Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w94 6/15 kur. 17-22
  • Fanya Fundisho Lenye Afya Liwe Njia Yako ya Maisha

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Fanya Fundisho Lenye Afya Liwe Njia Yako ya Maisha
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Njia ya Maisha Yenye Afya
  • Shauri kwa Wanaume Wenye Umri Mkubwa Zaidi
  • Kwa Wanawake Wenye Umri Mkubwa Zaidi
  • Kwa Wanawake Vijana
  • Kwa Wanaume Vijana
  • Kwa Watumwa na Watumishi
  • Watu Waliosafishwa
  • Kaeni Wenye Afya Katika Imani!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Kitabu cha Biblia Namba 56—Tito
    “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
  • Timotheo Anapata Mashauri kwa Mwanamume Mzee
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
  • Kitabu cha Biblia Namba 54—1 Timotheo
    “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
w94 6/15 kur. 17-22

Fanya Fundisho Lenye Afya Liwe Njia Yako ya Maisha

“Utauwa [ujitoaji kimungu, NW] hufaa kwa mambo yote.”—1 TIMOTHEO 4:8.

1, 2. Ni kwa kadiri gani watu huhangaikia afya yao, kukiwa na tokeo gani?

WATU wengi watakubali kwa haraka kwamba afya njema ni mojayapo mambo ya maana zaidi ambayo mtu aweza kuwa nayo maishani. Wao hutumia wakati na fedha nyingi ili kufanya afya yao iwe bora na kuhakikisha kwamba wanapata matibabu yafaayo wanapoyahitaji. Kwa kielelezo, katika Marekani, gharama za kila mwaka za utunzaji wa afya za mwaka wa hivi karibuni zilikuwa zaidi ya dola bilioni 900. Hiyo yajumlika kuwa zaidi ya dola 3,000 kila mwaka kwa kila mwanamume, mwanamke, na mtoto nchini humo, na gharama za mtu mmoja-mmoja katika nchi nyinginezo zilizoendelea ni karibu sawa.

2 Matumizi yote ya wakati, nishati, na fedha yameleta nini? Kwa kweli hakuna mtu anayeweza kukanusha kwamba, kwa ujumla, tuna vifaa na ugavi wa kitiba wa hali ya juu sana leo kuliko wakati mwingine wowote wa historia. Lakini, hiyo haimaanishi kwa njia ya moja kwa moja, kuwa na maisha yenye afya. Kwa kweli, katika hotuba moja iliyoorodhesha programu ya utunzaji wa afya iliyopendekezwa itumiwe Marekani, rais (wa nchi hiyo) alisema kwamba zaidi ya “ile gharama kubwa ya jeuri humu nchini,” wakazi wa Marekani “wana viwango vya juu zaidi vya UKIMWI, vya uvutaji wa sigareti na unywaji wa kupindukia, vya mimba za matineja, vya vitoto vyenye uzani mdogo vinapozaliwa” kuliko taifa jingine lililoendelea. Neno lake la mkataa? “Ni lazima tubadili njia zetu ikiwa twataka kuwa wenye afya kikweli tukiwa taifa.”—Wagalatia 6:7, 8.

Njia ya Maisha Yenye Afya

3. Kwa sababu ya utamaduni wa Ugiriki, Paulo alitoa shauri gani?

3 Katika karne ya kwanza, Wagiriki walijulikana kwa ajili ya ujitoaji wao kwa mazoezi ya mwili, kujenga mwili, na mashindano ya riadha. Juu ya msingi huo, mtume Paulo alipuliziwa kumwandikia kijana Timotheo hivi: “Kujizoeza kupata nguvu za mwili kwafaa kidogo, lakini utauwa [ujitoaji kimungu, NW] hufaa kwa mambo yote; yaani, unayo ahadi ya uzima wa sasa, na ya ule utakaokuwapo baadaye.” (1 Timotheo 4:8) Hivyo, Paulo alikuwa akionyesha yale ambayo watu leo wanakuja kukubali, yaani, kwamba maandalizi ya kitiba na kimwili hayatoi uhakikisho wa njia ya maisha yenye afya kikweli. Hata hivyo, Paulo atuhakikishia kwamba jambo la maana zaidi ni kusitawisha hali njema ya kiroho na ujitoaji kimungu.

4. Ni zipi manufaa za ujitoaji kimungu?

4 Mwendo huo ni wenye manufaa kwa ‘uhai wa sasa’ kwa sababu huo huandaa ulinzi dhidi ya mambo yote yenye kudhuru ambayo watu wasiomwogopa Mungu, au wale wenye “mfano [au, muonekano] wa utauwa [ujitoaji kimungu, NW]” tu, hujiletea wenyewe. (2 Timotheo 3:5; Mithali 23:29, 30; Luka 15:11-16; 1 Wakorintho 6:18; 1 Timotheo 6:9, 10) Wale wanaoruhusu ujitoaji kimungu ufinyange maisha yao wana staha ifaayo kwa sheria na matakwa ya Mungu, na hilo huwasukuma kufanya fundisho lenye afya la Mungu kuwa njia yao ya maisha. Mwendo huo huwaletea afya ya kiroho na ya kimwili, uradhi, na furaha. Nao ‘wanajiwekea wenyewe hazina salama yenye msingi mzuri kwa ajili ya wakati ujao, ili kwamba wao wapate kuwa na mshiko imara wa uhai ulio kwelikweli.’—1 Timotheo 6:19, NW.

5. Paulo alitoa maagizo gani katika sura ya pili ya barua yake kwa Tito?

5 Kwa kuwa maisha yanayoongozwa na fundisho lenye afya la Mungu huleta baraka hizo sasa na katika wakati ujao, twahitaji kujua, katika maana itumikayo, jinsi tunavyoweza kufanya fundisho lenye afya la Mungu kuwa njia yetu ya maisha. Mtume Paulo aliandaa jibu katika barua yake kwa Tito. Tutachunguza kipekee sura ya pili ya kitabu hicho, ambamo alimwagiza Tito ‘aendelee kunena mambo yapasayo fundisho lenye afya.’ Kwelikweli, kila mmoja wetu, vijana kwa wazee, wanaume kwa wanawake, twaweza kunufaika na ‘fundisho lenye afya’ kama hilo leo.—Tito 1:4, 5; 2:1, NW.

Shauri kwa Wanaume Wenye Umri Mkubwa Zaidi

6. Paulo alitoa shauri gani kwa “wanaume wenye umri mkubwa,” na kwa nini ilikuwa fadhili kwake kufanya hivyo?

6 Kwanza, Paulo alikuwa na shauri kwa wanaume wenye umri mkubwa zaidi kutanikoni. Tafadhali soma Tito 2:2. “Wazee [wanaume wenye umri mkubwa, NW],” wakiwa kikundi, hustahiwa na kutegemewa kuwa vielelezo vya imani na uaminifu-mshikamanifu. (Mambo ya Walawi 19:32; Mithali 16:31) Kwa sababu hiyo, huenda wengine wakasita kutoa shauri au madokezo kwa wanaume wenye umri mkubwa zaidi juu ya mambo mazito. (Ayubu 32:6, 7; 1 Timotheo 5:1) Kwa hiyo, Paulo aonyesha fadhili kwa kuwaandikia wanaume wenye umri mkubwa zaidi kwanza, na ingekuwa vema kwao kuzingatia moyoni maneno ya Paulo na kuhakikisha kwamba wao, kama vile Paulo, wastahili kuigwa.—1 Wakorintho 11:1; Wafilipi 3:17.

7, 8. (a) Kuwa mwenye “kiasi katika mazoea” hutia nini ndani? (b) Kwa nini kuwa ‘mzito’ kusawazishwe na kuwa “timamu katika akili”?

7 Kwanza, wanaume Wakristo wenye umri mkubwa zaidi wapaswa kuwa wenye “kiasi katika mazoea.” (NW) Ingawa neno la awali laweza kurejezea zoea la kunywa (“asiyelewa,” Kingdom Interlinear), pia lina maana ya kuwa mwenye kukesha, kulevuka, au kutunza hisi. (2 Timotheo 4:5; 1 Petro 1:13) Hivyo, iwe ni katika kunywa au katika mambo mengine, ni lazima wanaume wenye umri mkubwa zaidi wawe wenye kiasi, si walafi au wenye kupita mipaka.

8 Halafu, wao wapaswa pia kuwa “wastahivu [wachukua-mambo kwa uzito, NW]” na “wenye busara [timamu katika akili, NW].” Kwa kawaida, kuwa mwenye kuchukua mambo kwa uzito, au mwenye adhama, mwenye kuheshimika, na mwenye kustahili staha, huja na umri. Hata hivyo, wengine huelekea kuwa wenye kuchukua mambo kwa uzito kupita kiasi, wakikosa kuvumilia hekaheka zenye nishati nyingi za vijana. (Mithali 20:29) Ndiyo sababu “uzito” wasawazishwa na “timamu katika akili.” Wanaume wenye umri mkubwa zaidi wahitaji kudumisha uzito unaolingana na umri, na wakati uo huo wawe na usawaziko, wakidhibiti kikamili hisia na misukumo yao.

9. Kwa nini ni lazima wanaume wenye umri mkubwa zaidi wawe wenye afya katika imani na upendo na hasa katika uvumilivu?

9 Hatimaye, wanaume wenye umri mkubwa zaidi wapaswa kuwa “wazima katika imani na katika upendo na katika saburi [uvumilivu, NW].” Mara nyingi katika maandishi yake, Paulo aliorodhesha imani na upendo pamoja na tumaini. (1 Wakorintho 13:13; 1 Wathesalonike 1:3; 5:8) Hapa aliweka “tumaini” mahali pa “uvumilivu.” Labda ni kwa sababu hisia ya kukata tamaa yaweza kujiimarisha kwa urahisi, umri uongezekapo. (Mhubiri 12:1) Hata hivyo, kama vile Yesu alivyosema, “mwenye kuvumilia hata mwisho, ndiye atakayeokoka.” (Mathayo 24:13) Zaidi ya hayo, wale wenye umri mkubwa zaidi ni vielelezo vizuri kwa wengine, si kwa sababu ya umri wao au maarifa yao tu, bali kwa sababu ya sifa zao za kiroho zilizoimarika—imani, upendo, na uvumilivu.

Kwa Wanawake Wenye Umri Mkubwa Zaidi

10. Paulo aandaa shauri gani kwa “wanawake wenye umri mkubwa” kutanikoni?

10 Halafu Paulo alielekeza uangalifu wake kwa wanawake wenye umri mkubwa zaidi kutanikoni. Tafadhali soma Tito 2:3. “Wazee wa kike [wanawake wenye umri mkubwa, NW],” ni washiriki wa daraja la juu miongoni mwa wanawake kutanikoni, kutia na wake za “wanaume wenye umri mkubwa” na mama na nyanya za washiriki wengineo. Kwa hiyo, wao waweza kuwa na uvutano mkubwa, ama kwa mazuri ama kwa mabaya. Ndiyo sababu Paulo alitanguliza maneno yake kwa kusema ‘vivyo hivyo,’ kumaanisha kwamba “wanawake wenye umri mkubwa” pia wana madaraka fulani wanayotazamiwa kutimiza ili kukamilisha fungu lao kutanikoni.

11. Tabia yenye ustahifu ni nini?

11 Kwanza, “wanawake wenye umri mkubwa na wawe wastahifu katika tabia,” (NW) akasema Paulo. “Tabia” ni wonyesho wa nje wa mtazamo wa ndani na utu wa mtu, kama unavyoonyeshwa na mwenendo na sura pia. (Mathayo 12:34, 35) Basi mtazamo au utu wa mwanamke Mkristo mwenye umri mkubwa wapaswa kuwa nini? Kwa neno moja, ‘mstahifu.’ Hilo limetafsiriwa kutoka kwa neno la Kigiriki linalomaanisha “kile kinachofaa katika watu, matendo au vitu vilivyotolewa wakfu kwa Mungu.” Hili kwa kweli ni shauri linalofaa kwa sababu ya uvutano wanaokuwa nao juu ya wengine, hasa juu ya wanawake vijana kutanikoni.—1 Timotheo 2:9, 10.

12. Wote wapaswa kuepuka utumizi gani mbaya wa ulimi?

12 Halafu kuna tabia mbili zisizofaa: “si wachongezi, wala waliofanywa watumwa wa divai nyingi sana.” (NW) Inavuta fikira kwamba hayo mawili yamewekwa pamoja. “Nyakati za kale, divai ilipokuwa kinywaji pekee,” aonelea Profesa E. F. Scott, “ilikuwa kwenye karamu zao ndogo za divai ndiko wanawake wazee wangewachongea majirani wao.” Kwa kawaida wanawake huhangaikia watu zaidi ya wanaume, jambo linalostahili sifa. Lakini, kuhangaikia wengine kwaweza kugeuka kuwa porojo na hata uchongezi, hasa ulimi unapolegezwa na mvinyo. (Mithali 23:33) Kwelikweli, yafaa wote wanaofuatia njia ya maisha yenye afya, wanaume na wanawake, wawe macho kuona mtego huo.

13. Wanawake wenye umri mkubwa zaidi waweza kuwa wafundishaji kwa njia gani?

13 Ili kutumia ifaavyo wakati unaopatikana, wanawake wenye umri mkubwa zaidi wanatiwa moyo kuwa “wafundishaji wa lililo jema.” (NW) Kwingineko, Paulo alitoa maagizo ya waziwazi kwamba wanawake hawapaswi kuwa wafundishaji kutanikoni. (1 Wakorintho 14:34; 1 Timotheo 2:12) Hata hivyo, hilo haliwazuii kutoa ujuzi wa Mungu wenye thamani kwa watu wa nyumba zao na kwa umma. (2 Timotheo 1:5; 3:14, 15) Wao waweza pia kufanya vema sana kwa kuwa vielelezo vya Kikristo kwa wanawake vijana kutanikoni, kama vile mistari ifuatayo inavyoonyesha.

Kwa Wanawake Vijana

14. Wanawake Wakristo walio vijana waweza kuonyeshaje usawaziko katika kushughulikia kazi zao?

14 Akiwatia moyo wanawake wenye umri mkubwa zaidi kuwa “wafundishaji wa lililo jema,” Paulo alitaja hususa wanawake vijana. Tafadhali soma Tito 2:4, 5. Ingawa maagizo mengi yakazia mambo ya nyumbani, wanawake Wakristo walio vijana hawapaswi kupita kiasi, wakijiruhusu wahangaikie vitu vya kimwili maishani mwao mwote. Badala ya hivyo, wanapaswa kuwa “timamu katika akili, safi kiadili, . . . wema,” (NW) na zaidi ya yote, wawe tayari kuunga mkono mpango wa ukichwa wa Kikristo, “ili neno la Mungu lisitukanwe.”

15. Kwa nini wanawake wengi vijana kutanikoni wafaa kupongezwa?

15 Leo, hali ya familia imebadilika sana kutoka ilivyokuwako katika siku ya Paulo. Familia nyingi zimegawanyika kwa habari ya imani, na nyingine zina mzazi mmoja tu. Hata katika zile ziitwazo eti familia za kawaida, ni jambo linalozidi kuwa lisilo la kawaida kwamba mke au mama ni mtunza-nyumba wa wakati wote. Yote hayo huweka mkazo na daraka kubwa juu ya wanawake Wakristo walio vijana, lakini hilo haliwaondolei jukumu la kutimiza madaraka yao ya Kimaandiko. Kwa hiyo ni furaha kuu, kuona wanawake wengi vijana walio waaminifu wakifanya bidii ili kusawazisha madaraka yao mengi na bado waweze kutanguliza masilahi ya Ufalme, wengine hata wakiwa katika huduma ya wakati wote wakiwa mapainia wasaidizi au wa kawaida. (Mathayo 6:33) Wao wastahili sifa kwelikweli!

Kwa Wanaume Vijana

16. Paulo alikuwa na shauri gani la kuwapa wanaume vijana, na kwa nini hilo lilikuwa la wakati unaofaa?

16 Halafu Paulo akafikia wanaume vijana, kutia ndani Tito. Tafadhali soma Tito 2:6-8. Kwa sababu ya mwenendo wa kutojali madaraka na wa uharibifu wa vijana wengi leo—kuvuta sigareti, utumizi mbaya wa madawa ya kulevya na kileo, ngono haramu, na mambo mengine ya ulimwengu yanayofuatiwa, kama vile michezo isiyo na adabu na muziki na vitumbuizo visivyo vya staha—hili kwa kweli ni shauri la wakati unaofaa kwa vijana Wakristo wanaotaka kufuata njia ya maisha yenye afya na uradhi.

17. Mwanamume kijana aweza kuwaje “timamu katika akili” na “kielelezo cha matendo mema”?

17 Tofauti na vijana wa ulimwengu, mwanamume kijana aliye Mkristo apaswa kuwa mwenye “kiasi [timamu katika akili, NW]” na “kielelezo cha matendo mema.” Paulo alieleza kwamba akili timamu iliyokomaa haipatikani na wale wanaojifunza tu, bali na wale ambao “akili zao, kwa kutumiwa, zimezoezwa kupambanua mema na mabaya.” (Waebrania 5:14) Ni vizuri kama nini kuona vijana wakitoa wakati na nishati zao ili kuwa na ushiriki kamili katika kazi nyingi kwenye kutaniko la Kikristo, badala ya kupoteza nguvu zao za ujana kwa kufuatilia mambo ya ubinafsi! Kwa kufanya hivyo, wao, kama Tito, waweza kuwa vielelezo “vya matendo mema” katika kutaniko la Kikristo.—1 Timotheo 4:12.

18. Inamaanisha nini kutofisidika katika mafundisho, kuchukua mambo kwa uzito, na kuwa na usemi wenye afya?

18 Wanaume vijana wanakumbushwa kwamba wanapaswa kuwa ‘wakionyesha kutofisidika katika mafundisho yao, wakichukua mambo kwa uzito, wakiwa na usemi wenye afya usioweza kulaumiwa.’ (NW) Ni lazima mafundisho ‘yasiyofisidika’ yategemee kwa imara Neno la Mungu; kwa hiyo, ni lazima vijana wanaume wawe wanafunzi wa Biblia wenye bidii. Kama vile wanaume wenye umri mkubwa zaidi, wao pia wapaswa kuwa wazito. Wanahitaji kutambua kwamba kuwa mhudumu wa Neno la Mungu ni daraka zito, na kwa hiyo ni lazima ‘wajiendeshe kwa namna yenye kustahiki habari njema.’ (Wafilipi 1:27, NW) Vilevile usemi wao wapaswa kuwa “wenye afya” na “usioweza kulaumiwa” ili wasiwape wapinzani sababu yoyote ya kulalamika.—2 Wakorintho 6:3; 1 Petro 2:12, 15.

Kwa Watumwa na Watumishi

19, 20. Wale walioajiriwa waweza ‘kuyapambaje mafundisho ya Mwokozi wetu, Mungu’?

19 Hatimaye, Paulo alielekezea maneno yake wale walioajiriwa na wengine. Tafadhali soma Tito 2:9, 10. Si wengi kati yetu tulio watumwa au watumishi, lakini wengi ni waajiriwa na wafanyakazi wanaowatolea wengine huduma. Hivyo, kanuni zilizotolewa na Paulo hutumika vilevile leo.

20 ‘Kutii bwana zao, wakiwapendeza katika mambo yote’ kwamaanisha kwamba ni lazima Wakristo walioajiriwa waonyeshe waajiri na wasimamizi wao staha ya kweli. (Wakolosai 3:22) Ni lazima wao pia wawe na sifa ya kuwa wafanyakazi wenye kufuatia haki, wakimpa mwajiri wao utumishi wa siku nzima ipaswavyo. Na ni lazima wadumishe viwango vya juu vya mwenendo wa Kikristo kwenye mahali pao pa kazi bila kujali wengine wana tabia gani hapo. Yote hayo ni “ili wayapambe mafundisho ya Mwokozi wetu Mungu katika mambo yote.” Ni mara nyingi kama nini tunasikia juu ya matokeo mazuri wakati watazamaji wenye mioyo myeupe waitikiapo kweli kwa sababu ya mwenendo mzuri wa wafanyakazi wenzao au waajiriwa walio Mashahidi! Hiyo ni thawabu ambayo Yehova huwapa wale wanaofuata fundisho lake lenye afya hata kwenye mahali pao pa kazi.—Waefeso 6:7, 8.

Watu Waliosafishwa

21. Kwa nini Yehova ameandaa fundisho lenye afya, nasi twapaswa kuitikiaje?

21 Fundisho lenye afya ambalo Paulo alifafanua si orodha tu ya kanuni za uungwana au mwongozo wa kiadili ambao twaweza kuurejezea tutakapo. Paulo aliendelea kueleza juu ya kusudi la huo. Tafadhali soma Tito 2:11, 12. Kwa sababu ya upendo wake na fadhili zisizostahiliwa kwetu, Yehova Mungu ameandaa fundisho lenye afya ili tuweze kujifunza kuishi maisha yenye kusudi na uradhi katika nyakati hizi zilizo ngumu na zenye hatari. Je! uko tayari kukubali na kufanya fundisho lenye afya liwe njia yako ya maisha? Kufanya hivyo kutamaanisha wokovu wako.

22, 23. Twapata baraka gani kwa kufanya fundisho lenye afya kuwa njia yetu ya maisha?

22 Zaidi ya hayo, kufanya fundisho lenye afya liwe njia yako ya maisha hutuletea pendeleo la pekee sasa na tumaini lenye furaha wakati ujao. Tafadhali soma Tito 2:13, 14. Kwa kweli, kufanya fundisho lenye afya liwe njia yetu ya maisha hututenganisha na ulimwengu mfisadi unaokufa tukiwa watu waliosafishwa. Maneno ya Paulo yalingana na makumbusha ya Musa kwa wana wa Israeli kwenye Sinai: “Naye BWANA, . . . atakutukuza juu ya mataifa yote aliyoyafanya, kwa sifa, na jina, na heshima, nawe upate kuwa taifa takatifu kwa BWANA, Mungu wako, kama alivyosema.”—Kumbukumbu la Torati 26:18, 19.

23 Na tuthamini sikuzote pendeleo letu la kuwa watu wa Yehova waliosafishwa kwa kufanya fundisho lenye afya kuwa njia yetu ya maisha! Sikuzote uwe macho kukataa katakata uovu wa aina yoyote na tamaa za kilimwengu, hivyo uendelee kuwa safi na kufaa kutumiwa na Yehova katika kazi tukufu ambayo anatendesha leo.—Wakolosai 1:10.

Je! Wakumbuka?

◻ Kwa nini ujitoaji kimungu wafaa kwa mambo yote?

◻ Wanaume na wanawake Wakristo wenye umri mkubwa zaidi wanaweza kufuatiaje fundisho lenye afya kuwa njia ya maisha?

◻ Paulo alikuwa na fundisho gani lenye afya kwa ajili ya wanaume na wanawake vijana kutanikoni?

◻ Twaweza kupata pendeleo na baraka gani tukifanya fundisho lenye afya kuwa njia yetu ya maisha?

[Picha katika ukurasa wa 18]

Wengi leo wanatumia shauri lililoko kwenye Tito 2:2-4

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki