme, iliyotolewa katika mwaka 1528, iliamuru adhabu ya kifo kwa ye yote ambaye angekuwa Mwanaanabaptisti​—bila kufanyiwa kesi ya namna yo yote. Mateso yaliyotukia katika Austria yalisababisha Waanabaptisti walio wengi kutafuta kimbilio katika Moravia, Bohemia, na Polandi, na baadaye katika Hungari na Urusi.

Kwa sababu ya kifo cha wengi wa viongozi wa kwanza, lilikuwa jambo lisiloepukika kwamba wale wenye maoni ya kupita kiasi wangejitokeza. Walileta hali ya kukosa usawaziko iliyoongoza kwenye mvurugo mwingi na baadaye kuanguka kutoka kwa viwango vilivyokuwako siku za mwanzoni-mwanzoni. Kwa kuhuzunisha jambo hili lilionekana wazi katika mwaka 1534, wakati hawa wenye maoni ya kupita kiasi walipotwaa kwa nguvu serikali ya manispaa ya Munster, Westphalia. Mwaka uliofuata mji huo ulitekwa tena kukiwako umwagaji damu mwingi na mateso makali. Kituko hiki hakikupatana na mafundisho ya kweli ya Waanabaptisti nacho kiliwavunjia heshima sana. Wafuasi wengine walitafuta kulikataa lile jina Waanabaptisti wakipendelea jina “Wabaptisti.” Lakini hata wachague jina gani, bado walipingwa hasa na Baraza zenye ukatili za kuhukumu wazushi wa dini za Kikatoliki.

Hatimaye, vikundi vya Waanabaptisti vikahama vikitafuta uhuru na amani zaidi. Leo, tunawapata katika Amerika ya Kaskazini na kusini, na pia katika Ulaya. Mafundisho yao ya kwanza-kwanza yamekuwa na uvutano juu ya madhehebu mengi, kutia na Wakweka, wale Wabaptisti wa ki-siku-hizi na wale Wabrethreni wa Plymouth. Wakweka wanashiriki ile chuki ya vita ya Waanabaptisti na lile wazo la mwongozo wa ‘nuru ya ndani.’

Kusalimika kwa Waanabaptisti kunaonekana wazi sana leo katika vikundi viwili hasa. Cha kwanza ni Wabrethreni Wahuteri, walioitwa kwa jina la kiongozi wao wa karne ya 15, Jacob Hutter. Wao walianzisha makao ya ujamaa katika Uingereza, Kanada ya Magharibi, Paraguay, na Dakota ya Kusini katika United States. Wamenno ndicho kile kikundi kingine. Wao wanalipata jina lao kutokana na Menno Simons, aliyefanya mengi katika kufutilia maandishi mabaya yaliyokuwa yameachwa katika Uholanzi kufuatia kile kituko cha Munster. Simons alikufa katika 1561. Leo, Wamenonite wanapatikana katika Ulaya na Amerika ya Kaskazini, pamoja na Wamenonite Waamishi.

“Kile Kiolezo” cha Leo

Ijapokuwa huenda Waanabaptisti walitafuta “kile kiolezo cha maneno yenye afya,” wao hawakufaulu katika kukivumbua. Zaidi ya hilo, katika kitabu chake A History of Christianity, K. S. Latourette anasema hivi: “Mwanzoni-mwanzoni wakiwa wenye bidii ya kimisionari, mateso yalisababisha wao sana sana kurudi nyuma na kujikalia kitako wakijiendeleze wenyewe kwa uzawa badala ya wongofu.” Na ndivyo ilivyo hata sasa katika vikundi vidogo vinavyoweza kufuatiliwa kurudi nyuma mpaka kwa Waanabaptisti. Tamaa yao ya kuwa tofauti na ulimwengu na njia yayo imeongoza wao kuendeleza mitindo ya mavazi iliyo tofauti, wakitiwa moyo na maisha yao ya ujamaa ambayo mara nyingi huwa ya kujitenga.

Hivyo, basi, je! “kile kiolezo cha maneno yenye afya” kinaweza kweli kupatikana leo? Ndiyo, lakini inachukua wakati na upendo wa ukweli ili kukipata. Mbona usichunguze ili uone kama yale unayoitikadi yanalingana na “kiolezo” kilichofunuliwa kimungu? Si vigumu kuamua ni yapi yaliyo mapokeo ya kibinadamu na yale ambayo ni uhakika wa Kimaandiko. Mashahidi wa Yehova walio katika eneo lenu watafurahi kukusaidia wewe, kwa kuwa wao wenyewe wanathamini njia ambayo wamesaidiwa ili wafahamu “kile kiolezo cha maneno yenye afya.”

[Maelezo ya Chini]

a Ona Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) Agosti 1, 1981, kurasa 12-15.

[Picha katika ukurasa wa 23]

Mashahidi wa Yehova husiadia wengi wafahamu “kile kiolezo cha maneno yenye afya.”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki